Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Wewe Ni ‘Msimamizi-nyumba wa Fadhili Zisizostahiliwa za Mungu’?

Je, Wewe Ni ‘Msimamizi-nyumba wa Fadhili Zisizostahiliwa za Mungu’?

Je, Wewe Ni ‘Msimamizi-nyumba wa Fadhili Zisizostahiliwa za Mungu’?

“Katika upendo wa kindugu iweni na upendo mwororo kwa mtu na mwenzake. Katika kuonyeshana heshima iweni wa kwanza.”—ROM. 12:10.

1. Neno la Mungu linatuhakikishia nini?

NENO LA MUNGU linatuhakikishia tena na tena kwamba Yehova atatusaidia tukivunjika moyo au kushuka moyo. Kwa mfano, angalia maneno haya yenye kufariji: “Yehova anawategemeza wote wanaoanguka, naye anawainua wote ambao wameinama chini.” “Anawaponya wenye mioyo iliyovunjika, naye anafunga sehemu zao zenye maumivu.” (Zab. 145:14; 147:3) Zaidi ya hayo, Baba yetu wa mbinguni anasema hivi: “Mimi, Yehova Mungu wako, ninaushika mkono wako wa kuume, Mwenye kukuambia, ‘Usiogope. Mimi mwenyewe nitakusaidia.’”—Isa. 41:13.

2. Yehova anawategemeza watumishi wake jinsi gani?

2 Hata hivyo, Yehova ambaye anakaa katika mbingu zisizoonekana ‘anaushika mkono wetu’ jinsi gani? ‘Anatuinua’ namna gani ‘tunapoinama’ kwa sababu ya taabu? Yehova Mungu anatutegemeza kwa njia mbalimbali. Kwa mfano, anawapa watu wake “nguvu zinazopita zile za kawaida” kupitia roho yake takatifu. (2 Kor. 4:7; Yoh. 14:16, 17) Watumishi wa Mungu wanainuliwa pia na ujumbe ulio katika Neno la Mungu, Biblia, ambayo iliandikwa kwa mwongozo wa roho yake. (Ebr. 4:12) Je, kuna njia nyingine ambayo Yehova anatumia kutuimarisha? Swali hilo linajibiwa na kitabu cha Kwanza cha Petro.

‘Fadhili Zisizostahiliwa za Mungu Zinaonyeshwa kwa Njia Mbalimbali’

3. (a) Mtume Petro anasema nini kuhusu majaribu? (b) Ni jambo gani linalozungumziwa katika sehemu ya mwisho ya barua ya kwanza ya Petro?

3 Mtume Petro anapowaandikia waamini watiwa-mafuta, anasema kwamba wana sababu nzuri za kushangilia kwa sababu watapata thawabu kubwa. Kisha anaongeza hivi: “Ingawa kwa muda kidogo sasa, ikiwa ni lazima, mmehuzunishwa na majaribu ya namna mbalimbali.” (1 Pet. 1:1-6) Ona neno “mbalimbali.” Neno hilo linaonyesha kwamba majaribu yatakuwa tofauti-tofauti. Hata hivyo, Petro hakomei hapo na kuwaacha akina ndugu wakijiuliza ikiwa wataweza kuvumilia majaribu hayo ya namna mbalimbali. Badala yake, Petro anasema kuwa Wakristo wanaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atawasaidia kuvumilia kila jaribu wanalokabili, hata liwe la aina gani. Sehemu ya mwisho ya barua ya Petro inatoa uhakikishio huo, na katika sehemu hiyo mtume Petro anazungumza kuhusu “mwisho wa mambo yote.”—1 Pet. 4:7.

4. Kwa nini maneno ya 1 Petro 4:10 yanatufariji?

4 Petro anasema: “Kwa kadiri ambayo kila mmoja amepokea zawadi, itumieni katika kuhudumiana kama wasimamizi-nyumba wazuri wa fadhili zisizostahiliwa za Mungu zinazoonyeshwa kwa njia mbalimbali.” (1 Pet. 4:10) Petro anatumia tena neno “mbalimbali.” Ni kana kwamba anasema, ‘Majaribu yanakuja kwa njia nyingi mbalimbali, lakini Mungu anaonyesha fadhili zisizostahiliwa kwa njia nyingi mbalimbali pia.’ Kwa nini maneno hayo yanafariji? Yanamaanisha kwamba hata tupate jaribu la namna gani, sikuzote Mungu atatuonyesha fadhili zisizostahiliwa za kutusaidia kuvumilia jaribu hilo. Hata hivyo, je, uliona Petro anasema tunaonyeshwa fadhili zisizostahiliwa za Yehova kwa njia gani? Kupitia Wakristo wenzetu.

