Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Aliazimia Kutoa Ushahidi Kamili

Aliazimia Kutoa Ushahidi Kamili

Aliazimia Kutoa Ushahidi Kamili

“Alituagiza sisi tuwahubirie watu na kutoa ushahidi kamili.”—MDO. 10:42.

1. Ni kazi gani ambayo Petro alitilia mkazo alipokuwa akizungumza na Kornelio?

OFISA mmoja wa jeshi la Italia aliwakusanya watu wake wa ukoo na marafiki kwa ajili ya tukio jipya kabisa katika shughuli za Mungu pamoja na wanadamu. Mtu huyo aliyemwogopa Mungu aliitwa Kornelio. Mtume Petro alimwambia Kornelio na watu wake kwamba mitume waliagizwa ‘wawahubirie watu na kutoa ushahidi kamili’ kumhusu Yesu. Ushahidi wa Petro ulizaa matunda mengi sana. Watu wa Mataifa wasiotahiriwa walipokea roho ya Mungu na kubatizwa, nao wakapata nafasi ya kuwa wafalme mbinguni pamoja na Yesu. Bidii ya Petro ya kutoa ushahidi kamili ilikuwa na matokeo mazuri kama nini!—Mdo. 10:22, 34-48.

2. Tunajua jinsi gani kwamba agizo la kutoa ushahidi halikuwahusu wale mitume 12 peke yao?

2 Jambo hilo lilitukia mwaka wa 36 W.K. Miaka miwili hivi mapema, mtu fulani aliyewapinga Wakristo vikali aliona jambo lililobadili maisha yake. Sauli wa Tarso alikuwa njiani kwenda Damasko wakati Yesu alipomtokea na kumwambia hivi: ‘Ingia jijini, nawe utaambiwa jambo unalopaswa kufanya.’ Yesu alimhakikishia mwanafunzi Anania kwamba Sauli angetoa ushahidi “kwa mataifa na vilevile kwa wafalme na wana wa Israeli.” (Soma Matendo 9:3-6, 13-20.) Anania alisema hivi alipokuwa na Sauli: “Mungu wa mababu zetu amekuchagua . . . kwa sababu unapaswa kuwa shahidi kwa ajili yake kwa watu wote.” (Mdo. 22:12-16) Sauli, ambaye baadaye aliitwa Paulo, alichukua mgawo wake wa kutoa ushahidi kwa uzito kadiri gani?

Alitoa Ushahidi Kamili!

3. (a) Tutakazia uangalifu simulizi gani? (b) Wazee wa Efeso waliitikia jinsi gani ujumbe wa Paulo, na wanatuwekea mfano gani mzuri?

3 Ingesisimua sana kujifunza kwa undani mambo yote ambayo Paulo alifanya kuanzia wakati huo, lakini kwa sasa, acheni tukazie uangalifu hotuba ambayo Paulo alitoa karibu mwaka wa 56 W.K., kama ilivyoandikwa katika Matendo sura ya 20. Paulo alitoa hotuba hiyo alipokaribia mwisho wa safari yake ya tatu ya umishonari. Alikuwa ameshukia Mileto, bandari iliyo kwenye Bahari ya Aegea, na alikuwa ametuma ujumbe ili wazee wa kutaniko la Efeso waje kumwona. Jiji la Efeso lilikuwa umbali wa kilomita 50 hivi, hata hivyo, safari ya kwenda huko ilikuwa ndefu sana kwa sababu ya barabara zenye kupinda-pinda. Unaweza kuwazia msisimuko ambao wazee wa Efeso walikuwa nao walipopata ujumbe wa Paulo. (Linganisha na Methali 10:28.) Hata hivyo, walihitaji kufanya mipango ya kusafiri mpaka Mileto. Je, wengine wao waliomba ruhusa kazini au walifunga maduka yao? Wakristo wengi leo wanafanya hivyo ili wasikose hata kipindi kimoja cha kusanyiko lao la wilaya la kila mwaka.

