Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi Maneno ya Yesu Yanavyoleta Furaha

Jinsi Maneno ya Yesu Yanavyoleta Furaha

Jinsi Maneno ya Yesu Yanavyoleta Furaha

‘Yesu akapanda mlimani; na wanafunzi wake wakamjia; naye akaanza kuwafundisha.’—MT. 5:1, 2.

1, 2. (a) Yesu alitoa Mahubiri yake ya Mlimani katika hali gani? (b) Yesu alianza hotuba yake jinsi gani?

NI MWAKA wa 31 W.K. Yesu anasimamisha kwa muda mfupi safari yake ya kuhubiri Galilaya ili kwenda kuadhimisha Pasaka huko Yerusalemu. (Yoh. 5:1) Anaporudi Galilaya, anasali usiku wote na kuomba mwongozo wa Mungu katika kuchagua mitume 12. Siku inayofuata, umati wa watu unakusanyika Yesu anapoponya wagonjwa. Akiwa na wanafunzi wake pamoja na watu wengine, anaketi mlimani na kuanza kufundisha.—Mt. 4:23–5:2; Luka 6:12-19.

2 Yesu anaanza hotuba yake—Mahubiri yake ya Mlimani—kwa kuonyesha kwamba furaha inatokana na kuwa na uhusiano mzuri pamoja na Mungu. (Soma Mathayo 5:1-12.) Furaha ni ‘hali njema inayotokana na uradhi na shangwe nyingi.’ Mambo tisa yanayoleta furaha ambayo Yesu alitaja yanaonyesha kwa nini Wakristo ni wenye furaha, na mambo hayo ni yenye faida leo kama yalivyokuwa miaka 2,000 hivi iliyopita. Acheni sasa tuchunguze kila moja ya mambo hayo tisa.

“Wale Wanaotambua Uhitaji Wao wa Kiroho”

3. Inamaanisha nini kutambua uhitaji wetu wa kiroho?

3 “Wenye furaha ni wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho, kwa kuwa ufalme wa mbinguni ni wao.” (Mt. 5:3) “Wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho” wanajua kwamba wanahitaji mwongozo na rehema za Mungu.

4, 5. (a) Kwa nini wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho ni wenye furaha? (b) Tunaweza kutosheleza jinsi gani uhitaji wetu wa kiroho?

4 Wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho ni wenye furaha, “kwa kuwa ufalme wa mbinguni ni wao.” Kumkubali Yesu akiwa Masihi kuliwapa wanafunzi wake wa mapema nafasi ya kutawala pamoja naye katika Ufalme wa Mungu huko mbinguni. (Luka 22:28-30) Iwe tunatumaini kuwa warithi pamoja na Kristo huko mbinguni au tunatazamia uzima wa milele katika paradiso duniani chini ya utawala wa Ufalme, tunaweza kuwa wenye furaha ikiwa kwa kweli tunatambua uhitaji wetu wa kiroho na kutambua kabisa kwamba tunamtegemea Mungu.

5 Si watu wote wanaotambua uhitaji wao wa kiroho, kwa sababu wengi hawana imani na hawathamini mambo matakatifu. (2 The. 3:1, 2; Ebr. 12:16) Tunaweza kutosheleza uhitaji wetu wa kiroho kwa kujifunza Biblia kwa bidii, kushiriki kwa bidii katika kazi ya kufanya wanafunzi, na kuhudhuria kwa ukawaida mikutano ya Kikristo.—Mt. 28:19, 20; Ebr. 10:23-25.

Waombolezaji “Wenye Furaha”

6. Ni nani “wale wanaoomboleza,” na kwa nini ni “wenye furaha”?

6 “Wenye furaha ni wale wanaoomboleza, kwa kuwa watafarijiwa.” (Mt. 5:4) “Wale wanaoomboleza” ni sawa na “wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho.” Hawaombolezi kwa kulalamika kuhusu hali yao maishani. Wanaomboleza kwa kuhuzunika kwa sababu ya hali yao ya dhambi na pia hali zilizopo za kutokamilika kwa wanadamu. Kwa nini waombolezaji hao ni “wenye furaha”? Ni kwa sababu wanamwamini Mungu na Kristo na wanafarijiwa kwa kuwa na uhusiano mzuri pamoja na Yehova.—Yoh. 3:36.

