Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Unapaswa Kushikilia Mapendezi Yako?

Je, Unapaswa Kushikilia Mapendezi Yako?

Je, Unapaswa Kushikilia Mapendezi Yako?

WATOTO wawili wanacheza pamoja. Mtoto mmoja anamnyang’anya mwenzake kigari anachopenda sana huku akipiga kelele hivi: “Ni changu!” Toka utotoni, wanadamu wasio wakamilifu wanaonyesha ubinafsi au uchoyo kwa kadiri fulani. (Mwa. 8:21; Rom. 3:23) Zaidi ya hayo, ulimwengu kwa ujumla unasisitiza watu watangulize mapendezi yao binafsi. Ili tuepuke roho hiyo, ni lazima tupambane na mielekeo ya kutanguliza mapendezi yetu binafsi. Tusipofanya hivyo, tunaweza kuwakwaza wengine kwa urahisi na kuharibu uhusiano wetu pamoja na Yehova.—Rom. 7:21-23.

Mtume Paulo aliandika hivi ili kututia moyo tufikirie jinsi matendo yetu yanavyoweza kuwa na uvutano juu ya wengine: “Mambo yote ni halali; lakini si mambo yote yaliyo na faida. Mambo yote ni halali; lakini si mambo yote yanayojenga.” Pia Paulo alisema: “Epukeni kuwa vikwazo.” (1 Kor. 10:23, 32) Katika mambo yanayohusu mapendezi ya kibinafsi, ni jambo la hekima kujiuliza hivi: ‘Je, niko tayari kuacha mapendezi yangu amani ya kutaniko inapokuwa hatarini? Je, niko tayari kufuata kanuni za Biblia, hata wakati ambapo si rahisi kufanya hivyo?’

Unapochagua Kazi

Watu wengi wanaona kwamba kuchagua kazi ni uamuzi wa kibinafsi ambao hauwahusu sana wengine. Lakini fikiria kisa cha mfanyabiashara mmoja katika mji fulani mdogo wa Amerika Kusini. Alikuwa mchezaji wa kamari na mlevi. Hata hivyo, baada ya kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova, alifanya maendeleo ya kiroho na kubadili maisha yake. (2 Kor. 7:1) Alipoomba aanze kuhubiri pamoja na kutaniko, mzee mmoja alimtia moyo kwa busara afikirie kazi yake ya kimwili. Kwa muda fulani, mwanamume huyo alikuwa na duka kubwa la kuuza pombe ya miwa katika mji huo. Kwa kawaida, pombe hiyo inatumiwa kwa njia nyingi lakini katika eneo hilo watu waliichanganya na soda ili hasa walewe.

Mwanamume huyo alitambua kwamba ikiwa angewahubiria watu akiwa bado anafanya kazi hiyo ya kuwauzia watu pombe, sifa ya kutaniko ingeharibika na uhusiano wake pamoja na Mungu ungeharibika pia. Ingawa alihitaji kutegemeza familia yake kubwa, aliacha kuuza pombe. Sasa anaitegemeza familia yake kwa kuuza bidhaa zinazotengenezwa kwa karatasi. Sasa mwanamume huyo, mke wake, na watoto wawili kati ya watoto wao watano wamebatizwa. Wanahubiri habari njema kwa bidii wakiwa na uhuru wa kusema.

Unapochagua Marafiki

Je, kushirikiana na watu ambao si wa imani yetu ni uamuzi wa kibinafsi tu ambao hauhusishi kanuni zozote za Biblia? Dada mmoja alitaka kwenda kwenye karamu pamoja na kijana ambaye si Mkristo wa kweli. Ingawa dada huyo alionywa kuhusu hatari, aliona kwamba ana haki ya kufanya hivyo na basi akaenda kwenye karamu hiyo. Muda mfupi baada ya kufika kwenye karamu, dada huyo alipewa kinywaji kilichotiwa dawa kali ya kulevya. Aliamka saa kadhaa baadaye na kupata kwamba amenajisiwa na kijana huyo aliyedai kuwa rafiki yake.—Linganisha na Mwanzo 34:2.

Ingawa kushirikiana na watu ambao si waamini hakuongozi kila wakati kwenye hatari kama hiyo, Biblia inaonya hivi: “Anayetembea na watu wenye hekima atakuwa na hekima, lakini anayeshirikiana na wajinga atapatwa na mabaya.” (Met. 13:20) Ni wazi kwamba kuchagua mashirika yasiyofaa ni hatari! Andiko la Methali 22:3 linasema hivi: “Mtu mwerevu ni yule ambaye ameona msiba na kujificha, lakini wasio na uzoefu wameendelea mbele nao lazima waumie.” Wale tunaoshirikiana nao wanaweza kutupotosha na kuharibu uhusiano wetu pamoja na Mungu.—1 Kor. 15:33; Yak. 4:4.

