Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Thamini Daraka la Pekee la Yesu Katika Kusudi la Mungu

Thamini Daraka la Pekee la Yesu Katika Kusudi la Mungu

Thamini Daraka la Pekee la Yesu Katika Kusudi la Mungu

“Mimi ndiye njia na kweli na uzima. Hakuna anayekuja kwa Baba ila kupitia kwangu.”—YOH. 14:6.

1, 2. Kwa nini tuchunguze daraka la pekee la Yesu katika kusudi la Mungu?

KWA miaka mingi, watu wengi wamejitahidi sana kuwa tofauti na watu wengine, lakini ni wachache sana ambao wamefaulu. Ni watu wachache hata zaidi wanaoweza kudai kwamba ni wa pekee katika njia mbalimbali. Hata hivyo, Yesu Kristo, Mwana wa Mungu, ni wa pekee katika njia nyingi.

2 Kwa nini tunapendezwa na daraka la pekee la Yesu? Kwa sababu uhusiano wetu pamoja na Baba yetu wa mbinguni, Yehova, unahusika! Yesu alisema hivi: “Mimi ndiye njia na kweli na uzima. Hakuna anayekuja kwa Baba ila kupitia kwangu.” (Yoh. 14:6; 17:3) Acheni tuchunguze mambo fulani ambayo yanamfanya Yesu awe wa pekee. Tukifanya hivyo tutathamini zaidi daraka analotimiza katika kusudi la Mungu.

“Mwana Mzaliwa-Pekee”

3, 4. (a) Kwa nini tunaweza kusema kwamba Yesu ni wa pekee katika daraka lake akiwa Mwana mzaliwa-pekee? (b) Daraka la Yesu katika uumbaji lilikuwa la pekee jinsi gani?

3 Yesu si “mwana wa Mungu” tu kama vile Shetani alivyomwita alipokuwa akimshawishi. (Mt. 4:3, 6) Kwa kufaa, Yesu anaitwa pia “Mwana mzaliwa-pekee wa Mungu.” (Yoh. 3:16, 18) Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “mzaliwa-pekee” linafafanuliwa kuwa “wa pekee, wa aina yake,” “mshiriki wa pekee wa jamii fulani au kikundi fulani” au “asiye na kifani.” Yehova ana mamia ya mamilioni ya wana wa roho. Basi, ni katika maana gani Yesu ndiye mshiriki wa pekee “wa jamii fulani au kikundi fulani”?

4 Yesu ni wa pekee katika maana ya kwamba ni yeye tu aliyeumbwa moja kwa moja na Baba yake. Yeye ndiye Mwana mzaliwa wa kwanza. Kwa kweli, yeye ndiye “mzaliwa wa kwanza wa viumbe vyote.” (Kol. 1:15) Yeye ndiye “mwanzo wa uumbaji wa Mungu.” (Ufu. 3:14) Pia, daraka la Mwana mzaliwa-pekee katika uumbaji ni la pekee. Yeye hakuwa Muumba, au Mwanzilishi, wa uumbaji. Lakini Yehova alimtumia akiwa wakili, au njia, ya kuumba vitu vingine vyote. (Soma Yohana 1:3.) Mtume Paulo aliandika: “Kwa kweli kwetu sisi kuna Mungu mmoja aliye Baba, ambaye vitu vyote vimetoka kwake, na sisi kwa ajili yake; na kuna Bwana mmoja, Yesu Kristo, ambaye vitu vyote vimepitia kwake, na sisi kupitia yeye.”—1 Kor. 8:6.

5. Maandiko yanakazia jinsi gani kwamba Yesu ni wa pekee?

5 Hata hivyo, Yesu ni wa pekee katika njia nyingine nyingi. Maandiko yanamtaja kwa vyeo vingi au majina ambayo yanakazia daraka lake la pekee katika kusudi la Mungu. Acheni sasa tuchunguze vyeo au majina matano zaidi anayopewa Yesu katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. *

“Neno”