7. Tunapaswa kuhisi jinsi gani kuhusu ulimwengu wa Shetani?

7 Tukiwa mtu mmoja-mmoja, je, tunaomboleza kwa sababu ya kuenea kwa ukosefu wa uadilifu katika ulimwengu wa Shetani? Tunahisi jinsi gani kuhusu ahadi za ulimwengu huu? Mtume Yohana aliandika hivi: “Kila kitu kilicho katika ulimwengu—tamaa ya mwili na tamaa ya macho na mtu kujionyesha mali yake maishani—hakitokani na Baba.” (1 Yoh. 2:16) Lakini namna gani ikiwa tunahisi kwamba “roho ya ulimwengu,” yaani, nguvu zinazotawala wanadamu waliotengwa mbali na Mungu, inamomonyoa hali yetu ya kiroho? Ikiwa tunahisi hivyo, basi tusali kwa bidii, tujifunze Neno la Mungu, na tutafute msaada wa wazee. Tukimkaribia Yehova zaidi, ‘tutajipatia faraja,’ hata iwe tunafadhaishwa na jambo gani.—1 Kor. 2:12; Zab. 119:52; Yak. 5:14, 15.

“Walio na Tabia-Pole” Ni Wenye Furaha Sana!

8, 9. Inamaanisha nini kuwa mwenye tabia-pole, na kwa nini watu wenye tabia-pole ni wenye furaha?

8 “Wenye furaha ni wale walio na tabia-pole, kwa kuwa watairithi dunia.” (Mt. 5:5) “Tabia-pole,” au upole, si udhaifu au upole wa kinafiki. (1 Tim. 6:11) Ikiwa sisi ni wenye tabia-pole, tutaonyesha upole kwa kufanya mapenzi ya Yehova na kukubali mwongozo wake. Pia, tabia-pole itaonekana wazi kwa namna tunavyoshughulika na waamini wenzetu na watu wengine. Upole kama huo unapatana na shauri la mtume Paulo.—Soma Waroma 12:17-19.

9 Kwa nini walio na tabia-pole ni wenye furaha? Kwa sababu Yesu, mwenye tabia-pole, alisema “watairithi dunia.” Yeye ndiye Mrithi wa kwanza wa dunia. (Zab. 2:8; Mt. 11:29; Ebr. 2:8, 9) Hata hivyo, “warithi pamoja na Kristo” watarithi pia dunia. (Rom. 8:16, 17) Katika makao ya kidunia ya Ufalme wa Yesu, wapole wengine wengi watafurahia uzima wa milele.—Zab. 37:10, 11.

10. Kukosa upole kunaweza kuwa na matokeo gani kwa mapendeleo yetu ya utumishi na uhusiano wetu pamoja na wengine?

10 Kama Yesu, tunapaswa kuwa wenye tabia-pole. Lakini namna gani ikiwa tunajulikana kuwa na mwelekeo wa kutaka vita? Huenda mwelekeo huo wa ukali na uadui ukafanya watu watuepuke kabisa. Ikiwa sisi ni ndugu ambao wanatamani kuwa na mapendeleo katika kutaniko, mwelekeo huo unatufanya tusistahili kupewa mapendeleo hayo. (1 Tim. 3:1, 3) Paulo alimwambia Tito aendelee kuwakumbusha Wakristo wa huko Krete “wasiwe wataka-vita, wawe wenye usawaziko, wakionyesha upole wote kuelekea watu wote.” (Tito 3:1, 2) Upole kama huo ni baraka kwa wengine kama nini!

