Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Acha Maneno ya Yesu Yafinyange Mtazamo Wako

Acha Maneno ya Yesu Yafinyange Mtazamo Wako

Acha Maneno ya Yesu Yafinyange Mtazamo Wako

“Yule ambaye Mungu amemtuma husema maneno ya Mungu.”—YOH. 3:34.

1, 2. Maneno ya Yesu katika Mahubiri ya Mlimani yanaweza kulinganishwa na nini, na kwa nini tunaweza kusema kwamba yalitegemea “maneno ya Mungu”?

MOJAWAPO ya vipande vikubwa zaidi vya almasi vilivyopo leo ni kile kinachoitwa Nyota ya Afrika (Star of Africa) chenye uzito wa karati 530. Kwa kweli ni kito au hazina yenye thamani sana! Hata hivyo, hazina za kiroho zenye thamani zaidi zinapatikana katika Mahubiri ya Yesu ya Mlimani. Hilo halishangazi, kwa kuwa Yehova ndiye Chanzo cha maneno hayo ya Kristo! Biblia inasema hivi kumhusu Yesu: “Yule ambaye Mungu amemtuma husema maneno ya Mungu.”—Yoh. 3:34-36.

2 Ingawa Mahubiri ya Mlimani huenda yalitolewa kwa muda unaopungua nusu saa, yana manukuu 21 kutoka vitabu vinane vya Maandiko ya Kiebrania. Kwa hivyo, mahubiri hayo yalitegemea kabisa “maneno ya Mungu.” Acheni sasa tuone jinsi tunavyoweza kutumia maneno fulani yenye thamani yanayopatikana katika mahubiri hayo bora ya Mwana mpendwa wa Mungu.

“Kwanza Fanya Amani Yako Pamoja na Ndugu Yako”

3. Baada ya kuwaonya wanafunzi wake kuhusu matokeo mabaya ya ghadhabu, Yesu alitoa shauri gani?

3 Tukiwa Wakristo, sisi ni wenye furaha na wanaofanya amani kwa sababu tuna roho takatifu ya Mungu, na matunda yake yanatia ndani shangwe na amani. (Gal. 5:22, 23) Yesu hakutaka wanafunzi wake wapoteze amani na furaha yao. Hivyo, aliwaonya kuhusu matokeo mabaya ya kuendelea kuwa na ghadhabu. (Soma Mathayo 5:21, 22.) Baadaye alisema: “Basi, ikiwa unaleta zawadi yako kwenye madhabahu na hapo ukumbuke kwamba ndugu yako ana jambo fulani juu yako, acha zawadi yako hapo mbele ya madhabahu, na uende zako; kwanza fanya amani yako pamoja na ndugu yako, na ndipo, ukiisha kurudi, itoe zawadi yako.”Mt. 5:23, 24.

4, 5. (a) Yesu alikuwa akizungumzia “zawadi” gani katika Mathayo 5:23, 24? (b) Ni jambo la maana kadiri gani kufanya amani na ndugu ambaye tumemkosea?

4 “Zawadi” hiyo ambayo Yesu alizungumzia ilikuwa toleo lolote lile ambalo lilitolewa kwenye hekalu huko Yerusalemu. Kwa mfano, dhabihu za wanyama zilikuwa muhimu kwa sababu wakati huo zilikuwa sehemu ya ibada ambayo watu wa Yehova walimtolea. Hata hivyo, Yesu alikazia jambo fulani la maana zaidi, yaani, kufanya amani na ndugu ambaye tumemkosea kabla ya kumtolea Mungu zawadi.

5 Maneno “fanya amani yako” yanamaanisha ‘kupatana.’ Hivyo, ni somo gani ambalo tunaweza kujifunza kutokana na maneno hayo ya Yesu? Bila shaka, njia yetu ya kushughulika na wengine inahusiana moja kwa moja na uhusiano wetu pamoja na Yehova. (1 Yoh. 4:20) Kwa kweli, matoleo yaliyotolewa kwa Mungu nyakati za kale hayakuwa na maana yoyote ikiwa yule aliyeyatoa hakuwatendea vizuri wanadamu wenzake.—Soma Mika 6:6-8.

