Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Hii Ndiyo Njia. Tembeeni Ndani Yake”

“Hii Ndiyo Njia. Tembeeni Ndani Yake”

“Hii Ndiyo Njia. Tembeeni Ndani Yake”

Simulizi la Maisha la Emilia Pederson

Limesimuliwa na Ruth E. Pappas

MAMA yangu, Emilia Pederson, alizaliwa mwaka wa 1878. Ingawa alikuwa mwalimu wa shule, alitaka sana kutumia maisha yake kuwasaidia watu wamkaribie Mungu. Ili kutimiza tamaa hiyo, Mama aliweka sanduku kubwa katika nyumba yetu katika mji mdogo wa Jasper, Minnesota, Marekani. Alipanga kutumia sanduku hilo kusafirisha vitu vyake mpaka China, ambako alitaka kutumikia akiwa mmishonari. Hata hivyo, mama yake alipokufa, alivunja mipango hiyo na kubaki nyumbani ili kuwatunza ndugu na dada zake wadogo. Mwaka wa 1907, aliolewa na Theodore Holien. Nilizaliwa Desemba 2, 1925 (2/12/1925) nikiwa mtoto wa mwisho. Tulikuwa watoto saba.

Mama alikuwa na maswali ya Biblia na alijitahidi sana kutafuta majibu yake. Swali moja lilihusu fundisho la kwamba waovu watateswa motoni. Alimuuliza msimamizi mmoja mgeni wa Kanisa la Kilutheri amwonyeshe maandiko ya Biblia yanayounga mkono fundisho hilo. Msimamizi huyo alimwambia kwamba yale ambayo Biblia inasema si ya maana, watu wanahitaji kufundishwa kuhusu moto wa mateso.

Njaa Yake ya Kiroho Ilitoshelezwa

Muda mfupi baada ya mwaka wa 1900, Emma, dada ya Mama alienda kujifunza muziki huko Northfield, Minnesota. Aliishi katika nyumba ya mwalimu wake, Milius Christianson, ambaye mke wake alikuwa Mwanafunzi wa Biblia, kama Mashahidi wa Yehova walivyoitwa wakati huo. Emma alitaja kwamba dada yake alipenda sana kusoma Biblia. Muda si muda, Bi. Christianson alimwandikia Mama barua ambayo ilijibu maswali yake ya Biblia.

Siku moja, Mwanafunzi wa Biblia anayeitwa Lora Oathout alikuja kwa gari la moshi kutoka Sioux Falls, South Dakota, ili kuhubiri huko Jasper. Mama alijifunza vitabu vya kujifunzia Biblia alivyopokea, na mwaka wa 1915, alianza kuwafundisha wengine kweli za Biblia, na kusambaza vitabu ambavyo Lora alimpa.

Mwaka wa 1916, Mama alisikia kwamba Charles Taze Russell angehudhuria kusanyiko katika Sioux City, Iowa. Mama alitaka kuhudhuria kusanyiko hilo. Kufikia wakati huo, Mama alikuwa na watoto watano, na yule mchanga zaidi, Marvin, alikuwa na umri wa miezi mitano tu. Hata hivyo, alisafiri pamoja na watoto wote kwa gari la moshi umbali wa kilomita 160 mpaka Sioux City ili kuhudhuria kusanyiko hilo. Alisikia hotuba za Ndugu Russell na kutazama sinema ya “Photo-Drama of Creation,” kisha akabatizwa. Aliporudi nyumbani, aliandika makala katika gazeti moja (Jasper Journal) kuhusu kusanyiko hilo.

Mwaka wa 1922, Mama alikuwa miongoni mwa watu 18,000 hivi waliohudhuria kusanyiko huko Cedar Point, Ohio. Baada ya kusanyiko hilo, hakuacha kamwe kutangaza kuhusu Ufalme wa Mungu. Mfano wake ulituchochea kutii himizo hili: “Hii ndiyo njia. Tembeeni ndani yake.”—Isa. 30:21.

