Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Wimbo wa Baharini”—Hati Inayoziba Pengo

“Wimbo wa Baharini”—Hati Inayoziba Pengo

“Wimbo wa Baharini”—Hati Inayoziba Pengo

MNAMO Mei 22, 2007 (22/5/2007), kipande cha kitabu cha kukunjwa cha Kiebrania cha karne ya saba au nane W.K. kilianza kuonyeshwa katika Jumba la Makumbusho la Israel huko Jerusalem. Kipande hicho ni hati ya kitabu cha Kutoka 13:19–16:1. Hati hiyo inatia ndani ule “Wimbo wa Baharini”—wimbo wa ushindi ambao Waisraeli waliimba baada ya kukombolewa kimuujiza kwenye Bahari Nyekundu. Kwa nini kuonyeshwa kwa kipande hicho cha kitabu cha kukunjwa ni jambo la pekee?

Ni kwa sababu ya tarehe ya hati hiyo. Vile Vitabu vya Kukunjwa vya Bahari ya Chumvi viliandikwa kati ya karne ya tatu K.W.K. na karne ya kwanza W.K. Kabla vitabu hivyo havijagunduliwa miaka 60 hivi iliyopita, hati ya kale zaidi ya Kiebrania ilikuwa Aleppo Codex, ambayo iliandikwa mwaka wa 930 W.K. Isipokuwa vipande vichache vilivyopatikana, hakuna hati nyingine za Kiebrania za kipindi hicho cha katikati cha mamia ya miaka ambazo zimepatikana.

James S. Snyder, msimamizi wa Jumba la Makumbusho la Israel anasema: “Hati ya Wimbo wa Baharini inaziba pengo lililo kati ya Vitabu vya Kukunjwa vya Bahari ya Chumvi . . . na hati ya Aleppo Codex.” Kulingana naye, hati hiyo pamoja na maandishi mengine ya kale ya Biblia “ni mfano mzuri sana wa hati ambazo hazijabadilishwa.”

Inasemekana kwamba kipande hicho cha hati ni moja kati ya hati nyingi zilizogunduliwa mwishoni mwa karne ya 19 katika sinagogi fulani huko Cairo, Misri. Hata hivyo, mkusanyaji mmoja wa hati za Kiebrania hakujua umuhimu wake mpaka aliposhauriana na mtaalamu fulani mwishoni mwa miaka ya 1970. Tarehe ya kipande hicho ilichunguzwa wakati huo kisha kikahifadhiwa mpaka kilipopelekwa katika Jumba la Makumbusho la Israel.

Akizungumzia umuhimu wa kipande hicho cha hati ya kukunjwa, Adolfo Roitman, msimamizi wa Shrine of the Book, katika Jumba la Makumbusho la Israel na mtunzaji wa Vitabu vya Kukunjwa vya Bahari ya Chumvi, anasema hivi: “Hati ya Wimbo wa Baharini inaonyesha kwamba maandishi ya Wamasora ya Biblia yaliandikwa kwa uaminifu mwingi sana katika karne zilizopita. Inastaajabisha sana kuona kwamba maneno ya Wimbo wa Baharini yangali kama yalivyokuwa katika karne ya 7 mpaka ya 8.”

Biblia ni Neno la Mungu lililoandikwa kwa mwongozo wa roho, na Yehova ndiye hasa aliyeihifadhi. Zaidi ya hayo, waandishi waliyanakili Maandiko kwa uangalifu sana. Kwa hiyo, hakuna shaka kwamba maandishi ya Biblia tunayoyatumia leo yanategemeka.

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 32]

Courtesy of Israel Museum, Jerusalem