Tunapaswa Kuwa Wanyenyekevu

6, 7. Kwa nini unyenyekevu unahitajiwa tunapojitahidi kurudisha uhusiano wenye amani pamoja na ndugu ambaye tumemkosea?

6 Kufanya amani na ndugu ambaye tumemkosea kunaweza kujaribu unyenyekevu wetu. Watu wanyenyekevu hawabishani wala kugombana na waamini wenzao ili kujaribu kutetea haki zao. Hilo lingetokeza hali mbaya, kama ile iliyokuwapo wakati fulani kati ya Wakristo katika Korintho la kale. Kuhusu hali hiyo, mtume Paulo alitoa wazo hili lenye kuchochea: “Inamaanisha kushindwa kwenu kabisa kwamba mnakuwa na mashtaka ya kisheria mtu na mwenzake. Kwa nini msiache mkosewe badala ya hivyo? Kwa nini msiache mpunjwe badala ya hivyo?”—1 Kor. 6:7.

7 Yesu hakusema kwamba tunapaswa kwenda kumwona ndugu yetu ili tu kumsadikisha hatujakosea na kwamba yeye ndiye aliyetukosea. Kusudi letu linapaswa kuwa kurudisha uhusiano wenye amani. Ili kufanya amani, tunapaswa kueleza kwa unyoofu hisia zetu. Tunapaswa pia kutambua kwamba tumeumiza hisia za mtu mwingine. Na ikiwa tumekosea, bila shaka tunapaswa kuomba msamaha kwa unyenyekevu.

‘Ikiwa Jicho Lako la Kuume Linakufanya Ukwazike’

8. Eleza yale ambayo Yesu alisema kwenye Mathayo 5:29, 30.

8 Katika Mahubiri yake ya Mlimani, Yesu alitoa mashauri mazuri kuhusu maadili. Alijua kwamba miili yetu isiyokamilika inaweza kuwa na uvutano hatari juu yetu. Kwa hiyo, Yesu alisema hivi: “Ikiwa, sasa, hilo jicho lako la kuume linakufanya ukwazike, ling’oe ulitupilie mbali nawe. Kwa maana kuna faida zaidi kwako kimoja cha viungo vyako kipotee kuliko mwili wako wote utupwe ndani ya Gehena. Pia, mkono wako wa kuume ukikufanya ukwazike, ukate na kuutupilia mbali nawe. Kwa maana kuna faida zaidi kwako kimoja cha viungo vyako kipotee kuliko mwili wako wote uanguke ndani ya Gehena.”Mt. 5:29, 30.

9. “Jicho” au “mkono” wetu unaweza ‘kutukwaza’ jinsi gani?

9 “Jicho” ambalo Yesu alizungumzia linawakilisha nguvu au uwezo wa kukazia uangalifu jambo fulani, na “mkono” unahusiana na yale ambayo tunafanya kwa kutumia mikono yetu. Tusipokuwa waangalifu, sehemu hizo za mwili zinaweza kutufanya ‘tukwazike’ na kuacha “kutembea pamoja na Mungu.” (Mwa. 5:22; 6:9) Tunaposhawishiwa kutomtii Yehova, tunahitaji kuchukua hatua thabiti, tunapaswa kung’oa jicho au kuukata mkono wetu kwa njia ya mfano.

10, 11. Ni nini kinachoweza kutusaidia tuepuke mwenendo mpotovu kiadili?

10 Tunaweza kufanya nini ili kuzuia macho yetu yasitazame mambo mapotovu kiadili? Ayubu, mwanamume aliyemwogopa Mungu, alisema hivi: “Nimefanya agano pamoja na macho yangu. Basi nawezaje kukaza fikira kwa bikira?” (Ayu. 31:1) Ayubu alikuwa ameoa, naye aliazimia kutovunja sheria za Mungu za maadili. Tunapaswa kuwa na mtazamo huo iwe tumefunga ndoa au sisi ni waseja. Ili kuepuka mwenendo mpotovu kiadili, tunahitaji kuongozwa na roho takatifu ya Mungu, ambayo inatokeza sifa ya kujizuia ndani ya wale wanaompenda Mungu.—Gal. 5:22-25.

