Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tazama! Mtumishi wa Yehova Aliyekubaliwa

Tazama! Mtumishi wa Yehova Aliyekubaliwa

Tazama! Mtumishi wa Yehova Aliyekubaliwa

“Tazama! Mtumishi wangu, . . . ambaye nafsi yangu imemkubali!” —ISA. 42:1.

1. Watu wa Yehova wanatiwa moyo kufanya nini hasa Ukumbusho unapokaribia, na kwa nini?

WAKATI wa kuadhimisha kifo cha Kristo unapozidi kukaribia, watu wa Mungu wanatiwa moyo kufuata shauri la mtume Paulo la ‘kumtazama kwa makini Wakili Mkuu na Mkamilishaji wa imani yetu, Yesu.’ Paulo aliongeza hivi: “Kwa kweli, mfikirieni sana yeye ambaye amevumilia maneno ya aina hii yenye kupinga yanayotolewa na watenda-dhambi kinyume cha faida zao wenyewe, ili ninyi msichoke na kuzimia katika nafsi zenu.” (Ebr. 12:2, 3) Kuchunguza kwa makini maisha ya uaminifu ya Kristo, ambayo yalifikia upeo alipotoa dhabihu yake, kutawasaidia Wakristo watiwa-mafuta na waandamani wao wa kondoo wengine kuendelea kumtumikia Yehova kwa uaminifu na kuepuka ‘kuzimia katika nafsi zao.’—Linganisha na Wagalatia 6:9.

2. Tunaweza kujifunza nini kupitia unabii mbalimbali ambao Isaya aliandika kuhusu Mwana wa Mungu?

2 Yehova alimwongoza kwa roho nabii Isaya aandike unabii mbalimbali uliomhusu moja kwa moja Mwana wa Mungu. Unabii huo utatusaidia ‘kumtazama kwa makini Wakili Mkuu na Mkamilishaji wa imani yetu,’ Kristo Yesu. * Unabii huo unatufunulia utu wake, mateso yake, na jinsi alivyotukuzwa kuwa Mfalme na Mkombozi wetu. Utatusaidia kuelewa zaidi Ukumbusho, ambao tutaadhimisha mwaka huu Alhamisi (Siku ya 4), Aprili 9, baada ya jua kushuka.

Mtumishi Anatambulishwa

3, 4. (a) Neno “mtumishi” linatumiwa jinsi gani katika kitabu cha Isaya? (b) Biblia yenyewe inamtambulisha jinsi gani Mtumishi anayetajwa katika Isaya sura ya 42, 49, 50, 52, na 53?

3 Neno “mtumishi” linatajwa mara nyingi katika kitabu cha Isaya. Nyakati nyingine, linamhusu nabii Isaya mwenyewe. (Isa. 20:3; 44:26) Pindi nyingine linahusu taifa lote la Israeli, au Yakobo. (Isa. 41:8, 9; 44:1, 2, 21) Lakini namna gani ule unabii wa pekee kuhusu Mtumishi anayetajwa katika Isaya sura ya 42, 49, 50, 52, na 53? Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo yanamtambulisha wazi Mtumishi huyo wa Yehova anayetajwa katika sura hizo. Inapendeza kwamba yule ofisa Mwethiopia anayetajwa katika kitabu cha Matendo alikuwa akisoma unabii mmoja kati ya unabii mbalimbali kumhusu Masihi wakati mweneza-injili Filipo alipoagizwa na roho aende mahali alipokuwa. Ofisa huyo alisoma kifungu cha Biblia kinachopatikana sasa katika Isaya 53:7, 8, kisha akamuuliza Filipo: “Ninakuomba, Nabii anasema hivyo juu ya nani? Juu yake mwenyewe au juu ya mtu mwingine?” Papo hapo, Filipo akamweleza kwamba Isaya alikuwa akizungumza kuhusu Masihi, Yesu.—Mdo. 8:26-35.

