Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Utashikilia Kabisa Utimilifu Wako?

Je, Utashikilia Kabisa Utimilifu Wako?

Je, Utashikilia Kabisa Utimilifu Wako?

“Mpaka nitakapokata pumzi, sitajiondolea utimilifu wangu!”—AYU. 27:5.

1, 2. Tunahitaji kushiriki katika mradi gani wa ujenzi, na tutazungumzia maswali gani?

WAZIA unachunguza ramani za ujenzi za nyumba fulani. Unastaajabia jinsi nyumba hiyo itakavyokuwa yenye manufaa. Unachangamka unapofikiria faida ambazo wewe na familia yako mtapata mnapoishi katika nyumba hiyo. Hata hivyo, je, hukubali kwamba kuchunguza ramani hizo na kufikiri tu kuhusu nyumba hiyo ni kazi bure usipoijenga, usipoishi ndani yake, na kuitunza?

2 Vivyo hivyo, huenda tukaona utimilifu kuwa sifa ya maana inayoweza kutunufaisha sana na wale tunaowapenda. Lakini kuwa tu na maoni mazuri kuhusu utimilifu hakutatunufaisha sana ikiwa hatutajitahidi kujenga na kudumisha utimilifu wetu wa Kikristo. Katika ulimwengu wa leo, mara nyingi miradi ya ujenzi inagharimu pesa nyingi sana. (Luka 14:28, 29) Kwa njia hiyohiyo, wakati na jitihada nyingi zinahitajiwa ili kujenga utimilifu, lakini kuna faida nyingi za kufanya hivyo. Basi, acheni tuzungumzie maswali matatu: Tunaweza kufanya nini ili tuwe watimilifu? Tunaweza kufanya nini ili tudumishe utimilifu wetu wa Kikristo? Mtu anaweza kufanya nini ikiwa hakuonyesha utimilifu wakati fulani?

Tunaweza Kufanya Nini ili Tuwe Watimilifu?

3, 4. (a) Yehova anatumia njia gani kutusaidia kujenga utimilifu? (b) Tunaweza kujenga utimilifu jinsi gani kama Yesu?

3 Katika habari iliyotangulia tuliona kwamba Yehova ametuonyesha heshima kwa kuturuhusu tujiamulie ikiwa tutakuwa watimilifu. Hata hivyo, Yehova hatuachi tu bila msaada. Anatufundisha jinsi ya kujenga sifa hiyo yenye thamani, naye anatupa kwa wingi roho yake takatifu ambayo inatusaidia kutumia mafundisho yake. (Luka 11:13) Zaidi ya hayo, anawalinda kiroho wale wanaojitahidi kutembea kwa utimilifu.—Met. 2:7.

4 Yehova ametumia njia gani kutufundisha kuwa watimilifu? Njia kuu zaidi aliyotumia ni kumtuma Mwana wake, Yesu, duniani. Yesu alitii kikamilifu. Alikuwa “mtiifu mpaka kifo.” (Flp. 2:8) Yesu alimtii Baba yake wa mbinguni katika mambo yote, hata ilipokuwa vigumu sana kufanya hivyo. Alimwambia Yehova: “Acha, si mapenzi yangu, bali yako yatendeke.” (Luka 22:42) Kila mmoja wetu anapaswa kujiuliza, ‘Je, mimi ni mtiifu kama Yesu?’ Tukiendelea kuwa watiifu huku tukichochewa na nia nzuri, tutashikilia utimilifu wetu. Fikiria hali fulani maishani ambazo hasa zinahitaji utii.

5, 6. (a) Daudi alikazia jinsi gani umuhimu wa kuendelea kuwa mtimilifu hata wakati ambapo wanadamu wengine hawatuoni? (b) Wakristo leo wanakabili hali gani zinazojaribu utimilifu wao wanapokuwa peke yao?

5 Tunahitaji kumtii Yehova hata inapoonekana kwamba tuko peke yetu. Mtunga-zaburi Daudi aliona kwamba ni jambo la maana kuwa mtimilifu hata katika pindi ambazo alikuwa peke yake. (Soma Zaburi 101:2.) Akiwa mfalme, mara nyingi Daudi alikuwa pamoja na watu. Pindi nyingi, alikuwa kati ya mamia ya watu, hata maelfu ya watu. (Linganisha na Zaburi 26:12.) Lilikuwa jambo la maana kudumisha utimilifu katika pindi hizo, kwa kuwa mfalme alipaswa kuwawekea watu wake mfano mzuri. (Kum. 17:18, 19) Hata hivyo, Daudi alijifunza kwamba nyakati ambazo huenda alikuwa peke yake—‘ndani ya nyumba yake’—bado alihitaji kutembea kwa utimilifu. Namna gani sisi?

