Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

‘Njoo Uwe Mfuasi Wangu’

‘Njoo Uwe Mfuasi Wangu’

‘Njoo Uwe Mfuasi Wangu’

“Mtu yeyote akitaka kunifuata, na ajikane mwenyewe na kuuchukua mti wake wa mateso siku baada ya siku na kunifuata.”—LUKA 9:23.

1, 2. (a) Ni mwaliko gani wenye fadhili ambao Yesu alitoa? (b) Umeitikia jinsi gani mwaliko wa Yesu?

MWISHONI mwa huduma yake, Yesu alikuwa akihubiri huko Perea, eneo lililo ng’ambo ya Yordani, kaskazini-mashariki ya Yudea. Alifikiwa na mwanamume mmoja kijana ambaye alimuuliza kile ambacho alihitaji kufanya ili aurithi uzima wa milele. Baada ya Yesu kutambua kwamba kijana huyo alikuwa akifuata kwa uaminifu Sheria ya Musa, alimtolea mwaliko wa pekee. Alimwambia hivi: “Nenda, ukauze vitu ulivyo navyo uwape maskini, nawe utakuwa na hazina mbinguni, kisha uje uwe mfuasi wangu.” (Marko 10:21) Fikiria hilo—mwaliko wa kumfuata Yesu, Mwana mzaliwa-pekee wa Mungu Aliye Juu Zaidi!

2 Kijana huyo alikataa mwaliko huo, lakini wengine waliukubali. Mapema, Yesu alimwambia Filipo: “Uwe mfuasi wangu.” (Yoh. 1:43) Filipo alikubali na baadaye akawa mtume. Yesu alimwalika pia Mathayo, naye akakubali pia mwaliko huo. (Mt. 9:9; 10:2-4) Kwa kweli, Yesu alitoa mwaliko huohuo kwa wote ambao wanapenda uadilifu aliposema hivi: “Mtu yeyote akitaka kunifuata, na ajikane mwenyewe na kuuchukua mti wake wa mateso siku baada ya siku na kunifuata sikuzote.” (Luka 9:23) Kwa hiyo, mtu yeyote yule anaweza kuwa mfuasi wa Yesu ikiwa kwa kweli anataka. Je, unatamani kuwa mfuasi wake? Wengi wetu tayari wamekubali mwaliko wenye fadhili wa Yesu, na katika huduma ya shambani, tunawatolea wengine mwaliko huo.

3. Tunaweza kuepuka jinsi gani kupeperushwa na hivyo kuacha kumfuata Yesu?

3 Hata hivyo, inasikitisha kwamba watu fulani waliopendezwa na kweli za Biblia hawaendelei kujifunza. Badala yake, wanapunguza bidii yao na mwishowe ‘wanapeperushwa’ na hivyo wanaacha kumfuata Yesu. (Ebr. 2:1) Tunaweza kuepuka jinsi gani kutumbukia katika mtego huo? Ni jambo la maana kujiuliza wenyewe hivi: ‘Kwa nini niliamua kumfuata Yesu? Kumfuata Yesu kunamaanisha nini?’ Kufikiria majibu ya maswali hayo mawili kutatusaidia kuimarisha azimio letu la kubaki kwenye njia nzuri ya maisha tuliyochagua. Pia, kutatusaidia kuwatia wengine moyo wamfuate Yesu.

Kwa Nini Tumfuate Yesu?

4, 5. Kwa nini Yesu ndiye anayestahili kuwaongoza wanadamu?

4 Nabii Yeremia alisema hivi: “Ninajua vema, Ee Yehova, kwamba njia ya mtu wa udongo haimo katika uwezo wake. Mwanadamu anayetembea hana uwezo wa kuongoza hatua yake.” (Yer. 10:23) Historia imethibitisha ukweli wa maneno hayo ya Yeremia. Imethibitika zaidi na zaidi kwamba wanadamu wasio wakamilifu hawawezi kufaulu kujiongoza wenyewe. Tulikubali mwaliko wa kumfuata Yesu kwa sababu tulijifunza kwamba anastahili kuwa Kiongozi wetu na hakuna mwanadamu yeyote anayeweza kuongoza kama yeye. Fikiria sifa fulani zinazomfanya Yesu astahili.