4. Paulo alikuwa na desturi gani alipokuwa Efeso kwa miaka fulani?

4 Unafikiri Paulo alifanya nini Mileto kwa siku tatu au nne kabla ya wazee wa Efeso kufika? Wewe ungefanya nini? (Linganisha na Matendo 17:16, 17.) Maneno ya Paulo kwa wazee wa Efeso yanatoa jibu. Alieleza desturi aliyokuwa nayo kwa miaka mingi ya kuhubiri, kama alivyofanya mapema huko Efeso. (Soma Matendo 20:18-21.) Paulo alisema hivi akiwa na hakika kwamba hakuna mtu ambaye angepinga: “Ninyi mnajua vema jinsi tangu siku ya kwanza niliyokanyaga wilaya ya Asia . . . nilitoa ushahidi kikamili.” Ndiyo, aliazimia kutimiza kazi aliyopewa na Yesu. Alifanya hivyo kwa njia gani huko Efeso? Njia moja aliyotumia ni kuwahubiria Wayahudi, na alienda mahali ambapo angewapata wengi wao. Luka anaripoti kwamba Paulo alipokuwa Efeso karibu mwaka wa 52-55 W.K., ‘alitoa hotuba na kutumia ushawishi’ katika sinagogi. Wayahudi “walipoendelea kujifanya wenyewe wagumu na kutoamini,” Paulo aliwahubiria wengine, akahamia sehemu nyingine ya jiji na kuendelea kuhubiri. Kwa hiyo, alitoa ushahidi kamili kwa Wayahudi na Wagiriki katika jiji hilo kubwa.—Matendo 19:1, 8, 9.

5, 6. Kwa nini tunaweza kuwa na hakika kwamba kazi ya Paulo ya kuhubiri nyumba kwa nyumba ilitia ndani kuwahubiria wasio waamini?

5 Baada ya muda, watu fulani waliofanya maendeleo na kuwa Wakristo walistahili kuwa wazee, wale ambao Paulo alizungumza nao huko Mileto. Paulo aliwakumbusha njia ambayo alitumia kuhubiri: “Sikuepuka kuwaambia ninyi lolote kati ya mambo yenye faida wala kuwafundisha ninyi hadharani na nyumba kwa nyumba.” Wakati wetu, watu fulani wamedai Paulo alimaanisha kwamba alikuwa akifanya tu ziara za uchungaji kwa waamini wenzake. Lakini hakumaanisha hivyo. Usemi ‘kufundisha hadharani na nyumba kwa nyumba’ ulitumiwa hasa kuhusu kazi ya kuwahubiria watu wasio waamini. Maneno yanayofuata yanaonyesha hivyo waziwazi. Paulo alisema kwamba alitoa ushahidi “kwa Wayahudi na Wagiriki pia juu ya toba kwa Mungu na imani katika Bwana wetu Yesu.” Ni wazi kwamba Paulo alikuwa akitoa ushahidi kwa wasio waamini, ambao walihitaji kutubu na kumwamini Yesu.—Mdo. 20:20, 21.

6 Katika uchunguzi wa ndani wa Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, msomi mmoja alisema hivi kuhusu Matendo 20:20: “Paulo alikuwa amekaa Efeso kwa miaka mitatu. Alitembelea kila nyumba, au alihubiria angalau watu wote (mstari wa 26). Huo ndio msingi wa kimaandiko wa kazi ya kuhubiri nyumba kwa nyumba na pia katika mikutano ya watu wote.” Iwe alitembelea kila nyumba kihalisi, kama msomi huyo anavyodai, au hakufanya hivyo, Paulo hakutaka wazee wa Efeso wasahau jinsi alivyotoa ushahidi na matokeo ya ushahidi huo. Luka anaripoti hivi: “Wale wote waliokuwa wakikaa katika wilaya ya Asia wakasikia neno la Bwana, Wayahudi na Wagiriki pia.” (Mdo. 19:10) Lakini watu “wote” katika Asia walisikia kweli jinsi gani, na hilo linaonyesha nini kuhusu kazi yetu ya kutoa ushahidi?

