Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Ufunuo—II

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Ufunuo—II

Neno la Yehova Liko Hai

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Ufunuo—II

NI JAMBO gani litakalowapata watu wanaomwabudu Yehova Mungu na wale wasiomwabudu? Shetani na roho wake waovu watapatwa na nini? Wanadamu watiifu watapata baraka gani wakati wa Utawala wa Kristo wa Miaka Elfu Moja? Majibu ya maswali hayo na maswali mengine ya maana yanafunuliwa katika kitabu cha Ufunuo 13:1–22:21. * Sura hizo zina maono 9 ya mwisho kati ya maono 16 ambayo mtume Yohana alipokea karibu mwisho wa karne ya kwanza W.K.

Yohana anaandika hivi: “Mwenye furaha ni yeye anayesoma kwa sauti na wale wanaosikia maneno ya unabii huu, na wanaoshika mambo yaliyoandikwa humo.” (Ufu. 1:3; 22:7) Kusoma na kutumia mambo tunayojifunza katika kitabu cha Ufunuo kunaweza kuchochea moyo wetu, kuimarisha imani yetu katika Mungu na Mwana wake, Yesu Kristo, na kutupa tumaini zuri la wakati ujao. *Ebr. 4:12.

MABAKULI SABA YA HASIRA YA MUNGU YANAMWAGWA

(Ufu. 13:1–16:21)

Andiko la Ufunuo 11:18 linasema: “Mataifa wakawa na ghadhabu, nayo ghadhabu [ya Mungu] mwenyewe ikaja, na wakati uliowekwa kwa ajili ya . . . kuwaharibu wale wanaoiharibu dunia.” Maono ya nane yanatoa muktadha wa jambo hilo kwa kuzungumzia utendaji wa “mnyama-mwitu . . . mwenye pembe kumi na vichwa saba.”—Ufu. 13:1.

Katika maono ya tisa, Yohana anamwona “Mwana-Kondoo amesimama juu ya Mlima Sayuni” na pamoja naye “144,000.” Wao “walinunuliwa kutoka kati ya wanadamu.” (Ufu. 14:1, 4) Matangazo ya kimalaika yanafuata. Katika maono yanayofuata, Yohana anaona “malaika saba wenye mapigo saba.” Inaonekana kwamba Yehova mwenyewe anawaamuru malaika hao kumwaga “mabakuli saba ya hasira ya Mungu” juu ya sehemu mbalimbali za ulimwengu wa Shetani. Mabakuli hayo yana matangazo na maonyo ya hukumu ambazo Mungu atatekeleza. (Ufu. 15:1; 16:1) Maono hayo mawili yanatoa habari kuhusu hukumu nyingine za Ufalme zinazohusiana na ole wa tatu na kupulizwa kwa tarumbeta ya saba.—Ufu. 11:14, 15.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

13:8—“Kitabu cha kukunjwa cha uzima cha Mwana-Kondoo” ni nini? Hicho ni kitabu cha kukunjwa cha mfano chenye majina ya wale watakaotawala pamoja na Yesu Kristo katika Ufalme wake wa mbinguni. Kina majina ya Wakristo watiwa-mafuta ambao bado wako duniani na ambao wana tumaini la kupokea uzima mbinguni.

13:11-13—Ni kwa njia gani mnyama-mwitu mwenye pembe mbili anatenda kama joka na kufanya moto ushuke kutoka mbinguni? Ukweli wa kwamba mnyama-mwitu mwenye pembe mbili, yaani, Serikali ya Ulimwengu ya Uingereza na Marekani, inazungumza kama joka unaonyesha kwamba serikali hiyo inawatisha watu, inawashinikiza, na inatumia jeuri ili kuwalazimisha wakubali njia yake ya kutawala. Serikali hiyo inafanya moto ushuke kutoka mbinguni katika maana ya kwamba inatenda kama nabii kwa kudai kwamba ilishinda uovu katika vile vita viwili vya ulimwengu vya karne ya 20 na vita juu ya Ukomunisti.

16:17— “Hewa” ambayo juu yake bakuli la saba linamwagwa inawakilisha nini? “Hewa” hiyo inawakilisha fikira za kishetani, “roho [mwelekeo wa akili] ambayo sasa hutenda katika wana wa kutotii.” Hewa hiyo yenye sumu inapumuliwa na mfumo wote mwovu wa mambo wa Shetani.—Efe. 2:2.

