Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

‘Malaika wa Yehova Anapiga Kambi Pande Zote’

‘Malaika wa Yehova Anapiga Kambi Pande Zote’

‘Malaika wa Yehova Anapiga Kambi Pande Zote’

Limesimuliwa na Christabel Connell

Tulikazia akilini sana kujibu maswali ya Biblia ya Christopher hivi kwamba sote wawili hatukugundua usiku ulikuwa umesonga sana; wala hatukugundua kwamba Christopher aliangalia nje ya dirisha kila mara. Mwishowe, akatuangalia na kusema, “Sasa mnaweza kwenda hakuna hatari.” Kisha, akatusindikiza mahali tulipoweka baiskeli zetu na kutuaga. Alikuwa ameona hatari gani?

NILIZALIWA huko Sheffield, Uingereza, mwaka wa 1927 na wazazi wangu wakanipa jina Christabel Earl. Nyumba yetu ililipuliwa kwa bomu wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu, kwa hiyo, nilipelekwa kuishi na nyanya yangu huku nikiendelea na masomo. Katika shule moja ya watawa niliyosomea, sikuzote niliwauliza watawa kwa nini kuna jeuri na uovu mwingi sana. Watawa hao na watu wengine wa kidini hawakuweza kujibu maswali yangu kwa njia yenye kuridhisha.

Baada ya Vita vya Pili vya Ulimwengu, nilijifunza kazi ya uuguzi. Nilihamia London ili kufanya kazi katika Hospitali Kuu ya Paddington, lakini niliona jeuri zaidi katika jiji hilo. Baada tu ya ndugu yangu mkubwa kwenda kwenye Vita vya Korea, niliona watu wakipigana kijeuri nje ya hospitali hiyo. Mtu mmoja alipigwa mpaka akawa kipofu lakini hakuna mtu aliyemsaidia. Katika pindi hiyo, mama yangu alikuwa akienda pamoja nami kwenye mikutano ya watu waliowasiliana na pepo, lakini bado sikuelewa kwa nini uovu ulikuwa mwingi sana.

Nilitiwa Moyo Kujifunza Biblia

Siku moja ndugu yangu mkubwa, John, ambaye alikuwa Shahidi wa Yehova alitutembelea. Aliuliza hivi: “Unajua ni kwa nini mambo haya yote mabaya yanatukia?” Nikajibu, “Hapana.” Akafungua Biblia yake na kusoma andiko la Ufunuo 12:7-12. Sasa nilitambua kwamba Shetani na roho waovu ndio hasa wanaosababisha uovu ulimwenguni. Nilifuata mashauri ya John, nikakubali kujifunza Biblia muda mfupi baadaye. Hata hivyo, wakati huo sikutaka kubatizwa kwa sababu niliogopa wanadamu.—Met. 29:25.

Wakati huo, dada yangu, Dorothy, alikuwa Shahidi pia. Aliporudi kutoka kwenye kusanyiko la kimataifa la New York (1953) pamoja na mchumba wake, Bill Roberts, niliwaambia kwamba nilikuwa nimejifunza Biblia. Bill akaniuliza: “Je, ulisoma maandiko yote? Je, ulipiga majibu mistari katika kitabu?” Niliposema hapana, aliniambia hivi: “Basi hukujifunza kamwe! Mtafute dada aliyejifunza nawe ili mwanze tena!” Wakati huo, roho waovu walianza kunitesa. Ninaweza kukumbuka jinsi nilivyomwomba Yehova anilinde na kuniweka huru kutoka kwa uvutano wao.

Kufanya Upainia Huko Scotland na Ireland

Nilibatizwa Januari 16, 1954 (16/1/1954), nikamaliza kazi yangu ya muda ya uuguzi mnamo Mei, na nikaanza upainia Juni (Mwezi wa 6). Baada ya miezi minane, nilipewa mgawo wa kuwa painia wa pekee huko Grangemouth, Scotland. Nikiwa huko nilihisi kwamba malaika wa Yehova walikuwa ‘wakipiga kambi pande zote kunizunguka’ nilipokuwa nikihubiri katika eneo hilo la mashambani.—Zab. 34:7.

