Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Uendelee Kuwa Mtimilifu?

Kwa Nini Uendelee Kuwa Mtimilifu?

Kwa Nini Uendelee Kuwa Mtimilifu?

“Nihukumu, Ee Yehova, . . . kulingana na utimilifu wangu.”—ZAB. 7:8.

1, 2. Ni hali gani za kawaida zinazojaribu utimilifu wa Mkristo?

FIKIRIA hali hizi tatu: Mvulana anadhihakiwa na wanafunzi wenzake shuleni. Wanamchokoza ili akasirike, na labda wanataka awatukane au apigane nao. Je, atalipiza kisasi, au atajizuia na kuondoka? Mume yuko peke yake nyumbani akifanya utafiti kwa kutumia Intaneti. Kisha, kwa ghafula, anaona kwenye kompyuta tangazo fulani kuhusu kituo cha Intaneti chenye mambo machafu. Je, atashawishiwa kufungua kituo hicho, au atakiepuka kabisa? Mwanamke Mkristo anazungumza pamoja na dada wengine. Lakini mazungumzo yao yanageuka na kuwa porojo yenye kuumiza kuhusu dada fulani katika kutaniko. Je, mwanamke huyo atachangia mazungumzo hayo, au atajaribu kuyabadili?

2 Ingawa hali hizo zinatofautiana, zinafanana angalau kwa njia moja. Zote zinahusisha pambano la kudumisha utimilifu wa Kikristo. Je, unakumbuka utimilifu wako unapofikiria mahangaiko yako, mahitaji yako, na miradi yako maishani? Kila siku, watu wanafikiria sura yao, afya yao, matatizo ya kupata riziki, uhusiano wao na marafiki wao, na labda hata mahusiano ya kimapenzi. Huenda tukafikiria sana mambo hayo. Hata hivyo, Yehova anapendezwa hasa na nini anapochunguza moyo wetu? (Zab. 139:23, 24) Utimilifu wetu.

3. Yehova ametupa pendeleo la kufanya uamuzi gani, na tutachunguza nini katika habari hii?

3 Yehova, anayetoa “kila zawadi njema na kila tuzo kamilifu,” amempa kila mmoja wetu zawadi mbalimbali. (Yak. 1:17) Ametupa zawadi kama vile mwili, akili, afya ya kadiri fulani, na uwezo mbalimbali. (1 Kor. 4:7) Hata hivyo, Yehova hatulazimishi kuwa watimilifu. Anaturuhusu tujiamulie ikiwa tutasitawisha sifa hiyo. (Kum. 30:19) Hivyo, tunahitaji kuchunguza maana ya utimilifu. Pia, tutachunguza sababu tatu zinazoonyesha kwa nini utimilifu ni sifa ya maana sana.

Utimilifu Ni Nini?

4. Utimilifu unahusisha nini, nasi tunaweza kujifunza nini kutokana na sheria ya Yehova kuhusu dhabihu za wanyama?

4 Inaonekana kwamba watu wengi hawaelewi vizuri maana ya utimilifu. Wengine wanafikiri ni unyoofu. Unyoofu ni sifa ya maana, lakini ni sehemu tu ya utimilifu. Katika Biblia, utimilifu unahusisha kuwa na maadili kamili, bila kasoro. Maneno ya Kiebrania yanayohusiana na “utimilifu” yanatokana na shina linalomaanisha bila kasoro, -zima, au bila upungufu. Neno moja kati ya hayo linatumiwa kuhusiana na dhabihu zilizotolewa kwa Yehova. Yehova alimkubali mnyama aliyetolewa dhabihu ikiwa tu hakuwa na kasoro au alikuwa mzima. (Soma Mambo ya Walawi 22:19, 20.) Yehova aliwashutumu vikali wale walioasi kimakusudi mwongozo wake kwa kutoa wanyama vilema, wagonjwa, au vipofu kuwa dhabihu.—Mal. 1:6-8.

