Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mtumishi wa Yehova—‘Alichomwa kwa Silaha kwa Ajili ya Ukosaji Wetu’

Mtumishi wa Yehova—‘Alichomwa kwa Silaha kwa Ajili ya Ukosaji Wetu’

Mtumishi wa Yehova—‘Alichomwa kwa Silaha kwa Ajili ya Ukosaji Wetu’

“Alikuwa akichomwa kwa silaha kwa ajili ya ukosaji wetu; alikuwa akipondwa kwa ajili ya makosa yetu. . . . Kwa sababu ya majeraha yake sisi tumeponywa.”—ISA. 53:5.

1. Tunapaswa kukumbuka nini tunapoadhimisha Ukumbusho, na ni unabii gani utakaotusaidia kufanya hivyo?

TUNAADHIMISHA Ukumbusho ili kukumbuka kifo cha Kristo na mambo yote yaliyotimizwa kupitia kifo chake na ufufuo wake. Mwadhimisho huo unatukumbusha kuhusu kutetewa kwa enzi kuu ya Yehova, kutakaswa kwa jina lake, na kutimizwa kwa kusudi lake, kutia ndani wokovu wa wanadamu. Labda hakuna unabii mwingine katika Biblia ambao unazungumzia waziwazi dhabihu ya Kristo na mambo ambayo yalitimizwa na dhabihu hiyo kuliko ule ulioandikwa katika Isaya 53:3-12. Isaya alitabiri mateso ya Mtumishi huyo na kutoa habari hususa kuhusu kifo cha Kristo na baraka ambazo kifo hicho kingewaletea ndugu zake watiwa-mafuta na ‘kondoo wake wengine.’—Yoh. 10:16.

2. Unabii wa Isaya unathibitisha nini, nasi tutapata faida gani tunapouchunguza?

2 Miaka zaidi ya 700 kabla ya Yesu kuzaliwa duniani, Yehova alimwongoza Isaya kuandika kwamba Mtumishi Wake mchaguliwa atakuwa mwaminifu hata akijaribiwa mpaka mwisho. Jambo hilo la hakika linathibitisha kwamba Yehova alijua kabisa kuwa Mwana wake atabaki akiwa mshikamanifu. Tunapochunguza unabii huo, mioyo yetu itachangamshwa na imani yetu itatiwa nguvu.

“Alidharauliwa” na Kuhesabiwa “Kuwa Asiye na Maana”

3. Kwa nini Wayahudi walipaswa kumkaribisha Yesu, lakini walimpokea jinsi gani?

3 Soma Isaya 53:3. Hebu wazia jinsi Mwana wa Mungu alivyohisi alipolazimika kujinyima shangwe ya kutumikia kando ya Baba yake na kuja duniani na kudhabihu uhai wake ili kuwaokoa wanadamu kutoka katika dhambi na kifo! (Flp. 2:5-8) Dhabihu yake ilikusudiwa kuleta msamaha wa kweli wa dhambi, nayo ilifananishwa na dhabihu za wanyama zilizotolewa chini ya Sheria ya Musa. (Ebr. 10:1-4) Je, si kweli kwamba alipaswa kukaribishwa na kuheshimiwa, angalau na Wayahudi, ambao walikuwa wakimtarajia Masihi aliyeahidiwa? (Yoh. 6:14) Badala yake, kama Isaya alivyotabiri, Kristo “alidharauliwa” na Wayahudi, nao ‘wakamhesabu kuwa mtu asiye na maana.’ Mtume Yohana aliandika hivi: “Alikuja nyumbani kwake mwenyewe, lakini watu wake mwenyewe hawakumkaribisha.” (Yoh. 1:11) Mtume Petro aliwaambia Wayahudi hivi: “Mungu wa mababu zetu . . . amemtukuza Mtumishi wake, Yesu, ambaye ninyi mlimpeleka na kumkana mbele ya uso wa Pilato, alipokuwa ameamua kumfungua. Ndiyo, ninyi mlimkana huyo aliye mtakatifu na mwadilifu.”—Mdo. 3:13, 14.