“Kuhudumiana”

5. (a) Kila Mkristo anapaswa kufanya nini? (b) Ni maswali gani yanayotokea?

5 Petro anawaambia hivi washiriki wote wa kutaniko la Kikristo: “Zaidi ya mambo yote, iweni na upendo mkubwa ninyi kwa ninyi.” Halafu anaongeza hivi: “Kwa kadiri ambayo kila mmoja amepokea zawadi, itumieni katika kuhudumiana.” (1 Pet. 4:8, 10) Kwa hiyo, kila mtu katika kutaniko anapaswa kushiriki katika kuwajenga Wakristo wenzake. Tumekabidhiwa kitu cha thamani sana ambacho ni mali ya Yehova, nasi tuna wajibu wa kuwagawia wengine. Ni nini ambacho tumekabidhiwa? Petro anasema kwamba ni “zawadi.” Ni zawadi gani hiyo? ‘Tunaitumia jinsi gani kuhudumiana’?

6. Wakristo wamekabidhiwa zawadi gani?

6 Neno la Mungu linasema hivi: “Kila zawadi njema na kila tuzo kamilifu hutoka juu.” (Yak. 1:17) Kwa kweli, zawadi zote ambazo Yehova anawapa watu wake zinaonyesha fadhili zake zisizostahiliwa. Zawadi moja ya pekee ambayo Yehova anatupa ni roho takatifu. Zawadi hiyo inatuwezesha kusitawisha sifa za kimungu kama vile upendo, wema, na upole. Sifa hizo zinatuchochea kuwapenda waamini wenzetu kutoka moyoni na kuwa tayari kuwategemeza. Hekima ya kweli na ujuzi ni kati ya zawadi nzuri ambazo roho takatifu inatuwezesha kupata. (1 Kor. 2:10-16; Gal. 5:22, 23) Kwa kweli, nguvu, uwezo, na vipawa vyetu vyote vinaweza kuonwa kuwa zawadi ambazo tunapaswa kuzitumia kumletea sifa na heshima Baba yetu wa mbinguni. Mungu ametupa wajibu wa kutumia uwezo na sifa zetu ili kuwaonyesha waamini wenzetu fadhili zisizostahiliwa za Mungu.

“Itumieni Katika Kuhudumiana”—Jinsi Gani?

7. (a) Maneno “kwa kadiri” yanamaanisha nini? (b) Tunapaswa kujiuliza maswali gani, na kwa nini?

7 Petro anasema hivi pia kuhusu zawadi ambazo tumepokea: “Kwa kadiri ambayo kila mmoja amepokea zawadi, itumieni.” Maneno “kwa kadiri” yanaonyesha kwamba tunaweza kuwa na sifa na uwezo tofauti-tofauti na pia kwa viwango mbalimbali. Hata hivyo, kila mmoja anahimizwa ‘aitumie [yaani, atumie zawadi yoyote aliyo nayo] katika kuhudumiana.’ Kwa kuongezea, maneno “itumieni . . . kama wasimamizi-nyumba wazuri” ni amri. Kwa hiyo, tunapaswa kujiuliza hivi: ‘Je, kweli ninatumia zawadi ambazo nimekabidhiwa kuwatia nguvu waamini wenzangu?’ (Linganisha na 1 Timotheo 5:9, 10.) ‘Au ninatumia uwezo ambao nilipewa na Yehova ili kujifaidi mwenyewe tu—labda kupata utajiri au cheo?’ (1 Kor. 4:7) Tukitumia zawadi zetu “katika kuhudumiana,” tutampendeza Yehova.—Met. 19:17; soma Waebrania 13:16.

8, 9. (a) Wakristo ulimwenguni pote wanawahudumia waamini wenzao katika njia gani mbalimbali? (b) Ndugu na dada katika kutaniko lenu wanasaidiana jinsi gani?

8 Neno la Mungu linataja njia mbalimbali ambazo kupitia hizo Wakristo wa karne ya kwanza walihudumiana. (Soma Waroma 15:25, 26; 2 Timotheo 1:16-18.) Vivyo hivyo leo, Wakristo wa kweli wanafuata kwa moyo wote amri ya kutumia zawadi zao kuwahudumia waamini wenzao. Angalia jinsi wanavyofanya hivyo.