7. Ni kwa njia gani huenda mahubiri ya Paulo yalikuwa na matokeo kwa wale ambao hakuwahubiria moja kwa moja?

7 Wengi walisikia ujumbe wake kwa sababu Paulo alihubiri katika maeneo ya watu wote na nyumba kwa nyumba. Je, unafikiri kwamba wote waliosikia ujumbe wake huenda waliishi Efeso, hawakusafiri kwingineko kufanya biashara, kuwatembelea watu wa ukoo, au kutafuta mahali patulivu pa kuishi mbali na jiji lenye hekaheka nyingi? Haiwezekani. Watu wengi leo wamehama kwa sababu kama hizo; labda hata wewe umehama. Pia, nyakati hizo, watu kutoka sehemu nyingine walienda Efeso kwa sababu ya shughuli za kijamii au za kibiashara. Wakiwa huko, huenda walikutana na Paulo au walimsikia akitoa ushahidi. Huenda walifanya nini waliporudi nyumbani? Inaelekea wale waliokubali kweli walitoa ushahidi. Huenda wengine hawakukubali kweli, hata hivyo, inaelekea kwamba walizungumza kuhusu mambo waliyosikia wakiwa Efeso. Hivyo, inaelekea watu wa ukoo, majirani, au watu walionunua bidhaa walisikia kweli, na huenda wengine wao walikubali kweli. (Linganisha na Marko 5:14.) Hilo linaonyesha nini kuhusu matokeo unayoweza kupata ukitoa ushahidi kamili?

8. Huenda watu katika wilaya yote ya Asia walisikia kweli jinsi gani?

8 Kuhusu huduma yake ya mapema huko Efeso, Paulo aliandika kwamba ‘alifunguliwa mlango mkubwa unaoongoza kwenye utendaji.’ (1 Kor. 16:8, 9) Ni mlango gani huo, na alifunguliwa mlango huo jinsi gani? Paulo alieneza habari njema alipoendelea kuhubiri huko Efeso. Fikiria Kolosai, Laodikia, na Hierapolisi, majiji matatu yaliyokuwa maeneo ya ndani kutoka Efeso. Paulo hakuyatembelea kamwe, lakini habari njema ilifika huko. Epafra alitoka katika sehemu hiyo. (Kol. 2:1; 4:12, 13) Je, Epafra alipata kuwa Mkristo baada ya kumsikia Paulo akitoa ushahidi huko Efeso? Biblia haisemi waziwazi. Lakini huenda Epafra alimwakilisha Paulo kwa kueneza kweli katika eneo lao la nyumbani. (Kol. 1:7) Huenda ujumbe wa Kikristo pia ulifika katika majiji mengine kama vile Filadelfia, Sardisi, na Thiatira katika miaka ambayo Paulo alikuwa akitoa ushahidi huko Efeso.

9. (a) Paulo alitamani nini kutoka moyoni? (b) Ni andiko gani litakalokuwa andiko la mwaka wa 2009?

9 Kwa hiyo, wazee wa Efeso walikuwa na sababu za kutosha za kukubali maneno haya ya Paulo: “Siifanyi nafsi yangu kuwa kitu chenye thamani sana kwangu, kama tu ningepata kumaliza mwendo wangu na huduma niliyopokea kutoka kwa Bwana Yesu, kutoa ushahidi kamili kuhusu habari njema ya fadhili zisizostahiliwa za Mungu.” Mstari huo una andiko la mwaka wa 2009 ambalo linatutia moyo na kutuchochea: ‘Toa ushahidi kamili kuhusu habari njema.’—Mdo. 20:24.

Kutoa Ushahidi Kamili Leo

10. Tunajua jinsi gani kwamba tunapaswa kutoa ushahidi kamili?

10 Agizo la ‘kuwahubiria watu na kutoa ushahidi kamili’ liliwahusu wengine zaidi ya mitume. Yesu aliyefufuliwa alipozungumza na wanafunzi wake waliokusanyika huko Galilaya, ambao huenda walikuwa 500, alitoa amri hii: “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, mkiwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu, na kuwafundisha kushika mambo yote ambayo nimewaamuru ninyi.” Amri hiyo inawahusu Wakristo wote wa kweli leo, kama maneno haya ya Yesu yanavyoonyesha: “Tazama! mimi nipo pamoja nanyi siku zote mpaka umalizio wa mfumo wa mambo.”—Mt. 28:19, 20.