5, 6. (a) Ni mifano gani inayoonyesha kwamba tunathamini vitu vizima, au vilivyo kamili? (b) Kwa habari ya wanadamu wasio wakamilifu, je, utimilifu ni sawa na ukamilifu? Eleza.

5 Si vigumu kuelewa wazo la kutafuta na kuthamini kitu ambacho ni kizima au kamili. Tuseme mtu anayependa kukusanya vitabu amepata kitabu chenye thamani baada ya kukitafuta kwa muda mrefu, lakini anagundua kwamba hakina kurasa fulani muhimu. Anavunjika moyo na kukirudisha kwenye kabati. Au tuseme mwanamke ameenda sokoni kununua samaki waliokaushwa. Wengine wamevunjika-vunjika. Anachunguza samaki mmoja baada ya mwingine ili aone samaki wanaofaa kabisa. Unafikiri atachagua samaki wa aina gani? Atachagua samaki wazima, walio kamili, ambao hawajavunjika. Vivyo hivyo, Mungu anawatafuta watu walio kamili, au wanaomtumikia kwa moyo wote.—2 Nya. 16:9.

6 Lakini, huenda ukajiuliza ikiwa mtu anahitaji kuwa mkamilifu ili awe mtimilifu. Kwa sababu tumerithi dhambi na hali ya kutokamilika, huenda tukajilinganisha kwa kadiri fulani na kitabu kisichokamilika au samaki ambaye si kamili. Je, ndivyo unavyohisi nyakati nyingine? Uwe na hakika kwamba Yehova hatarajii tuwe wakamilifu katika maana kamili. Hatarajii tutimize mambo tusiyoweza. * (Zab. 103:14; Yak. 3:2) Lakini, anatarajia tuendelee kuwa watimilifu. Basi, je, kuna tofauti kati ya ukamilifu na utimilifu? Ndiyo. Kwa mfano: Mwanamume fulani kijana anampenda msichana fulani ambaye atakuwa mke wake. Kijana huyo angekuwa mpumbavu ikiwa angetazamia msichana huyo awe mkamilifu. Hata hivyo, ni jambo la hekima kutarajia msichana huyo ampende kwa moyo wote, yaani, amwonyeshe yeye peke yake upendo wa kimahaba. Vivyo hivyo, Yehova ni “Mungu anayetaka watu wajitoe kikamili.” (Kut. 20:5) Hatarajii tuwe wakamilifu, bali anataka tumpende kwa moyo wote, na kumwabudu yeye peke yake.

7, 8. (a) Yesu aliweka mfano gani kuhusu utimilifu? (b) Kulingana na Maandiko, utimilifu unamaanisha nini hasa?

7 Huenda tukakumbuka jibu la Yesu alipoulizwa ni sheria gani iliyo kuu zaidi kati ya zote. (Soma Marko 12:28-30.) Yesu hakujibu tu; alionyesha hivyo kwa matendo. Aliweka mfano bora zaidi wa kumpenda Yehova kwa akili, moyo, nafsi, na nguvu zake zote. Alionyesha kwamba utimilifu hauonyeshwi kwa maneno matupu, bali kwa matendo mazuri yanayochochewa na nia nzuri. Ili tuendelee kuwa watimilifu tunahitaji kufuata hatua za Yesu.—1 Pet. 2:21.

8 Basi, kulingana na Maandiko, utimilifu unamaanisha hasa: kujitoa kwa moyo wote kwa Mtu mmoja aliye mbinguni, Yehova Mungu, na kujitoa kutimiza mapenzi na kusudi lake. Kuendelea kuwa watimilifu kunamaanisha kwamba katika maisha ya kila siku, tutajitahidi hasa kumpendeza Yehova Mungu. Tutatanguliza maishani mambo anayoyaona kuwa ya maana zaidi. Acheni tuchunguze sababu tatu zinazoonyesha kwa nini hilo ni jambo la maana sana.