6 Katika Zaburi 101:3, tunapata maneno haya ya Daudi: “Sitaweka mbele ya macho yangu kitu chochote kisichofaa.” Kuna hali nyingi leo zinazoweza kutufanya tuweke mbele ya macho yetu vitu visivyofaa, hasa tunapokuwa peke yetu. Wengi wamejaribiwa wanapotumia Intaneti. Ni rahisi kushawishiwa kutazama habari zisizofaa, au hata ponografia (picha au habari za ngono). Lakini je, kufanya hivyo ni kumtii Mungu aliyemwongoza Daudi kuandika maneno hayo? Ponografia inamdhuru mtu, kwa kuwa inachochea tamaa zisizofaa na za pupa, inachafua dhamiri, inavunja ndoa, na kumshushia heshima kila mtu anayehusika.—Met. 4:23; 2 Kor. 7:1; 1 The. 4:3-5.

7. Ni kanuni gani inayoweza kutusaidia kuendelea kuwa watimilifu tunapokuwa peke yetu?

7 Kwa kweli, hakuna mtumishi yeyote wa Yehova ambaye anakuwa peke yake wakati wowote ule. Baba yetu anatutazama kwa upendo. (Soma Zaburi 11:4.) Yehova anafurahi kama nini anapoona ukishinda kishawishi fulani! Kwa kufanya hivyo, unatii onyo la Yesu katika Mathayo 5:28. Azimia kutotazama picha zinazoweza kukushawishi kutenda mabaya. Usipoteze utimilifu wako wenye thamani kwa sababu ya tendo lenye kuaibisha la kutazama au kusoma ponografia!

8, 9. (a) Utimilifu wa Danieli na marafiki wake ulijaribiwa jinsi gani? (b) Vijana Wakristo leo wanamfurahisha jinsi gani Yehova na Wakristo wenzao?

8 Pia, tunaweza kuwa watimilifu kwa kumtii Yehova tunapokuwa na watu ambao si waamini. Mfikirie Danieli na marafiki wake watatu. Wakiwa vijana, walipelekwa utekwani Babiloni. Wakiwa huko, katikati ya watu ambao hawakuwa waamini na ambao hawakumjua Yehova hata kidogo, Waebrania hao wanne walishinikizwa wale vyakula vilivyokatazwa na Sheria ya Mungu. Wavulana hao wangetoa visingizio vingi ili wasitii sheria hiyo ya Mungu. Wazazi wao, makuhani, na wazee hawangeona mambo ambayo vijana hao wanne walikuwa wakifanya. Je, kuna mtu yeyote ambaye angejua? Ni Yehova tu ambaye angejua. Kwa hiyo, walisimama imara na kumtii hata ingawa walishinikizwa na walikabili hatari.—Dan. 1:3-9.

9 Ulimwenguni pote, vijana ambao ni Mashahidi wa Yehova wanasimama imara pia, na wanashikilia kanuni za Mungu zinazowaongoza Wakristo na kupinga vishawishi vyenye kudhuru kutoka kwa vijana wenzao. Ninyi vijana mnapokataa kutumia dawa za kulevya, kutenda jeuri, kutumia usemi wa matusi, kufanya uasherati, na mambo mengine mabaya, mnamtii Yehova. Hivyo, mnaendelea kushikilia utimilifu wenu. Mnapata faida, nanyi mnamfurahisha Yehova na Wakristo wenzenu!—Zab. 110:3.

10. (a) Ni maoni gani yasiyofaa kuhusu uasherati ambayo yamefanya vijana fulani wasiendelee kuwa watimilifu? (b) Utimilifu unatuchochea kufanya nini kuhusiana na hatari ya uasherati?

