Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wasaidieni Warudi Haraka!

Wasaidieni Warudi Haraka!

Wasaidieni Warudi Haraka!

“Bwana, tutaenda kwa nani? Wewe una maneno ya uzima wa milele.”—YOH. 6:68.

1. Petro alisema nini wanafunzi wengi walipomwacha Yesu?

WAKATI fulani, wanafunzi wengi wa Yesu Kristo walimwacha kwa sababu ya jambo fulani ambalo alifundisha. Yesu aliwauliza mitume wake: “Je, ninyi pia mnataka kwenda?” Petro akamjibu: “Bwana, tutaenda kwa nani? Wewe una maneno ya uzima wa milele.” (Yoh. 6:51-69) Hawangeweza kwenda mahali pengine. Dini ya Kiyahudi haikuwa na “maneno ya uzima wa milele,” na kwa hakika maneno hayo hayawezi kupatikana leo katika Babiloni Mkubwa, milki ya ulimwengu ya dini ya uwongo. Mtu yeyote ambaye ameacha kushirikiana na kundi la Mungu lakini anataka kumpendeza Yehova anapaswa kutambua kwamba hii ndiyo ‘saa ya kuamka kutoka katika usingizi’ na kurudi katika kundi.—Rom. 13:11.

2. Ni jambo gani tunalopaswa kukumbuka kuhusu mambo ya siri au ya kihukumu?

2 Yehova aliwahangaikia kondoo waliopotea wa Israeli. (Soma Ezekieli 34:15, 16.) Vivyo hivyo, wazee Wakristo wanataka na wana wajibu wa kumsaidia mtu aliye kama kondoo ambaye ameacha kushirikiana na kundi. Wakimpa mhubiri mgawo wa kujifunza na mtu asiyetenda ambaye anataka kusaidiwa, mhubiri huyo anapaswa kufanya nini akigundua kwamba mtu huyo amefanya dhambi nzito? Badala ya kutoa shauri kuhusu jambo lolote la kihukumu au la siri, mhubiri huyo anapaswa kumpendekezea azungumze na wazee. Asipofanya hivyo, mhubiri mwenyewe anapaswa kuwajulisha wazee.—Law. 5:1; Gal. 6:1.

3. Mtu aliyekuwa na kondoo 100 alifanya nini alipompata kondoo aliyepotea?

3 Katika habari iliyotangulia, tulitaja mfano wa Yesu kuhusu mtu aliyekuwa na kondoo 100. Kondoo mmoja alipopotea, mtu huyo aliacha wale 99 na kumtafuta huyo kondoo mmoja. Mtu huyo alishangilia sana alipompata kondoo huyo! (Luka 15:4-7) Sisi pia tunashangilia kondoo mmoja aliyepotea wa Mungu anaporudi katika kundi. Wakichochewa na upendo, wazee na wengine katika kutaniko huenda wamemtembelea mtu asiyetenda. Wao pia wanataka kumwona mtu huyo akirudi katika kundi, akitegemezwa, kulindwa, na kubarikiwa na Mungu. (Kum. 33:27; Zab. 91:14; Met. 10:22) Ni mambo gani wanayoweza kufanya ili kumsaidia mtu huyo?

4. Tunajifunza nini katika Wagalatia 6:2, 5?

4 Labda wanaweza kumtia moyo mtu huyo arudi katika kutaniko kwa kumwonyesha kwa fadhili kwamba Yehova anawapenda kondoo Wake na anataka tufanye tu mambo tunayoweza kufanya. Mambo hayo yanatia ndani kujifunza Biblia, kuhudhuria mikutano ya Kikristo, na kuhubiri habari njema ya Ufalme. Huenda ikafaa kusoma Wagalatia 6:2, 5 na kutaja kwamba Wakristo wanaweza kubebeana mizigo mizito, lakini “kila mmoja ataubeba mzigo wake mwenyewe” wa kuwa na wajibu mbele za Yehova. Hakuna mtu yeyote yule anayeweza kuwa mwaminifu kwa Mungu kwa ajili yetu.