1. Utimilifu Wetu na Suala la Enzi Kuu

9. Kuna uhusiano gani kati ya utimilifu wetu na suala la enzi kuu ya ulimwengu wote mzima?

9 Enzi kuu ya Yehova, haitegemei utimilifu wetu. Enzi yake kuu ni ya haki, ya milele, na ya ulimwengu wote mzima. Itakuwa hivyo nyakati zote, hata kiumbe yeyote yule aseme au afanye nini. Hata hivyo, enzi kuu ya Mungu imeletewa suto kubwa mbinguni na duniani. Hivyo, utawala wake unahitaji kutetewa mbele ya viumbe wote wenye akili, yaani, kuthibitishwa kuwa unafaa, ni wa haki, na wenye upendo. Tukiwa Mashahidi wa Yehova, tunapenda kuzungumzia enzi kuu ya Mungu ya ulimwengu wote mzima pamoja na mtu yeyote aliye tayari kusikiliza. Hata hivyo, tunaweza kufanya nini ili kuonyesha kwamba sisi binafsi tumechukua msimamo kuhusiana na suala hilo? Tunaonyesha jinsi gani kwamba tumekubali Yehova awe Mtawala wetu Mkuu? Kwa kuendelea kuwa watimilifu.

10. Shetani ametoa shtaka gani kuhusu utimilifu wa wanadamu, na ungependa kujibu shtaka hilo jinsi gani?

10 Hebu ona jinsi utimilifu wako unavyohusika. Shetani amedai kwamba hakuna mwanadamu atakayeunga mkono enzi kuu ya Mungu, kwamba hakuna yeyote atakayemtumikia Yehova akichochewa na upendo usio na ubinafsi. Ibilisi alimwambia Yehova hivi mbele ya kusanyiko kubwa la viumbe wa roho: “Ngozi kwa ngozi, na kila kitu alicho nacho mtu atakitoa kwa ajili ya nafsi yake.” (Ayu. 2:4) Ona kwamba Shetani hakudai hivyo kumhusu yule mwanamume mwadilifu Ayubu tu bali kuhusu wanadamu wote kwa jumla. Hivyo, Biblia inamwita Shetani “mshtaki wa ndugu zetu.” (Ufu. 12:10) Anamdhihaki Yehova akidai kwamba Wakristo—kutia ndani wewe—hawataendelea kuwa waaminifu. Shetani anadai kwamba unaweza kumsaliti Yehova ili uiokoe nafsi yako. Unahisi jinsi gani kuhusu mashtaka hayo yanayokuhusu? Je, hungefurahi kupata nafasi ya kumthibitisha Shetani kuwa mwongo? Kwa kuendelea kuwa mtimilifu, unaweza kumthibitisha kuwa mwongo.

11, 12. (a) Ni mifano gani inayoonyesha kwamba maamuzi tunayofanya kila siku yanahusiana na suala la utimilifu wetu? (b) Kwa nini ni pendeleo kuendelea kuwa mtimilifu?

11 Hivyo, kwa sababu ya suala la utimilifu wako, mwenendo na maamuzi unayofanya kila siku ni ya maana sana. Fikiria tena zile hali tatu zilizotajwa mwanzoni. Yule mvulana, mume, na mke wangefanya nini ili kuendelea kuwa watimilifu? Yule mvulana anayedhihakiwa na wanafunzi wenzake anashawishiwa sana kulipiza kisasi, lakini anakumbuka shauri hili: “Wapendwa, msijilipizie kisasi wenyewe bali iachieni nafasi ghadhabu; kwa maana imeandikwa: ‘Kisasi ni changu; mimi nitalipa, asema Yehova.’” (Rom. 12:19) Hivyo, anaamua kuondoka. Yule mume anayetumia Intaneti angeweza kutazama picha zinazosisimua tamaa ya ngono, lakini anakumbuka kanuni iliyo katika maneno haya ya Ayubu: “Nimefanya agano pamoja na macho yangu. Basi nawezaje kukaza fikira kwa bikira?” (Ayu. 31:1) Vivyo hivyo, mwanamume huyo anaepuka kutazama picha hizo zinazochukiza, anaziepuka kama sumu. Yule mwanamke anayezungumza na akina dada wengine wakati ambapo mazungumzo yanageuka na kuwa porojo yenye kuumiza anajizuia asichangie porojo hizo, akikumbuka agizo hili: “Kila mmoja wetu na ampendeze jirani yake katika yaliyo mema kwa ajili ya kujengwa kwake.” (Rom. 15:2) Ikiwa angechangia porojo hizo, hangesema mambo yenye kujenga. Angekuwa akimharibia sifa dada yake Mkristo; naye hangempendeza Baba yake wa mbinguni. Kwa hiyo, mwanamke huyo anazuia ulimi wake na kubadili mazungumzo.