5 Kwanza, Yesu alichaguliwa na Yehova mwenyewe kuwa Kiongozi ambaye ni Masihi. Muumba wetu ndiye anayejua vizuri zaidi ni nani anayestahili kuwekwa rasmi kuwa Kiongozi wetu. Pili, Yesu ana sifa zenye kuvutia ambazo tunaweza kuiga. (Soma Isaya 11:2, 3.) Yeye ni kielelezo kikamilifu. (1 Pet. 2:21) Tatu, Yesu anawajali sana wale wanaomfuata, kama alivyoonyesha alipotoa uhai wake kwa ajili yao. (Soma Yohana 10:14, 15.) Na anaonyesha kwamba yeye ni mchungaji mwenye kujali anapotuongoza kwenye maisha yenye furaha sasa na wakati ujao ulio bora kabisa. (Yoh. 10:10, 11; Ufu. 7:16, 17) Kwa sababu hizo na nyingine, tulifanya uamuzi wa hekima tulipochagua kumfuata. Hata hivyo, ni nini kinachohusika katika kumfuata Yesu?

6. Kumfuata Yesu kunamaanisha nini?

6 Kuwa wafuasi wa Kristo kunamaanisha mengi zaidi ya kujiita tu Wakristo. Leo, watu karibu bilioni mbili wanadai kuwa Wakristo, lakini matendo yao yanaonyesha kwamba wao ni “wenye matendo ya uasi-sheria.” (Soma Mathayo 7:21-23.) Watu mmoja-mmoja wanapopendezwa na mwaliko wa kumfuata Yesu, tunawaeleza kwamba Wakristo wa kweli wanapatanisha maisha yao yote na mafundisho na mfano wa Yesu, nao wanafanya hivyo siku zote za maisha yao. Ili kuelewa jambo hilo, fikiria mambo fulani ambayo tunajua kumhusu Yesu.

Iga Mfano wa Yesu wa Hekima

7, 8. (a) Hekima ni nini, na kwa nini Yesu alikuwa na hekima nyingi sana? (b) Yesu alionyesha jinsi gani hekima, na tunaweza kumwiga jinsi gani?

7 Yesu alionyesha sifa nyingi nzuri sana, lakini tutakazia fikira sifa nne: hekima yake, unyenyekevu wake, bidii yake, na upendo wake. Kwanza, fikiria hekima yake, yaani, uwezo wake wa kutumia ujuzi na uelewaji katika njia inayofaa. Mtume Paulo aliandika hivi: “Hazina zote za hekima na za ujuzi zimefichwa kwa uangalifu ndani [ya Yesu].” (Kol. 2:3) Yesu aliipata wapi hekima hiyo? Yeye mwenyewe alisema hivi: “Kama vile Baba alivyonifundisha, ndivyo ninavyosema mambo haya.” (Yoh. 8:28) Hekima yake ilitoka kwa Yehova, hivyo hatushangai kwamba Yesu alikuwa akifanya maamuzi mazuri.

8 Kwa mfano, Yesu alifanya uamuzi mzuri alipochagua jinsi angetumia maisha yake. Aliamua kuwa na maisha rahisi, na kukazia fikira jambo moja tu: kufanya mapenzi ya Mungu. Alitumia kwa hekima wakati na nguvu zake kuendeleza mambo ya Ufalme. Tunafuata mfano wa Yesu kwa kujitahidi kuwa na ‘jicho rahisi’ na hivyo kuepuka kujitwika mizigo ya mambo yasiyo ya lazima ambayo yanamaliza nguvu zetu na wakati wetu. (Mt. 6:22) Wakristo wengi wameamua kurahisisha mtindo wao wa maisha ili waweze kutumia wakati mwingi zaidi katika huduma. Wengine wameanza utumishi wa upainia. Ikiwa wewe ni mmoja wao, unastahili kupongezwa sana. “Kuutafuta kwanza ufalme” kunaleta furaha kubwa na uradhi.—Mt. 6:33.

Uwe Mnyenyekevu Kama Yesu

9, 10. Yesu alionyesha unyenyekevu jinsi gani?