4. Yesu alizoeana na ugonjwa katika njia gani?

4 Pia, Isaya alitabiri kwamba Yesu alikusudiwa “kuzoeana na ugonjwa.” Wakati wa huduma yake, bila shaka Yesu alichoka mara kwa mara, lakini hakuna andiko linalosema kwamba aliwahi kuwa mgonjwa. (Yoh. 4:6) Hata hivyo, alijua na alizoea magonjwa ya watu aliowahubiria. Aliwasikitikia na kuwaponya wengi. (Marko 1:32-34) Hivyo, Yesu alitimiza unabii unaosema hivi: “Kwa kweli yeye mwenyewe aliyachukua magonjwa yetu; na kwa habari ya maumivu yetu, yeye aliyabeba.”—Isa. 53:4a; Mt. 8:16, 17.

Ni Kana Kwamba ‘Alipigwa na Mungu’

5. Wayahudi wengi walikuwa na maoni gani kuhusu kifo cha Yesu, na kwa nini jambo hilo lilimfanya ateseke hata zaidi?

5 Soma Isaya 53:4b. Watu wengi wa siku za Yesu hawakuelewa kwa nini aliteseka na kufa. Waliamini kwamba Mungu anamwadhibu, kana kwamba anampiga kwa ugonjwa wenye kuchukiza sana. (Mt. 27:38-44) Wayahudi walidai kwamba Yesu alikufuru. (Marko 14:61-64; Yoh. 10:33) Bila shaka, Yesu hakutenda dhambi wala kukufuru. Lakini kwa kuwa alimpenda sana Baba yake, ni wazi kwamba Mtumishi huyo wa Yehova aliteseka hata zaidi alipowazia kwamba angekufa kwa kushtakiwa kuwa amekufuru. Ingawa hivyo, alikuwa tayari kujitiisha kwa mapenzi ya Yehova.—Mt. 26:39.

6, 7. Ni katika maana gani Yehova ‘alimponda’ Mtumishi wake mwaminifu, na kwa nini jambo hilo ‘lilimpendeza’ Mungu?

6 Si vigumu kuelewa maneno ya unabii wa Isaya yanayoonyesha kwamba watu fulani wangefikiri kuwa Kristo ‘amepigwa na Mungu,’ lakini inaweza kuwa vigumu kuelewa maneno haya yaliyotabiriwa katika unabii huohuo: “Yehova alipendezwa kumponda.” (Isa. 53:10) Je, kweli Yehova ‘angependezwa kumponda’ mtumishi wake na tayari alikuwa amesema hivi: “Tazama! Mtumishi wangu, . . . mchaguliwa wangu, ambaye nafsi yangu imemkubali”? (Isa. 42:1) Jambo hilo lilimletea Yehova shangwe katika maana gani?

7 Ili tuelewe sehemu hiyo ya unabii huo, tunapaswa kukumbuka kwamba Shetani alipotilia shaka uhalali wa enzi kuu ya Yehova, alitilia shaka ushikamanifu wa watumishi wote wa Mungu mbinguni na duniani. (Ayu. 1:9-11; 2:3-5) Yesu alipoendelea kuwa mwaminifu kufikia kifo, alijibu kikamili dai la Shetani. Hivyo, ingawa Yehova aliruhusu maadui wamuue Kristo, bila shaka Yehova aliteseka alipomwona Mtumishi wake mchaguliwa akiuawa. Hata hivyo, Yehova alipendezwa sana alipomwona Mwana wake akidumisha uaminifu kikamili. (Met. 27:11) Zaidi ya hayo, Yehova alipata shangwe kubwa kwa sababu alijua faida ambazo kifo cha Mwana wake kingewaletea wanadamu wanaotubu.—Luka 15:7.

‘Alichomwa kwa Silaha kwa Ajili ya Ukosaji Wetu’

8, 9. (a) Yesu ‘alichomwa kwa silaha kwa ajili ya ukosaji wetu’ katika maana gani? (b) Petro alithibitisha jambo hilo jinsi gani?

8 Soma Isaya 53:6. Kama kondoo waliopotea, wanadamu wenye dhambi wameenda huku na huku, wakitafuta kukombolewa kutoka kwa magonjwa na kifo ambacho walirithi kutoka kwa Adamu. (1 Pet. 2:25) Kwa kuwa wazao wa Adamu si wakamilifu, hakuna hata mmoja wao ambaye angeweza kulipia kile ambacho Adamu alipoteza. (Zab. 49:7) Hata hivyo, akichochewa na upendo wake mwingi, “Yehova amefanya kosa letu sote likutane na huyo,” Mwana wake mpendwa na Mtumishi mchaguliwa. Kwa kukubali ‘kuchomwa kwa silaha kwa ajili ya ukosaji wetu’ na ‘kupondwa kwa ajili ya makosa yetu,’ Kristo alichukua dhambi zetu juu ya mti na kufa badala yetu.