4 Yesu alipokuwa mtoto, mwanamume fulani mwadilifu aliyeitwa Simeoni alitangaza huku akiongozwa na roho takatifu kwamba “mtoto mchanga Yesu” atakuwa “nuru ya kuondoa utaji kwa mataifa,” kama ilivyotabiriwa katika Isaya 42:6 na 49:6. (Luka 2:25-32) Zaidi ya hayo, unabii ulio katika Isaya 50:6-9 ulitabiri mateso yenye kufedhehesha yaliyompata Yesu usiku ambao kesi yake ilifanywa. (Mt. 26:67; Luka 22:63) Baada ya Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K., mtume Petro alimtambulisha Yesu waziwazi kuwa “Mtumishi” wa Yehova. (Isa. 52:13; 53:11; soma Matendo 3:13, 26.) Tunaweza kujifunza nini katika unabii huo mbalimbali kumhusu Masihi?

Yehova Anamzoeza Mtumishi Wake

5. Mtumishi huyo alipata mazoezi gani?

5 Unabii mmoja wa Isaya kuhusu Mtumishi wa Mungu unafunua uhusiano wa karibu ambao Yehova alikuwa nao pamoja na Mwana wake mzaliwa wa kwanza kabla ya Mwana huyo kuja duniani. (Soma Isaya 50:4-9.) Mtumishi huyo mwenyewe anafunua kwamba Yehova alimzoeza sikuzote, anaposema: “Yeye . . . huliamsha sikio langu ili lisikie kama wale waliofundishwa,” au wanafunzi. (Isa. 50:4) Wakati huo wote, Mtumishi wa Yehova alimsikiliza Baba yake na kujifunza kutoka kwake, na hivyo akawa mwanafunzi mwenye kujitiisha. Ni pendeleo la pekee kama nini kufundishwa na Muumba wa ulimwengu wote mzima!

6. Mtumishi huyo alionyesha jinsi gani kwamba anajitiisha kikamili kwa Baba yake?

6 Katika unabii huo, Mtumishi huyo anamtaja Baba yake kuwa “Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova.” Hilo linaonyesha kwamba Mtumishi huyo alikuwa amejifunza ukweli wa msingi kuhusu enzi kuu ya Yehova ya ulimwengu wote mzima. Ili kuonyesha kwamba anajitiisha kikamili kwa Baba yake, alisema hivi: “Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova mwenyewe amelifungua sikio langu, nami kwa upande wangu sikuwa mwasi. Sikugeuka upande ulio kinyume.” (Isa. 50:5) Alikuwa ‘kando ya Yehova akiwa stadi wa kazi’ wakati wa kuumbwa kwa mwanadamu na ulimwengu wote mzima. ‘Stadi huyo wa kazi’ alikuwa ‘akifurahi mbele za Yehova wakati wote, akifurahi kwa sababu ya dunia yake yenye kutoa mazao, na vitu ambavyo Mwana huyo wa Mungu alipenda sana vilihusiana na wana wa binadamu.’—Met. 8:22-31.

7. Ni nini kinachoonyesha kwamba Mtumishi huyo alikuwa na uhakika kwamba Baba yake angemtegemeza wakati wa majaribu?

7 Mazoezi ambayo Mtumishi huyo alipokea na upendo wake kwa wanadamu ulimtayarisha kabisa kwa ajili ya maisha yake duniani na upinzani mkali aliokabili. Aliendelea kufurahia kufanya mapenzi ya Baba yake, hata alipoteswa vikali. (Zab. 40:8; Mt. 26:42; Yoh. 6:38) Katika majaribu yote aliyopata duniani, Yesu alikuwa na uhakika kwamba Baba yake alimkubali na angemtegemeza. Kama ilivyotabiriwa katika unabii wa Isaya, Yesu alisema: “Yeye anayenitangaza mimi kuwa mwadilifu yupo karibu. Ni nani anayeweza kushindana nami? . . . Tazama! Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova mwenyewe atanisaidia.” (Isa. 50:8, 9) Bila shaka, Yehova alimsaidia Mtumishi wake mwaminifu katika huduma yake yote duniani, kama unabii mwingine wa Isaya unavyoonyesha.