9 Sifa ya pili ya utu wa Yesu ambayo tutachunguza ni unyenyekevu wake. Wanadamu wasio wakamilifu wanapopewa mamlaka, mara nyingi wanajiona kuwa watu wa maana sana. Yesu alikuwa tofauti kama nini! Ingawa alikuwa na mgawo wa maana sana katika kutimizwa kwa kusudi la Yehova, Yesu hakuwa na majivuno yoyote. Na tunatiwa moyo kuiga mtazamo huo wake wa unyenyekevu. Mtume Paulo aliandika hivi: “Iweni na mtazamo huu wa akili ndani yenu ambao ulikuwa pia ndani ya Kristo Yesu, ambaye, ingawa alikuwa katika umbo la Mungu, hakufikiria kufanya unyakuzi, yaani, kwamba yeye awe sawa na Mungu. Hapana, bali alijiondolea mwenyewe hali yake na kuchukua umbo la mtumwa na kuwa kama wanadamu.” (Flp. 2:5-7) Hilo lilimaanisha nini?

10 Yesu alifurahia pendeleo tukufu la kuwa mbele za Baba yake wa kimbingu, lakini alikubali kwa kupenda ‘kujiondolea mwenyewe hali yake.’ Uhai wake ulihamishwa na kuwekwa ndani ya tumbo la uzazi la bikira Myahudi, na humo alikua kwa miezi tisa mpaka alipozaliwa akiwa mtoto mchanga nyumbani kwa seremala maskini. Yesu aliendelea kukua hatua kwa hatua katika nyumba ya Yosefu mpaka alipoanza kutambaa, akawa kivulana, kisha tineja. Hakuwa na dhambi. Hata hivyo, katika ujana wake aliendelea kujitiisha kwa wazazi wa kibinadamu ambao walikuwa wenye dhambi na wasio wakamilifu. (Luka 2:51, 52) Ni unyenyekevu mkubwa kama nini!

11. Ni katika njia gani tunaweza kuiga unyenyekevu wa Yesu?

11 Tunaiga unyenyekevu wa Yesu tunapokubali kwa kupenda migawo ambayo huenda ikaonekana kuwa ya hali ya chini. Kwa mfano, fikiria mgawo wa kuhubiri habari njema. Huenda kazi hiyo ikaonekana kuwa ya hali ya chini, hasa watu wanapoonyesha ubaridi, dhihaka, au upinzani. Hata hivyo, tunapoendelea kudumu katika kazi ya kuhubiri, tunawasaidia wengine wakubali mwaliko wa Yesu wa kumfuata. Hivyo, tunasaidia kuokoa uhai. (Soma 2 Timotheo 4:1-5.) Mfano mwingine unahusu kutunza Jumba letu la Ufalme. Hilo linaweza kutia ndani mambo kama vile kutupa takataka, kusafisha sakafu, na kusafisha vyoo. Kazi zote hizo zinahitaji unyenyekevu! Hata hivyo, tunatambua kwamba kutunza Jumba letu la Ufalme—kituo cha ibada safi katika eneo letu—ni sehemu ya utumishi wetu mtakatifu. Kwa kukubali kutimiza kazi ambazo huenda zikaonekana kuwa za hali ya chini, tunaonyesha unyenyekevu na hivyo kumwiga Kristo.

Uwe Mwenye Bidii Kama Yesu

12, 13. (a) Yesu alionyesha bidii jinsi gani, na ni nini kilichomchochea? (b) Ni nini kitakachotuchochea kuwa wenye bidii katika huduma?

12 Fikiria bidii ya Yesu katika huduma. Yesu alitimiza mambo mengi alipokuwa duniani. Mapema katika miaka yake ya ujana, inaelekea Yesu alifanya kazi pamoja na baba yake mlezi Yosefu akiwa seremala. Wakati wa huduma yake, Yesu alifanya miujiza, kutia ndani kuponya wagonjwa na kufufua wafu. Lakini kazi yake kubwa ilikuwa kuhubiri habari njema na kuwafundisha wale waliokuwa tayari kusikiliza. (Mt. 4:23) Tukiwa wafuasi wake, tuna kazi kama hiyo ya kutimiza. Tunaweza kufuata mfano wake jinsi gani? Kwanza kabisa, tunaweza kusitawisha nia ambayo Yesu alikuwa nayo.