6. Kwa nini Yesu anaitwa kwa kufaa “Neno”?

6 Soma Yohana 1:14. Kwa nini Yesu anaitwa “Neno,” au Logos? Cheo hicho kinaonyesha daraka ambalo anatimiza tangu viumbe wengine wenye akili walipoumbwa. Yehova alimtumia Mwana wake kuwapa habari na maagizo wana wengine wa roho, kama vile alivyomtumia Mwana huyo kuwapa wanadamu walio duniani ujumbe Wake. Uhakika wa kwamba Yesu ni Neno, au Msemaji wa Mungu, unathibitishwa na mambo ambayo Kristo aliwaambia wasikilizaji wake Wayahudi: “Yale ninayofundisha si yangu, bali ni yake yeye aliyenituma. Ikiwa yeyote anatamani kufanya mapenzi Yake, atajua kama fundisho hilo limetoka kwa Mungu au kama ninasema mambo ambayo nimetunga mimi mwenyewe.” (Yoh. 7:16, 17) Yesu anaendelea kuitwa “Neno la Mungu” hata baada ya kurudi katika utukufu wa kimbingu.—Ufu. 19:11, 13, 16.

7. Tunaweza kuiga jinsi gani unyenyekevu ambao Yesu anaonyesha anapotimiza daraka lake akiwa “Neno”?

7 Hebu fikiria kile kinachomaanishwa na cheo hicho. Ingawa Yesu ndiye mwenye hekima zaidi kati ya viumbe wote wa Yehova, hategemei hekima yake mwenyewe. Anasema kama anavyoagizwa na Baba yake. Sikuzote anaelekeza uangalifu kwa Yehova wala si kwake mwenyewe. (Yoh. 12:50) Ametuwekea mfano mzuri kama nini! Sisi pia tumepewa pendeleo lenye thamani la ‘kutangaza habari njema ya mambo mema.’ (Rom. 10:15) Kuthamini mfano mzuri wa unyenyekevu wa Yesu kunapaswa kutuchochea kuepuka kusema mambo yetu wenyewe. Tunapotangaza ujumbe unaookoa uhai ulio katika Maandiko, hatupaswi ‘kupita mambo yaliyoandikwa.’—1 Kor. 4:6.

“Amina”

8, 9. (a) Neno “amina” linamaanisha nini, na kwa nini Yesu anaitwa “Amina”? (b) Yesu alitimiza jinsi gani daraka lake akiwa “Amina”?

8 Soma Ufunuo 3:14. Kwa nini Yesu anaitwa “Amina”? Neno linalotafsiriwa “amina” ni neno la lugha ya Kiebrania ambalo linamaanisha “na iwe hivyo,” au “bila shaka.” Shina la neno hilo katika Kiebrania linamaanisha “kuwa mwaminifu” au “mwenye kutegemeka.” Neno hilohilo linatumiwa kuelezea uaminifu wa Yehova. (Kum. 7:9; Isa. 49:7) Kwa hiyo, Yesu anapoitwa “Amina” anakuwa wa pekee katika njia gani? Ona jinsi andiko la 2 Wakorintho 1:19, 20 linavyojibu swali hilo: “Mwana wa Mungu, Kristo Yesu, aliyehubiriwa katikati yenu . . . , hakuwa Ndiyo na pia Siyo, bali Ndiyo imekuwa Ndiyo kuhusiana naye. Kwa maana hata ahadi za Mungu ziwe nyingi kadiri gani, zimekuwa Ndiyo kwa njia yake. Kwa hiyo kupitia yeye pia ‘Amina’ husemwa kwa Mungu kwa ajili ya utukufu.”

9 Yesu ni “Amina” kuhusiana na ahadi zote za Mungu. Maisha yake yasiyo na kasoro hapa duniani, kutia ndani kifo chake cha kidhabihu, yalithibitisha na kufanya ahadi zote za Yehova Mungu zitimizwe. Kwa kubaki mwaminifu, Yesu alithibitisha pia uwongo wa dai la Shetani linalopatikana katika kitabu cha Ayubu, kwamba chini ya hali ngumu, mateso, na majaribu, watumishi wa Mungu wanaweza kumkana. (Ayu. 1:6-12; 2:2-7) Kati ya viumbe wote wa Mungu, ni Mwana mzaliwa wa kwanza tu aliyejibu dai hilo kwa njia ya kukata maneno. Zaidi ya hayo, Yesu alitoa uthibitisho bora zaidi uliomuunga mkono Baba yake katika suala kuu zaidi la haki ya Yehova ya kutawala akiwa mwenye enzi kuu ya ulimwengu wote.