10 Pia tunahitaji kuwa watiifu tunaposhughulika na watu wa jinsia tofauti. Tunajua kwamba Neno la Mungu linakataza uasherati. Hata hivyo, ni rahisi kuacha kuwa watiifu na kuanza kukubali mambo mengine yasiyofaa. Kwa mfano, vijana fulani wamejihusisha na ngono ya mdomo au ulawiti au zoea la kupigana punyeto wakifikiri kwamba mambo hayo si mabaya sana kwa sababu kwa maoni yao “hawafanyi ngono” kihalisi. Vijana hao wanasahau—au huenda wanapuuza—kwamba neno ambalo Biblia inatumia kwa ajili ya uasherati linatia ndani mazoea yote hayo, mazoea mabaya ambayo yanaweza kumfanya mtu atengwe na ushirika. * Na jambo baya hata zaidi ni kwamba wanapuuza utimilifu. Kwa kuwa tunajitahidi kuendelea kuwa watimilifu, hatutafuti visababu vya kutofuata sheria. Hatujaribu kukaribia sana kufanya dhambi eti kwa sababu hatutaadhibiwa. Hatufikiri tu kuhusu nidhamu ya kihukumu ambayo tunaweza kupata kwa kufanya dhambi. Badala yake, tunajitahidi kufanya mambo yatakayompendeza Yehova na kuepuka mambo ambayo yataumiza hisia zake. Badala ya kufikiria ni kwa kadiri gani tunaweza kukaribia kufanya dhambi bila kuadhibiwa, tunaepuka kabisa dhambi na ‘kuukimbia uasherati.’ (1 Kor. 6:18) Hivyo, tunaonyesha kwamba kwa kweli sisi ni watimilifu.

Tunaweza Kufanya Nini ili Tuendelee Kuwa Watimilifu?

11. Kwa nini kila tendo la utii ni la maana? Toa mfano.

11 Tunajenga utimilifu kwa kutii, hivyo, tunaendelea kuwa watimilifu kwa kuendelea kutii. Huenda tukaona tendo moja la utii kuwa jambo dogo sana ambalo halina maana sana. Hata hivyo, matendo hayo ya utii yanatusaidia tuwe watimilifu siku baada ya siku. Kwa mfano: Huenda tofali likaonekana kuwa dogo sana, lakini tukiunganisha matofali mengi pamoja, tunaweza kujenga nyumba yenye kupendeza. Kwa hiyo, tukiendelea kutii siku baada ya siku, tunaendelea kuwa watimilifu.—Luka 16:10.

12. Daudi aliweka mfano gani wa kuendelea kuwa mtimilifu alipoteswa na kutendewa isivyo haki?

12 Utimilifu wetu unaonekana hasa tunapovumilia matatizo, mateso, au ukosefu wa haki. Fikiria mfano wa Biblia wa Daudi. Alipokuwa kijana, alivumilia mateso kutoka kwa mfalme aliyepaswa kuwakilisha mamlaka ya Yehova. Hata hivyo, Mfalme Sauli alikuwa amepoteza kibali cha Yehova na alimwonea wivu sana Daudi, aliyekubaliwa na Mungu. Hata hivyo, Sauli aliendelea kutawala kwa muda na alitumia jeshi la Israeli kumfukuza na kumfadhaisha Daudi. Yehova aliruhusu ukosefu huo wa haki uendelee kwa miaka fulani. Je, Daudi alimkasirikia Mungu? Je, aliona kwamba hakuna haja ya kuvumilia? Hapana. Aliendelea kuheshimu sana cheo cha Sauli akiwa mtiwa-mafuta wa Mungu na akakataa kulipiza kisasi juu ya Sauli alipopata nafasi ya kufanya hivyo.—1 Sam. 24:2-7.

13. Tunaweza kufanya nini ili kuendelea kuwa watimilifu hata tunapoumizwa au kukasirishwa?

13 Daudi alituwekea mfano mzuri kama nini! Sisi ni sehemu ya kutaniko la ulimwenguni pote la wanadamu wasio wakamilifu, na yeyote kati ya wanadamu hao anaweza kutukosea au hata kutokuwa mwaminifu. Bila shaka, tuna pendeleo la kuishi wakati ambapo watu wa Yehova kwa ujumla hawawezi kupotoshwa. (Isa. 54:17) Hata hivyo, tutafanya nini mtu fulani anapotuvunja moyo au kuumiza hisia zetu? Tukimfungia kinyongo mwabudu mwenzetu, tutakuwa tukihatarisha utimilifu wetu kwa Mungu. Mwenendo wa wengine haupaswi kamwe kuwa kisingizio cha kumkasirikia Mungu au kuacha kuwa waaminifu. (Zab. 119:165) Kuvumilia hata wakati wa majaribu kutatusaidia kuendelea kuwa watimilifu.