9 Mtume Petro aliandika hivi: “Mliitwa kwenye mwendo huu, kwa sababu hata Kristo aliteseka kwa ajili yenu, akiwaachia ninyi kielelezo ili mfuate hatua zake kwa ukaribu. Yeye mwenyewe alichukua dhambi zetu katika mwili wake mwenyewe juu ya mti, ili tuachane kabisa na dhambi na kuishi kwa uadilifu.” Kisha, akinukuu unabii wa Isaya, Petro aliongeza hivi: “Na ‘kwa mapigo yake mliponywa.’” (1 Pet. 2:21, 24; Isa. 53:5) Hilo liliwawezesha watenda-dhambi kupatanishwa na Mungu, kama maneno haya ya Petro yanavyoonyesha: “Kristo alikufa mara moja kwa wakati wote kuzihusu dhambi, mtu mwadilifu kwa ajili ya wasio waadilifu, ili awaongoze ninyi kwa Mungu.”—1 Pet. 3:18.

‘Aliletwa Kama Kondoo Machinjioni’

10. (a) Yohana Mbatizaji alisema nini kumhusu Yesu? (b) Kwa nini maneno ya Yohana yalifaa?

10 Soma Isaya 53:7, 8Yohana Mbatizaji alipomwona Yesu akimjia, alisema hivi: “Ona, Mwana-Kondoo wa Mungu ambaye huondolea mbali dhambi ya ulimwengu!” (Yoh. 1:29) Yohana alipomtaja Yesu kuwa Mwana-Kondoo, huenda alikuwa akikumbuka maneno haya ya Isaya: “Alikuwa akiletwa kama kondoo [au, mwana-kondoo] machinjioni.” (Isa. 53:7) Isaya alitabiri hivi: “Aliimwaga nafsi yake mpaka kufa.” (Isa. 53:12) Ndiyo, usiku ambao Yesu alianzisha Ukumbusho wa kifo chake, aliwapa wale mitume 11 waaminifu kikombe cha divai na kusema hivi: “Hii inamaanisha ‘damu yangu ya agano,’ ambayo itamwagwa kwa ajili ya wengi kwa msamaha wa dhambi.”—Mt. 26:28.

11, 12. (a) Tendo la Isaka la kukubali kwa kupenda kutolewa kuwa dhabihu linaonyesha nini kuhusu dhabihu ya Kristo? (b) Tunapoadhimisha Ukumbusho, tunapaswa kukumbuka nini kumhusu Abrahamu Mkuu Zaidi, Yehova?

11 Kama Isaka, Yesu alikuwa tayari kutolewa akiwa dhabihu juu ya madhabahu ya mapenzi ya Yehova kwa ajili yake. (Mwa. 22:1, 2, 9-13; Ebr. 10:5-10) Ingawa Isaka alikubali kwa kupenda kutolewa kuwa dhabihu, Abrahamu ndiye aliyejaribu kutoa dhabihu hiyo. (Ebr. 11:17) Vivyo hivyo, Yesu alikubali kwamba atakufa, lakini Yehova ndiye Mwanzilishi wa mpango wa dhabihu ya ukombozi. Dhabihu ya Mwana wake ilionyesha kwamba Mungu anawapenda sana wanadamu.

12 Yesu mwenyewe alisema hivi: “Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akamtoa Mwana wake mzaliwa-pekee, ili kila mtu anayemwamini asiangamizwe bali awe na uzima wa milele.” (Yoh. 3:16) Mtume Paulo aliandika hivi: “Mungu hupendekeza upendo wake mwenyewe kwetu kwa kuwa, tulipokuwa tungali watenda-dhambi, Kristo alikufa kwa ajili yetu.” (Rom. 5:8) Kwa hiyo, tunapomheshimu Kristo kwa kukumbuka kifo chake, hatupaswi kamwe kusahau kwamba yule aliyeamua jinsi dhabihu hiyo itakavyolipwa si mwingine ila Abrahamu Mkuu Zaidi, Yehova. Tunaadhimisha Ukumbusho ili kumsifu.