13 Zaidi ya yote, kumpenda Mungu kulimchochea Yesu kuhubiri na kufundisha. Lakini Yesu alipenda pia kweli alizofundisha. Aliziona kweli hizo kuwa hazina zenye thamani sana, na alikuwa na hamu ya kuwaambia wengine kuzihusu. Tukiwa walimu, au ‘wafundishaji wa watu wote,’ tuna maoni hayohayo. Hebu fikiria kweli fulani zenye thamani ambazo tumejifunza kutoka katika Neno la Mungu! Tunajua suala la enzi kuu na jinsi litakavyotatuliwa. Tunaelewa vizuri yale ambayo Maandiko yanafundisha kuhusu hali ya wafu na baraka za wakati ujao katika ulimwengu mpya wa Mungu. Iwe tumejifunza kweli hizo hivi karibuni au zamani, hazipotezi kamwe thamani yake. Ziwe za zamani au mpya, kweli hizo, kwa hakika ni hazina zenye thamani sana. (Soma Mathayo 13:52.) Tunapohubiri kwa uchangamfu, tunawaonyesha wengine kwamba tunapenda mambo ambayo Yehova ametufundisha.

14. Tunaweza kuiga jinsi gani njia ya Yesu ya kufundisha?

14 Ona pia, jinsi Yesu alivyofundisha. Sikuzote alielekeza wasikilizaji wake kwenye Maandiko. Mara nyingi kabla ya kutaja jambo fulani la maana alisema kwanza: “Imeandikwa.” (Mt. 4:4; 21:13) Katika maneno yake yaliyorekodiwa, Yesu alinukuu moja kwa moja au kutaja zaidi ya nusu ya vitabu vya Maandiko ya Kiebrania. Kama Yesu, tunaitegemea sana Biblia katika huduma yetu na tunajitahidi kukazia Maandiko kadiri iwezekanavyo. Katika njia hiyo, tunawasaidia watu wenye mioyo minyoofu kujionea wenyewe kwamba tunafundisha mawazo ya Mungu, bali si yetu. Tunafurahi sana mtu anapokubali tusome naye Biblia na kuzungumzia faida na maana ya Neno la Mungu! Na wakati watu kama hao wanapokubali mwaliko wa kumfuata Yesu, tunapata shangwe nyingi zaidi.

Kumfuata Yesu Kunamaanisha Kuwapenda Wengine

15. Ni sifa gani ya Yesu ambayo ilikuwa ya pekee, na tunaweza kuchochewa jinsi gani tunapoifikiria?

15 Jambo la mwisho kuhusu utu wa Yesu ambalo tutazungumzia ni lenye kuchangamsha moyo zaidi, yaani, upendo wake kwa wanadamu. Mtume Paulo aliandika hivi: “Upendo alio nao Kristo hutulazimisha.” (2 Kor. 5:14) Tunapofikiria jinsi Yesu anavyowapenda wanadamu kwa ujumla na jinsi anavyompenda kila mtu mmoja-mmoja, tunaguswa moyo sana na kuona kwamba tuna wajibu wa kufuata kielelezo chake.

16, 17. Yesu aliwaonyesha wengine upendo katika njia gani?

16 Yesu alionyesha jinsi gani kwamba aliwapenda wengine? Alionyesha upendo wake kwa njia kubwa zaidi alipoitoa nafsi yake kwa ajili ya wanadamu kwa kupenda. (Yoh. 15:13) Hata hivyo, wakati wa huduma yake, Yesu alionyesha pia upendo katika njia nyingine. Kwa mfano, aliwahurumia wale waliokuwa wakiteseka. Alipomwona Maria na wenzake wakilia kwa sababu ya kifo cha Lazaro, aliguswa moyo sana kwa sababu ya huzuni yao. Ingawa alikuwa karibu kumfufua Lazaro, Yesu alihuzunika sana hivi kwamba ‘alitokwa na machozi.’—Yoh. 11:32-35.

17 Mapema katika huduma ya Yesu, mtu fulani mwenye ukoma alimkaribia Yesu na kumwambia: “Ikiwa tu unataka, unaweza kunitakasa.” Yesu aliitikia jinsi gani? Simulizi linasema hivi: “Akamsikitikia.” Ndipo akafanya jambo la ajabu. “Akanyoosha mkono wake akamgusa, akamwambia: ‘Ninataka. Takasika.’ Na mara moja ule ukoma ukamtoka, naye akawa safi.” Chini ya Sheria ya Musa, watu wenye ukoma hawakuwa safi, na bila shaka Yesu angeweza kumponya mtu huyo bila kumgusa. Hata hivyo, Yesu alipomponya mtu huyo mwenye ukoma, alimwezesha kuhisi kwamba ameguswa na mwanadamu mwingine, labda kwa mara ya kwanza katika muda wa miaka mingi. Hilo lilikuwa tendo la huruma kama nini!—Marko 1:40-42.