14. Watu watimilifu wanafanya nini kunapokuwa na marekebisho katika utaratibu wa kufanya mambo na katika mafundisho?

14 Pia, tunaweza kuendelea kuwa watimilifu kwa kuepuka kutafuta-tafuta makosa ya wengine au kuwachambua-chambua. Bila shaka, hilo linamaanisha tuwe washikamanifu kwa Yehova. Anawabariki watu wake sasa kuliko wakati mwingine wowote. Ibada safi haijapata kamwe kuinuliwa duniani kama ilivyo sasa. (Isa. 2:2-4) Marekebisho yanapofanywa katika uelewaji wa maandiko ya Biblia au katika utaratibu wa kufanya mambo, tunapaswa kuyakubali. Tunafurahi kuona uthibitisho wa kwamba nuru ya kiroho inaongezeka. (Met. 4:18) Tukiona ni vigumu kuelewa badiliko fulani, tunamwomba Yehova atusaidie kuelewa jambo hilo. Na wakati huohuo tunaendelea kuwa watiifu, ndiyo, tunaendelea kuwa watimilifu.

Namna Gani Mtu Akiacha Kuwa Mtimilifu?

15. Ni nani tu anayeweza kukunyang’anya utimilifu wako?

15 Hilo ni swali zito, sivyo? Kama tulivyoona katika makala iliyotangulia, utimilifu ni sifa ya maana sana. Bila utimilifu, hatuwezi kuwa na uhusiano na Yehova wala tumaini halisi. Kumbuka: Ni mtu mmoja tu katika ulimwengu wote anayeweza kukunyang’anya utimilifu wako. Mtu huyo si mwingine ila wewe. Ayubu alielewa kabisa jambo hilo la kweli. Alisema: “Mpaka nitakapokata pumzi, sitajiondolea utimilifu wangu!” (Ayu. 27:5) Ukiwa na azimio hilohilo na ukiendelea kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Yehova, hutapoteza kamwe utimilifu wako.—Yak. 4:8.

16, 17. (a) Mtu akitumbukia katika dhambi nzito, hapaswi kufanya nini? (b) Anapaswa kufanya nini?

16 Hata hivyo, wengine wanashindwa kuendelea kuwa watimilifu. Kama ilivyokuwa wakati wa mitume, leo wengine wanazoea kutenda dhambi nzito. Ikiwa uko katika hali hiyo, je, inamaanisha kwamba huna tumaini lolote? Si lazima iwe hivyo. Unaweza kufanya nini? Acheni kwanza tuzungumzie mambo ambayo hupaswi kufanya. Mwelekeo wa mwanadamu ni kuficha kosa ili wazazi, Wakristo wenzake, au wazee wasijue. Hata hivyo, Biblia inatukumbusha hivi: “Anayefunika makosa yake hatafanikiwa, lakini yeye anayeyaungama na kuyaacha ataonyeshwa rehema.” (Met. 28:13) Wale wanaojaribu kuficha dhambi wanafanya kosa hatari sana, kwa maana Mungu hawezi kufichwa lolote. (Soma Waebrania 4:13.) Wengine hata wanajaribu kuwa na nyuso mbili, wanajifanya wanamtumikia Yehova huku wakiendelea kutenda dhambi. Hayo si maisha ya utimilifu—ni kinyume kabisa cha utimilifu. Yehova hapendezwi na matendo ya ibada yanayofanywa na watu wanaoficha dhambi nzito. Badala yake, unafiki huo unamkasirisha.—Met. 21:27; Isa. 1:11-16.

17 Ikiwa Mkristo amefanya dhambi nzito, anajua wazi hatua ya kuchukua. Anapaswa kutafuta msaada kutoka kwa wazee Wakristo. Yehova amefanya mpango wa kuwashughulikia watu wenye ugonjwa hatari wa kiroho. (Soma Yakobo 5:14.) Usikose kutafuta matibabu ya kiroho eti kwa sababu unaogopa kutiwa nidhamu au kurekebishwa. Je, mtu mwenye hekima ataepuka kutibiwa ugonjwa unaoweza kusababisha kifo eti kwa sababu anaogopa maumivu ya muda ya kudungwa sindano au kufanyiwa upasuaji?—Ebr. 12:11.

