Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Katika Nehemia 8:10, Wayahudi waliambiwa ‘wale vitu vinono,’ hata ingawa Sheria ilisema hivi katika Mambo ya Walawi 3:17: “Msile mafuta yoyote.” Maandiko hayo mawili yanaweza kupatanishwa kwa njia gani?

Katika lugha ya awali, maneno yanayotafsiriwa “vitu vinono” katika Nehemia 8:10 na “mafuta” katika Mambo ya Walawi 3:17 ni tofauti. Neno la Kiebrania cheʹlev, ambalo linatafsiriwa “mafuta” katika Mambo ya Walawi 3:17, linamaanisha mafuta ya wanyama au ya mwili wa mwanadamu. (Law. 3:3; Amu. 3:22) Mistari inayozunguka mstari wa 17 inaonyesha kwamba Waisraeli hawakupaswa kula mafuta yaliyofunika matumbo na figo za wanyama wa dhabihu wala mafuta yaliyokuwa juu ya viuno kwa sababu “mafuta yote ni ya Yehova.” (Law. 3:14-16) Kwa hiyo, mafuta yaliyokuwa ndani ya miili ya wanyama hayakupaswa kuliwa, yalipaswa kutolewa kwa Yehova.

Kwa upande mwingine, neno linalotafsiriwa “vitu vinono” katika Nehemia 8:10 ni mash·man·nimʹ, na linapatikana kwenye andiko hilo moja tu katika Maandiko ya Kiebrania. Linatokana na kitenzi sha·menʹ, ambacho kinamaanisha “nona, nenepa.” Inaonekana kwamba maneno yanayohusiana na kitenzi hicho kimsingi yanamaanisha ufanisi na hali njema. (Linganisha na Isaya 25:6.) Moja ya maneno ambayo kwa kawaida yanatokana na kitenzi hicho ni nomino sheʹmen, ambayo kwa kawaida inatafsiriwa “mafuta” kama vile katika usemi ‘mafuta ya zeituni.’ (Kum. 8:8; Law. 24:2) Inaonekana neno mash·man·nimʹ  ambalo linatumiwa katika Nehemia 8:10, linamaanisha chakula kilichopikwa kwa mafuta mengi na huenda hata kilitia ndani nyama yenye kiasi kidogo cha mafuta bali si mafuta mengi matupu ya mnyama.

Ingawa Waisraeli walikatazwa kula mafuta mengi ya wanyama, wangeweza kula chakula kitamu kinachojenga mwili. Vyakula fulani, kama vile keki za nafaka, ziliokwa kwa mafuta ya mboga, hasa mafuta ya zeituni, bali si mafuta ya wanyama. (Law. 2:7) Hivyo, kitabu Insight on the Scriptures (Étude perspicace des Écritures) kinaeleza kwamba “vitu vinono” vinamaanisha “vyakula vitamu vyenye mchuzi vinavyojenga mwili, vilivyotayarishwa kwa mafuta ya mboga, bali si vyakula vikavu.”

Bila shaka, Wakristo wanakumbuka kwamba amri ya kutokula mafuta ilikuwa sehemu ya Sheria. Hawako chini ya Sheria, wala chini ya matakwa yake yanayohusu dhabihu za wanyama.—Rom. 3:20; 7:4, 6; 10:4; Kol. 2:16, 17.