11 Ili kuepuka mwenendo mpotovu kiadili, tunapaswa kujiuliza, ‘Je, ninaruhusu macho yangu yachochee ndani yangu tamaa ya mambo mapotovu yaliyo katika vitabu, televisheni, au Intaneti?’ Acheni pia tukumbuke maneno haya ya mwanafunzi Yakobo: “Kila mtu hujaribiwa kwa kuvutwa na kushawishiwa na tamaa yake mwenyewe. Kisha tamaa, wakati imetunga mimba, huzaa dhambi; nayo dhambi, wakati imetimizwa, huleta kifo.” (Yak. 1:14, 15) Kwa kweli, ikiwa mtu aliyejiweka wakfu kwa Mungu “anaendelea kumtazama” mtu wa jinsia tofauti kwa nia potovu, anahitaji kufanya mabadiliko makubwa yanayofananishwa na kung’oa jicho na kulitupa mbali.—Soma Mathayo 5:27, 28.

12. Ni shauri gani la Paulo linaloweza kutusaidia kupambana na tamaa potovu?

12 Kwa kuwa matumizi mabaya ya mikono yetu yanaweza kutuongoza kuvunja viwango vya maadili vya Yehova, ni lazima tuazimie kabisa kubaki safi kiadili. Kwa hiyo, tunapaswa kutii shauri hili la Paulo: “Viueni viungo vya mwili wenu vilivyo duniani kwa habari ya uasherati, uchafu, hamu ya ngono, tamaa yenye madhara, na kutamani, ambako ni ibada ya sanamu.” (Kol. 3:5) Neno “viueni” linakazia hatua thabiti ambazo zinapaswa kuchukuliwa ili kupambana na tamaa potovu za mwili.

13, 14. Kwa nini ni jambo la maana sana kuepuka mawazo na matendo mapotovu?

13 Ili kulinda uhai wake, mtu anaweza kukubali kukatwa kiungo chake kimoja. ‘Kutupilia mbali’ jicho na mkono wetu kwa njia ya mfano ni jambo la maana kwetu ili kuepuka mawazo na matendo mapotovu ambayo yanaweza kutuangamiza kiroho. Kubaki safi kiakili, kiadili, na kiroho ndiyo njia pekee ya kuepuka uharibifu wa milele unaofananishwa na Gehena.

14 Kwa sababu ya dhambi na kutokamilika ambako tulirithi, tunahitaji kujitahidi sana ili kubaki safi kiadili. Paulo alisema: “Naupigapiga mwili wangu na kuuongoza kama mtumwa, ili, baada ya mimi kuwahubiria wengine, mimi mwenyewe nisikataliwe kwa njia fulani.” (1 Kor. 9:27) Acheni basi tuazimie kufuata shauri la Yesu kuhusu maadili, kwa kutojiruhusu kamwe kutenda katika njia ambazo zinaonyesha kwamba hatuthamini dhabihu ya ukombozi.—Mt. 20:28; Ebr. 6:4-6.

“Muwe na Mazoea ya Kuwapa Watu”

15, 16. (a) Yesu aliweka mfano gani katika kutoa? (b) Maneno ya Yesu kwenye Luka 6:38 yanamaanisha nini?

15 Yesu aliwachochea watu kuwa na roho ya kutoa kupitia maneno na mfano wake bora. Alionyesha ukarimu mkubwa kwa kuja duniani kwa faida ya wanadamu wasio wakamilifu. (Soma 2 Wakorintho 8:9.) Yesu alikubali kuacha utukufu wake wa kimbingu ili kuwa mwanadamu na kutoa uhai wake kwa ajili ya wanadamu wenye dhambi, na wengine wao watapata baraka nyingi mbinguni wakiwa warithi pamoja naye katika Ufalme. (Rom. 8:16, 17) Na bila shaka Yesu aliwatia watu moyo kuwa wakarimu aliposema hivi:

