Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maandishi ya Kale ya Kikabari na Biblia

Maandishi ya Kale ya Kikabari na Biblia

Maandishi ya Kale ya Kikabari na Biblia

BAADA ya lugha ya wanadamu kuvurugwa huko Babeli, mitindo mbalimbali ya kuandika ilianzishwa. Watu walioishi Mesopotamia, kama vile Wasumeria na Wababiloni, walitumia maandishi ya kikabari. Neno la Kilatini linalotafsiriwa kuwa maandishi ya kikabari linamaanisha “-enye umbo kama la kabari,” na linahusu alama za pembe tatu ambazo zilichorwa kwenye udongo ulio majimaji kwa kifaa chenye ncha kali.

Wachimbuaji wa vitu vya kale wamechimbua maandishi ya kikabari yanayotaja watu na matukio yaliyo katika Maandiko. Tunajua nini kuhusu mtindo huo wa zamani wa kuandika? Na maandishi hayo yanathibitisha jinsi gani kwamba Biblia inategemeka?

Rekodi Ambazo Zimedumu

Wasomi wanaamini kwamba mwanzoni watu wa Mesopotamia walitumia maandishi ya picha. Alama au picha fulani iliwakilisha neno au wazo fulani. Kwa mfano, mwanzoni walichora kichwa cha ng’ombe-dume kuwakilisha ng’ombe-dume. Kadiri uhitaji wa kuhifadhi maandishi ulivyoongezeka, ndivyo maandishi ya kikabari yalivyositawi. Kitabu kimoja (NIV Archaeological Study Bible) kinaeleza hivi: “Sasa ishara zilitumiwa kuwakilisha si maneno tu bali pia silabi, na ishara kadhaa ziliunganishwa ili kuwakilisha silabi za neno.” Mwishowe, “maneno, misamiati na kanuni zote za lugha ziliweza kuwakilishwa kwa usahihi kabisa” kupitia ishara mbalimbali 200 hivi.

Kufikia wakati wa Abrahamu, karibu mwaka wa 2,000 K.W.K., maandishi hayo yalikuwa yamesitawi sana. Katika karne 20 zilizofuata, lugha 15 hivi zilitumia maandishi hayo. Zaidi ya asilimia 99 ya maandishi ya kikabari ambayo yamepatikana yaliandikwa kwenye mabamba ya udongo. Katika miaka 150 ambayo imepita, mabamba mengi kama hayo yamepatikana huko Ur, Uruk, Babylon, Nimrud, Nippur, Ashur, Nineveh, Mari, Ebla, Ugarit, na Amarna. Kitabu kimoja (Archaeology Odyssey) kinasema: “Wataalamu wanakadiria kwamba mabamba ya kikabari kati ya milioni moja na milioni mbili tayari yamechimbuliwa, na mengine 25,000 hivi yanapatikana kila mwaka.”

Wasomi wa maandishi hayo ulimwenguni pote wana kazi kubwa sana ya kuyatafsiri. Kulingana na kadirio moja, “ni hati 1 tu kati ya kila hati 10 za maandishi ya kikabari zilizopo ndizo zimesomwa angalau wakati mmoja katika nyakati za kisasa.”

Kugunduliwa kwa maandishi ya kikabari yenye lugha mbili na yale yenye lugha tatu kuliwasaidia sana watu kuelewa maandishi hayo. Wasomi walitambua kwamba mabamba hayo yalikuwa na maandishi yaleyale ya kikabari katika lugha tofauti-tofauti. Walifaulu kuyatafsiri walipogundua kwamba majina, vyeo, ukoo wa watawala, na hata maneno ya kujisifu yalirudiwa-rudiwa mara nyingi.

Kufikia miaka ya 1850, wasomi waliweza kusoma lugha ya mawasiliano iliyotumiwa zamani katika Mashariki ya Kati, Akadi, Ashuru na Babiloni ambayo iliandikwa kwa maandishi ya kikabari. Kitabu kimoja (Encyclopædia Britannica) kinaeleza hivi: “Mara tu Kiakadi kilipotafsiriwa, mtindo wa maandishi hayo ulieleweka, na njia ya kutafsiri lugha nyingine zilizoandikwa kwa maandishi ya kikabari iligunduliwa.” Maandishi hayo yanahusiana jinsi gani na Maandiko?

Ushahidi Unaopatana na Biblia

Biblia inasema kwamba jiji la Yerusalemu lilitawaliwa na wafalme Wakanaani mpaka Daudi alipowashinda, karibu mwaka wa 1070 K.W.K. (Yos. 10:1; 2 Sam. 5:4-9) Lakini wasomi fulani walikuwa na shaka kuhusu hilo. Hata hivyo, katika mwaka wa 1887 mwanamke fulani mkulima alipata bamba la udongo huko Amarna, Misri. Mwishowe, iligunduliwa kwamba barua 380 zilizoandikwa kwenye bamba hilo zilikuwa barua za kiserikali kati ya watawala wa Misri (Amenhotep wa 3 na Akhenaton) na falme za Kanaani. Barua sita ziliandikwa na ‘Abdi-Heba, mtawala wa Yerusalemu.