Wana Njaa ya “Uadilifu”

11-13. (a) Inamaanisha nini kuwa na njaa na kiu kwa ajili ya uadilifu? (b) Wale walio na njaa na kiu kwa ajili ya uadilifu ‘wanashibishwa’ jinsi gani?

11 “Wenye furaha ni wale walio na njaa na walio na kiu kwa ajili ya uadilifu, kwa kuwa watashibishwa.” (Mt. 5:6) “Uadilifu” ambao Yesu alikuwa akizungumzia ni sifa ya kufanya yaliyo sawa kupatana na mapenzi na amri za Mungu. Mtunga-zaburi alisema kwamba alikuwa ‘amepondeka kwa kutamani’ maamuzi yenye uadilifu ya hukumu za Mungu. (Zab. 119:20) Je, tunathamini sana uadilifu hivi kwamba tuna njaa na kiu ya kupata sifa hiyo?

12 Yesu alisema kwamba wale walio na njaa na kiu ya uadilifu watakuwa wenye furaha kwa sababu “watashibishwa,” au watatoshelezwa kabisa. Hilo liliwezekana baada ya Pentekoste mwaka wa 33 W.K., kwa kuwa wakati huo roho takatifu ya Yehova ilianza ‘kuupa ulimwengu uthibitisho wenye kusadikisha kuhusu uadilifu.’ (Yoh. 16:8) Kupitia roho takatifu, Mungu aliwaongoza wanaume kuandika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, ambayo ni yenye faida sana “kwa kutia nidhamu katika uadilifu.” (2 Tim. 3:16) Pia, roho ya Mungu inatuwezesha “kuvaa utu mpya ulioumbwa kulingana na mapenzi ya Mungu katika uadilifu wa kweli.” (Efe. 4:24) Je, haifariji sana kujua kwamba wale wanaotubu na kutafuta msamaha wa dhambi zao kwa msingi wa dhabihu ya ukombozi ya Yesu wanaweza kuwa na msimamo wa uadilifu machoni pa Mungu?—Soma Waroma 3:23, 24.

13 Ikiwa tuna tumaini la kuishi duniani, njaa na kiu yetu kwa ajili ya uadilifu itatoshelezwa kabisa wakati tutakapopokea uzima wa milele chini ya hali zenye uadilifu duniani. Tunapongojea wakati huo, acheni tuazimie kuishi kulingana na viwango vya Yehova. Yesu alisema: “Endeleeni kuutafuta kwanza ufalme na uadilifu [wa Mungu].” (Mt. 6:33) Kufanya hivyo kutatuwezesha kuwa na mengi ya kufanya katika kazi ya Mungu na hivyo mioyo yetu itajawa na furaha ya kweli.—1 Kor. 15:58.

Kwa Nini “Wale Walio na Rehema” Ni Wenye Furaha?

14, 15. Tunaweza kuonyesha rehema jinsi gani, na kwa nini “wale walio na rehema” ni wenye furaha?

14 “Wenye furaha ni wale walio na rehema, kwa kuwa wataonyeshwa rehema.” (Mt. 5:7) “Wale walio na rehema” wanachochewa na huruma na wanawasikitikia wengine. Yesu aliwaponya kimuujiza watu wengi waliokuwa wakiteseka kwa kuwa aliwasikitikia. (Mt. 14:14) Rehema inaonyeshwa katika maana ya kihukumu wakati watu wanapowasamehe wale wanaowakosea, kama vile tu Yehova anavyowasamehe wale wanaotubu. (Kut. 34:6, 7; Zab. 103:10) Tunaweza kuonyesha rehema katika njia hiyo na kwa maneno na matendo yetu ya fadhili ambayo yanawafariji watu wa hali ya chini. Njia bora ya kuonyesha rehema ni kuwaambia wengine kweli za Biblia. Kwa sababu ya kuusikitikia umati, Yesu ‘alianza kuwafundisha mambo mengi.’—Marko 6:34.