9 Ndugu wengi wanatumia saa nyingi kila mwezi kutayarisha sehemu za mikutano. Maneno ya busara wanayosema katika mikutano wanapoeleza hazina fulani za kiroho walizopata katika funzo lao la Biblia yanawachochea wote kutanikoni wavumilie. (1 Tim. 5:17) Ndugu na dada wengi wanajulikana kwa sababu ya uchangamfu wao na jinsi wanavyowahurumia waamini wenzao. (Rom. 12:15) Wengine wanawatembelea kwa ukawaida wale walioshuka moyo na kusali pamoja nao. (1 The. 5:14) Wengine wanawajali Wakristo wenzao ambao wanakabili jaribu kwa kuwaandikia maneno yenye kutia moyo. Na kwa fadhili, wengine wanawasaidia wale wenye udhaifu wa kimwili kuhudhuria mikutano ya kutaniko. Maelfu ya Mashahidi wanashiriki katika kazi ya kutoa misaada na kuwasaidia waamini wenzao kujenga upya nyumba ambazo zimeharibiwa na misiba ya asili. Upendo mwororo na msaada unaotolewa na ndugu na dada hao wenye kujali unaonyesha “fadhili zisizostahiliwa za Mungu zinazoonyeshwa kwa njia mbalimbali.”—Soma 1 Petro 4:11.

Ni Jambo Gani Lililo la Maana Zaidi?

10. (a) Paulo alihangaikia sehemu gani mbili za utumishi wake kwa Mungu? (b) Tunamwiga Paulo leo jinsi gani?

10 Watumishi wa Mungu hawajakabidhiwa tu zawadi ya kuwahudumia waamini wenzao bali pia wamekabidhiwa ujumbe wa kuwatangazia wanadamu wenzao. Mtume Paulo alitambua sehemu hizo mbili za utumishi wake kwa Yehova. Aliliandikia kutaniko la Efeso kuhusu “usimamizi-nyumba wa fadhili zisizostahiliwa za Mungu” ambao alipewa kwa faida yao. (Efe. 3:2) Hata hivyo, alisema pia hivi: “Tumethibitishwa na Mungu kuwa tunafaa kukabidhiwa habari njema.” (1 The. 2:4) Kama Paulo, sisi pia tunatambua kwamba tumekabidhiwa mgawo wa kutumikia tukiwa wahubiri wa Ufalme wa Mungu. Tunaposhiriki kwa bidii katika kazi ya kuhubiri, tunajitahidi kumwiga Paulo ambaye alitangaza habari njema bila kuchoka. (Mdo. 20:20, 21; 1 Kor. 11:1) Tunajua kwamba kuhubiri ujumbe wa Ufalme kunaweza kuokoa uhai. Hata hivyo, tunajitahidi pia kumwiga Paulo kwa kutafuta nafasi za ‘kuwapa waamini wenzetu sehemu ya zawadi ya kiroho.’—Soma Waroma 1:11, 12; 10:13-15.

11. Tunapaswa kuwa na maoni gani kuhusu mgawo wetu wa kuhubiri na wa kuwajenga ndugu zetu?

11 Ni utendaji gani ulio wa maana zaidi kati ya sehemu hizo mbili za utendaji wa Kikristo? Kuuliza swali hilo ni kama kuuliza hivi kumhusu ndege, Ni ubawa gani kati ya mabawa yake mawili ulio wa maana zaidi? Jibu ni wazi. Ndege anahitaji kutumia mabawa yote mawili ili aruke vizuri. Vivyo hivyo, tunahitaji kushiriki katika sehemu zote mbili za utumishi wetu kwa Mungu ili tuwe Wakristo kamili. Kwa hiyo, badala ya kufikiri kwamba mgawo wetu wa kuhubiri habari njema hauhusiani na mgawo wa kuwajenga waamini wenzetu, tunapaswa kuona kwamba migawo hiyo inakamilishana, kama mtume Petro na Paulo walivyoiona. Jinsi gani?

12. Tunatumiwa na Yehova kwa njia gani?

12 Tukiwa waeneza-injili, tunatumia uwezo wowote wa kufundisha tulio nao ili kujaribu kugusa mioyo ya wanadamu wenzetu kwa ujumbe wenye kutia moyo wa Ufalme wa Mungu. Kwa njia hiyo, tunatumaini kwamba tutawasaidia wawe wanafunzi wa Kristo. Hata hivyo, tunatumia pia uwezo wowote na zawadi nyingine ambazo huenda tunazo kujitahidi kuwatia moyo waamini wenzetu kwa maneno yenye kujenga na kuwasaidia kwa matendo na hivyo kuwaonyesha fadhili zisizostahiliwa za Mungu. (Met. 3:27; 12:25) Tukifanya hivyo, tunatumaini kwamba tutawasaidia waendelee kuwa wanafunzi wa Kristo. Katika utendaji wote huo, yaani, tunapowahubiria watu na “kuhudumiana,” tuna pendeleo zuri ajabu la kutumiwa na Yehova.—Gal. 6:10.