18, 19. (a) Mfano wa Daudi unaonyesha jinsi gani kwamba mtu anaweza kuwa mtimilifu tena? (b) Umeazimia kufanya nini kuhusiana na utimilifu wako?

18 Je, kuna tumaini la kupona kabisa? Je, mtu aliyepoteza utimilifu anaweza kuwa mtimilifu tena? Fikiria tena mfano wa Daudi. Alitumbukia katika dhambi nzito. Alimtazama mke wa mtu mwingine kwa tamaa, akafanya uzinzi naye, na kufanya mipango ili mume wake asiye na hatia auawe. Ni wazi kwamba Daudi hakuwa mtimilifu wakati huo, sivyo? Hata hivyo, je, inamaanisha kwamba hakuwa na tumaini lolote? Daudi alihitaji na alipokea nidhamu kali. Hata hivyo, Yehova alimwonyesha rehema kwa kuwa alitubu kikweli. Daudi alijifunza kutokana na nidhamu hiyo na akawa mtimilifu tena kwa kumtii Mungu na kuendelea kuwa mtiifu. Maisha ya Daudi yalithibitisha maneno haya ya Methali 24:16: “Huenda mwadilifu akaanguka hata mara saba, naye hakika atasimama.” Matokeo yalikuwa nini? Fikiria yale ambayo Yehova alimwambia Sulemani kumhusu Daudi baada ya kifo cha Daudi. (Soma 1 Wafalme 9:4.) Mungu alimkumbuka Daudi kuwa mtu mtimilifu. Ndiyo, Yehova anaweza kusafisha madoa ya watenda-dhambi wanaotubu, hata dhambi zao nzito.—Isa. 1:18.

19 Ndiyo, utakuwa mtimilifu ukitii kwa upendo. Endelea kuwa mvumilivu na mshikamanifu, na ukitenda dhambi nzito, onyesha toba ya kweli. Utimilifu ni hazina iliyoje! Acheni kila mmoja wetu aazimie hivi kama Daudi: “Mimi nami nitatembea katika utimilifu wangu.”—Zab. 26:11.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 10 Ona gazeti la Mnara wa Mlinzi la Februari 15, 2004, ukurasa wa 13, fungu la 15.

Ungesema Nini?

• Unaweza kufanya nini ili uwe mtimilifu?

• Unaweza kufanya nini ili uendelee kuwa mtimilifu?

• Mtu anaweza kufanya nini ili awe mtimilifu tena?

[Maswali ya Funzo]

[Sanduku katika ukurasa wa 8]

“ALIFANUA JAMBO ZURI SANA”

Mwanamke mmoja aliyekuwa na mimba ya miezi mitano alisema hivyo kuhusu fadhili na unyoofu wa msichana fulani ambaye hakumjua. Mwanamke huyo alikuwa ameenda kwenye hoteli, na saa chache baadaye akatambua kwamba alikuwa amesahau kifuko chake cha pesa kwenye hoteli hiyo. Kifuko hicho kilikuwa na dola 2,000, na kwa kawaida hakuwa na zoea la kubeba kiasi hicho cha pesa. Baadaye aliliambia gazeti moja hivi: “Nilifadhaika sana.” Hata hivyo, msichana mmoja alipata kifuko hicho na papo hapo akaanza kumtafuta mwenye kifuko. Alipokosa kumpata, alipeleka kifuko hicho kwenye kituo cha polisi, na polisi wakampata mwanamke yule mwenye mimba. Mwanamke huyo alisema hivi kwa shukrani: “Alifanya jambo zuri sana sana.” Kwa nini msichana huyo alijitahidi sana kurudisha pesa hizo? Gazeti hilo linasema kwamba kwa kuwa yeye ni Shahidi wa Yehova, “anaamini kwamba yeye ni mnyoofu kwa sababu ya jinsi alivyofundishwa na dini yake tangu alipokuwa mtoto.”

[Picha katika ukurasa wa 9]

Vijana wanaweza kuendelea kuwa watimilifu wanapojaribiwa

[Picha katika ukurasa wa 10]

Daudi alishindwa kuwa mtimilifu kwa muda, lakini alirudia utimilifu wake