15 Tuna sababu nzuri ya kukubaliana na maneno ya Yesu: “Wenye furaha ni wale walio na rehema, kwa kuwa wataonyeshwa rehema.” Tukiwatendea wengine kwa rehema, inaelekea wao pia watatutendea kwa rehema. Hivyo basi, ikiwa tumewaonyesha wengine rehema, huenda Mungu akaamua kutoleta hukumu kali juu yetu wakati anapotuhukumu. (Yak. 2:13) Wenye rehema ndio tu wanaostahili kusamehewa dhambi na kupata uzima wa milele.—Mt. 6:15.

Kwa Nini “Wale Walio Safi Moyoni” Ni Wenye Furaha?

16. Inamaanisha nini kuwa “safi moyoni,” na wale walio na sifa hiyo ‘wanamwona Mungu’ jinsi gani?

16 “Wenye furaha ni wale walio safi moyoni, kwa kuwa watamwona Mungu.” (Mt. 5:8) Ikiwa sisi ni “safi moyoni,” usafi huo utaonekana wazi katika mahusiano, tamaa, na nia yetu. Tutaonyesha “upendo kutokana na moyo safi.” (1 Tim. 1:5) Tukiwa safi kwa ndani ‘tutamwona Mungu.’ Hilo halimaanishi hasa kumwona Yehova kihalisi, kwa kuwa “hakuna mwanadamu anayeweza [kumwona Mungu] na bado aishi.” (Kut. 33:20) Hata hivyo, kwa kuwa alionyesha kwa ukamilifu utu wa Mungu, Yesu alisema hivi: “Yule ambaye ameniona mimi amemwona Baba pia.” (Yoh. 14:7-9) Tukiwa waabudu wa Yehova duniani, tunaweza ‘kumwona Mungu’ kwa kuona jinsi anavyotenda kwa faida yetu. (Ayu. 42:5) Wakristo watiwa-mafuta wanamwona Mungu kwa njia isiyo na kifani wanapofufuliwa kwenye uhai wa roho na kumwona kihalisi Baba yao wa mbinguni.—1 Yoh. 3:2.

17. Kuwa safi moyoni kutakuwa na uvutano gani juu yetu?

17 Kwa kuwa mtu aliye na moyo safi ni safi kiadili na kiroho, hakazii fikira mambo ambayo ni machafu machoni pa Yehova. (1 Nya. 28:9; Isa. 52:11) Ikiwa sisi ni safi moyoni, yale tunayosema na tunayofanya yatakuwa safi, na hakutakuwa na jambo lolote la unafiki katika utumishi wetu kwa Yehova.

“Wale Wanaofanya Amani” Wanakuwa Wana wa Mungu

18, 19. “Wale wanaofanya amani” wanajiendesha jinsi gani?

18 “Wenye furaha ni wale wanaofanya amani, kwa kuwa wataitwa ‘wana wa Mungu.’” (Mt. 5:9) “Wale wanaofanya amani” wanatambuliwa kwa yale wanayofanya na kwa yale ambayo hawawezi kufanya. Ikiwa sisi ni aina ya watu ambao Yesu alikuwa akizungumzia, basi sisi ni wafanya-amani na hivyo ‘hatumlipi yeyote ubaya kwa ubaya.’ Badala yake, ‘sikuzote tunafuatilia yaliyo mema kuelekea wengine.’—1 The. 5:15.

19 Ili tuwe kati ya wale wanaofanya amani, ni lazima tujitahidi kuendeleza amani. Wale wanaofanya amani hawafanyi jambo lolote ambalo ‘linawatenganisha wale wanaofahamiana.’ (Met. 16:28) Tukiwa watu wanaofanya amani, tunachukua hatua zinazofaa ili ‘kufuatilia amani pamoja na watu wote.’—Ebr. 12:14.

