Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Ufunuo—I

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Ufunuo—I

Neno la Yehova Liko Hai

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Ufunuo—I

AKIWA kifungoni katika kisiwa cha Patmo, mtume Yohana aliyezeeka, anaandika maono 16. Katika maono hayo, anaona mambo ambayo Yehova Mungu na Yesu Kristo wanatimiza katika siku ya Bwana—kipindi kinachoanza wakati Ufalme wa Mungu unaposimamishwa mbinguni mwaka wa 1914 na kuendelea mpaka mwisho wa Utawala wa Yesu wa Miaka Elfu. Kitabu cha Ufunuo, kilichoandikwa na Yohana karibu mwaka wa 96 W.K., kinasimulia maono hayo kwa njia yenye kusisimua.

Acheni sasa tuchunguze mambo makuu katika Ufunuo 1:1–12:17. Sura hizo zinaeleza maono saba ya kwanza ambayo Yohana alipokea. Tunapendezwa na maono hayo kwa sababu yanahusu mambo yanayotukia ulimwenguni sasa na yanaonyesha jinsi Yehova atakavyochukua hatua hivi karibuni. Wale wanaosoma masimulizi ya maono hayo kwa imani, wanafarijiwa na kutiwa moyo sana.—Ebr. 4:12.

“MWANA-KONDOO” ANAFUNGUA MIHURI SITA KATI YA ILE MIHURI SABA

(Ufu. 1:1–7:17)

Kwanza, Yohana anamwona Yesu Kristo aliyetukuzwa, naye anapokea ujumbe mbalimbali ambao anapaswa ‘kuuandika katika kitabu cha kukunjwa kisha autume kwa yale makutaniko saba.’ (Ufu. 1:10, 11) Halafu Yohana anapokea maono kuhusu kiti cha ufalme kikiwa mahali pake mbinguni. Yule aliyeketi juu ya kiti hicho cha ufalme ameshika katika mkono wake wa kuume kitabu cha kukunjwa kilichofungwa kwa mihuri saba. “Simba ambaye ni wa kabila la Yuda,” au ‘mwana-kondoo aliye na pembe saba na macho saba,’ ndiye “anayestahili kukifungua kile kitabu cha kukunjwa.”—Ufu. 4:2; 5:1, 2, 5, 6.

Maono ya tatu yanafunua kinachotukia wakati “Mwana-Kondoo” anapofungua mihuri sita ya kwanza, mmoja baada ya mwingine. Muhuri wa sita unapofunguliwa, tetemeko kubwa la nchi linatokea na siku kuu ya ghadhabu inafika. (Ufu. 6:1, 12, 17) Lakini maono yanayofuata yanaonyesha ‘malaika wanne wamezishika sana zile pepo nne za dunia’ mpaka kazi ya kuwatia muhuri wale 144,000 iwe imekamilika. “Umati mkubwa” wa wale ambao hawajatiwa muhuri unaonekana ‘ukiwa umesimama mbele ya kiti cha ufalme na mbele ya Mwana-Kondoo.’—Ufu. 7:1, 9.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

1:4; 3:1; 4:5; 5:6—Maneno “zile roho saba” yanamaanisha nini? Namba saba inamaanisha ukamili kwa maoni ya Mungu. Hivyo, kwa ujumla, ujumbe kwa “yale makutaniko saba” unawahusu watu wote wa Mungu wanaokutanika pamoja katika makutaniko zaidi ya 100,000 duniani pote. (Ufu. 1:11, 20) Kwa kuwa Yehova anatoa roho takatifu kulingana na kile anachotaka kutimiza, maneno “zile roho saba” yanaonyesha kwamba inatumika kikamili kuwasaidia wale wanaosikiliza kwa makini unabii huu ili wauelewe na kupata baraka. Inaonekana kwamba katika masimulizi ya kitabu cha Ufunuo, namba saba inarudiwa-rudiwa. Katika masimulizi hayo, namba saba inamaanisha ukamili, na kwa kweli, kitabu hicho kinazungumzia jinsi ‘ile siri takatifu ya Mungu itakavyomalizika,’ au kukamilishwa.—Ufu. 10:7.