Je, “Mahangaiko ya Maisha” Yamepunguza Bidii Yao?

5, 6. (a) Kwa nini ni jambo la maana tusikilize kwa makini waamini wenzetu wasiotenda wanapotueleza hisia zao? (b) Unaweza kuwasaidia jinsi gani wasiotenda waone kwamba wamepata hasara kwa kutoshirikiana na watu wa Mungu?

5 Ili kujua jinsi ambavyo watawasaidia waamini wenzao wasiotenda, wazee na wahubiri wengine wakomavu wanahitaji kusikiliza kwa makini wakati watu hao wasiotenda wanapoeleza hisia zao. Tuseme wewe ni mzee na umewatembelea wenzi wa ndoa ambao wameacha kushirikiana na kutaniko kwa sababu ya “mahangaiko ya maisha.” (Luka 21:34) Huenda matatizo ya kifedha au madaraka ya familia yameongezeka na kuwafanya wawe wasiotenda kiroho. Labda wanahisi kwamba wanahitaji kupumzika kiroho, lakini unaweza kuwaeleza kwamba suluhisho si kujitenga na wengine. (Soma Methali 18:1.) Unaweza kuwauliza hivi kwa busara: “Je, mmepata furaha zaidi tangu mlipoacha kuhudhuria mikutano? Je, familia yenu imefanikiwa zaidi? Je, bado shangwe ya Yehova ni ngome yenu?”—Neh. 8:10.

6 Kutafakari kuhusu maswali hayo kunaweza kuwasaidia wasiotenda kuona kwamba kwa sababu ya kuacha kushirikiana na kutaniko, hali yao ya kiroho na furaha yao imepungua. (Mt. 5:3; Ebr. 10:24, 25) Unaweza kuwasaidia kuona kwamba shangwe yao imepungua pia kwa sababu ya kuacha kuhubiri habari njema. (Mt. 28:19, 20) Hivyo basi, ni hatua gani ya hekima wanayopaswa kuchukua?

7. Tunaweza kuwatia moyo wale walioacha kushirikiana na kundi wafanye nini?

7 Yesu alisema hivi: “Jiangalieni ninyi wenyewe kwamba mioyo yenu isilemewe kamwe na kula kupita kiasi na kunywa sana na mahangaiko ya maisha . . . Endeleeni kukesha wakati wote mkiomba dua ili mpate kufanikiwa kuponyoka mambo yote hayo yaliyokusudiwa kutukia.” (Luka 21:34-36) Wale ambao wameacha kushirikiana na kundi na wanataka tena kupata furaha wanaweza kutiwa moyo kusali kwa ajili ya roho takatifu na msaada kutoka kwa Mungu na kutenda kupatana na sala zao.—Luka 11:13.

Je, Walikwazwa?

8, 9. Mzee anaweza kumsaidia jinsi gani mtu aliyekwazwa?

8 Kwa kuwa wanadamu si wakamilifu, nyakati nyingine wanaweza kukosana, na mmoja wao anaweza kukwazika. Wengine wamekwazwa kwa sababu mtu mwenye kuheshimika katika kutaniko hakufuata kanuni za Biblia. Ikiwa mtu asiyetenda amekwazwa kwa sababu hiyo, mzee ambaye amemtembelea anaweza kutaja kwamba Yehova hamkwazi mtu yeyote. Kwa hiyo, kwa nini mtu avunje uhusiano wake pamoja na Mungu na watu Wake? Badala yake, anapaswa kuendelea kumtumikia Mungu, na kuwa na uhakika kwamba “Mwamuzi wa dunia yote” anajua mambo yaliyotendeka na atayashughulikia kwa njia inayofaa. (Mwa. 18:25; Kol. 3:23-25) Mtu akijikwaa kihalisi na kuanguka, hawezi kuendelea kukaa chini bila hata kujaribu kusimama.