12 Katika hali zote hizo, kupitia uamuzi wanaofanya, ni kana kwamba Wakristo hao wanasema: ‘Yehova ni Mtawala wangu. Nitajitahidi kufanya mambo yanayompendeza katika jambo hili.’ Unapofanya maamuzi ya kibinafsi, je, unaona mambo kwa njia hiyo? Ukifanya hivyo, basi utakuwa ukitii maneno haya yenye kutia moyo ya Methali 27:11: “Uwe na hekima, mwanangu, na kuufanya moyo wangu ushangilie, ili nipate kumjibu anayenidhihaki.” Tuna pendeleo kubwa kama nini la kuufanya moyo wa Mungu ushangilie! Basi, je, hatupaswi kufanya yote tuwezayo ili kuendelea kuwa watimilifu?

2. Mungu Anatuhukumu kwa Msingi wa Utimilifu Wetu

13. Maneno ya Ayubu na ya Daudi yanaonyesha jinsi gani kwamba Yehova anatuhukumu kwa msingi wa utimilifu?

13 Tunaona kwamba utimilifu unatuwezesha kuunga mkono enzi kuu ya Yehova. Hivyo, Mungu anatuhukumu kwa msingi wa utimilifu wetu. Ayubu alielewa vizuri ukweli huo. (Soma Ayubu 31:6.) Ayubu alijua kwamba Mungu anawapima wanadamu wote katika “mizani sahihi,” akitumia kiwango Chake kikamilifu cha haki ili kuona ikiwa sisi ni watimilifu. Pia, Daudi alisema hivi: “Yehova mwenyewe atavihukumu vikundi vya watu. Nihukumu, Ee Yehova, kulingana na uadilifu wangu na kulingana na utimilifu wangu. . . . Na Mungu akiwa mwadilifu anapima moyo na figo.” (Zab. 7:8, 9) Tunajua kwamba Mungu anaweza kumchunguza mtu ndani kabisa, yaani, anaweza kuchunguza “moyo na figo” za mfano. Hata hivyo, tunapaswa kukumbuka kile anachotafuta. Kama Daudi alivyosema, Yehova anatuhukumu kulingana na utimilifu wetu.

14. Kwa nini hatupaswi kufikiri kwamba hali yetu ya kutokamilika inatuzuia tusiendelee kuwa watimilifu?

14 Yehova Mungu anachunguza mabilioni ya mioyo ya wanadamu leo. (1 Nya. 28:9) Unafikiri ni mara ngapi ambapo anampata mtu ambaye anadumisha utimilifu wa Kikristo? Ni mara chache sana! Hata hivyo, hatupaswi kufikiri kwamba tuna makosa mengi sana hivi kwamba hatuwezi kudumisha utimilifu. Badala yake, kama Daudi na Ayubu, tuna sababu nzuri za kuamini kwamba Yehova atatupata tukidumisha utimilifu, hata ingawa sisi si wakamilifu. Kumbuka kwamba kuwa wakamilifu hakumaanishi kwamba tutaendelea kuwa watimilifu. Ni wanadamu watatu tu wakamilifu ambao wameishi duniani, na wawili kati yao, Adamu na Hawa, walishindwa kuendelea kuwa watimilifu. Hata hivyo, mamilioni ya wanadamu wasio wakamilifu wamefaulu kuendelea kuwa watimilifu. Wewe pia unaweza kufaulu.