1:8, 17—Majina ya cheo “Alfa na Omega” na “wa Kwanza na wa Mwisho” yanamhusu nani? Jina la cheo “Alfa na Omega” linamhusu Yehova, nalo linakazia kwamba hakukuwa na Mungu mweza-yote kabla yake wala hakutakuwa na mwingine baada yake. Yeye ndiye “mwanzo na mwisho.” (Ufu. 21:6; 22:13) Yehova anatajwa kuwa “wa kwanza na wa mwisho” katika Ufunuo 22:13, kumaanisha kwamba hakuna mwingine aliyekuwapo kabla yake wala hakutakuwa na mwingine baada yake. Hata hivyo, mistari mingine katika sura ya kwanza ya Ufunuo inaonyesha kwamba katika sura hiyo ya kwanza, jina la cheo “wa Kwanza na wa Mwisho” linamhusu Yesu Kristo. Yeye ndiye mwanadamu wa kwanza kufufuliwa kwenye uhai wa roho usioweza kufa, naye ndiye wa mwisho kufufuliwa kwa njia hiyo na Yehova mwenyewe.—Kol. 1:18.

2:7—“Paradiso ya Mungu” ni nini? Kwa kuwa Wakristo watiwa-mafuta ndio wanaoambiwa maneno hayo, paradiso hiyo inamaanisha makao ya mbinguni yaliyo kama paradiso, yaani, kuwapo kwa Mungu mwenyewe. Watiwa-mafuta waaminifu watapata thawabu ya kula “matunda kutokana na ule mti wa uzima.” Watapokea kutoweza kufa.—1 Kor. 15:53.

3:7—Ni wakati gani ambapo Yesu alipokea “ufunguo wa Daudi,” naye amekuwa akiutumia kufanya nini? Yesu alipobatizwa mwaka wa 29 W.K., alipata kuwa Mfalme Aliyechaguliwa wa ukoo wa Daudi. Hata hivyo, Yesu hakupokea ufunguo huo wa Daudi mpaka mwaka wa 33 W.K. alipoinuliwa kwenye mkono wa kuume wa Mungu huko mbinguni. Akiwa huko, alirithi haki zote za Ufalme wa Daudi. Tangu wakati huo, Yesu ameutumia ufunguo huo kuwafungulia wengine mapendeleo yanayohusiana na Ufalme. Mwaka wa 1919, Yesu ‘aliuweka ufunguo wa nyumba ya Daudi’ juu ya bega la “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” kwa kumweka rasmi mtumwa huyo “juu ya mali zake zote.”—Isa. 22:22; Mt. 24:45, 47.

3:12—‘Jina jipya’ la Yesu linamaanisha nini? Jina hilo linahusiana na cheo kipya na mapendeleo mapya ya Yesu. (Flp. 2:9-11) Ingawa hakuna yeyote anayepata kulijua jina hilo kama Yesu anavyolijua, Yesu analiandika juu ya ndugu zake waaminifu katika makao ya mbinguni, na kwa kufanya hivyo anakuwa na uhusiano wa karibu pamoja nao. (Ufu. 19:12) Hata wanapokea pia mapendeleo fulani ambayo Yehova anampa Yesu.

Mambo Tunayojifunza:

1:3. Kwa kuwa “wakati uliowekwa [wa kutekelezwa kwa hukumu za Mungu juu ya ulimwengu wa Shetani] uko karibu,” tunahitaji kufanya haraka kuelewa ujumbe wa kitabu cha Ufunuo na kuutii.