Matokeo ya Huduma ya Ufalme

Mwanzoni mwa miaka ya 1920, wazazi wangu walihamia nyumba nyingine nje ya mji wa Jasper. Baba alikuwa na biashara iliyofanikiwa na familia kubwa ambayo alihitaji kuitunza. Hakujifunza Biblia sana kama Mama, lakini aliunga mkono kwa moyo wote kazi ya kuhubiri naye aliwakaribisha wahudumu wanaosafiri nyumbani kwetu. Mara nyingi, ndugu aliyesafiri alipotoa hotuba nyumbani kwetu, watu mia moja au zaidi, walihudhuria—walijaa sebuleni, katika chumba cha kulia chakula, na chumba chetu cha kulala.

Nilipokuwa na umri wa miaka saba hivi, shangazi yangu, Lettie, alipiga simu na kusema kwamba majirani wake, Ed Larson na mke wake, walitaka kujifunza Biblia. Walikubali mara moja kweli za Biblia na baadaye wakamwalika jirani mwingine, Martha Van Daalen, ambaye alikuwa mama mwenye watoto wanane, ajiunge nao katika funzo. Martha na familia yake yote wakawa pia Wanafunzi wa Biblia. *

Karibu wakati huo, Gordon Kammerud, mwanamume fulani kijana aliyeishi kilomita chache kutoka kwetu, alianza kufanya kazi na Baba. Gordon alikuwa ameonywa hivi: “Jihadhari na mabinti wa mkubwa wako wa kazi. Dini yao ni ya ajabu-ajabu.” Hata hivyo, Gordon alianza kujifunza Biblia na punde si punde akasadiki kwamba alikuwa amepata kweli. Miezi mitatu baadaye, alibatizwa. Wazazi wake pia wakawa waamini, na familia zetu, yaani, familia ya Holien, Kammerud, na ya Van Daalen, zikawa na urafiki wa karibu.

Alitiwa Nguvu na Makusanyiko

Mama alitiwa moyo sana na kusanyiko la Cedar Point hivi kwamba hakutaka kamwe kukosa kusanyiko lolote. Kwa hiyo, ninakumbuka kwamba nilipokuwa mtoto tulisafiri mbali sana ili kuhudhuria makusanyiko hayo. Kusanyiko la Columbus, Ohio, lililofanywa mwaka wa 1931 lilikuwa la pekee sana kwa sababu wakati huo ndipo tulipoanza kutumia jina Mashahidi wa Yehova. (Isa. 43:10-12) Ninakumbuka pia vizuri kusanyiko la Washington, D.C., la mwaka wa 1935, ambapo hotuba ya kihistoria ilitambulisha “mkutano mkubwa,” au “umati mkubwa,” unaotajwa katika Ufunuo. (Ufu. 7:9; Union Version) Dada zangu Lilian na Eunice walikuwa kati ya watu zaidi ya 800 waliobatizwa kwenye kusanyiko hilo.

Familia yetu ilisafiri na kuhudhuria makusanyiko huko Columbus, Ohio, mwaka wa 1937; Seattle, Washington, mwaka wa 1938; na New York City mwaka wa 1939. Familia ya Van Daalen na ya Kammerud na nyinginezo zilisafiri pamoja nasi, na tulipiga kambi njiani. Eunice aliolewa na Leo Van Daalen mwaka wa 1940, na wakawa mapainia. Mwaka huohuo, Lilian aliolewa na Gordon Kammerud, nao pia wakawa mapainia.

Kusanyiko la mwaka wa 1941 ambalo lilifanyiwa huko St. Louis, Missouri, lilikuwa la pekee. Kwenye kusanyiko hilo, maelfu ya vijana walipokea kitabu kinachoitwa Children (Watoto). Kusanyiko hilo lilibadili kabisa maisha yangu. Muda mfupi baadaye, mnamo Septemba 1, 1941, mimi, ndugu yangu Marvin na mke wake, Joyce, tukawa mapainia. Nilikuwa na umri wa miaka 15.