11. Mashahidi wa Yehova wanajulikana kwa kazi gani ya maana?

11 Wakristo wenye bidii wanaendelea kutii amri hiyo ya Yesu, wakijitahidi “kutoa ushahidi kamili kuhusu habari njema.” Njia kuu ya kufanya hivyo ni ile ambayo Paulo aliwaambia wazee wa Efeso, njia ya kuhubiri nyumba kwa nyumba. Katika kitabu kimoja cha mwaka wa 2007 kuhusu kazi ya umishonari yenye mafanikio, David G. Stewart, Jr., alisema hivi: “Njia inayotumiwa na Mashahidi wa Yehova ya kuwafundisha watu ili wawafundishe wengine kuhusu imani yao ni yenye mafanikio zaidi kuliko kuwahimiza tu watu kwa mdomo [kutoka katika majukwaa ya kanisa]. Mashahidi wengi wa Yehova wanapenda sana kuzungumza na wengine kuhusu imani yao.” Wamepata matokeo gani? “Mwaka wa 1999, ni watu wawili tu kati ya watu wanne niliowahoji katika miji miwili mikubwa ya Ulaya Mashariki waliosema kwamba wamewahi kuhubiriwa na wamishonari wa dini ya ‘Mormon’ (Latter-day Saints). Zaidi ya asilimia 70 walisema kwamba wamewahi kuhubiriwa kibinafsi na Mashahidi wa Yehova, na wengi wametembelewa mara nyingi.”

12. (a) Kwa nini tunawatembelea watu katika eneo letu “mara nyingi”? (b) Simulia kisa cha mtu fulani ambaye mtazamo wake kuelekea ujumbe wetu ulibadilika.

12 Huenda watu katika eneo lenu wametembelewa pia mara nyingi na Mashahidi wa Yehova. Inaelekea kwamba wewe pia umewatembelea. ‘Unapowahubiria kibinafsi’ watu katika huduma ya nyumba kwa nyumba, unazungumza na wanaume, wanawake, na vijana wakiwa nyumbani. Huenda wengine hawasikilizi hata ingawa “wametembelewa mara nyingi.” Huenda wengine wanasikiliza kwa muda mfupi tu unapowaonyesha andiko la Biblia au wazo la Kimaandiko. Hata hivyo, umefaulu kuwatolea wengine ushahidi mzuri, na wamekubali kweli. Watu wanaitikia kwa njia hizo mbalimbali ‘tunapotoa ushahidi kamili kuhusu habari njema.’ Inaelekea kwamba unajua watu wengi ambao hawakupendezwa sana ingawa walitembelewa “mara nyingi,” lakini baadaye walibadilika. Labda wao au wapendwa wao walipatwa na hali fulani ambayo ilifungua akili na mioyo yao na kuwafanya wakubali kweli. Sasa ni ndugu na dada zetu. Kwa hiyo, usikate tamaa, hata ikiwa hivi karibuni hujapata watu wengi ambao wanakusikiliza. Hatutazamii kila mtu aingie katika kweli. Lakini Mungu anatarajia tujitahidi kuendelea kutoa ushahidi kamili kwa bidii.

Matokeo Mazuri Ambayo Huenda Hatujui

13. Tunapotoa ushahidi tunaweza kupata matokeo mazuri namna gani bila kujua?

13 Paulo hakuwasaidia tu wale ambao aliwafundisha moja kwa moja katika huduma yake wakawa Wakristo; wala sisi hatufanyi hivyo. Tunajitahidi kushiriki kwa ukawaida katika huduma ya nyumba kwa nyumba, na kuwahubiria watu wengi iwezekanavyo. Tunawahubiria habari njema majirani wetu, wafanyakazi wenzetu, wanashule wenzetu, na watu wetu wa ukoo. Je, tunajua matokeo yote ya kazi yetu? Wengine wanakubali mara moja ujumbe wetu. Nyakati nyingine, huenda mbegu za kweli zikakaa kwa muda fulani bila kuchipuka, halafu zinaanza kutia mizizi katika moyo wa mtu ambao ni kama udongo, kisha zinakua. Hata zisipokua, huenda watu tunaozungumza nao wakawaambia wengine mambo tuliyosema, yale tunayoamini, na jinsi tunavyotenda. Ndiyo, huenda bila kujua wanapanda mbegu hizo katika udongo mwingine unaofaa.

14, 15. Ndugu mmoja alipata matokeo gani mazuri kwa sababu ya kutoa ushahidi?