20. Kwa sasa “wana wa Mungu” ni nani, na mwishowe ni nani wengine watakaokuwa watoto wa Mungu?

20 Wale wanaofanya amani ni wenye furaha kwa sababu “wataitwa ‘wana wa Mungu.’” Wakristo watiwa-mafuta waaminifu wamefanywa na Yehova kuwa wana, nao ni “wana wa Mungu.” Tayari wana uhusiano wa karibu pamoja na Yehova wakiwa watoto wake kwa sababu wana imani katika Kristo na wanamwabudu kwa moyo wote “Mungu wa upendo na wa amani.” (2 Kor. 13:11; Yoh. 1:12) Namna gani “kondoo wengine” wa Yesu wanaofanya amani? Yesu atakuwa ‘Baba yao wa Milele’ wakati wa Utawala wake wa Miaka Elfu, lakini mwishoni mwa miaka hiyo yeye mwenyewe atajitiisha kwa Yehova na hao kondoo wengine watakuwa watoto wa Mungu kwa ukamili.—Yoh. 10:16; Isa. 9:6; Rom. 8:21; 1 Kor. 15:27, 28.

21. Tutatenda jinsi gani ikiwa “tunaishi kwa roho”?

21 Ikiwa “tunaishi kwa roho,” amani itakuwa moja ya sifa zetu ambazo wengine wataona wazi. ‘Hatutachochea mashindano juu ya mtu na mwenzake’ au “kuchokozana . . . mtu na mwingine.” (Gal. 5:22-26; New International Version) Badala yake, tutajitahidi kuwa “wenye kufanya amani na watu wote.”—Rom. 12:18.

Wenye Furaha Ingawa Wanateswa!

22-24. (a) Kwa nini wale wanaoteswa kwa ajili ya uadilifu ni wenye furaha? (b) Tutachunguza nini katika makala mbili zinazofuata?

22 “Wenye furaha ni wale ambao wameteswa kwa ajili ya uadilifu, kwa kuwa ufalme wa mbinguni ni wao.” (Mt. 5:10) Kisha, Yesu akaongezea hivi: “Wenye furaha ni ninyi wakati watu wanapowashutumu na kuwatesa na kusema kwa uwongo kila namna ya jambo baya juu yenu kwa ajili yangu. Shangilieni na kuruka kwa shangwe, kwa kuwa thawabu yenu ni kubwa mbinguni; kwa maana hivyo ndivyo walivyowatesa manabii waliokuwa kabla yenu.”Mt. 5:11, 12.

23 Kama manabii wa kale wa Mungu, Wakristo wanatazamia kushutumiwa, kuteswa, na kusemwa kwa uwongo “kwa ajili ya uadilifu.” Hata hivyo, tunapovumilia kwa uaminifu majaribu kama hayo, tunapata uradhi kwa kuwa tunamfurahisha na kumheshimu Yehova. (1 Pet. 2:19-21) Kuteseka hakuwezi kupunguza furaha yetu ya kumtumikia Yehova sasa au wakati ujao. Hakuwezi kupunguza furaha ya kutawala pamoja na Kristo katika Ufalme wa mbinguni au shangwe ya kupokea uzima wa milele tukiwa raia wa kidunia wa serikali hiyo. Baraka hizo ni uthibitisho wa kibali, wema, na ukarimu wa Mungu.

24 Kuna mambo mengi zaidi ya kujifunza kutokana na Mahubiri ya Mlimani. Mambo hayo yanazungumziwa katika makala mbili zinazofuata. Basi, acheni tuone jinsi tunavyoweza kutumia maneno hayo ya Yesu Kristo.

Ungesema Nini?

• Kwa nini “wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho” ni wenye furaha?

• Kwa nini “wale walio na tabia-pole” ni wenye furaha?

• Kwa nini Wakristo ni wenye furaha hata ingawa wanateswa?

• Kati ya mambo yanayoleta furaha ambayo Yesu alitaja, ni jambo gani linalokuvutia zaidi?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 7]

Mambo tisa yanayoleta furaha ambayo Yesu alizungumzia yana faida leo kama yalivyokuwa zamani

[Picha katika ukurasa wa 8]

Njia bora ya kuonyesha rehema ni kuwaambia wengine kweli za Biblia