Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mazishi ya Kikristo Ni Yenye Heshima, Kiasi, na Yanampendeza Mungu

Mazishi ya Kikristo Ni Yenye Heshima, Kiasi, na Yanampendeza Mungu

Mazishi ya Kikristo Ni Yenye Heshima, Kiasi, na Yanampendeza Mungu

WATU wanalia kwa huzuni. Waombolezaji ambao wamevaa mavazi meusi ya pekee wanaomboleza na kujitupa-tupa chini kwa huzuni. Wachezaji wa dansi wanacheza dansi kulingana na mdundo wa muziki unaopigwa. Lakini wengine wanakula na kusherehekea wakicheka kwa sauti na kwa shangwe. Wachache wamelala chini kwa kuwa wamelewa kutokana na pombe ya mnazi na pombe ya aina nyingine inayotiririka kama maji. Kwani kuna sherehe gani? Katika sehemu fulani za ulimwengu, mambo hayo yanaonekana wakati wa mazishi ambapo mamia ya watu wanakusanyika kuwaaga wafu.

Mashahidi wengi wa Yehova wanaishi katika jamii ambazo watu wa ukoo na marafiki wanaamini sana ushirikina na wanaogopa wafu. Mamilioni ya watu wanaamini kwamba mtu anapokufa, anageuka na kuwa roho ya mababu yenye nguvu za kuwasaidia au kuwaumiza walio hai. Imani hiyo inahusiana sana na desturi nyingi za mazishi. Bila shaka, ni kawaida kuhuzunika mtu anapokufa. Pindi fulani, Yesu na wanafunzi wake waliomboleza kwa sababu ya vifo vya wapendwa wao. (Yoh. 11:33-35, 38; Mdo. 8:2; 9:39) Lakini hakuna wakati ambapo walijihusisha katika matendo ya kuomboleza kupita kiasi yaliyofanywa na wengi katika siku zao. (Luka 23:27, 28; 1 The. 4:13) Kwa nini? Sababu moja ni kwamba walijua ukweli kuhusu kifo.

Biblia inasema hivi waziwazi: “Walio hai wanajua kwamba watakufa; lakini wafu, hawajui lolote kamwe . . . Upendo wao na chuki yao na wivu wao tayari zimepotea . . . Hakuna kazi, wala utungaji wala ujuzi wala hekima katika Kaburi, mahali unapokwenda.” (Mhu. 9:5, 6, 10) Mistari hiyo ya Biblia inaonyesha wazi kwamba mtu anapokufa, hana fahamu tena. Hawezi kufikiri, kuhisi, kuwasiliana na watu, au kuelewa chochote. Kuelewa ukweli huo muhimu wa Biblia kunapaswa kubadili jinsi gani maoni yetu kuhusu mazishi ya Kikristo?

“Mwache Kugusa Kitu Kilicho Najisi”

Hata wawe wa kabila au utamaduni gani, Mashahidi wa Yehova wanaepuka kabisa desturi zozote zinazohusiana na imani ya kwamba wafu wana fahamu na wanaweza kuwa na uvutano juu ya walio hai. Desturi kama vile kukesha, sherehe za baada ya mazishi, sherehe za kila mwaka za kukumbuka siku ya mazishi, kutoa dhabihu kwa ajili ya wafu, na desturi za kuwatakasa wajane ni chafu na hazimpendezi Mungu kwa sababu zinahusiana na fundisho lisilo la Kimaandiko na la kishetani la kwamba nafsi au roho haifi. (Eze. 18:4) Wakristo wa kweli ‘hawawezi kunywa kikombe cha Yehova na kikombe cha roho waovu,’ kwa hiyo hawashiriki katika desturi hizo. (1 Kor. 10:21) Wanatii amri hii: “Mjitenge, . . . na mwache kugusa kitu kilicho najisi.” (2 Kor. 6:17) Hata hivyo, si rahisi nyakati zote kuchukua msimamo huo.