3. Utimilifu Ni Sifa ya Maana kwa Tumaini Letu

15. Daudi alionyesha jinsi gani kwamba utimilifu ni wa maana kwa tumaini lake la wakati ujao?

15 Kwa kuwa Yehova anatuhukumu kwa msingi wa utimilifu wetu, utimilifu ni wa maana kwa tumaini letu la wakati ujao. Daudi alijua ukweli wa jambo hilo. (Soma Zaburi 41:12.) Daudi alithamini sana tumaini la kukubaliwa na Mungu milele. Kama Wakristo wa kweli leo, Daudi alitumaini kuishi milele na kuendelea kumkaribia Yehova Mungu huku akimtumikia. Daudi alijua kwamba alihitaji kuendelea kuwa mtimilifu ili aone tumaini hilo likitimia. Vivyo hivyo, Yehova anatutegemeza, anatufundisha, anatuongoza, na anatubariki tunapoendelea kuwa watimilifu.

16, 17. (a) Kwa nini umeazimia sikuzote kushikilia kabisa utimilifu wako? (b) Habari inayofuata itazungumzia maswali gani?

16 Ili tuwe wenye furaha tunahitaji kuwa na tumaini. Tumaini linaweza kutuletea shangwe tunayohitaji ili kuvumilia hali ngumu. Pia, tumaini linaweza kulinda fikira zetu. Kumbuka kwamba Biblia inafananisha tumaini na kofia ya chuma. (1 The. 5:8) Kama vile kofia ya chuma inavyolinda kichwa cha askari-jeshi aliye vitani, tumaini linalinda akili zetu ili zisipenywe na mawazo yasiyofaa ambayo Shetani anaendeleza kupitia ulimwengu huu wa kale unaopitilia mbali. Ni wazi kwamba bila tumaini, maisha hayana kusudi. Tunahitaji kujichunguza kwa unyoofu, na kuchanganua kwa makini hali ya utimilifu wetu na tumaini linalohusiana nalo. Usisahau kwamba unapoendelea kuwa mtimilifu, unaunga mkono enzi kuu ya Yehova na kulinda tumaini lako la wakati ujao lenye thamani. Ndiyo, shikilia kabisa utimilifu wako sikuzote!

17 Kwa kuwa utimilifu ni sifa ya maana sana, tunahitaji kufikiria maswali mengine. Tunajenga utimilifu jinsi gani? Tunaweza kufanya nini ili tuendelee kuwa watimilifu? Na mtu anaweza kufanya nini ikiwa alishindwa kuwa mtimilifu kwa muda fulani? Habari inayofuata itazungumzia maswali hayo.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 6 Yesu alisema: “Lazima ninyi basi muwe wakamilifu, kama Baba yenu wa mbinguni alivyo mkamilifu.” (Mt. 5:48) Inaelekea alielewa kwamba hata wanadamu wasio wakamilifu wanaweza kuwa kamili, au wakamilifu kwa kadiri fulani. Tunaweza kutimiza amri ya kuwapenda wengine kutoka moyoni, na hivyo kumpendeza Mungu. Hata hivyo, Yehova ni mkamilifu katika maana kamili. Neno “utimilifu” linapotumiwa kumhusu, linahusisha pia ukamilifu.—Zab. 18:30.

Ungesema Nini?

• Utimilifu ni nini?

• Kuna uhusiano gani kati ya utimilifu na suala la enzi kuu ya ulimwengu wote mzima?

• Utimilifu ni msingi wa tumaini letu jinsi gani?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 5]

Kila siku utimilifu wetu unajaribiwa kwa njia nyingi