Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Hupaswi Kumsahau Yehova

Hupaswi Kumsahau Yehova

Hupaswi Kumsahau Yehova

WAISRAELI fulani walikuwa wamevuka maji mengi mapema. Hata hivyo, ilikuwa mara ya kwanza na ya pekee kwa wengi wao kuvuka bonde la maji bila kulowa. Yehova alikuwa tu amefanya maji ya Mto Yordani yasimame kama ukuta. Kisha, mamilioni ya Waisraeli wakiwa katika msafara mkubwa na mrefu sana wakavuka bonde la mto huo na kuingia katika Nchi ya Ahadi. Kama ilivyokuwa kwa mababu zao miaka 40 mapema katika Bahari Nyekundu, Waisraeli wengi waliokuwa wakivuka Yordani huenda walijiambia hivi: ‘Sitasahau kamwe jambo hili ambalo Yehova amefanya.’—Yos. 3:13-17.

Hata hivyo, Yehova alijua kwamba Waisraeli fulani ‘wangesahau upesi kazi zake.’ (Zab. 106:13) Kwa hiyo, alimwamuru kiongozi wa Waisraeli, Yoshua, achukue mawe 12 kutoka katikati ya mto huo na kuyaweka mahali ambapo wangepiga kambi yao ya kwanza. Yoshua alieleza hivi: “Mawe haya yatakuwa ukumbusho kwa wana wa Israeli.” (Yos. 4:1-8) Mawe hayo ya ukumbusho yangelikumbusha taifa hilo matendo yenye nguvu ya Yehova na kwa nini walipaswa kumtumikia kwa ushikamanifu sikuzote.

Je, simulizi hilo lina maana yoyote kwa watu wa Mungu leo? Ndiyo. Sisi pia hatupaswi kamwe kumsahau Yehova, na ni lazima tuendelee kumtumikia kwa ushikamanifu. Maonyo mengine yaliyotolewa kwa taifa la Israeli yanawahusu watumishi wa Yehova leo. Fikiria maneno haya ya Musa: “Jiangalie usije ukamsahau Yehova Mungu wako kwa kutozishika amri zake na maamuzi yake ya hukumu na sheria zake.” (Kum. 8:11) Hilo linamaanisha kwamba kumsahau Yehova kunaweza kumfanya mtu akose kumtii Yehova kimakusudi. Tunakabili hatari hiyo leo pia. Mtume Paulo alipowaandikia Wakristo aliwaonya wasifuate “kielelezo kilekile cha kutotii” ambacho Waisraeli walionyesha nyikani.—Ebr. 4:8-11.

Acheni tuzungumzie matukio fulani katika historia ya Waisraeli ambayo yatakazia kwamba hatupaswi kumsahau Mungu. Kwa kuongezea, mifano ya wanaume wawili Waisraeli waliokuwa washikamanifu itatusaidia kumtumikia Yehova kwa uvumilivu na shukrani.

Sababu za Kumkumbuka Yehova

Katika miaka yote ambayo Waisraeli walikuwa Misri, Yehova hakuwasahau kamwe. ‘Alikumbuka agano lake pamoja na Abrahamu, Isaka na Yakobo.’ (Kut. 2:23, 24) Kwa kweli, hawakupaswa kusahau kamwe hatua aliyochukua ili kuwaweka huru kutoka katika utumwa.

Yehova alipiga Misri kwa mapigo tisa. Makuhani wa Farao wenye kufanya uchawi hawakuwa na nguvu za kuyazuia. Hata hivyo, Farao alimkaidi Yehova, akakataa kuwaruhusu Waisraeli waende. (Kut. 7:14–10:29) Lakini matokeo ya pigo la kumi, yalimlazimisha mtawala huyo mwenye kiburi atii mapenzi ya Mungu. (Kut. 11:1-10; 12:12) Chini ya uongozi wa Musa, taifa la Israeli liliondoka Misri pamoja na jamii kubwa iliyochangamana nao, huenda kwa ujumla walikuwa watu 3,000,000. (Kut. 12:37, 38) Kabla hawajafika mbali, Farao alibadili maoni yake. Aliamuru magari yake ya vita na askari wake wapanda-farasi, jeshi lenye nguvu zaidi duniani wakati huo, wawarudishe tena watumwa hao aliowaweka huru. Wakati huo, Yehova alimwambia Musa awapeleke Waisraeli mahali palipoitwa Pihahirothi, kati ya Bahari Nyekundu na safu ya milima. Ilionekana kwamba hawakuwa na njia ya kutokea.—Kut. 14:1-9.