9 Katika jitihada zake za kutoa msaada wa kiroho, mzee anaweza kutaja kwamba baada ya muda, watu fulani wanagundua kwamba mambo yaliyowafanya wakwazike si ya maana sana kama walivyoyaona mbeleni. Na kwa kweli, huenda hali iliyowakwaza haipo tena. Ikiwa mtu alikwazika kwa sababu alitiwa nidhamu, kusali na kutafakari kunaweza kumfanya atambue kwamba yeye mwenyewe alikosea kwa kadiri fulani na kwamba hakupaswa kuruhusu nidhamu imkwaze.—Zab. 119:165; Ebr. 12:5-13.

Je, Walikwazwa na Fundisho Fulani?

10, 11. Ni hoja gani zinazoweza kumsaidia mtu ambaye alielewa fundisho fulani la Biblia kwa njia tofauti?

10 Huenda wengine waliliacha kundi la Mungu kwa sababu hawakukubaliana na fundisho fulani la Biblia. Waisraeli waliowekwa huru kutoka utekwani huko Misri ‘walisahau kazi’ ambazo Mungu alifanya kwa ajili yao, nao “hawakungojea shauri lake.” (Zab. 106:13) Unaweza kumsaidia mtu asiyetenda kwa kumkumbusha kwamba “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” ndiye anayeandaa chakula bora cha kiroho. (Mt. 24:45) Hivyo ndivyo mtu huyo alivyojifunza kweli. Kwa hiyo, kwa nini asiazimie kutembea tena katika kweli?—2 Yoh. 4.

11 Anapojitahidi kuwasaidia wale ambao wameacha kushirikiana na kundi la Mungu, mzee anaweza kuzungumzia jinsi wanafunzi walivyomwacha Yesu kwa sababu walikataa jambo fulani ambalo alifundisha. (Yoh. 6:53, 66) Walipoacha kushirikiana na Kristo na wafuasi wake waaminifu, hawakuthamini tena mambo ya kiroho nao wakapoteza shangwe yao. Je, wale ambao wameacha kushirikiana na kutaniko la Kikristo wamepata mahali pengine penye chakula kingi cha kiroho? Hapana, kwa maana hakuna pengine!

Je, Walifanya Dhambi Nzito?

12, 13. Mtu aliyeacha kushirikiana na kundi akikubali kwamba ametenda dhambi nzito, anaweza kusaidiwa jinsi gani?

12 Watu fulani wanaacha kuhubiri na kuhudhuria mikutano kwa sababu wamefanya dhambi nzito. Huenda wakahisi kwamba wakiungama dhambi yao kwa wazee, watatengwa na ushirika. Lakini hawawezi kutengwa na ushirika wa kutaniko ikiwa wameacha zoea hilo lisilopatana na Maandiko na ikiwa wametubu kikweli. (2 Kor. 7:10, 11) Badala yake, watakaribishwa tena, na wazee watawapa msaada wa kiroho ambao wanahitaji.

13 Ikiwa wewe ni mhubiri mkomavu na umepewa mgawo wa kumsaidia mtu asiyetenda, unapaswa kufanya nini akikuambia kwamba amefanya dhambi nzito? Kama ilivyotajwa mapema, badala ya kujihusisha zaidi na kisa hicho, mpendekezee awafikie wazee. Ikiwa hataki kufanya hivyo, onyesha kwamba unalihangaikia jina la Yehova na hali ya kiroho ya kutaniko kwa kufuata mwelekezo wa Mungu kuhusu kushughulikia kisa cha aina hiyo. (Soma Mambo ya Walawi 5:1.) Wazee watajua jinsi ya kumsaidia mtu yeyote anayetaka kurudi na kuishi kupatana na mapenzi ya Mungu. Huenda nidhamu yenye upendo ikahitajiwa. (Ebr. 12:7-11) Mtu huyo akikubali kwamba amemtendea Mungu dhambi, ameacha kutenda dhambi, na ametubu kikweli, wazee watamsaidia, na Yehova anaweza kumsamehe.—Isa. 1:18; 55:7; Yak. 5:13-16.