18. Tunaweza kuonyesha “hisia-mwenzi” jinsi gani?

18 Tukiwa wafuasi wa Kristo, tunaamuriwa tuonyeshe upendo wetu kwa kuwa na “hisia-mwenzi.” (1 Pet. 3:8) Huenda isiwe rahisi kuelewa hisia za mwamini mwenzetu ambaye anasumbuliwa na ugonjwa wa kudumu au kushuka moyo, hasa ikiwa sisi wenyewe hatujapatwa na mambo kama hayo. Hata hivyo, Yesu alielewa hisia za wagonjwa hata ingawa yeye mwenyewe hakuwahi kuwa mgonjwa. Tunaweza kusitawisha jinsi gani hisia-mwenzi? Kwa kuwasikiliza kwa subira wale wanaoteseka wakati wanapotufunulia yaliyo moyoni mwao. Pia, tunaweza kujiuliza hivi: ‘Ikiwa ningekuwa katika hali yao, ningehisi jinsi gani?’ Tukisitawisha uwezo wa kuelewa hisia za wengine, tutaweza ‘kusema vizuri zaidi tunapozifariji nafsi zilizohuzunika.’ (1 The. 5:14) Hivyo, tutakuwa tukimfuata Yesu.

19. Mfano wa Yesu unatuchochea katika njia gani?

19 Maneno na matendo ya Yesu Kristo yanatufundisha mambo yenye kusisimua kama nini! Kadiri tunavyojifunza kumhusu Yesu, ndivyo tutakavyotaka kuwa kama yeye, na ndivyo tutakavyotaka kuwasaidia wengine kufanya vivyo hivyo. Basi, acheni tufurahie kumfuata Mfalme wa Kimasihi, sasa na milele!

Je, Unaweza Kueleza?

• Tunaweza kuonyesha hekima jinsi gani kama Yesu alivyofanya?

• Tunaweza kuonyesha unyenyekevu katika njia gani?

• Tunaweza kusitawisha jinsi gani bidii kwa ajili ya huduma?

• Ni katika njia gani tunaweza kumwiga Yesu kwa kuwaonyesha wengine upendo?

[Maswali ya Funzo]

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 5]

KITABU KINACHOTUSAIDIA KUMWIGA KRISTO

Wakati wa programu ya kusanyiko la wilaya la 2007, kitabu chenye kurasa 192 chenye kichwa ‘Njoo Uwe Mfuasi Wangu’ kilitolewa. Kitabu hicho kimekusudiwa kuwasaidia Wakristo wamkazie fikira Yesu, na hasa sifa na matendo yake. Baada ya sura mbili za kwanza za utangulizi, sehemu ya kwanza inazungumzia kwa ujumla sifa za pekee za Yesu—unyenyekevu wake, ujasiri wake, hekima yake, utii wake, na uvumilivu wake.

Sehemu zinazofuata zinazungumzia utendaji mbalimbali wa Yesu akiwa mwalimu, mhubiri wa habari njema, na pia njia fulani alizotumia kuonyesha upendo wake mkuu. Kitabu chote kina habari zinazokusudiwa kumsaidia Mkristo amwige Yesu.

Tuna hakika kwamba kitabu hicho kitatuchochea sisi sote kujichunguza na kujiuliza hivi: ‘Je, ninamfuata Yesu kwelikweli? Ninaweza kumfuata jinsi gani kwa ukaribu zaidi?’ Pia, kitawasaidia “wale wote [wenye] mwelekeo unaofaa kwa ajili ya uzima wa milele” kuwa wafuasi wa Kristo.—Mdo. 13:48.

[Picha katika ukurasa wa 4]

Yesu alikubali kuja duniani na kuzaliwa akiwa mtoto mchanga wa kibinadamu. Alihitaji kuonyesha sifa gani?

[Picha katika ukurasa wa 6]

Ni nini kitakachotuchochea kuwa wenye bidii katika huduma?