Mtumishi Huyo Anawaletea “Watu Wengi Msimamo wa Uadilifu”

13, 14. Ni kwa njia gani Mtumishi wa Yehova amewaletea “watu wengi msimamo wa uadilifu”?

13 Soma Isaya 53:11, 12. Yehova alisema hivi kuhusu Mtumishi wake mchaguliwa: “Mtu mwadilifu, mtumishi wangu, atawaletea watu wengi msimamo wa uadilifu.” Jinsi gani? Sehemu ya mwisho ya mstari wa 12 inatoa wazo linalotusaidia kupata jibu. “[Mtumishi huyo] aliingilia kati kwa ajili ya wakosaji.” Wazao wote wa Adamu wanazaliwa wakiwa watenda-dhambi, au “wakosaji,” na hivyo wanapata “mshahara ambao dhambi hulipa,” yaani, kifo. (Rom. 5:12; 6:23) Ni lazima mwanadamu mwenye dhambi apatanishwe na Yehova. Sura ya 53 ya unabii wa Isaya inaeleza kwa njia yenye kuvutia sana jinsi ambavyo Yesu “aliingilia kati” au kuwa mpatanishi kwa ajili ya wanadamu wenye dhambi, inaposema hivi: “Adhabu iliyokusudiwa kuleta amani yetu ilikuwa juu yake, na kwa sababu ya majeraha yake sisi tumeponywa.”—Isa. 53:5.

14 Kwa kubeba dhambi zetu na kufa kwa ajili yetu, Kristo aliwaletea “watu wengi msimamo wa uadilifu.” Paulo aliandika hivi: “Mungu aliona ni vema ujazo wote ukae katika yeye [Kristo], na kupitia yeye apatanishe tena kwake mwenyewe vitu vingine vyote kwa kufanya amani kupitia damu aliyomwaga juu ya mti wa mateso, hata kama ni vitu vilivyo duniani au vitu vilivyo mbinguni.”—Kol. 1:19, 20.

15. (a) “Vitu vilivyo mbinguni” vilivyotajwa na Paulo ni akina nani? (b) Ni nani tu ambao wanastahili kula mkate na kunywa divai wakati wa Ukumbusho, na kwa nini?

15 “Vitu vilivyo mbinguni” ambavyo vimepatanishwa na Yehova kupitia damu ya Kristo iliyomwagwa ni wale Wakristo watiwa-mafuta, walioitwa watawale pamoja na Kristo mbinguni. Wakristo ambao ni “washiriki wa mwito wa mbinguni” wanatangazwa kuwa “waadilifu kwa ajili ya uzima.” (Ebr. 3:1; Rom. 5:1, 18) Hivyo, Yehova anawakubali kuwa wana wake wa kiroho. Roho takatifu inawatolea ushahidi kwamba wao ni “warithi pamoja na Kristo,” walioitwa wawe wafalme na makuhani katika Ufalme wake wa mbinguni. (Rom. 8:15-17; Ufu. 5:9, 10) Wanakuwa sehemu ya taifa la Israeli la kiroho, “Israeli wa Mungu,” nao wanaingizwa katika “agano jipya.” (Yer. 31:31-34; Gal. 6:16) Wakiwa washiriki wa agano jipya, wanastahili kula na kunywa ile mifano ya Ukumbusho, ambayo inatia ndani kikombe cha divai nyekundu, ambacho Yesu alisema hivi kukihusu: “Kikombe hiki kinamaanisha agano jipya kwa msingi wa damu yangu, ambayo itamwagwa kwa ajili yenu.”—Luka 22:20.

16. “Vitu vilivyo duniani” ni akina nani, na ni kwa njia gani wanawezeshwa kuwa na msimamo wa uadilifu mbele za Yehova?