Katika maeneo yetu ya ukulima, ilikuwa vigumu kwa ndugu wote kuhudhuria makusanyiko kwa sababu mara nyingi yalifanywa wakati wa mavuno. Kwa hiyo, baada ya makusanyiko, tulizungumza kuhusu makusanyiko hayo nje ya nyumba yetu kwa faida ya wale ambao hawakuhudhuria. Pindi hizo zilifurahisha sana.

Migawo ya Gileadi na ya Nchi za Kigeni

Mnamo Februari (Mwezi wa 2) 1943, Shule ya Gileadi ilianzishwa ili kuwazoeza mapainia kwa ajili ya utumishi wa umishonari. Darasa la kwanza lilikuwa na washiriki sita wa familia ya Van Daalen, yaani, Emil, Arthur, Homer, na Leo; binamu yao Donald; na mke wa Leo, yaani, dada yangu Eunice. Tuliagana tukiwa na hisia mbalimbali, kwa kuwa hatukujua wakati ambapo tungewaona tena. Baada ya kuhitimu, wote sita walitumwa Puerto Riko, ambako kulikuwa na Mashahidi wa Yehova wasiozidi 12.

Baada ya mwaka mmoja, Lilian na Gordon na pia Marvin na Joyce walihudhuria darasa la tatu la Gileadi. Wao pia walitumwa Puerto Riko. Kisha, mnamo Septemba 1944, nilihudhuria darasa la nne la Gileadi nikiwa na umri wa 18. Baada ya kuhitimu mnamo Februari 1945, nilijiunga na ndugu na dada zangu huko Puerto Riko. Hilo lilikuwa jambo jipya kabisa maishani mwangu! Ingawa haikuwa rahisi kujifunza Kihispania, muda si muda baadhi yetu tulikuwa tukiongoza mafunzo ya Biblia zaidi ya 20 kila mmoja. Yehova alibariki kazi hiyo. Leo, kuna Mashahidi 25,000 hivi nchini Puerto Riko!

Msiba Wapata Familia Yetu

Leo na Eunice walibaki Puerto Riko baada ya mwana wao, Mark, kuzaliwa mwaka wa 1950. Mwaka wa 1952, walipanga kuchukua likizo ili kuwatembelea watu wa ukoo nyumbani. Mnamo Aprili 11, waliondoka kwa ndege. Jambo la kuhuzunisha ni kwamba muda mfupi baada ya ndege hiyo kupaa, ilianguka baharini. Leo na Eunice wakafa. Mark aliyekuwa na umri wa miaka miwili alipatikana akielea baharini. Mtu mmoja aliyeokoka alimrusha ndani ya mashua ya kuokolea, akampulizia hewa mdomoni, na hivyo akaendelea kuishi. *

Miaka mitano baadaye, mnamo Machi 7, 1957, Mama na Baba walikuwa wakienda kwenye Jumba la Ufalme wakati gurudumu la gari lao lilipopasuka. Walipokuwa wakibadili gurudumu hilo kando ya barabara, Baba aligongwa na gari lililokuwa likipita akafa papo hapo. Watu 600 hivi walihudhuria hotuba ya mazishi, na ushahidi mzuri ukatolewa katika eneo letu ambako Baba aliheshimiwa sana.

Migawo Mipya

Kabla ya Baba kufa, nilipokea mgawo wa kutumikia huko Argentina. Mnamo Agosti 1957, nilifika katika mji wa Mendoza chini ya Milima ya Andes. Mwaka wa 1958, George Pappas, aliyehitimu katika darasa la 30 la Gileadi alipewa mgawo wa kutumika nchini Argentina. Mimi na George tukawa marafiki wakubwa, na tulifunga ndoa Aprili 1960. Mwaka wa 1961, Mama alikufa akiwa na umri wa miaka 83. Alikuwa ametembea kwa uaminifu katika njia ya ibada ya kweli na aliwasaidia watu wengi kufanya vivyo hivyo.