Farao aliamini kwamba Waisraeli walikuwa wameingia ndani ya mtego, na jeshi lake lilijitayarisha kuwashambulia. Lakini Yehova aliwazuia Wamisri wasiwakaribie kwa kuweka nguzo ya wingu na nguzo ya moto kati yao na Waisraeli. Kisha Mungu akaitenganisha Bahari Nyekundu, na kutokeza njia katika bonde la bahari hiyo huku kuta za maji labda zenye urefu wa mita 15 hivi zikisimama kila upande. Waisraeli walianza kuvuka bahari hiyo juu ya nchi kavu. Punde si punde, Wamisri wakafika ufuoni, wakawaona Waisraeli wakielekea upande wa pili wa bahari.—Kut. 13:21; 14:10-22.

Kiongozi mwenye busara zaidi angeacha kuwafuata Waisraeli, lakini Farao hakuacha. Huku akijiamini kupita kiasi, aliamuru magari yake ya vita na askari wapanda-farasi wawafuate haraka ndani ya bonde la bahari. Wamisri wakaendesha magari yao mbiombio. Lakini kabla ya Wamisri kuwashambulia Waisraeli kutoka nyuma, mbio zao za wazimu zilifika mwisho. Magari ya vita ya Wamisri yalikwama! Yehova aliondoa magurudumu kutoka kwenye magari yao.—Kut. 14:23-25; 15:9.

Wamisri walipokuwa wakijaribu kuyaendesha kwa shida magari yao ya vita yaliyovunjika, Waisraeli wote walifika kwenye ufuo wa mashariki. Sasa Musa akaunyoosha mkono wake juu ya Bahari Nyekundu. Ndipo, Yehova akafanya maji yaliyosimama pande mbili kama kuta yaporomoke. Mamilioni ya tani za maji yalimfunika Farao na mashujaa wake wa vita, wakazama wote. Hakuna hata mmoja kati ya adui hao aliyeokoka. Waisraeli walikuwa huru!—Kut. 14:26-28; Zab. 136:13-15.

Habari za tukio hilo zilifanya mataifa yaliyozunguka yaogope kwa muda mrefu sana. (Kut. 15:14-16) Miaka 40 baadaye, Rahabu wa Yeriko aliwaambia hivi wanaume wawili Waisraeli: “Tumeshikwa na hofu kwa sababu yenu, . . . kwa maana tumesikia jinsi ambavyo Yehova aliyakausha maji ya Bahari Nyekundu mbele yenu wakati mlipotoka Misri.” (Yos. 2:9, 10) Hata mataifa hayo ya kipagani hayakusahau jinsi Yehova alivyowakomboa watu wake. Ni wazi kwamba Waisraeli walikuwa na sababu nyingi zaidi za kumkumbuka Yehova.

‘Aliwalinda Kama Mboni ya Jicho Lake’

Baada ya kuvuka Bahari Nyekundu, Waisraeli waliingia katika Jangwa la Sinai, “nyika kubwa na yenye kuogopesha.” Walipotembea katika ‘nchi hiyo yenye ukame ambayo haina maji’ wala chakula cha kulisha umati huo mkubwa sana wa watu, mkono wa Yehova haukuwa mfupi. Musa alikumbuka hivi: ‘[Yehova] aliwapata [Waisraeli] katika nchi ya nyika, na katika jangwa tupu, lenye kulia. Alianza kuwazunguka, kuwatunza, kuwalinda kama mboni ya jicho lake.’ (Kum. 8:15; 32:10) Mungu aliwatunza jinsi gani?

Yehova aliwapa “mkate kutoka mbinguni,” unaoitwa mana, ambao ulitokea kimuujiza “juu ya uso wa nyika.” (Kut. 16:4, 14, 15, 35) Yehova pia alifanya maji yatiririke kutoka “katika jiwe gumu.” Kwa baraka za Mungu, mavazi yao hayakuchakaa, wala miguu yao haikuvimba miaka 40 waliyokaa nyikani. (Kum. 8:4) Yehova alikuwa na haki ya kutazamia nini kutoka kwao? Musa aliwaambia Waisraeli hivi: “Jiangalie na kuitunza vema nafsi yako, ili usisahau mambo ambayo macho yako yameona, nayo yasiondoke moyoni mwako siku zote za maisha yako.” (Kum. 4:9) Ikiwa Waisraeli wangekumbuka na kushukuru kwa ajili ya matendo ya Yehova ya kuwaokoa, wangemtumikia na kujitahidi sikuzote kutii sheria zake. Waisraeli walifanya nini?