Katika Afrika na kwingineko, watu wengi wanaamini kwamba desturi fulani zisipofuatwa, roho za mababu zitakasirika. Kukosa kufuata desturi hizo kunaonwa kuwa kosa zito linaloweza kumfanya mtu alaaniwe na watu katika jamii au apatwe na msiba. Kwa sababu ya kukataa kushiriki katika desturi za mazishi zisizopatana na Maandiko, watu wengi wa Yehova wameshutumiwa, wametukanwa, na kukataliwa na watu wa kijiji chao au watu wa familia zao. Hata wengine wamelaumiwa kuwa watu wasiotaka kuchangamana na wengine na wasiowaheshimu wafu. Nyakati nyingine, watu ambao si waamini wameingilia mipango ya mazishi ya Mkristo. Hivyo basi, tunaweza kufanya nini ili kuepuka kupambana na watu wanaosisitiza sana kufuata desturi za mazishi ambazo hazimpendezi Mungu? Zaidi ya yote, tunaweza kufanya nini ili kuendelea kujitenga na desturi na mazoea yasiyo safi ambayo yanaweza kuharibu uhusiano wetu pamoja na Yehova?

Eleza Msimamo Wako Waziwazi

Katika sehemu fulani za ulimwengu, ni kawaida kwa wazee wa ukoo na watu wengine wa ukoo ambao si sehemu ya familia ya karibu kufanya maamuzi yanayohusu mazishi. Hivyo, ni lazima Mkristo mwaminifu aseme wazi kwamba mazishi yake yatapangwa na kufanywa na Mashahidi wa Yehova kupatana na kanuni za Biblia. (2 Kor. 6:14-16) Wakati wa mazishi ya Kikristo, hatupaswi kufanya mambo ambayo yatasumbua dhamiri za waamini wenzetu au kuwakwaza wengine wanaojua mambo tunayoamini na mambo tunayofundisha kuhusu wafu.

Mwakilishi wa kutaniko la Kikristo anapoombwa aongoze mazishi, wazee waliowekwa rasmi wanaweza kutoa mapendekezo yanayofaa na kuwategemeza kiroho waliofiwa ili mipango yote ipatane na miongozo ya Kimaandiko. Watu fulani ambao si Mashahidi wakitaka kuingiza mazoea yasiyo safi, ni muhimu kusimama imara na kueleza kwa ujasiri msimamo wetu wa Kikristo kwa fadhili na kwa heshima. (1 Pet. 3:15) Lakini namna gani watu wa ukoo ambao si waamini wakisisitiza kuingiza desturi zisizo safi katika mipango yenu? Basi familia ya waamini inaweza kuamua kujiondoa katika mazishi hayo. (1 Kor. 10:20) Hilo linapotukia, hotuba fupi ya mazishi inaweza kutolewa kwenye Jumba la Ufalme au mahali pengine panapofaa ili kuwapa “faraja kutokana na Maandiko” wale ambao wamehuzunishwa kikweli na kifo cha mpendwa wao. (Rom. 15:4) Hata ingawa mwili wa aliyekufa hautakuwepo, mpango huo ni wenye kuheshimika na unafaa kabisa. (Kum. 34:5, 6, 8) Vurugu zinazosababishwa na watu ambao si waamini zinaweza kuzidisha mfadhaiko na huzuni kwenye pindi hiyo, lakini tunaweza kufarijiwa tunapokumbuka kwamba Mungu anaona azimio letu la kufanya yaliyo sawa, naye anaweza kutupa “nguvu zinazopita zile za kawaida.”—2 Kor. 4:7.

Andika Msimamo Wako

Mtu anapoandika maagizo yake kuhusu mipango ya mazishi yake, ni rahisi zaidi kuelewana na watu wa familia ambao si Mashahidi, kwa kuwa inaelekea wataheshimu matakwa ya aliyekufa. Mambo ya maana yanayohitaji kuandikwa yanatia ndani jinsi ambavyo mazishi yatafanywa, mahali ambapo yatafanyiwa, na wale wenye mamlaka pekee ya kupanga na kusimamia mazishi hayo. (Mwa. 50:5) Hati ambayo imetiwa sahihi mbele ya mashahidi ina uzito sana. Wale wanaopangia wakati ujao kwa busara na hekima wakitegemea kanuni za Biblia wanajua kwamba hawahitaji kungoja mpaka wanapozeeka sana au kuwa wagonjwa karibu kufa ili wachukue hatua hiyo.—Met. 22:3; Mhu. 9:12.