“Iweni na Upendo Mwororo kwa Mtu na Mwenzake”

13. Matokeo yatakuwa nini tukikosa “kuhudumiana”?

13 Paulo aliwahimiza hivi waamini wenzake: “Katika upendo wa kindugu iweni na upendo mwororo kwa mtu na mwenzake. Katika kuonyeshana heshima iweni wa kwanza.” (Rom. 12:10) Kwa kweli, kuwapenda ndugu zetu kunatuchochea kutumikia kwa moyo wote tukiwa wasimamizi-nyumba wa fadhili zisizostahiliwa za Mungu. Tunatambua kwamba Shetani akifanikiwa kutuzuia ‘tusihudumiane,’ atadhoofisha umoja wetu. (Kol. 3:14) Na tukikosa umoja, hatutashiriki kwa bidii katika kazi ya kuhubiri. Shetani anajua vizuri kwamba anahitaji kuvunja ubawa wetu mmoja wa mfano ili tushindwe kutimiza madaraka yetu.

14. Ni nani wanaofaidika ‘tunapohudumiana’? Toa mfano.

14 “Kuhudumiana” hakuwafaidi tu wale wanaopokea fadhili zisizostahiliwa za Mungu bali pia wale wanaozionyesha. (Met. 11:25) Kwa mfano, wafikirie Ryan na Roni, wenzi wa ndoa wanaoishi Illinois, Marekani. Walipopata habari kwamba Kimbunga cha Katrina kilikuwa kimeharibu mamia ya nyumba za Mashahidi wenzao, upendo wa kindugu uliwachochea kuacha kazi zao na nyumba yao, wakanunua gari kubwa, wakalirekebisha, na kusafiri umbali wa kilomita 1,400 mpaka Louisiana. Waliishi huko kwa zaidi ya mwaka mmoja wakitumia wakati, nguvu, na mali yao kuwasaidia ndugu zao. Ryan mwenye umri wa miaka 29 anasema hivi: “Kushiriki katika kazi ya kutoa misaada kulinifanya nimkaribie Mungu zaidi. Niliona jinsi Yehova anavyowatunza watu wake.” Ryan anaongeza hivi: “Kufanya kazi na ndugu wazee kwa umri kulinifunza mengi kuhusu jinsi ya kuwatunza akina ndugu. Nilijifunza pia kwamba sisi vijana tuna mengi ya kufanya katika tengenezo la Yehova.” Roni, mwenye umri wa miaka 25, anasema: “Ninashukuru sana kwa sababu nilishiriki katika kuwasaidia wengine. Sijawahi kamwe kuwa na furaha nyingi hivyo katika maisha yangu yote. Ninajua kwamba katika miaka inayokuja, pendeleo hilo zuri litaendelea kuninufaisha.”

15. Tuna sababu gani nzuri za kuendelea kutumikia tukiwa wasimamizi-nyumba wa fadhili zisizostahiliwa za Mungu?

15 Kwa kweli, kutii amri za Mungu za kuhubiri habari njema na kuwajenga waamini wenzetu kunaleta baraka kwa wote. Watu wapya tunaowasaidia wanatiwa nguvu kiroho, nasi tunapata shangwe ya moyoni ambayo inapatikana tu kwa kutoa. (Mdo. 20:35) Kwa ujumla, kutaniko linakuwa na uchangamfu zaidi kadiri kila mshiriki anavyowajali wengine kwa upendo. Zaidi ya hayo, upendo ambao tunaonyeshana unatutambulisha waziwazi kuwa Wakristo wa kweli. Yesu alisema: “Kwa jambo hili wote watajua kwamba ninyi ni wanafunzi wangu, mkiwa na upendo kati yenu wenyewe.” (Yoh. 13:35) Zaidi ya yote, Baba yetu mwenye kujali, Yehova, anapata sifa kwa sababu watumishi wake duniani wanaonyesha tamaa yake ya kuwatia nguvu wenye uhitaji. Kwa hiyo, tuna sababu nzuri kama nini za kutumia zawadi yetu “kuhudumiana kama wasimamizi-nyumba wazuri wa fadhili zisizostahiliwa za Mungu”! Je, utaendelea kufanya hivyo?—Soma Waebrania 6:10.

Je, Unakumbuka?

• Yehova anawatia nguvu watumishi wake katika njia gani?

• Tumekabidhiwa nini?

• Taja njia fulani ambazo tunaweza kuwatumikia waamini wenzetu.

• Ni nini kitakachotuchochea kuendelea kutumia zawadi yetu katika “kuhudumiana”?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 13]

Je, unatumia “zawadi” yako kuwatumikia wengine au kujipendeza mwenyewe?

[Picha katika ukurasa wa 15]

Tunawahubiria wengine habari njema na kuwategemeza Wakristo wenzetu

[Picha katika ukurasa wa 16]

Wafanyakazi wa kujitolea wanastahili kupongezwa kwa sababu ya roho yao ya kujidhabihu