Kumsahau Yehova Kuliwafanya Wakose Shukrani

Musa alitangaza hivi: “Mwamba aliyekuzaa wewe, ulimsahau, nawe ukaanza kumwondoa Mungu katika kumbukumbu.” (Kum. 32:18) Muda si muda, Waisraeli walipuuza au kusahau matendo ya Yehova katika Bahari Nyekundu, maandalizi yake ambayo yaliendeleza uhai wa taifa hilo nyikani, na mambo mengine yote mazuri ambayo Yehova alikuwa amewafanyia. Waisraeli wakawa waasi.

Wakati mmoja, Waisraeli walimshutumu Musa kwa sababu walifikiri hawangepata maji. (Hes. 20:2-5) Walilalamika hivi kuhusu mana ambayo iliwawezesha kuwa hai: “Nafsi yetu imeuchukia huu mkate wa kudharaulika.” (Hes. 21:5) Walitilia shaka hukumu ya Mungu na kumkataa Musa awe kiongozi wao, huku wakisema: “Laiti tungalikufa katika nchi ya Misri, au laiti tungalikufa katika nyika hii! . . . Na tuchague kiongozi, nasi turudi Misri!”—Hes. 14:2-4.

Yehova alihisi namna gani kuhusu kutotii kwa Waisraeli? Mtunga-zaburi mmoja aliandika hivi baadaye alipokumbuka matukio hayo: “Jinsi walivyomwasi mara nyingi nyikani, wakamhuzunisha jangwani! Nao wakawa wakimjaribu Mungu tena na tena, nao wakamtia uchungu Mtakatifu wa Israeli. Hawakuukumbuka mkono wake, ile siku ambayo aliwakomboa kutoka kwa mpinzani, jinsi alivyoweka ishara zake katika Misri.” (Zab. 78:40-43) Ndiyo, usahaulifu wa Waisraeli ulimuumiza sana Yehova.

Wanaume Wawili Ambao Hawakusahau

Hata hivyo, Waisraeli fulani hawakumsahau Yehova. Waisraeli hao ni Yoshua na Kalebu. Walikuwa katika kikundi cha wapelelezi 12 ambao walitumwa Kadesh-barnea ili kuipeleleza Nchi ya Ahadi. Wapelelezi 10 walitoa ripoti mbaya, lakini Yoshua na Kalebu waliwaambia watu hivi: “Nchi tuliyoipitia ili kuipeleleza ni nchi nzuri sana, sana. Ikiwa Yehova amependezwa nasi, basi kwa hakika atatuingiza katika nchi hii na kutupa sisi, nchi inayotiririka maziwa na asali. Ila tu msimwasi Yehova.” Watu waliposikia maneno hayo, wakasema Yoshua na Kalebu wapigwe mawe. Lakini hao wawili walisimama imara wakiwa na uhakika katika Yehova.—Hes. 14:6-10.

Baada ya miaka mingi, Kalebu alimwambia Yoshua hivi: “Musa mtumishi wa Yehova aliponituma kutoka Kadesh-barnea kwenda kuipeleleza nchi, nami nikamletea habari kama vile ilivyokuwa ndani ya moyo wangu. Na ndugu zangu walioenda pamoja nami wakaifanya mioyo ya watu iyeyuke; lakini mimi nilimfuata kikamilifu Yehova Mungu wangu.” (Yos. 14:6-8) Kalebu na Yoshua walivumilia matatizo mbalimbali huku wakimtegemea Mungu. Waliazimia kumkumbuka Yehova siku zote za maisha yao.

Kalebu na Yoshua pia walionyesha shukrani, wakitambua kwamba Yehova alitimiza ahadi yake ya kuwapa watu wake nchi yenye rutuba. Ndiyo, Waisraeli walipaswa kumshukuru Yehova ambaye alikuwa ameokoa uhai wao. Yoshua aliandika hivi: “Yehova akawapa Israeli nchi yote ambayo alikuwa ameapa kuwapa mababu zao . . . Hakuna ahadi hata moja iliyokosa kutimia katika ahadi zote nzuri ambazo Yehova alikuwa ameipa nyumba ya Israeli; mambo yote yalitimia.” (Yos. 21:43, 45) Tunaweza kuonyesha shukrani jinsi gani leo kama Kalebu na Yoshua?

Onyesha Shukrani

Mtu mmoja aliyemwogopa Mungu aliuliza hivi: “Nitamlipa Yehova nini kwa ajili ya faida zake zote kwangu?” (Zab. 116:12) Tuna deni kubwa sana kuelekea Mungu kwa sababu ya kutubariki kimwili, kutuongoza kiroho, na kuandaa njia ya kutuokoa wakati ujao, hivi kwamba hatuwezi kumlipa kikamili hata kwa umilele wote. Kwa kweli, hatuwezi kamwe kumlipa Yehova. Lakini sote tunaweza kuonyesha shukrani kwa yale anayotufanyia.