Huduma ya Mtumishi Huyo Duniani

8. Ni jambo gani linalothibitisha kwamba Yesu ndiye “mchaguliwa” wa Yehova aliyetabiriwa katika Isaya 42:1?

8 Biblia inasema jambo lililotukia Yesu alipobatizwa mwaka wa 29 W.K.: “Roho takatifu . . . ikashuka juu yake, na sauti ikatoka mbinguni: ‘Wewe ni Mwanangu, mpendwa; nimekukubali wewe.’” (Luka 3:21, 22) Hivyo, Yehova alimtambulisha waziwazi “mchaguliwa” wake aliyetajwa katika unabii wa Isaya. (Soma Isaya 42:1-7.) Wakati wa huduma yake duniani, Yesu alitimiza unabii huo kwa njia ya pekee. Katika masimulizi yake ya Injili, Mathayo alinukuu maneno yanayopatikana katika Isaya 42:1-4 na kuonyesha jinsi yanavyomhusu Yesu.—Mt. 12:15-21.

9, 10. (a) Yesu alitimiza jinsi gani Isaya 42:3 wakati wa huduma yake? (b) Ni kwa njia gani Kristo ‘alileta haki’ alipokuwa duniani, na ni wakati gani ambapo ‘ataweka haki duniani’?

9 Viongozi wa kidini Wayahudi waliwadharau watu wa kawaida. (Yoh. 7:47-49) Watu hao walitendewa kwa ukali na wangeweza kulinganishwa na ‘matete yaliyovunjika’ au ‘tambi za kitani’ zilizo karibu kuzimika kabisa. Hata hivyo, Yesu aliwahurumia maskini na watu wanaoteseka. (Mt. 9:35, 36) Aliwaalika kwa fadhili watu wa aina hiyo aliposema: “Njooni kwangu, nyote mnaotaabika na kulemewa na mizigo, nami nitawaburudisha ninyi.” (Mt. 11:28) Zaidi ya hayo, Yesu ‘alileta haki’ kwa kufundisha kanuni za Yehova kuhusu mema na mabaya. (Isa. 42:3) Pia, alionyesha kwamba Sheria ya Mungu ilipaswa kutumiwa kwa usawaziko na rehema. (Mt. 23:23) Vilevile, Yesu alionyesha haki kwa kuwahubiria matajiri na maskini bila ubaguzi.—Mt. 11:5; Luka 18:18-23.

10 Pia, unabii wa Isaya unatabiri kwamba “mchaguliwa” wa Yehova ‘ataweka haki duniani.’ (Isa. 42:4) Atafanya hivyo hivi karibuni wakati atakapoharibu falme zote za kisiasa na kusimamisha utawala wake wenye uadilifu akiwa Mfalme wa Ufalme wa Kimasihi. Ataleta ulimwengu mpya, ambamo “uadilifu utakaa.”—2 Pet. 3:13; Dan. 2:44.

“Nuru” na “Agano”

11. Ni kwa njia gani Yesu alikuwa “nuru ya mataifa” katika karne ya kwanza, na leo pia?

11 Kwa kweli, Yesu alikuwa “nuru ya mataifa,” na hivyo akatimiza unabii wa Isaya 42:6. Wakati wa huduma yake duniani, alileta nuru ya kiroho hasa kwa Wayahudi. (Mt. 15:24; Mdo. 3:26) Lakini Yesu alisema hivi: “Mimi ndiye nuru ya ulimwengu.” (Yoh. 8:12) Alikuwa nuru kwa Wayahudi na kwa mataifa si tu kwa kuwapa nuru ya kiroho bali pia kwa kudhabihu uhai wake mkamilifu akiwa mwanadamu ili awe dhabihu ya ukombozi kwa ajili ya wanadamu wote. (Mt. 20:28) Baada ya ufufuo wake, aliwaagiza wanafunzi wake wawe mashahidi wake “mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.” (Mdo. 1:8) Wakati wa huduma yao, Paulo na Barnaba walitaja maneno “nuru ya mataifa” na kuutumia kuhusu kazi ya kuhubiri ambayo walikuwa wakifanya kati ya watu wasio Wayahudi. (Mdo. 13:46-48; linganisha na Isaya 49:6.) Kazi hiyo bado inafanywa na ndugu za Yesu watiwa-mafuta walio duniani na waandamani wao ambao wanasambaza nuru ya kiroho na kuwasaidia watu kumwamini Yesu, ambaye ndiye “nuru ya mataifa.”