10. Tunaweza kumwiga Yesu jinsi gani katika daraka lake la pekee akiwa “Amina”?

10 Tunaweza kumwiga Yesu jinsi gani katika daraka lake la pekee akiwa “Amina”? Kwa kubaki waaminifu kwa Yehova na kuunga mkono enzi yake kuu. Tukifanya hivyo, tutakuwa tukijibu ombi lililo kwenye Methali 27:11: “Uwe na hekima, mwanangu, na kuufanya moyo wangu ushangilie, ili nipate kumjibu anayenidhihaki.”

“Mpatanishi wa Agano Jipya”

11, 12. Daraka la Yesu akiwa Mpatanishi ni la pekee jinsi gani?

11 Soma 1 Timotheo 2:5, 6Yesu ndiye yule “mpatanishi mmoja kati ya Mungu na wanadamu.” Yeye ni “mpatanishi wa agano jipya.” (Ebr. 9:15; 12:24) Hata hivyo, Musa anaitwa pia mpatanishi, yaani, mpatanishi wa agano la Sheria. (Gal. 3:19) Hivyo basi, daraka la Yesu akiwa Mpatanishi ni la pekee jinsi gani?

12 Neno la lugha ya awali linalotafsiriwa “mpatanishi” ni neno la kisheria. Linamhusu Yesu akiwa Mpatanishi wa kisheria (au, katika maana fulani, wakili) wa agano jipya ambalo liliwezesha kuzaliwa kwa taifa jipya, “Israeli wa Mungu.” (Gal. 6:16) Taifa hilo linafanyizwa na Wakristo watiwa-mafuta, ambao wanakuwa “ukuhani wa kifalme” wa kimbingu. (1 Pet. 2:9; Kut. 19:6) Agano la Sheria ambalo Musa alikuwa mpatanishi wake, halikuweza kutokeza taifa kama hilo.

13. Daraka la Yesu akiwa Mpatanishi linatia ndani nini?

13 Daraka la Yesu akiwa Mpatanishi linatia ndani nini? Yehova anatumia thamani ya damu ya Yesu kwa wale wanaoingizwa katika agano jipya. Katika njia hiyo, Yehova anawapa kisheria haki ya kuwa waadilifu. (Rom. 3:24; Ebr. 9:15) Kisha, Mungu anawaona kuwa wanastahili kuingia katika agano jipya wakiwa na tumaini la kuwa wafalme na makuhani wa kimbingu! Akiwa Mpatanishi wao, Yesu anawasaidia wadumishe msimamo safi mbele za Mungu.—Ebr. 2:16.

14. Kwa nini Wakristo wote, hata wakiwa na tumaini gani, wanapaswa kuthamini kabisa daraka la Yesu akiwa Mpatanishi?

14 Namna gani wale ambao hawamo katika agano jipya, wale ambao wanatumaini kuishi milele duniani, si mbinguni? Ingawa si washiriki wa hilo agano jipya, wao wanafaidika nalo. Wanasamehewa dhambi zao na wanatangazwa kuwa waadilifu na kuwa marafiki wa Mungu. (Yak. 2:23; 1 Yoh. 2:1, 2) Iwe tuna tumaini la kuishi mbinguni au duniani, kila mmoja wetu ana sababu nzuri ya kuthamini daraka la Yesu akiwa Mpatanishi wa agano jipya.

“Kuhani Mkuu”

15. Daraka la Yesu akiwa Kuhani Mkuu ni tofauti jinsi gani na la wanaume wengine wote ambao walitumikia wakiwa makuhani wakuu?

15 Wakati uliopita wanaume wengi walitumikia wakiwa makuhani wakuu, hata hivyo daraka la Yesu akiwa Kuhani Mkuu ni la pekee sana. Jinsi gani? Paulo anaeleza hivi: “Yeye hahitaji kila siku, kama wale makuhani wakuu wanavyofanya, kutoa dhabihu, kwanza kwa ajili ya dhambi zake mwenyewe kisha kwa ajili ya zile za watu: (kwa maana yeye alifanya hilo mara moja kwa wakati wote alipojitoa mwenyewe;) kwa maana Sheria huweka rasmi kuwa makuhani wakuu watu walio na udhaifu, lakini neno la kiapo rasmi lililokuja baada ya Sheria humweka rasmi Mwana, ambaye amekamilishwa milele.”—Ebr. 7:27, 28. *