Mwaka wa 1956, niliombwa niende kutumika huko Ireland. Nilitumwa pamoja na dada wengine wawili katika mji wa Galway. Siku ya kwanza kabisa, nilimtembelea kasisi fulani. Muda mfupi baadaye, polisi mmoja alifika na kunipeleka mimi na mwenzangu kwenye kituo cha polisi. Tulipomwambia majina yetu na mahali tulipoishi, mara moja alipiga simu. Tulimsikia akisema hivi: “Ndiyo, Kasisi, ninajua vizuri wanakoishi.” Kumbe alikuwa ametumwa na kasisi huyo! Mwenye nyumba tuliyokodi, alishurutishwa atufukuze, kwa hiyo ofisi ya tawi ikapendekeza tutoke katika eneo hilo. Tulifika kwenye kituo cha magari-moshi tukiwa tumechelewa kwa dakika kumi. Lakini bado gari-moshi lilikuwapo, na kulikuwa na mtu fulani aliyekuwa akingoja ili kuhakikisha kwamba tumepanda gari-moshi hilo. Tulikuwa tumekaa Galway kwa majuma matatu tu!

Tulitumwa huko Limerick, mji mwingine ambako Kanisa Katoliki lilikuwa na uvutano mkubwa sana. Kwa kawaida, tulidhihakiwa na umati wa watu. Watu wengi waliogopa kutukaribisha nyumbani mwao. Mwaka uliotangulia ndugu mmoja alikuwa amepigwa katika mji wa karibu wa Cloonlara. Kwa hiyo, tulifurahi kukutana na Christopher, aliyetajwa mwanzoni, ambaye alituomba turudi ili kujibu maswali yake ya Biblia. Tulipokuwa tumemtembelea, kasisi mmoja aliingia na kumwamuru Christopher atufukuze. Alimpinga kasisi huyo kwa kusema hivi: “Niliwaalika wanawake hawa katika nyumba yangu na waligonga mlango kabla ya kuingia. Wewe hukualikwa, wala hukugonga mlango.” Kasisi huyo aliondoka kwa hasira.

Bila sisi kujua, kasisi huyo alikuwa amekusanya kikundi kikubwa cha wanaume, na walikuwa wakitungojea nje ya nyumba ya Christopher. Christopher alijua kwamba walikuwa na hasira sana, hivyo alitenda kama ilivyoelezwa mwanzoni mwa simulizi hili. Alitufanya tukae kwake mpaka walipoondoka. Baadaye tulipata habari kwamba yeye pamoja na familia yake walifukuzwa kutoka katika eneo hilo, kisha wakahamia Uingereza.

Tunaalikwa Gileadi

Tayari nilikuwa nikipanga kuhudhuria Kusanyiko la Kimataifa la Mapenzi ya Mungu, mwaka wa 1958 huko New York, nilipoalikwa kuhudhuria darasa la 33 la Gileadi. Badala ya kurudi nyumbani baada ya kusanyiko, nilitumika huko Collingwood, Ontario, Kanada, mpaka Shule ya Gileadi ilipoanza mwaka wa 1959. Lakini wakati wa kusanyiko, nilikutana na Eric Connell. Alijifunza kweli mwaka wa 1957 naye akaanza upainia mwaka wa 1958. Baada ya kusanyiko, aliniandikia kila siku nilipokuwa huko Kanada na wakati wote nilipokuwa katika Shule ya Gileadi. Nilijiuliza tungefanya nini baada ya mimi kuhitimu.

Kuhudhuria Shule ya Gileadi lilikuwa jambo la pekee sana katika maisha yangu. Tulikuwa katika darasa moja na Dorothy na mume wake. Walipewa mgawo wa kwenda Ureno wakiwa wamishonari. Nilishangaa nilipopewa mgawo wa kwenda Ireland. Nilivunjika moyo sana kwa kuwa singeenda na dada yangu! Nilimuuliza mmoja wa walimu wetu ikiwa nilikuwa nimefanya kosa. Akajibu: “Hapana. Wewe na mwenzi wako, Eileen Mahoney, mlikubali kwenda mahali popote ulimwenguni,” na bila shaka Ireland ilitiwa ndani.

Ninarudi Ireland

Nilifika Ireland Agosti (Mwezi wa 8) 1959, nikatumwa katika Kutaniko la Dun Laoghaire. Wakati huo, Eric alikuwa amerudi Uingereza na alifurahi sana kwamba nilikuwa karibu naye. Yeye pia alitaka kuwa mmishonari. Aliona kwamba kwa kuwa wamishonari walikuwa wakitumwa Ireland wakati huo, angefanya upainia huko. Alihamia Dun Laoghaire, na tukafunga ndoa mwaka wa 1961.

Miezi sita baadaye, Eric alipata msiba mbaya sana akiendesha pikipiki. Fuvu lake la kichwa lilipasuka, na madaktari hawakuwa na uhakika ikiwa wangeweza kuokoa uhai wake. Baada ya kulazwa hospitalini kwa majuma matatu, nilimtunza akiwa nyumbani kwa miezi mitano mpaka alipopona. Niliendelea na huduma yangu kadiri nilivyoweza.