12. Yehova amemtoa jinsi gani Mtumishi wake “kuwa agano la watu”?

12 Katika unabii huohuo, Yehova alimwambia hivi Mtumishi wake mchaguliwa: “Nitakulinda na kukutoa kuwa agano la watu.” (Isa. 42:6) Shetani alijitahidi sana kumwangamiza Yesu na kumzuia asimalize huduma yake duniani, lakini Yehova alimlinda mpaka wakati uliowekwa wa kifo chake. (Mt. 2:13; Yoh. 7:30) Kisha Yehova akamfufua Yesu na kumtoa kuwa “agano,” au ahadi, kwa watu walio duniani. Ahadi hiyo rasmi ilitoa uhakikisho wa kwamba Mtumishi huyo mwaminifu wa Mungu angeendelea kuwa “nuru ya mataifa,” na hivyo kuwaweka huru wale walio katika giza la kiroho.—Soma Isaya 49:8, 9. *

13. Ni kwa njia gani Yesu aliwakomboa “wale wanaoketi gizani” wakati wa huduma yake duniani, naye anaendelea kufanya hivyo jinsi gani?

13 Kupatana na ahadi hiyo, Mtumishi mchaguliwa wa Yehova ‘angeyafungua macho yenye upofu,’ ‘angemtoa mfungwa katika gereza la shimoni,’ na kuwakomboa “wale wanaoketi gizani.” (Isa. 42:7) Wakati wa huduma yake duniani, Yesu alifanya hivyo kwa kufunua mapokeo ya uwongo ya kidini na kuhubiri habari njema ya Ufalme. (Mt. 15:3; Luka 8:1) Hivyo, aliwakomboa kutoka katika dini ya uwongo Wayahudi ambao walikuja kuwa wanafunzi wake. (Yoh. 8:31, 32) Vivyo hivyo, Yesu amewakomboa kiroho mamilioni ya watu wasio Wayahudi. Amewaagiza wafuasi wake ‘waende na kufanya wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote,’ na kuahidi kwamba atakuwa pamoja na wafuasi wake “mpaka umalizio wa mfumo wa mambo.” (Mt. 28:19, 20) Akiwa katika cheo chake mbinguni, Kristo Yesu anasimamia kazi ya kuhubiri ulimwenguni pote.

Yehova Alimwinua “Mtumishi” Huyo

14, 15. Kwa nini Yehova alimwinua Mtumishi wake, naye alifanya hivyo jinsi gani?

14 Katika unabii mwingine kuhusu Mtumishi wake wa Kimasihi, Yehova anasema hivi: “Tazama! Mtumishi wangu atatenda kwa ufahamu. Atakuwa na cheo cha juu na hakika yeye atainuliwa na kutukuzwa sana.” (Isa. 52:13) Kwa kuwa Mwana wake alijitiisha kwa ushikamanifu chini ya enzi Yake kuu na akaendelea kuwa mwaminifu wakati wa jaribu kali zaidi, Yehova alimwinua.

15 Mtume Petro aliandika hivi kumhusu Yesu: “Yeye yuko mkono wa kuume wa Mungu, kwa maana alienda zake mbinguni; na malaika na mamlaka na nguvu vilitiishwa kwake.” (1 Pet. 3:22) Vivyo hivyo, mtume Paulo aliandika hivi: “Alijinyenyekeza naye akawa mtiifu mpaka kifo, ndiyo, kifo juu ya mti wa mateso. Kwa sababu hii pia Mungu alimpandisha kwenye cheo cha juu zaidi na kumpa kwa fadhili jina lililo juu ya kila jina lingine, ili katika jina la Yesu kila goti lipigwe la wale walio mbinguni na wale walio duniani na wale walio chini ya nchi, na kila ulimi ukiri waziwazi kwamba Yesu Kristo ni Bwana kwa utukufu wa Mungu Baba.”—Flp. 2:8-11.