3:17, 18. Ili tuwe matajiri kiroho, tunahitaji kununua kutoka kwa Yesu “dhahabu iliyosafishwa kwa moto.” Yaani, tunapaswa kujitahidi kuwa matajiri katika matendo mazuri. (1 Tim. 6:17-19) Pia tunahitaji kuvaa “mavazi meupe ya nje,” ambayo yanaonyesha wazi sisi ni wafuasi wa Kristo, na tunapaswa kutumia “dawa ya macho,” kama vile mashauri yanayochapishwa katika gazeti la Mnara wa Mlinzi, ili tuwe na utambuzi wa kiroho.—Ufu. 19:8.

7:13, 14. Wale wazee 24 wanawakilisha wale 144,000 wakiwa katika utukufu wao mbinguni, ambako wanatumika wakiwa wafalme na pia makuhani. Walifananishwa na makuhani wa Israeli la kale, ambao Mfalme Daudi aliwapanga katika migawanyo 24. Mmoja wa wazee hao anamfunulia Yohana utambulisho wa umati mkubwa. Kwa hiyo, lazima ufufuo wa Wakristo watiwa-mafuta uwe ulianza muda fulani kabla ya mwaka wa 1935. Kwa nini? Kwa sababu mwaka huo watumishi wa Mungu watiwa-mafuta waliokuwa duniani walijulishwa umati mkubwa ni akina nani hasa.—Luka 22:28-30; Ufu. 4:4; 7:9.

KUFUNGULIWA KWA MUHURI WA SABA KWAFANYA TARUMBETA SABA ZIPIGWE

(Ufu. 8:1–12:17)

Mwana-kondoo anafungua muhuri wa saba. Malaika saba wanapokea tarumbeta saba. Malaika sita wanapiga tarumbeta zao na kutangaza ujumbe wa hukumu juu ya sehemu “ya tatu” ya wanadamu—dini zinazodai kuwa za Kikristo. (Ufu. 8:1, 2, 7-12; 9:15, 18) Hayo ndiyo mambo ambayo Yohana anaona katika maono ya tano. Akishiriki katika maono yanayofuata, Yohana anakula kitabu kidogo cha kukunjwa na kupima patakatifu pa hekalu. Baada ya kupigwa kwa tarumbeta ya saba, sauti kubwa zinatangaza: “Ufalme wa ulimwengu umekuwa ufalme wa Bwana wetu na wa Kristo wake.”—Ufu. 10:10; 11:1, 15.

Maono ya saba yanafafanua mambo yanayotajwa katika Ufunuo 11:15, 17. Ishara kubwa inaonekana mbinguni. Mwanamke wa kimbingu anazaa mtoto wa kiume. Ibilisi anatupwa kutoka mbinguni. Akiwa na ghadhabu kumwelekea yule mwanamke wa kimbingu, Ibilisi anaenda zake ‘kupigana vita na wale waliobaki wa uzao wa mwanamke huyo.’—Ufu. 12:1, 5, 9, 17.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

8:1-5—Kwa nini kimya kilitokea mbinguni, na ni nini kilichotupwa duniani? Kimya cha mfano kilitokea mbinguni ili “sala za watakatifu” duniani ziweze kusikilizwa. Jambo hilo lilitukia mwishoni mwa vita vya kwanza vya ulimwengu. Wakristo watiwa-mafuta hawakwenda mbinguni mwishoni mwa Nyakati za Mataifa, kama vile wengi walivyotazamia. Walikabili hali ngumu wakati wa vita. Kwa hiyo, walisali kwa bidii ili wapate mwongozo. Kwa sababu ya sala zao, malaika alitupa duniani moto wa mfano ambao uliwachochea Wakristo hao watiwa-mafuta kushiriki kwa bidii katika utendaji wa kiroho. Ingawa walikuwa wachache, walianza kampeni ya kuhubiri ulimwenguni pote ambayo ilifanya Ufalme wa Mungu uwe suala moto, na hivyo kuwasha moto katika dini zinazodai kuwa za Kikristo. Maonyo makali kutoka katika Biblia yalitangazwa, kweli ya Biblia ikajulishwa, na misingi ya dini ya uwongo ikatikiswa, kama majengo yanavyotikiswa na tetemeko la nchi.