Je, mashauri ya Yehova yamekusaidia kuepuka matatizo? Je, msamaha wake umekusaidia kupata tena dhamiri safi? Matendo hayo ya Mungu yanakuletea faida za kudumu, na hivyo unapaswa kumshukuru daima. Msichana mwenye umri wa miaka 14 anayeitwa Sandra alikabili matatizo mazito lakini akayashinda kwa msaada wa Yehova. Anasema hivi: “Nilimwomba Yehova msaada, na njia aliyotumia kunisaidia imenigusa moyo sana. Sasa ninajua kwa nini baba yangu alizungumza na mimi mara nyingi kuhusu Methali 3:5, 6: ‘Mtegemee Yehova kwa moyo wako wote wala usitegemee uelewaji wako mwenyewe. Mtambue yeye katika njia zako zote, naye atanyoosha mapito yako.’ Nina hakika kwamba Yehova ataendelea kunisaidia sikuzote kama vile ambavyo amenisaidia mpaka leo hii.”

Onyesha Kwamba Unamkumbuka Yehova kwa Kuvumilia

Biblia inakazia sifa nyingine inayohusiana na kumkumbuka Yehova: “Acheni uvumilivu ukamilishe kazi yake, ili muwe kamili na timamu katika mambo yote, bila kukosa kitu chochote.” (Yak. 1:4) ‘Kuwa kamili na timamu katika mambo yote’ kunatia ndani nini? Kunatia ndani kusitawisha sifa ambazo zitatusaidia kukabiliana na majaribu tunayopata huku tukimtegemea Yehova na kuazimia kuvumilia bila kukata tamaa. Uvumilivu wa aina hiyo unaleta uradhi mkubwa majaribu ya imani yanapokoma. Na sikuzote majaribu hayo yanafikia mwisho.—1 Kor. 10:13.

Mkristo fulani ambaye amemtumikia Yehova kwa muda mrefu na ambaye amekabiliana na magonjwa mengi makali anataja kile ambacho kimemsaidia kuvumilia: “Ninajitahidi kufikiria mambo ambayo Yehova anafanya, si mambo ninayotaka kufanya. Utimilifu unamaanisha kukazia macho makusudi ya Mungu, bali si tamaa zangu. Ninapokabili matatizo, sisemi, ‘Yehova, kwa nini matatizo yananipata mimi tu?’ Ninaendelea tu kumtumikia na kushikamana naye hata nikipata matatizo kwa ghafula.”

Leo, kutaniko la Kikristo linamwabudu Yehova “kwa roho na kweli.” (Yoh. 4:23, 24) Wakiwa kikundi, Wakristo wa kweli hawatamsahau Mungu kamwe kama taifa la Israeli lilivyomsahau. Lakini kuwa tu sehemu ya kutaniko hakuthibitishi kwamba sisi binafsi tutabaki watimilifu. Kama Kalebu na Yoshua, kila mmoja wetu anapaswa kuonyesha shukrani na uvumilivu katika utumishi wa Yehova. Tuna sababu nzuri ya kufanya hivyo, kwa kuwa Yehova anaendelea kumwongoza na kumtunza kila mmoja wetu katika wakati huu mgumu wa mwisho.

Kama yale mawe ya ukumbusho ambayo Yoshua alisimamisha, rekodi ya matendo ya kuokoa ya Mungu inatuhakikishia kwamba hatawaacha watu wake. Basi uwe na mtazamo kama wa mtunga-zaburi aliyeandika hivi: “Nitavikumbuka vitendo vya Yah; kwa maana nitayakumbuka matendo yako ya ajabu ya zamani za kale. Nami hakika nitautafakari utendaji wako wote, nami nitajishughulisha mwenyewe na matendo yako.”—Zab. 77:11, 12.

[Picha katika ukurasa wa 7]

Taifa lote la Israeli lilitembea katika ‘nchi yenye ukame ambayo haina maji’

[Hisani]

Pictorial Archive (Near Eastern History) Est.

[Picha katika ukurasa wa 8]

Waisraeli walipokuwa wamepiga kambi Kadesh-barnea, wapelelezi walitumwa katika Nchi ya Ahadi

[Hisani]

Pictorial Archive (Near Eastern History) Est.

[Picha katika ukurasa wa 9]

Baada ya kukaa nyikani kwa miaka mingi, Waisraeli wangeweza kumshukuru Mungu kwa ajili ya Nchi ya Ahadi yenye rutuba

[Hisani]

Pictorial Archive (Near Eastern History) Est.

[Picha katika ukurasa wa 10]

Kukazia macho makusudi ya Yehova kunatusaidia kuvumilia matatizo yoyote tunayokabili