Mambo Tunayojifunza:

13:1-4, 18. “Mnyama-mwitu” anayewakilisha serikali za wanadamu anapanda “kutoka katika bahari,” yaani, kutoka katika jamii za wanadamu zenye msukosuko. (Isa. 17:12, 13; Dan. 7:2-8, 17) Mnyama huyo, aliyefanyizwa na kupewa nguvu na Shetani, ana namba 666, ambayo inawakilisha kutokamilika kabisa. Kuelewa mnyama-mwitu ni nani kunatusaidia tusimfuate kwa mshangao wala kumwabudu kama wanadamu wengine wanavyofanya.—Yoh. 12:31; 15:19.

13:16, 17. Hata tukikabili magumu gani katika shughuli zetu za kila siku kama vile “kununua au kuuza,” hatupaswi kukubali maisha yetu yatawaliwe na huyo mnyama-mwitu. Kukubali ‘alama ya mnyama-mwitu katika mkono wetu wa kuume au juu ya paji la uso wetu’ ni sawa na kukubali huyo mnyama-mwitu aongoze matendo yetu na mawazo yetu.

14:6, 7Tangazo la malaika linatufundisha kwamba tunapaswa kutangaza kwa haraka habari njema ya Ufalme wa Mungu uliosimamishwa. Tunapaswa kuwasaidia wanafunzi wetu wa Biblia wasitawishe woga unaofaa kumwelekea Yehova Mungu na kumpa utukufu.

14:14-20. “Mavuno ya dunia,” yaani, mavuno ya wale watakaookolewa yatakapomalizika, utakuwa wakati wa malaika kutupa “mzabibu wa dunia” uliokusanywa ndani ya “shinikizo kubwa la divai la hasira ya Mungu.” Kisha, mzabibu huo, yaani, mfumo wa Shetani wenye ufisadi wa serikali mbalimbali ambao unaonekana na ambao una “vishada” vya matunda maovu, utaharibiwa kabisa. Tunapaswa kuazimia kutoshawishiwa na mzabibu wa dunia.

16:13-16. Yale ‘maneno machafu yaliyoongozwa na roho’ yanawakilisha propaganda ya roho waovu ambayo imekusudiwa kuwafanya wafalme wa dunia wawe na uhakika kuwa hawatayumbishwa wakati mabakuli saba ya hasira ya Mungu yanapomwagwa, badala yake maneno hayo yanawaongoza wafalme hao wampinge Yehova.—Mt. 24:42, 44.

16:21. Kadiri mwisho wa ulimwengu huu unavyokaribia, huenda tangazo la hukumu za Yehova juu ya mfumo mwovu wa Shetani likahusisha maneno makali isivyo kawaida ya hukumu za Mungu, ambayo huenda yanafananishwa na maji ya barafu. Hata hivyo, wanadamu wengi wataendelea kumkufuru Mungu.

MFALME MSHINDI ANATAWALA

(Ufu. 17:1–22:21)

“Babiloni Mkubwa,” milki ya ulimwengu ya dini ya uwongo, ni sehemu yenye kuchukiza ya ulimwengu mwovu wa Shetani. Katika maono ya 11, anaonyeshwa akiwa “kahaba mkubwa”—mwanamke mwenye maadili yaliyopotoka—ambaye “ameketi juu ya mnyama-mwitu mwenye rangi nyekundu.” Ataharibiwa kabisa na “pembe kumi” za mnyama-mwitu anayembeba. (Ufu. 17:1, 3, 5, 16) Katika maono yanayofuata, kahaba huyo anafananishwa na “jiji kubwa,” tangazo la kuanguka kwake linatolewa, na watu wa Mungu wanaambiwa ‘watoke kwake’ haraka. Wengi wanaomboleza kwa sababu ya anguko la jiji hilo kubwa. Hata hivyo, kunakuwa na shangwe mbinguni kwa sababu ya “ndoa ya Mwana-Kondoo.” (Ufu. 18:4, 9, 10, 15-19; 19:7) Katika maono ya 13, mpandaji wa “farasi mweupe” anaenda kupigana na mataifa. Anakomesha ulimwengu mwovu wa Shetani.—Ufu. 19:11-16.

Namna gani “yule nyoka wa zamani, ambaye ni Ibilisi na Shetani”? Ni wakati gani ambapo ‘atatupwa ndani ya lile ziwa la moto’? Hayo ni kati ya mambo yanayozungumziwa katika maono ya 14. (Ufu. 20:2, 10) Maono mawili ya mwisho yanaonyesha jinsi maisha yatakavyokuwa wakati wa ile Miaka Elfu Moja. “Ufunuo” unapokaribia mwisho wake, Yohana anaona ‘mto wa maji ya uzima ukiteremka kupitia katikati ya njia pana,’ na mwaliko wa pekee unatolewa kwa “yeyote anayeona kiu.”—Ufu. 1:1; 22:1, 2, 17.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

17:16; 18:9, 10—Kwa nini “wafalme wa dunia” wanaombolezea tengenezo ambalo wao wenyewe wametokeza? Huzuni yao inachochewa na ubinafsi tu. Baada ya uharibifu wa Babiloni Mkubwa, wafalme wa dunia wanatambua kwamba Babiloni Mkubwa aliwasaidia sana. Babiloni Mkubwa alifanya matendo yao ya uonevu yaonekane kuwa yanakubaliwa na dini. Pia, Babiloni Mkubwa aliwasaidia kupata vijana wa kupigana vitani. Zaidi ya hayo, alitimiza daraka kubwa katika kuwatiisha watu.