Kwa miaka kumi, mimi na George tulitumikia pamoja na wamishonari wengine katika makao mbalimbali ya wamishonari. Kisha tulifanya kazi ya mzunguko kwa miaka saba. Mwaka wa 1975, tulirudi Marekani ili kuwasaidia washiriki wa familia yetu waliokuwa wagonjwa. Mwaka wa 1980, mume wangu aliombwa awe mwangalizi wa mzunguko katika eneo la Kihispania. Wakati huo kulikuwa na makutaniko ya Kihispania 600 hivi nchini Marekani. Kwa miaka 26, tulitembelea makutaniko mengi na tuliona hesabu ya makutaniko ikiongezeka kufikia makutaniko zaidi ya 3,000.

Wametembea Kwenye Ile “Njia”

Mama pia alifurahi kuona washiriki wachanga wa familia yetu wakiingia katika huduma ya wakati wote. Kwa mfano, Carol, binti ya dada yangu mkubwa, Ester, alianza kupainia mwaka wa 1953. Aliolewa na Dennis Trumbore, nao wamefanya huduma ya wakati wote tangu wakati huo. Lois, binti mwingine wa Ester, aliolewa na Wendell Jensen. Walihudhuria darasa la 41 la Gileadi na kutumikia kwa miaka 15 wakiwa wamishonari huko Nigeria. Mark, ambaye wazazi wake walikufa katika msiba wa ndege, alilelewa na dada ya Leo, Ruth La Londe, na mume wake, Curtiss. Mark na mke wake, Lavonne, walifanya upainia kwa miaka mingi na kuwalea watoto wao wanne katika ile “njia.”—Isa. 30:21.

Orlen, ndugu yangu wa pekee ambaye yuko hai, ana umri wa miaka 90 na kitu. Angali anamtumikia Yehova kwa uaminifu. Mimi na George tunaendelea kwa shangwe katika huduma ya wakati wote.

Kile Ambacho Mama Aliacha

Sasa nina kitu fulani ambacho Mama alithamini sana, yaani, meza yake. Baba yangu alimpa meza hiyo kama zawadi ya arusi. Kabati moja la meza hiyo lina kitabu cha Mama cha zamani, ambacho kina barua na makala za magazeti zilizochapishwa ambazo aliandika, na zilitoa ushahidi mzuri sana kuhusu Ufalme. Baadhi ya makala hizo ni za mwanzoni mwa miaka ya 1900. Meza hiyo pia ina barua za maana sana ambazo Mama aliandikiwa na watoto wake wamishonari. Jinsi ninavyofurahia kuzisoma tena na tena! Na sikuzote barua alizotuandikia zilitutia moyo sana, zilijaa mambo yenye kujenga. Tamaa ya Mama ya kuwa mmishonari haikutimia kamwe. Hata hivyo, bidii aliyokuwa nayo kwa ajili ya utumishi wa umishonari ilichochea mioyo ya wengine kwa vizazi vingi vilivyoishi baada yake. Ninatazamia kwa hamu kama nini wakati familia yetu itakapokutana na Mama na Baba katika paradiso duniani!—Ufu. 21:3, 4.

[Maelezo ya chini]

^ fu. 13 Simulizi la maisha la Emil H. Van Daalen liko katika gazeti la Mnara wa Mlinzi, la Kiingereza la Juni 15, 1983 (15/6/1983), ukurasa wa 27-30 au la Kifaransa la Septemba 15, 1983 (15/9/1983), ukurasa wa 27-30.

^ fu. 24 Ona Amkeni! la Kiingereza la Juni 22, 1952, ukurasa wa 3-4.

[Picha katika ukurasa wa 17]

Emilia Pederson

[Picha katika ukurasa wa 18]

Mwaka wa 1916: Mama, Baba (akiwa amembeba Marvin); chini, kushoto kwenda kulia: Orlen, Ester, Lilian, Mildred

[Picha katika ukurasa wa 19]

Leo na Eunice, muda mfupi kabla ya kufa

[Picha katika ukurasa wa 20]

Mwaka wa 1950: Kushoto kwenda kulia, juu: Ester, Mildred, Lilian, Eunice, Ruth; chini: Orlen, Mama, Baba, na Marvin

[Picha katika ukurasa wa 20]

George na Ruth Pappas katika kazi ya mzunguko, mwaka wa 2001