Gazeti moja (Biblical Archaeology Review) linasema hivi: “Mabamba ya Amarna yanathibitisha wazi kwamba Yerusalemu ulikuwa mji, wala si mtaa, na kwamba ‘Abdi-Heba alikuwa . . . gavana ambaye aliishi Yerusalemu na askari-jeshi wake 50 Wamisri walilinda Yerusalemu, na hilo linadokeza kwamba Yerusalemu ilikuwa nchi ndogo ya kifalme yenye milima.” Gazeti hilo lilisema hivi baadaye: “Kwa msingi wa barua za Amarna, tunaweza kuwa na uhakika kwamba kulikuwa na mji ambao ulikuwa maarufu wakati huo.”

Majina Katika Rekodi za Ashuru na Babiloni

Waashuru, na baadaye Wababiloni, waliandika historia yao kwenye mabamba ya udongo, na pia kwenye mianzi, miche, na mawe ya ukumbusho. Kwa hiyo, wasomi walipotafsiri maandishi ya kikabari ya Kiakadi, waligundua kwamba maandishi hayo yana majina ya watu wanaotajwa katika Biblia.

Kitabu kimoja (The Bible in the British Museum) kinasema hivi: “Katika hotuba aliyotoa mwaka wa 1870 kwa washiriki wa shirika jipya la Society of Biblical Archaeology, Dakt. Samuel Birch alitambua [katika maandishi ya kikabari majina ya] wafalme wafuatao Waebrania, Omri, Ahabu, Yehu, Azaria . . . , Menahemu, Peka, Hoshea, Hezekia na Manase, na wafalme wa Ashuru, Tiglath-Pilesa . . . [wa 3], Sargoni, Senakeribu, Esarhadoni na Ashurbanipali, . . . na wafalme wa Siria, Benhadadi, Hazaeli na Resini.”

Kitabu kimoja (The Bible and Radiocarbon Dating) kinalinganisha historia ya Israeli na Yuda katika Biblia na maandishi ya kale ya kikabari. Matokeo ni nini? “Kwa ujumla, wafalme 15 au 16 wa Yuda na Israeli wanatajwa katika rekodi za wakati huo kutoka katika nchi nyingine. Majina na nyakati walizoishi zinapatana kabisa na habari zinazotajwa katika [kitabu cha Biblia cha] Wafalme. Hakuna kosa hata moja kuhusiana na nchi za wafalme hao, wala rekodi hizo hazimtaji mfalme ambaye hatujapata jina lake katika kitabu cha Wafalme.”

Mchoro fulani maarufu wa kikabari uliopatikana mwaka wa 1879, ambao unaitwa Mwanzi wa Koreshi, unaonyesha kwamba baada ya kuteka Babiloni mwaka wa 539 K.W.K., Koreshi alifuata sera yake ya kuwarudisha mateka kwenye nchi zao. Wayahudi walikuwa miongoni mwa watu waliofaidika kutokana na sera hiyo. (Ezra 1:1-4) Wasomi wengi wa karne ya 19 walitilia shaka agizo la Koreshi linalotajwa katika Biblia. Hata hivyo, maandishi ya kikabari ya enzi za Waajemi, kutia ndani na Mwanzi wa Koreshi, yanatoa uthibitisho wenye kusadikisha kwamba rekodi ya Biblia ni sahihi.

Mwaka wa 1883, maktaba yenye maandishi ya kikabari zaidi ya 700 ilipatikana huko Nippur, karibu na Babiloni. Majina 70 hivi kati ya majina 2,500 yanayotajwa katika maandishi hayo yanatambuliwa kuwa majina ya Kiyahudi. Mwanahistoria Edwin Yamauchi anasema kwamba hayo ni majina ya “watu waliofanya mikataba, mawakili, mashahidi, wakusanya-kodi, na maofisa wa mfalme.” Uthibitisho wa kwamba Wayahudi waliendelea kufanya shughuli hizo karibu na Babiloni katika kipindi hicho ni muhimu. Unaunga mkono unabii wa Biblia wa kwamba wakati “mabaki” ya Waisraeli waliporudi Yudea kutoka uhamishoni huko Ashuru na Babiloni, wengi hawakurudi.—Isa. 10:21, 22.

Katika milenia ya kwanza K.W.K., maandishi ya kikabari yalitumiwa pamoja na maandishi ya alfabeti. Lakini mwishowe Waashuru na Wababiloni waliacha maandishi ya kikabari na kutumia maandishi ya alfabeti.

Mamia ya maelfu ya mabamba yaliyohifadhiwa katika majumba ya makumbusho hayajachunguzwa. Yale ambayo tayari wataalamu wametafsiri yanatoa uthibitisho wenye kusadikisha kwamba Biblia inategemeka. Huenda maandishi ambayo hayajachunguzwa yatatoa uthibitisho zaidi wa kwamba Biblia inategemeka.

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 21]

Photograph taken by courtesy of the British Museum