Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Unakumbuka?

Je, Unakumbuka?

Je, Unakumbuka?

Je, umefurahia kusoma matoleo ya hivi karibuni ya Mnara wa Mlinzi? Ona kama unaweza kujibu maswali yafuatayo:

• Tunaweza jinsi gani kuzungumza kwa ufasaha ile “lugha safi,” yaani, kweli kumhusu Mungu na makusudi yake? (Sef. 3:9)

Kama lugha nyinginezo, ili tuzungumze “lugha safi” kwa ufasaha tunahitaji kusikiliza kwa uangalifu, kuiga wasemaji wenye ufasaha, kukumbuka majina ya vitabu vya Biblia na maandiko fulani ya Biblia, kurudia-rudia mambo tunayojifunza, kusoma kwa sauti, kuchunguza kanuni au kielelezo cha kweli, kuendelea kufanya maendeleo, kuwa na wakati hususa wa kujifunza, na kujizoeza “kuzungumza” ile lugha safi.—8/15, ukurasa wa 21-25.

• Kumjua Mungu kunahusisha mambo gani?

“Yehova ndilo jina lake,” naye anataka tumjue kwa jina lake. (Kut. 15:3) Yeye ni “Mungu wa upendo na amani.” (2 Kor. 13:11) Ni “Mungu wa ujuzi” na “wa wokovu.” (1 Sam. 2:3; Zab. 25:5) Mungu atawakaribia wale wanaomjua.—9/1, ukurasa wa 4-7.

• Wazo la “kamba yenye nyuzi tatu” linahusu ndoa jinsi gani?

Maneno “kamba yenye nyuzi tatu” ni ya mfano. (Mhu. 4:12) Mfano huo unapotumiwa kuhusu ndoa, mume na mke ndio kamba mbili za kwanza, nao wamesokotwa pamoja na kamba ya katikati, ambayo ni Mungu. Wenzi hao wanapounganishwa pamoja na Mungu wanapata nguvu za kiroho za kushughulikia matatizo na kupata furaha.—9/15, ukurasa wa 16.

• “Kuwekewa mikono” kunakotajwa katika Waebrania 6:2 kunamaanisha nini?

Badala ya kuwahusu wazee Wakristo waliowekwa rasmi, inaelekea kwamba kunamaanisha kuwawekea wengine mikono ili wapate zawadi za kimuujiza za roho takatifu. (Mdo. 8:14-17; 19:6)—9/15, ukurasa wa 32.

• Baba mzuri anatambua kwamba watoto wake wana mahitaji gani?

Mahitaji yao yanatia ndani (1) upendo wa baba, (2) mfano mzuri, (3) mazingira yenye furaha, (4) elimu ya mambo ya kiroho, (5) nidhamu, (6) ulinzi.—10/1, ukurasa wa 18-21.

• Wale wanaoongoza wanaweza kuwaheshimu wengine jinsi gani?

Njia moja ambayo mzee anaweza kufanya hivyo ni kutowaomba wafanye mambo ambayo yeye mwenyewe hana nia ya kuyafanya. Pia, anawaheshimu wengine kwa kuwaambia kwa nini anawaomba wafanye jambo fulani au wafuate maagizo fulani.—10/15, ukurasa wa 22.

• Taja hatua fulani za kudumisha uwajibikaji katika ndoa.

Hatua mbili kati ya hizo ni: (1) Tanguliza ndoa yako. (2) Usikose uaminifu katika njia yoyote ile. Iwe ndoa yako ni imara au ina matatizo, mwenzi wako anahitaji kujua kwamba unajitahidi kufanikisha ndoa yenu; hatua hizo mbili zinaweza kusaidia.—11/1, ukurasa wa 18-21.

• Mzee Mkristo anaweza kujifunza nini kutokana na jinsi mchungaji Mwisraeli alivyotumia bakora iliyopindika?

Mchungaji katika Israeli la kale alitumia fimbo au bakora ndefu iliyopindika ili kuliongoza kundi lake. Kondoo walipoingia au kutoka katika zizi, ‘walipita chini ya bakora’ hiyo na kuhesabiwa na mchungaji. (Law. 27:32) Vivyo hivyo, mchungaji Mkristo anahitaji kujua hali ya kundi la Mungu lililo chini ya utunzaji wake.—11/15, ukurasa wa 9.

• Mama anaweza kuonyesha jinsi gani kwamba anaona usafi kuwa jambo la maana?

Chakula kinaweza kupata uchafu katika njia mbalimbali, kwa hiyo, ananawa mikono kabla ya kutayarisha chakula kisha anakifunika. Anasafisha nyumba ili kuepuka matatizo ya panya na wadudu. Hatua nyingine zinatia ndani kufua nguo na kuoga kwa ukawaida. Hatua hizo zinapatana na mashauri ya Biblia.—12/1, ukurasa wa 9-11.