16. Kwa nini dhabihu ya Yesu ni ya pekee sana?

16 Yesu alikuwa mwanadamu mkamilifu, aliyelingana kabisa na Adamu kabla hajatenda dhambi. (1 Kor. 15:45) Kwa hiyo, Yesu alikuwa ndiye mwanadamu pekee ambaye angeweza kutoa dhabihu kamilifu, aina ya dhabihu ambayo haikuhitaji kutolewa tena na tena. Chini ya Sheria ya Musa, dhabihu zilitolewa kila siku. Hata hivyo, dhabihu zote hizo na huduma za kikuhani zilikuwa kivuli tu cha yale ambayo Yesu angetimiza. (Ebr. 8:5; 10:1) Kwa hiyo, cheo cha Yesu akiwa Kuhani Mkuu ni cha pekee kwa kuwa anaweza kutimiza mengi zaidi kuliko wale makuhani wakuu wengine na atatumikia daima katika daraka lake.

17. Kwa nini tunapaswa kuthamini daraka la Yesu akiwa Kuhani wetu Mkuu, na tunaweza kufanya hivyo jinsi gani?

17 Tunahitaji huduma za Yesu akiwa Kuhani Mkuu ili tuweze kuwa na msimamo mzuri mbele za Mungu. Tuna Kuhani Mkuu mzuri ajabu kama nini! Paulo aliandika hivi: “Tuna kuhani mkuu, si mtu ambaye hawezi kuusikitikia udhaifu wetu, bali yeye ambaye amejaribiwa katika mambo yote kama sisi wenyewe, lakini bila kuwa na dhambi.” (Ebr. 4:15) Kwa kweli, tukithamini jambo hilo tutachochewa ‘tusiishi tena kwa ajili yetu wenyewe, bali kwa ajili ya yeye aliyekufa kwa ajili yetu.’—2 Kor. 5:14, 15; Luka 9:23.

“Uzao” Uliotabiriwa

18. Ni unabii gani uliotolewa baada ya Adamu kutenda dhambi, na ni mambo gani yaliyofunuliwa baadaye kuhusu unabii huo?

18 Katika Edeni, ilipoonekana kwamba wanadamu wamepoteza kila kitu, yaani, msimamo safi mbele za Mungu, uzima wa milele, furaha, na Paradiso—Yehova Mungu alitabiri kuja kwa Mkombozi. Mkombozi huyo alitajwa kuwa “uzao.” (Mwa. 3:15) Fumbo hilo kuhusu Uzao lilikuja kuwa msingi wa unabii mwingi wa Biblia kwa miaka mingi. Uzao huo ungetoka katika ukoo wa Abrahamu, Isaka, na Yakobo. Pia, ungetoka katika ukoo wa Mfalme Daudi.—Mwa. 21:12; 22:16-18; 28:14; 2 Sam. 7:12-16.

19, 20. (a) Ni nani aliye Uzao ulioahidiwa? (b) Kwa nini inaweza kusemwa kwamba uzao uliotabiriwa unatia ndani watu wengine zaidi ya Yesu?

19 Ni nani aliyekuwa Uzao huo ulioahidiwa? Jibu kwa swali hilo linaweza kupatikana kwenye Wagalatia 3:16. (Soma.) Hata hivyo, baadaye katika sura hiyohiyo, mtume Paulo anaendelea kuwaambia hivi Wakristo watiwa-mafuta: “Zaidi ya hayo, ikiwa ninyi ni wa Kristo, ninyi kwa kweli ni uzao wa Abrahamu, warithi kuhusiana na ahadi.” (Gal. 3:29) Kwa kuwa wengine wanatiwa ndani, Kristo ni Uzao ulioahidiwa katika maana gani?

20 Mamilioni ya watu wamedai kuwa wazao wa Abrahamu, wengine hata wamejifanya kuwa manabii. Dini fulani zinakazia kwamba manabii wake ni wazao wa Abrahamu. Lakini je, manabii wote hao ni Uzao ulioahidiwa? Hapana. Kama mtume Paulo anavyoonyesha kwa mwongozo wa roho ya Mungu, si wazao wote wa Abrahamu wanaoweza kudai kuwa Uzao ulioahidiwa. Wazao wa wana wengine wa Abrahamu hawakutumiwa kuwabariki wanadamu. Uzao wa baraka ungekuja kupitia tu Isaka. (Ebr. 11:18) Mwishowe, ni mwanadamu mmoja tu, Yesu Kristo, ambaye ndiye sehemu ya msingi ya uzao uliotabiriwa, na Biblia inathibitisha kwamba alitokana na Abrahamu. * Wengine wote ambao baadaye walikuja kuwa sehemu ya pili ya uzao wa Abrahamu wanakubaliwa kwa sababu “ni wa Kristo.” Ndiyo, daraka la Yesu katika kutimiza unabii huo ni la pekee sana.