19:12—Ni kwa njia gani Yesu tu ndiye anayejua jina lake ambalo halijatajwa? Inaonekana jina hilo linawakilisha cheo na mapendeleo, kama yale yanayotajwa kwenye Isaya 9:6, ambayo Yesu anafurahia katika siku ya Bwana. Hakuna anayejua jina hilo ila yeye mwenyewe kwa kuwa mapendeleo yake ni ya pekee na ni yeye tu anayeweza kuelewa kinachomaanishwa na kuwa na cheo hicho cha juu. Hata hivyo, Yesu anashiriki mapendeleo fulani na washiriki wa jamii ya bibi-arusi wake, hivyo ni kana kwamba ‘anaandika juu yao hilo jina lake jipya.’—Ufu. 3:12.

19:14—Ni nani watakaomfuata Yesu juu ya farasi wakati wa Har–Magedoni? ‘Majeshi ya mbinguni’ yanayojiunga na Yesu katika vita vya Mungu yanatia ndani malaika na watiwa-mafuta washindi ambao tayari wamepokea thawabu yao ya kimbingu.—Mt. 25:31, 32; Ufu. 2:26, 27.

20:11-15—Ni majina ya nani ambayo yameandikwa katika “kitabu [cha kukunjwa] cha uzima”? Kitabu hicho cha kukunjwa kina majina ya wote wale wanaotarajia kupokea uzima wa milele—Wakristo watiwa-mafuta, washiriki wa umati mkubwa, na watumishi waaminifu wa Mungu ambao watapata “ufufuo wa waadilifu.” (Mdo. 24:15; Ufu. 2:10; 7:9) Majina ya wale watakaofufuliwa katika ‘ufufuo wa wasio waadilifu’ yataandikwa katika ‘kitabu cha kukunjwa cha uzima’ ikiwa tu watatenda kupatana na “mambo yale yaliyoandikwa katika vile vitabu” vyenye maagizo ambavyo vitafunguliwa wakati wa ile Miaka Elfu Moja. Hata hivyo, majina hayo hayajaandikwa kwa wino usiofutika. Majina ya watiwa-mafuta yanaandikwa kwa wino wa kudumu wanapokuwa waaminifu mpaka kifo. (Ufu. 3:5) Majina ya wale wanaopokea uzima duniani yanaandikwa kwa njia ya kudumu wanapopita mtihani wa mwisho mwishoni mwa ile miaka elfu.—Ufu. 20:7, 8.

Mambo Tunayojifunza:

17:3, 5, 7, 16. “Hekima inayotoka juu” inatusaidia kuelewa “fumbo la yule mwanamke na la yule mnyama-mwitu [mwenye rangi nyekundu] anayembeba.” (Yak. 3:17) Mnyama-mwitu huyo wa mfano alianza akiwa Ushirika wa Mataifa na baadaye akawa Umoja wa Mataifa. Je, kufumbuliwa kwa fumbo hilo hakupaswi kutuchochea tuwe na bidii zaidi katika kuhubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu na kutangaza siku ya hukumu ya Yehova?

21:1-6. Tunaweza kuwa na uhakika kabisa kwamba baraka zilizotabiriwa zitakuwepo wakati wa utawala wa Ufalme. Kwa nini? Kwa sababu kuhusu baraka hizo au mambo hayo inasemwa hivi: “Yamekuwa!”

22:1, 17. “Mto wa maji ya uzima” unawakilisha maandalizi ya Yehova ya kuwakomboa wanadamu watiifu kutoka katika dhambi na kifo. Maji hayo yanapatikana kwa kiasi fulani sasa. Na tukubali kwa uchangamfu mwaliko wa kuja na ‘kuchukua maji ya uzima bure’ na pia kuwatolea wengine kwa shauku mwaliko huo!

[Maelezo ya chini]

^ fu. 4 Ili upate maelezo ya mstari kwa mstari ya kitabu cha Ufunuo, ona kitabu Ufunuo—Upeo Wao Mtukufu U Karibu!

[Picha katika ukurasa wa 5]

Wanadamu watiifu watapata baraka nzuri ajabu chini ya utawala wa Ufalme!