16 “Muwe na mazoea ya kuwapa watu, na watu watawapa ninyi. Watawamwagia katika mfuko wa nguo zenu kipimo kizuri, kilichoshindiliwa, kilichotikiswa pamoja na kufurika. Kwa maana kwa kipimo mnachopimia, watawapimia ninyi pia.” (Luka 6:38) ‘Kumwaga katika mfuko wa nguo’ kunarejelea desturi ya wachuuzi fulani ya kujaza vitu katika mkunjo wa vazi la juu la mnunuzi, ambalo lilifungwa kwa mshipi ili liwe mfuko wa kubebea vitu. Huenda ukarimu wetu wa kutoka moyoni ukatufanya tupokee kipimo kizuri, labda wakati tunapokuwa na uhitaji.—Mhu. 11:2.

17. Yehova aliweka jinsi gani mfano bora zaidi katika kutoa, na tunaweza kupata shangwe tukitoa kwa njia gani?

17 Yehova anawapenda na kuwapa thawabu wale wanaotoa kwa uchangamfu. Yeye mwenyewe aliweka mfano bora zaidi, kwa kumtoa Mwana wake mzaliwa-pekee “ili kila mtu anayemwamini asiangamizwe bali awe na uzima wa milele.” (Yoh. 3:16) Paulo aliandika: “Yeye anayepanda kwa wingi atavuna pia kwa wingi. Kila mmoja na afanye kama alivyoazimia moyoni mwake, si kwa kutopenda wala kwa kulazimishwa, kwa maana Mungu humpenda mtoaji mchangamfu.” (2 Kor. 9:6, 7) Kutoa wakati wetu, nguvu, na mali za kimwili ili kuendeleza ibada ya kweli bila shaka kutatuletea shangwe na thawabu nyingi.—Soma Methali 19:17; Luka 16:9.

“Usipige Tarumbeta Mbele Yako”

18. Ni mambo gani ambayo yatafanya ‘tusiwe na thawabu’ kutoka kwa Baba yetu wa mbinguni?

18 “Iweni waangalifu sana kwamba msionyeshe uadilifu wenu mbele ya watu kusudi mwonekane nao; ama sivyo hamtakuwa na thawabu kwa Baba yenu aliye mbinguni.” (Mt. 6:1) Yesu alipotaja “uadilifu,” alimaanisha mwenendo ambao unapatana na mapenzi ya Mungu. Hakumaanisha kwamba matendo ya kimungu hayapaswi kufanywa hadharani, kwa kuwa aliwaambia wanafunzi wake ‘waache nuru yao iangaze mbele ya watu.’ (Mt. 5:14-16) Hata hivyo, ‘hatutakuwa na thawabu’ kutoka kwa Baba yetu wa mbinguni tukifanya mambo ‘kusudi tuonekane’ na kusifiwa kama waigizaji wanaofanya maonyesho jukwaani. Ikiwa tuna nia hiyo, hatutakuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Mungu wala kupokea baraka za milele za utawala wa Ufalme.

19, 20. (a) Yesu alimaanisha nini aliposema ‘tusipige tarumbeta’ tunapotoa “zawadi za rehema”? (b) Ni katika maana gani haturuhusu mkono wetu wa kushoto ujue yale ambayo mkono wa kuume unafanya?