8:6-12; 9:1, 13; 11:15—Wale malaika saba walijitayarisha lini kupiga tarumbeta zao, na tarumbeta hizo zilipigwa jinsi gani na wakati gani? Kujitayarisha kupiga zile tarumbeta saba kulitia ndani kutoa mwongozo kwa washiriki waliotiwa nguvu mpya wa jamii ya Yohana duniani kuanzia mwaka wa 1919 hadi 1922. Jamii hiyo ilikuwa imetiwa nguvu mpya. Wakati huo watiwa-mafuta walikuwa na kazi nyingi ya kupanga upya kazi ya kuhubiri na kujenga viwanda vya uchapishaji. (Ufu. 12:13, 14) Kupigwa kwa tarumbeta kunamaanisha kutangaza kwa ujasiri hukumu za Yehova juu ya ulimwengu wa Shetani. Kazi hiyo inayofanywa na watu wa Mungu wakishirikiana na malaika, ilianza hasa wakati wa kusanyiko la Cedar Point, Ohio, mwaka wa 1922 na itaendelea mpaka wakati wa dhiki kuu.

8:13; 9:12; 11:14—Mipigo ya tarumbeta tatu za mwisho ni “ole” katika njia gani? Ingawa mipigo ya tarumbeta nne za kwanza ni matangazo yanayofunua kwamba dini zinazodai kuwa za Kikristo zimekufa kiroho, mipigo mitatu ya mwisho ni ole kwa sababu inahusu matukio hususa. Mpigo wa tano unahusiana na kuachiliwa kwa watu wa Mungu kutoka “abiso” ya kutotenda mwaka wa 1919, na pia kazi yao ya kuhubiri kwa bidii, ambayo ilikuwa kama tauni yenye kutesa dini zinazodai kuwa za Kikristo. (Ufu. 9:1) Mpigo wa sita unahusu shambulio kubwa zaidi katika historia yote la askari wapanda-farasi, na pia kampeni ya kuhubiri ulimwenguni pote iliyoanza mwaka wa 1922. Mpigo wa mwisho unahusu kuzaliwa kwa Ufalme wa Kimasihi.

Mambo Tunayojifunza:

9:10, 19. Ujumbe wenye nguvu kutoka katika Biblia ambao unachapishwa katika vichapo vya “mtumwa mwaminifu na mwenye busara,” unauma. (Mt. 24:45) Ujumbe huo unalingana na mikia ya nzige ambayo ina “miiba kama nge” na unafananishwa na askari-jeshi wapanda-farasi, ambao “mikia yao ni kama nyoka.” Kwa nini? Kwa sababu vichapo hivyo vinaonya juu ya ‘siku ya kisasi ya Yehova.’ (Isa. 61:2) Na tuvisambaze kwa ujasiri na bidii.

9:20, 21. Watu wengi wapole wanaoishi katika mataifa yanayodai kuwa si ya Kikristo wamekubali ujumbe tunaotangaza. Hata hivyo, hatutazamii watu wengi sana wa dini zisizo za Kikristo, ambao wanatajwa kuwa “wale wanadamu wengine,” wakubali ujumbe wetu. Ingawa hivyo, tunaendelea na kazi ya kuhubiri.

12:15, 16. “Dunia,” yaani, sehemu fulani za mfumo wa Shetani, au watawala wa nchi mbalimbali, walitetea uhuru wa ibada. Kuanzia miaka ya 1940, watawala hao ‘walimeza mto wa mateso ambao yule joka mkubwa aliutapika kutoka katika kinywa chake.’ Kwa kweli, Yehova anaweza kutumia serikali za ulimwengu kutimiza mapenzi yake akiamua kufanya hivyo. Kwa hiyo, kwa kufaa andiko la Methali 21:1 linasema hivi: “Moyo wa mfalme ni kama vijito vya maji mkononi mwa Yehova. Huugeuza kuelekea popote anapopenda.” Jambo hilo linapasa kutia nguvu imani yetu katika Mungu.