Wengine wameogopa kuandika maagizo kama hayo. Lakini kufanya hivyo kunaonyesha kwamba mtu ni Mkristo mkomavu na anawapenda wengine. (Flp. 2:4) Ni afadhali kushughulikia mambo hayo kibinafsi kuliko kuwaachia watu wa familia wayashughulikie, kwa kuwa wanaweza kushurutishwa wakubali mazoea yasiyo safi ambayo mtu aliyekufa hakuyaamini wala kuyakubali.

Mazishi Yawe ya Kiasi

Katika sehemu nyingi za Afrika, watu wengi wanaamini kwamba ni lazima mazishi yawe na watu wengi na yavutie sana ili roho za mababu zisikasirike. Wengine wanatumia mazishi ‘kuonyesha’ kiwango chao cha maisha na cha kifedha. (1 Yoh. 2:16) Wakati, jitihada, na pesa nyingi zinatumiwa ili aliyekufa apate mazishi “yanayofaa.” Ili kuwavutia watu wengi iwezekanavyo, picha kubwa zenye matangazo kuhusu mtu aliyekufa zinawekwa sehemu mbalimbali, na hivyo watu wote wanatangaziwa kuhusu mazishi. Fulana zenye picha ya aliyekufa zinashonwa na kugawanywa ili waombolezaji wazivae. Sanduku la bei ghali na lenye madoido mengi linanunuliwa ili kuwavutia watazamaji. Katika nchi moja ya Afrika, wengine wanatengeneza masanduku yanayofanana na magari, ndege, mashua, na vitu vingine vinavyoonyesha utajiri, cheo, na anasa. Mwili unaweza kutolewa ndani ya sanduku na kuwekwa juu ya kitanda kilichopambwa kwa njia ya pekee. Mwanamke anaweza kuvalishwa nguo nyeupe ya arusi na kupambwa kwa vito vingi, shanga, na kupodolewa. Je, ni sawa kwa watu wa Mungu kushiriki katika mazoea hayo?

Wakristo wakomavu wanaona hekima ya kuepuka kufanya mambo yanayopita kiasi kama watu wa ulimwengu ambao hawajui wala hawajali kanuni za Mungu. Tunafahamu kwamba desturi na mazoea yanayopita kiasi na yasiyo ya kimaandiko ‘hayatokani na Mungu, bali hutokana na ulimwengu ambao unapitilia mbali.’ (1 Yoh. 2:15-17) Ni lazima tuwe waangalifu sana ili tusipotoshwe na roho ya mashindano isiyo ya Kikristo ya kujaribu kuwa bora kuliko wengine. (Gal. 5:26) Mambo ya hakika yanaonyesha kwamba ikiwa utamaduni na maisha ya watu yanaongozwa na woga wa wafu, mara nyingi mazishi yanakuwa makubwa na inakuwa vigumu kuyasimamia na yanaweza kwa urahisi kupita kiasi. Ibada ya wafu inaweza kuwachochea watu ambao si waamini wajihusishe na mwenendo mchafu. Kwenye mazishi hayo, huenda wengine wakapiga kelele na kuomboleza kupita kiasi, wakikumbatia mwili wa aliyekufa, wakizungumza na mwili huo kana kwamba uko hai, na kubandika pesa na vitu vingine kwenye mwili. Hilo likitukia kwenye mazishi ya Kikristo, huenda jina la Yehova na la watu wake likaletewa suto kubwa.—1 Pet. 1:14-16.