16 “Vitu vilivyo duniani” ni kondoo wengine wa Kristo, ambao wana tumaini la kuishi milele duniani. Mtumishi mchaguliwa wa Yehova anawawezesha pia kuwa na msimamo wa uadilifu mbele za Yehova. Kwa kuwa wana imani katika dhabihu ya ukombozi ya Kristo na “wamefua kanzu zao na kuzifanya nyeupe katika damu ya Mwana-Kondoo,” Yehova anawatangaza kuwa waadilifu, si ili wawe wana wa kiroho, bali ili wawe marafiki wake, na kuwapa tumaini zuri ajabu la kuokoka “ile dhiki kuu.” (Ufu. 7:9, 10, 14; Yak. 2:23) Kwa kuwa hawako katika lile agano jipya na hawana tumaini la kuishi mbinguni, kondoo hao wengine hawali mkate wala kunywa divai wakati wa Ukumbusho bali wanahudhuria wakiwa watazamaji wenye heshima.

Tunamshukuru Sana Yehova na Mtumishi Wake Aliyekubaliwa!

17. Kuchunguza unabii mbalimbali wa Isaya kuhusu Mtumishi huyo kumetusaidia jinsi gani kutayarisha akili zetu kwa ajili ya Ukumbusho?

17 Kuchunguza unabii mbalimbali wa Isaya kuhusu Mtumishi huyo ni njia nzuri sana ya kutayarisha akili zetu kwa ajili ya Ukumbusho wa kifo cha Kristo. Kupitia uchunguzi huo, ‘tumemtazama kwa makini Wakili Mkuu na Mkamilishaji wa imani yetu.’ (Ebr. 12:2) Tumejifunza kwamba Mwana wa Mungu si mwasi. Yeye si kama Shetani, bali anafurahia kufundishwa na Yehova, naye anamtambua kuwa Bwana Mwenye Enzi Kuu. Tumeona kwamba wakati wa huduma ya Yesu duniani, aliwahurumia watu aliowahubiria na kuwaponya wengi wao kimwili na kiroho. Hivyo, alionyesha mambo atakayofanya akiwa Mfalme wa Kimasihi katika mfumo mpya wa mambo wakati “atakapoweka haki duniani.” (Isa. 42:4) Bidii aliyoonyesha alipohubiri kuhusu Ufalme akiwa “nuru ya mataifa,” inawakumbusha wafuasi wake wahubiri habari njema kwa bidii katika dunia yote.—Isa. 42:6.

18. Kwa nini unabii wa Isaya unachochea mioyo yetu kumshukuru sana Yehova na Mtumishi wake mwaminifu?

18 Pia, unabii wa Isaya unatusaidia kuelewa vizuri zaidi jinsi Yehova alivyojidhabihu sana alipomtuma Mwana wake mpendwa duniani ateseke na kufa kwa ajili yetu. Yehova hakupendezwa kuona Mwana wake akiteseka, lakini alipendezwa kuona Yesu akiendelea kuwa mwaminifu kikamili mpaka kifo. Kama Yehova, tunapaswa pia kupendezwa na jambo hilo, na kutambua mambo yote ambayo Yesu alifanya ili kuthibitisha kwamba Shetani ni mwongo na kulitakasa jina la Yehova, na hivyo kutetea uhalali wa enzi Yake kuu. Zaidi ya hayo, Kristo alibeba dhambi zetu na kufa kwa ajili yetu. Kwa njia hiyo, aliwezesha kundi dogo la ndugu zake watiwa-mafuta na kondoo wengine kuwa na msimamo wa uadilifu mbele za Yehova. Tutakapokusanyika pamoja kwa ajili ya Ukumbusho, acheni mioyo yetu ichochewe kumshukuru sana Yehova na Mtumishi wake mwaminifu.

Kwa Kupitia

• Ni kwa njia gani Yehova “alipendezwa” kuona Mwana wake ‘akipondwa’?

• Ni kwa njia gani Yesu ‘alichomwa kwa silaha kwa ajili ya ukosaji wetu’?

• Mtumishi wa Yehova ‘aliwaletea watu wengi msimamo wa uadilifu’ jinsi gani?

• Kuchunguza unabii mbalimbali kumhusu Mtumishi wa Yehova kumekusaidia jinsi gani kutayarisha akili na moyo wako kwa ajili ya Ukumbusho?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 26]

“Alidharauliwa, nasi tulimhesabu kuwa asiye na maana”

[Picha katika ukurasa wa 28]

“Aliimwaga nafsi yake mpaka kufa”

[Picha katika ukurasa wa 29]

“Kondoo wengine” wanahudhuria Ukumbusho wakiwa watazamaji wenye heshima