Walishangilia Mwana Aliporudi

14. Simulia kwa maneno yako mwenyewe mfano wa Yesu kuhusu mwana mpotevu.

14 Mhubiri aliyepewa mgawo wa kumsaidia kondoo aliyepotea anaweza kusimulia mfano wa Yesu katika Luka 15:11-24. Katika mfano huo, kijana anapoteza urithi wake wote kwa kuponda raha. Mwishowe, anachukia maisha yake ya upotovu. Ana njaa, anatamani sana kuona watu wa familia yao, naye anaazimia kurudi nyumbani! Akiwa mbali, baba yake anamwona, kisha anakimbia, anamwangukia shingoni, anambusu kwa wororo, na kujawa na shangwe. Mtu aliyeacha kushirikiana na kundi akitafakari kuhusu mfano huo anaweza kuchochewa kurudi katika kundi. Kwa kuwa mfumo huu wa mambo utaharibiwa hivi karibuni, anapaswa “kurudi nyumbani” haraka.

15. Kwa nini watu fulani wanaacha polepole kushirikiana na kutaniko?

15 Wengi wanaoacha kushirikiana na kutaniko si kama yule mwana mpotevu. Wengine wanaliacha kundi hatua kwa hatua kama mashua iliyo baharini inayokwenda polepole mbali na nchi kavu. Wengine wanalemewa sana na mahangaiko hivi kwamba wanapuuza mambo ya kiroho. Zaidi ya hayo, wengine wanajiruhusu wakwazwe na mtu fulani katika kutaniko, au wanaacha kushirikiana na kutaniko kwa sababu hawakubaliani na fundisho fulani la Biblia. Wachache wanatumbukia katika mwenendo usiopatana na maandiko. Hata hivyo, mambo yote tuliyoyazungumzia yanaweza kukusaidia katika jitihada zako za kuwasaidia wale walioliacha kundi kwa sababu hizo au nyinginezo ili warudi kungali na wakati.

“Mwanangu, Karibu Nyumbani!”

16-18. (a) Mzee mmoja Mkristo alimsaidia jinsi gani ndugu fulani ambaye kwa miaka mingi alikuwa asiyetenda? (b) Ni nini kilichomfanya ndugu huyo awe asiyetenda, na kutaniko lilimpokea jinsi gani?

16 Mzee mmoja Mkristo alisema hivi: “Baraza letu la wazee linajitahidi sana kuwatembelea wasiotenda. Pindi moja, nilimkumbuka ndugu fulani ambaye nilijifunza Biblia pamoja naye na kumsaidia kupata ujuzi wa kweli. Alikuwa mhubiri asiyetenda kwa miaka 25 hivi naye alikuwa akikabili hali ngumu sana, hivyo nilimweleza jinsi kufuata kanuni za Biblia kunavyoweza kumsaidia. Baada ya muda fulani, alianza kuja kwenye Jumba la Ufalme naye akakubali kujifunza Biblia ili aimarishe azimio lake la kurudi katika kundi.”

17 Ni nini kilichomfanya ndugu huyo awe asiyetenda? Anakubali hivi: “Nilianza kukazia fikira zaidi mambo ya ulimwengu kuliko mambo ya kiroho. Kisha nikaacha kujifunza, kushiriki katika huduma, na kuhudhuria mikutano. Punde si punde, nikaacha kushirikiana kabisa na kutaniko la Kikristo. Lakini nilisaidiwa kurudi kwa sababu mzee huyo alinihangaikia na kunijali kwa moyo wote.” Matatizo ya ndugu huyo yalianza kupungua alipokubali kujifunza tena Biblia. Alisema hivi: “Nilitambua kwamba kile nilichokosa maishani ni upendo na mwongozo wa Yehova na wa tengenezo lake.”