Bila shaka, kujua ukweli kuhusu hali ya wafu kunapaswa kutupa ujasiri wa kufanya mazishi yetu bila kuingiza jambo lolote la kilimwengu. (Efe. 4:17-19) Ingawa Yesu alikuwa mwanadamu mkuu zaidi na wa maana zaidi aliyepata kuishi, mazishi yake yalikuwa ya kiasi na hayakuhudhuriwa na watu wengi. (Yoh. 19:40-42) Wale walio na “akili ya Kristo” wanaona mazishi kama hayo kuwa yenye kuheshimika. (1 Kor. 2:16) Bila shaka, kufanya mazishi ya Kikristo kwa njia rahisi na ya kiasi ni njia bora ya kuepuka mambo machafu yasiyopatana na Maandiko, na kudumisha hali yenye utulivu, yenye kuheshimika, yenye kupendeza, na inayowafaa watu wanaompenda Mungu.

Je, Watu Washangilie?

Baada ya mazishi, huenda watu wa ukoo, majirani, na wengine wakawa na desturi ya kukusanyika kwa wingi ili kusherehekea na kucheza dansi huku kukiwa na muziki wenye sauti ya juu. Mara nyingi sherehe hizo za mazishi zinahusianishwa na ulevi na upotovu wa maadili. Watu fulani wanadai kwamba sherehe hizo za furaha zinaondoa huzuni ya kifo. Wengine wanahisi kwamba kufanya hivyo ni sehemu ya utamaduni wao. Hata hivyo, watu wengi wanaamini kwamba sherehe kama hizo ni za lazima ili kuheshimu na kusifu wafu na kuiwezesha nafsi ya aliyekufa kuungana na mababu zake.

Wakristo wa kweli wanaona hekima ya himizo hili la Maandiko: “Afadhali sikitiko kuliko kicheko, maana kwa kukunjamana uso moyo huwa afadhali.” (Mhu. 7:3) Zaidi ya hayo, wanajua faida za kutafakari kimyakimya kuhusu ufupi wa maisha na tumaini la ufufuo. Ndiyo, wale walio na uhusiano wa karibu pamoja na Yehova wanajua kwamba ‘siku ya kufa ni bora kuliko siku ya kuzaliwa.’ (Mhu. 7:1) Hivyo, kwa kuwa Wakristo wa kweli wanajua kwamba sherehe za wakati wa mazishi zinahusianishwa na imani za kuwasiliana na pepo na upotovu wa maadili, wanaona kwamba haifai kabisa kupanga wala hata kuhudhuria sherehe hizo. Mtu akishirikiana na watu wanaoponda raha kwenye mazishi anaweza kuonyesha kwamba hamheshimu Mungu wala dhamiri za waabudu wenzake wa Yehova.

Acha Wengine Waone Tofauti

Tunashukuru kama nini kwamba tumewekwa huru kutokana na woga usiofaa wa wafu ambao unawahangaisha sana wale walio katika giza la kiroho! (Yoh. 8:32) Kwa kuwa sisi ni “watoto wa nuru” tunahuzunika kwa njia inayoonyesha kwamba tuna ujuzi wa kiroho, kiasi, heshima, na tumaini hakika la ufufuo. (Efe. 5:8; Yoh. 5:28, 29) Tumaini hilo litatuzuia tusionyeshe huzuni kupita kiasi kama wanavyofanya mara nyingi watu “wasio na tumaini.” (1 The. 4:13) Litatupa ujasiri kusimama imara kwa ajili ya ibada safi, na kutoshindwa na woga wa wanadamu.—1 Pet. 3:13, 14.

Tukishikamana kwa uaminifu na kanuni za Maandiko tutawasaidia watu ‘kuona tofauti kati ya watu wanaomtumikia Mungu na watu ambao hawamtumikii.’ (Mal. 3:18) Siku moja, kifo hakitakuwapo tena. (Ufu. 21:4) Tunapongojea utimizo wa ahadi hiyo tukufu, acheni Yehova atupate tukiwa bila doa, bila dosari, na tukiwa tumejitenga kabisa na ulimwengu huu mwovu na mazoea yake yasiyomletea Mungu heshima.—2 Pet. 3:14.

[Picha katika ukurasa wa 30]

Ni jambo la hekima kuandika jinsi tunavyotaka mazishi yetu yafanywe

[Picha katika ukurasa wa 31]

Mazishi ya Kikristo yanapaswa kuwa ya kiasi na yenye kuheshimika