14 Kwa mfano, mfikirie Ryan na mke wake, Mandi, ambao wanaishi Florida, Marekani. Ryan alimhubiria isivyo rasmi mfanyakazi mwenzake wakiwa kazini. Mtu huyo ambaye alikuwa Mhindu, alivutiwa sana na mavazi ya Ryan na jinsi alivyozungumza. Ryan alizungumza naye mambo kama vile ufufuo na hali ya wafu. Jioni moja mwezi wa Januari (Mwezi wa 1), mtu huyo alimuuliza Jodi, mke wake, mambo aliyojua kuhusu Mashahidi wa Yehova. Jodi alikuwa Mkatoliki, na alisema kwamba alijua tu kwamba Mashahidi “wanahubiri nyumba kwa nyumba.” Kwa hiyo, Jodi alitafuta jina “Mashahidi wa Yehova” kwenye Intaneti, akapata kituo chetu (www.watchtower.org). Kwa miezi mingi, Jodi alisoma habari zinazopatikana katika kituo hicho, kutia ndani Biblia na habari nyingine zenye kuvutia.

15 Baada ya muda, Jodi alikutana na Mandi, kwa kuwa wote wawili ni wauguzi. Mandi alifurahia sana kujibu maswali ya Jodi. Baada ya muda fulani, walikuwa na mazungumzo ambayo Jodi anasema yalianza na “Adamu mpaka Har–Magedoni.” Jodi alikubali mpango wa kujifunza Biblia nyumbani. Punde si punde, alianza kwenda kwenye Jumba la Ufalme. Mwezi wa Oktoba (Mwezi wa 10), Jodi aliwekwa kuwa mhubiri ambaye hajabatizwa, kisha akabatizwa mnamo Februari. Anaandika hivi: “Sasa kwa kuwa ninajua kweli, maisha yangu ni yenye furaha na yenye kuridhisha.”

16. Jambo ambalo ndugu mmoja wa Florida alipata linaonyesha nini kuhusu jitihada zetu za kutoa ushahidi kamili?

16 Ryan hakujua kamwe kwamba ushahidi aliomtolea mtu mmoja ungemsaidia mwingine kuingia katika kweli. Ni wazi kwamba katika kisa hicho, Ryan alijua matokeo mazuri aliyopata kwa sababu ya kuazimia “kutoa ushahidi kamili.” Hata hivyo, huenda ukahubiri katika nyumba fulani, kazini, shuleni, au isivyo rasmi, na kupitia mahubiri hayo unaweza kueneza kweli kwa wengine bila kujua. Kama vile ambavyo Paulo hakujua matokeo yote ya kazi yake katika “wilaya ya Asia,” huenda usijue matokeo yote mazuri unayopata kwa kutoa ushahidi kamili. (Soma Matendo 23:11; 28:23.) Lakini ni jambo la maana sana kwamba uendelee kufanya hivyo!

17. Umeazimia kufanya nini katika mwaka wa 2009?

17 Katika mwaka wa 2009, acheni sote tuchukue kwa uzito kazi yetu ya kutoa ushahidi nyumba kwa nyumba na katika njia nyinginezo. Tukifanya hivyo tutaweza kusema kama Paulo alivyosema: “Siifanyi nafsi yangu kuwa kitu chenye thamani sana kwangu, kama tu ningepata kumaliza mwendo wangu na huduma niliyopokea kutoka kwa Bwana Yesu, kutoa ushahidi kamili kuhusu habari njema ya fadhili zisizostahiliwa za Mungu.”

Ungesema Nini?

• Mtume Petro na Paulo na wengine katika karne ya kwanza walitoa ushahidi kamili jinsi gani?

• Kwa nini huenda kazi yetu ya kuhubiri ikawa na matokeo mengi mazuri kuliko tunavyojua?

• Andiko la mwaka wa 2009 litakuwa andiko gani, na kwa nini unafikiri kwamba linafaa?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 19]

Andiko la mwaka wa 2009 litakuwa: ‘Toa ushahidi kamili kuhusu habari njema.’—Mdo. 20:24.

[Picha katika ukurasa wa 17]

Wazee wa Efeso walijua kwamba Paulo alikuwa na desturi ya kutoa ushahidi nyumba kwa nyumba

[Picha katika ukurasa wa 18]

Ukitoa ushahidi kamili utapata matokeo mengi mazuri jinsi gani?