19 Ikiwa tuna mtazamo mzuri, tutafuata shauri hili la Yesu: “Kwa sababu hiyo wakati unapotoa zawadi za rehema, usipige tarumbeta mbele yako, kama vile wanafiki wanavyofanya katika masinagogi na barabarani, ili watukuzwe na watu. Kwa kweli ninawaambia ninyi, wanapata thawabu yao kwa ukamili.” (Mt. 6:2) “Zawadi za rehema” zilitolewa ili kuwasaidia maskini. (Soma Isaya 58:6, 7.) Yesu na mitume wake walikuwa na hazina ya pamoja ya kuwasaidia maskini. (Yoh. 12:5-8; 13:29) Kwa kuwa tarumbeta hazikupigwa kihalisi kabla ya kuwasaidia maskini, ni wazi kwamba Yesu alitumia maneno ya kutia chumvi aliposema kwamba hatupaswi ‘kupiga tarumbeta’ mbele yetu tunapotoa “zawadi za rehema.” Hatupaswi kutangaza tunapotoa zawadi hizo, kama walivyofanya Wayahudi Mafarisayo. Yesu aliwaita wanafiki kwa sababu walitangaza “katika masinagogi na barabarani” michango ya rehema waliyotoa. Wanafiki hao ‘walipata thawabu yao kwa ukamili.’ Kusifiwa na watu na kuketi kwenye viti vya mbele kando ya marabi maarufu katika sinagogi ndiyo thawabu pekee ambayo wangepata, kwa kuwa Yehova hangewapa kitu chochote. (Mt. 23:6) Hivyo basi, wanafunzi wa Kristo walipaswa kutenda jinsi gani? Yesu aliwaambia hivi, na sisi pia:

20 “Lakini wewe, unapotoa zawadi za rehema, usiache mkono wako wa kushoto ujue lile ambalo mkono wako wa kuume unafanya, ili zawadi zako za rehema zitolewe katika siri; ndipo Baba yako anayetazama akiwa mahali pa siri atakulipa.” (Mt. 6:3, 4) Kwa kawaida mikono yetu inafanya kazi pamoja. Kwa hiyo, kutoacha mkono wa kushoto ujue yale ambayo mkono wa kuume unafanya kunamaanisha kwamba hatutangazi matendo yetu ya rehema, hata kwa wale walio na uhusiano wa karibu nasi kama vile mkono wetu wa kushoto ulivyo karibu na mkono wa kuume.

21. Yule “anayetazama akiwa mahali pa siri” anatulipa kwa njia gani?

21 Tukiepuka kujisifu tunapowasaidia wengine, ‘zawadi zetu za rehema’ zitatolewa kwa siri. Kisha Baba yetu “anayetazama akiwa mahali pa siri” atatulipa. Baba yetu wa mbinguni anakaa “mahali pa siri” kwa sababu yuko mbinguni na wanadamu hawamwoni. (Yoh. 1:18) Yule “anayetazama akiwa mahali pa siri” anatulipa kwa kuwa na uhusiano wa karibu sana pamoja nasi, kusamehe dhambi zetu, na kutupa uzima wa milele. (Met. 3:32; Yoh. 17:3; Efe. 1:7) Mambo hayo ni bora zaidi kuliko kusifiwa na wanadamu.

Maneno Yenye Thamani Yanayopaswa Kuthaminiwa

22, 23. Kwa nini tunapaswa kuthamini maneno ya Yesu?

22 Bila shaka, Mahubiri ya Mlimani yamejaa hazina za kiroho zenye mambo mengi ya kuvutia. Hapana shaka kwamba mahubiri hayo yana maneno yenye thamani ambayo yanaweza kutuletea shangwe hata katika ulimwengu huu wenye taabu. Ndiyo, tutakuwa wenye furaha tukithamini maneno ya Yesu na kuyaruhusu yafinyange mtazamo wetu na njia yetu ya maisha.

23 Kila mtu “anayesikia” na ‘kutenda’ mambo ambayo Yesu alifundisha atabarikiwa. (Soma Mathayo 7:24, 25.) Hivyo basi, acheni tuazimie kutii mashauri ya Yesu. Maneno zaidi aliyosema katika Mahubiri ya Mlimani yatachunguzwa katika habari ya mwisho ya mfululizo huu.

Ungesema Nini?

• Kwa nini ni jambo la maana kufanya amani na ndugu ambaye tumemkosea?

• Tunaweza kuepuka jinsi gani kukwazwa na ‘jicho letu la kuume’?

• Tunapaswa kuwa na mtazamo gani kuhusu kutoa?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 11]

Ni jambo zuri kama nini ‘kufanya amani yako’ na mwamini mwenzako ambaye umemkosea!

[Picha katika ukurasa wa 12, 13]

Yehova anawabariki wale ambao wanatoa kwa uchangamfu