Katika Mavazi na Mapambo

Mitindo inabadilika kila wakati. Hata hivyo, kanuni za Biblia kuhusu mavazi na mapambo hazibadiliki. Paulo aliwahimiza wanawake Wakristo “wajipambe kwa mavazi yenye mpangilio mzuri, pamoja na kiasi na utimamu wa akili”—na kanuni hiyo inawahusu wanaume pia. (1 Tim. 2:9) Paulo hakuwa akipendekeza kwamba watu wasivalie nguo maridadi, wala hakumaanisha kwamba Wakristo wote wanapaswa kuvalia kwa mtindo mmoja. Lakini namna gani kuhusu sifa ya kiasi? Kuwa na kiasi kunahusisha kutojifikiria kuwa bora sana. Kunatia ndani pia kuvalia, kusema, na kujiendesha kwa njia inayofaa.

Tunapaswa kujiuliza hivi: ‘Je, kweli mimi ni mwenye kiasi ikiwa ninasisitiza kwamba nina haki ya kuvaa ninavyopenda ingawa mavazi yangu yanafanya wengine wanitazame sana? Je, njia yangu ya kuvalia inafanya wengine wawe na maoni yasiyofaa kunihusu au kuhusu maadili yangu?’ Tunaweza kuepuka ‘kutoa sababu yoyote ya kukwaza’ kwa ‘kuendelea kuangalia, si faida za kibinafsi za mambo yetu wenyewe tu, bali pia faida za kibinafsi za wengine.’—2 Kor. 6:3; Flp. 2:4.

Katika Mambo ya Kibiashara

Matatizo mazito yalipotokea kuhusu shughuli zilizopotoka au za upunjaji katika kutaniko la Korintho, Paulo aliandika hivi: “Kwa nini msiache mkosewe badala ya hivyo? Kwa nini msiache mpunjwe badala ya hivyo?” Paulo aliwashauri Wakristo kuwa tayari kupata hasara fulani badala ya kumpeleka ndugu mahakamani. (1 Kor. 6:1-7) Ndugu mmoja nchini Marekani alichukua kwa uzito shauri hilo. Hakuelewana na mkubwa wake kazini kuhusu pesa za mshahara ambazo alimdai mkubwa wake huyo ambaye alikuwa Mkristo. Kwa kufuata mwongozo wa Maandiko, ndugu hao wawili walikutana mara kwa mara bila kutatua tatizo lao. Mwishowe, walifikisha jambo hilo mbele ya “kutaniko,” ambalo linawakilishwa na wazee Wakristo.—Mt. 18:15-17.

Inasikitisha kwamba tatizo hilo bado halikuweza kutatuliwa. Baada ya kusali sana, mfanyakazi huyo aliamua kupoteza pesa nyingi alizokuwa akimdai mkubwa wake. Kwa nini? Baadaye alisema hivi: “Hali hiyo ya kutoelewana ilikuwa ikininyima shangwe na kuchukua muda mwingi wenye thamani ambao ningeweza kutumia kwa mambo ya kiroho.” Baada ya kufanya uamuzi huo, ndugu huyo alianza kupata shangwe tena, naye akaona baraka za Yehova juu ya utumishi wake.

Hata Katika Mambo Madogo

Tunapata baraka tusiposhikilia mapendezi yetu hata katika mambo madogo. Siku ya kwanza ya kusanyiko la wilaya, wenzi fulani wa ndoa mapainia walifika mapema na kuhifadhi viti mahali walipotaka kukaa. Programu ilipokuwa ikianza, familia kubwa yenye watoto kadhaa iliingia haraka katika uwanja uliokuwa tayari umejaa. Wenzi hao mapainia waliona kwamba familia hiyo inatafuta mahali pa kuketi, hivyo wakawaachia viti vyao viwili. Hivyo, familia hiyo yote iliweza kuketi pamoja. Siku chache baada ya kusanyiko, mapainia hao walipokea barua ya shukrani kutoka kwa familia hiyo. Katika barua hiyo, walieleza jinsi walivyovunjika moyo sana walipofika kwenye kusanyiko wakiwa wamechelewa. Lakini wakapata shangwe na kushukuru kwa sababu ya fadhili ambazo mapainia hao waliwaonyesha.

Tunapopata nafasi, acheni tujinyime mapendezi yetu kwa faida ya wengine. Tunapoonyesha upendo ambao “hautafuti faida zake wenyewe,” tunasaidia kudumisha amani katika kutaniko na pamoja na majirani wetu. (1 Kor. 13:5) Lakini jambo la maana hata zaidi ni kwamba tunaendelea kuwa marafiki wa Yehova.

[Picha katika ukurasa wa 20]

Je, uko tayari kuacha mapendezi yako unapochagua mitindo ya mavazi?

[Picha katika ukurasa wa 20, 21]

Je, uko tayari kuwaachia ndugu zako kiti chako?