21. Ni nini kinachokuvutia kuhusu jinsi ambavyo Yesu ametimiza daraka lake la pekee katika kusudi la Yehova?

21 Tumejifunza nini kupitia mazungumzo haya mafupi kuhusu daraka la pekee la Yesu katika kusudi la Yehova? Kwa kweli, tangu alipoumbwa, Mwana mzaliwa-pekee wa Mungu amekuwa wa pekee na asiye na kifani. Hata hivyo, Mwana huyo wa pekee wa Mungu ambaye alikuja kuwa Yesu sikuzote ametumikia kwa unyenyekevu kupatana na mapenzi ya Baba yake, na hajaribu kamwe kujitukuza mwenyewe. (Yoh. 5:41; 8:50) Ni mfano bora kama nini kwetu leo! Kama Yesu, na tuwe na mradi wa ‘kufanya mambo yote kwa utukufu wa Mungu.’—1 Kor. 10:31.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Baadhi ya vyeo hivyo au majina hayo yametajwa pamoja na neno la Kigiriki linaloonyesha wazi kwamba “kwa njia fulani ni ya ‘pekee,’” kama anavyosema msomi mmoja.

^ fu. 15 Kulingana na msomi mmoja wa Biblia, neno linalotafsiriwa “mara moja kwa wakati wote” linatoa wazo la maana sana la Kibiblia ambalo “linaonyesha kwamba kifo cha Kristo ni hakika, cha pekee, au hakina kifani.”

^ fu. 20 Hata ikiwa Wayahudi katika karne ya kwanza W.K. walifikiri kwamba walikuwa na kibali cha Mungu, kwa kuwa walikuwa watoto au wazao halisi wa Abrahamu, walitazamia kuja kwa mtu mmoja akiwa Masihi, au Kristo.—Yoh. 1:25; 7:41, 42; 8:39-41.

Je, Unakumbuka?

• Umejifunza nini kuhusu daraka la pekee la Yesu kutokana na vyeo au majina yake? (Ona sanduku.)

• Unaweza kuiga jinsi gani mfano wa Mwana wa pekee wa Yehova?

[Maswali ya Funzo]

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 15]

Vyeo Fulani Vinavyoonyesha Daraka la Pekee la Yesu Katika Kusudi la Mungu

Mwana Mzaliwa-Pekee. (Yoh. 1:3) Yesu tu ndiye aliyeumbwa moja kwa moja na Baba yake.

Neno. (Yoh. 1:14) Yehova anamtumia Mwana wake akiwa Msemaji wake ili kutoa habari na maagizo kwa viumbe wengine.

Amina. (Ufu. 3:14) Maisha ya Yesu yasiyo na kasoro hapa duniani, kutia ndani kifo chake cha kidhabihu, yalithibitisha na kufanya ahadi zote za Yehova Mungu zitimizwe.

Mpatanishi wa Agano Jipya. (1 Tim. 2:5, 6) Akiwa Mpatanishi wa kisheria, Yesu aliwezesha kuanzishwa kwa taifa jipya, “Israeli wa Mungu,” linalofanyizwa na Wakristo ambao watakuwa “ukuhani wa kifalme” wa kimbingu.—Gal. 6:16; 1 Pet. 2:9.

Kuhani Mkuu. (Ebr. 7:27, 28) Yesu alikuwa ndiye mwanadamu pekee ambaye angeweza kutoa dhabihu kamilifu, dhabihu ambayo haikuhitaji kutolewa tena na tena. Anaweza kusafisha dhambi zetu na kutuweka huru kutokana na kifo kinachosababishwa na dhambi.

Uzao Ulioahidiwa. (Mwa. 3:15) Ni mwanadamu mmoja tu, Yesu Kristo, ambaye ndiye sehemu ya msingi ya uzao huo uliotabiriwa. Wengine wote ambao baadaye walikuja kuwa sehemu ya pili ya uzao wa Abrahamu “ni wa Kristo.”—Gal. 3:29.