18 Ndugu huyo alipokewa jinsi gani katika kutaniko? Anasema hivi: “Ninahisi kama yule mwana mpotevu aliyetajwa na Yesu Kristo. Kwa hakika, dada mmoja mwenye umri mkubwa ambaye alikuwapo miaka 30 iliyopita na ambaye bado anamtumikia Yehova kwa uaminifu aliniambia, ‘Mwanangu, karibu nyumbani!’ Hilo lilinigusa moyo sana. Kwa kweli, nilikuwa nimerudi nyumbani. Ningependa kumshukuru kutoka moyoni mzee huyo na kutaniko lote kwa sababu ya kunionyesha upendo, uchangamfu, subira, na kunijali. Upendo wao kwa Yehova na jirani ulinisaidia kwelikweli kurudi katika kundi.”

Wahimizeni Wachukue Hatua Sasa!

19, 20. Unaweza kuwatia moyo jinsi gani watu wasiotenda warudi haraka katika kundi, na unaweza kuwaonyesha jinsi gani kwamba Mungu hatazamii tufanye mambo ambayo hatuwezi?

19 Tunaishi katika siku za mwisho, na mwisho wa mfumo huu wa mambo uko karibu. Kwa hiyo, watieni moyo wale wasiotenda wahudhurie mikutano ya Kikristo. Wahimizeni waanze kuhudhuria bila kukawia. Wakumbusheni kwamba Shetani anajaribu kuharibu uhusiano wao pamoja na Mungu na kuwafanya wafikiri kwamba matatizo yao yanaweza kusuluhishwa wakiacha ibada ya kweli. Wahakikishieni kwamba wanaweza kupata burudisho la kweli ikiwa tu wataendelea kuwa wafuasi waaminifu wa Yesu.—Soma Mathayo 11:28-30.

20 Wakumbusheni wasiotenda kwamba Mungu anatazamia tufanye yale tu ambayo tunaweza. Maria, dada ya Lazaro, aliposhutumiwa kwa kumpaka Yesu mafuta yenye marashi ya bei ghali, Yesu alisema hivi: “Mwacheni. . . . Alifanya jambo ambalo aliweza.” (Marko 14:6-8) Yesu alimsifu mjane mwenye uhitaji ambaye alitoa mchango mdogo sana katika hekalu. Yeye pia alifanya jambo ambalo aliweza. (Luka 21:1-4) Wengi wetu tunaweza kuhudhuria mikutano ya Kikristo na kufanya kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme. Kwa msaada wa Yehova, watu wengi ambao sasa ni wasiotenda wataweza kufanya mambo hayo.

21, 22. Unaweza kuwahakikishia nini wale wanaomrudia Yehova?

21 Ikiwa kondoo aliyeacha kushirikiana na kundi anaogopa kukutana tena na ndugu zake, unaweza kumkumbusha jinsi watu walivyoshangilia wakati mwana mpotevu aliporudi nyumbani. Wale wanaorudi katika kutaniko wanawachochea wengine kuwa na shangwe kama hiyo. Watie moyo wachukue hatua sasa ya kumpinga Ibilisi na kumkaribia Mungu.—Yak. 4:7, 8.

22 Wale wanaomrudia Yehova watakaribishwa kwa shangwe. (Omb. 3:40) Bila shaka, mambo waliyofanya zamani katika utumishi wa Mungu yaliwaletea shangwe kubwa. Wale wanaorudi haraka katika kundi watapata baraka nyingi wakati ujao!

Ungesema Nini?

• Unaweza kumsaidia jinsi gani Mkristo ambaye alikwazwa na kuwa asiyetenda?

• Ni hoja gani zinazoweza kumsaidia mtu aliyeliacha kundi la Mungu kwa sababu ya kutokubaliana na fundisho fulani?

• Unaweza kumsaidia jinsi gani mtu anayesitasita kurudi katika kutaniko?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 13]

Sikiliza kwa makini mwamini mwenzako asiyetenda anapozungumza

[Picha katika ukurasa wa 15]

Watu fulani wanaweza kuchochewa kurudi katika kundi wakitafakari kuhusu mfano wa Yesu wa mwana mpotevu