Mwaka wa 1965, tulitumwa kwenye kutaniko lenye wahubiri wanane huko Sligo, bandari iliyo kwenye pwani ya kaskazini-magharibi. Miaka mitatu baadaye, tulienda kwenye kutaniko lingine dogo huko Londonderry, upande wa juu zaidi wa kaskazini. Siku moja, tulipokuwa tukitoka katika utumishi tulikuta barabara ya kwenda tulikoishi ikiwa imefungwa kwa ua wa seng’enge. Misukosuko ya Ireland Kaskazini ilikuwa imeanza. Magenge ya vijana yalichoma moto magari. Tayari jiji liligawanywa katika maeneo ya Waprotestanti na ya Wakatoliki. Ilikuwa hatari sana kuvuka kutoka eneo moja la jiji kwenda eneo lingine.

Kuishi na Kuhubiri Wakati wa Misukosuko

Hata hivyo, tulihubiri kila mahali. Kwa mara nyingine tena, tulihisi kana kwamba malaika walikuwa wakipiga kambi pande zote kutuzunguka. Tulipojikuta katika maeneo yenye fujo, tuliondoka haraka na kurudi baada ya fujo kutulia. Pindi moja kulipokuwa na fujo karibu na jengo tulimoishi, vitu fulani vililipuka katika duka la karibu la rangi ambalo lilikuwa likichomwa moto, navyo vikaanguka kwenye dirisha letu. Hatukuweza kulala kwa sababu tuliogopa kwamba moto ungeshika jengo tulimoishi. Baada ya kuhamia Belfast mwaka wa 1970, tulipata habari kwamba bomu la petroli lilikuwa limechoma kabisa duka hilo la rangi na jengo tulilokuwa tukiishi ndani yake liliungua kabisa.

Wakati mwingine, nilipokuwa nikihubiri na dada mmoja, tuliona kipande cha bomba cha ajabu-ajabu kwenye kizingiti cha dirisha moja. Tukaendelea kutembea. Punde si punde, kikalipuka. Watu wa mtaa huo walikuja na kufikiri kwamba sisi ndio tuliotega bomu hilo! Dada aliyeishi katika eneo hilo alikuja mara moja na kutuingiza katika nyumba yake. Majirani wake walipoona hilo walitambua kwamba hatukuwa na hatia.

Mwaka wa 1971, tulirudi Londonderry kumtembelea dada mmoja. Tulipokuwa tukimweleza njia tuliyofuata na kizuizi tulichopita njiani, alituuliza, “Hakukuwa na mtu yeyote kwenye kizuizi hicho?” Tuliposema, “Ndiyo walikuwapo, lakini walitupuuza tu,” alishangaa sana. Kwa nini? Kwa sababu siku zilizotangulia gari la polisi na gari la daktari mmoja lilitekwa na kuchomwa moto.

Mwaka wa 1972 tulihamia Cork. Baadaye, tulitumika huko Naas, kisha Arklow. Mwishowe, mwaka wa 1987, tulitumwa Castlebar, ambako tungali mpaka leo. Tukiwa Castlebar tumepata pendeleo kubwa sana la kusaidia kujenga Jumba la Ufalme. Eric alikuwa mgonjwa sana mwaka wa 1999. Hata hivyo, kwa msaada wa Yehova na utegemezo wenye upendo wa kutaniko, nilimtunza tena mpaka alipopona.

Mimi na Eric tumehudhuria Shule ya Utumishi wa Painia mara mbili. Bado anatumika akiwa mzee wa kutaniko. Nina ugonjwa mbaya sana wa baridi yabisi na nyonga zangu na magoti yote mawili yaliondolewa nikawekewa nyonga na magoti bandia. Ingawa nimekabili upinzani mkali wa kidini na nimeishi katika nyakati zenye misukosuko mibaya ya kisiasa na ya kijamii, moja ya matatizo makubwa niliyokabili lilikuwa kuacha kuendesha gari. Hilo lilikuwa jaribu kwa sababu sasa nilikosa uhuru wa kwenda popote pale nilipotaka. Kutaniko limenisaidia sana na kunitegemeza kabisa. Sasa ninaweza kutembea huku na huku kwa fimbo, na ninaenda sehemu za mbali nikitumia pikipiki yenye magurudumu matatu na inayotumia betri.

Mimi na Eric tumetumika tukiwa mapainia wa pekee kwa jumla ya miaka zaidi ya 100, na miaka 98 kati ya miaka hiyo tumetumikia nchini Ireland. Hatutaki kuacha kazi hii eti kwa sababu tumezeeka. Hatutegemei miujiza, lakini tunaamini kwamba malaika wenye nguvu wa Yehova ‘wanapiga kambi pande zote kuwazunguka’ wale wanaomwogopa na kumtumikia kwa uaminifu.