16. Yesu ‘alitukuzwa sana’ jinsi gani mwaka wa 1914, na ametimiza nini tangu wakati huo?

16 Katika mwaka wa 1914, Yehova alimwinua Yesu hata zaidi. ‘Alitukuzwa sana’ wakati Yehova alipomtawaza kuwa Mfalme wa Ufalme wa Kimasihi. (Zab. 2:6; Dan. 7:13, 14) Tangu wakati huo, Kristo ‘ameenda akitiisha katikati ya adui zake.’ (Zab. 110:2) Kwanza, alimtiisha Shetani na roho wake waovu, kwa kuwatupa chini katika ujirani wa dunia. (Ufu. 12:7-12) Kisha, akitenda akiwa Koreshi Mkuu, Kristo aliwakomboa mabaki ya ndugu zake watiwa-mafuta walio duniani kutoka katika utekwa wa “Babiloni Mkubwa.” (Ufu. 18:2; Isa. 44:28) Amesimamia kazi ya kuhubiri ulimwenguni pote, na kupitia kazi hiyo, ndugu zake “waliobaki” wamekusanywa kwanza, halafu mamilioni ya “kondoo wengine” wamekusanywa pia, ambao ni waandamani washikamanifu wa “kundi dogo.”—Ufu. 12:17; Yoh. 10:16; Luka 12:32.

17. Tumejifunza nini kufikia sasa kwa kuchunguza unabii wa Isaya kuhusu “mtumishi” huyo?

17 Bila shaka, kujifunza unabii huo wa pekee katika kitabu cha Isaya kumetusaidia tumthamini zaidi Mfalme na Mkombozi wetu, Kristo Yesu. Utii wake akiwa Mwana wakati wa huduma yake duniani unaonyesha kwamba alizoezwa alipokuwa kando ya Baba yake kabla ya kuja duniani. Amejithibitisha kuwa “nuru ya mataifa” kupitia huduma yake mwenyewe na kazi ya kuhubiri ambayo ameisimamia mpaka leo hii. Kama tutakavyoona katika habari inayofuata, unabii mwingine kuhusu Mtumishi huyo wa Kimasihi ulifunua kwamba angeteseka na kudhabihu uhai wake kwa faida yetu. Hayo ni mambo ambayo tunapaswa ‘kuyatazama kwa makini’ kadiri Ukumbusho wa kifo chake unavyokaribia.—Ebr. 12:2, 3.

[Maelezo ya chini]

^ fu. 2 Unabii huo unapatikana katika Isaya 42:1-7; 49:1-12; 50:4-9; na 52:13–53:12.

^ fu. 12 Ili upate habari zaidi kuhusu unabii ulio katika Isaya 49:1-12, soma kitabu Unabii wa Isaya—Nuru kwa Wanadamu Wote II, ukurasa wa 136-145.

Kwa Kupitia

• “Mtumishi” anayetajwa katika unabii wa Isaya ni nani, nasi tunajua hilo jinsi gani?

• Mtumishi huyo alipata mazoezi gani kutoka kwa Yehova?

• Ni kwa njia gani Yesu ni “nuru ya mataifa”?

• Mtumishi huyo aliinuliwa jinsi gani?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 21]

Filipo alimtambulisha waziwazi “mtumishi” aliyetajwa na Isaya kuwa Yesu, yule Masihi

[Picha katika ukurasa wa 23]

Akiwa Mtumishi mchaguliwa wa Yehova, Yesu aliwahurumia maskini na wanaoteseka

[Picha katika ukurasa wa 24]

Yesu alitukuzwa na Baba yake na kutawazwa kuwa Mfalme wa Ufalme wa Kimasihi