Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maandiko yanataja “kitabu cha Yashari” na “kitabu cha Vita vya Yehova.” (Yos. 10:13; Hes. 21:14) Vitabu hivyo viwili havipatikani katika orodha ya vitabu vya Biblia. Je, ni vitabu vilivyopotea ambavyo viliandikwa kwa mwongozo wa roho takatifu?

Hatuna sababu ya kukata kauli kwamba vitabu hivyo viwili viliandikwa kwa mwongozo wa roho takatifu na vikapotea baadaye. Waandikaji wa Biblia walioongozwa na roho takatifu walitaja vitabu vingine vingi. Kwa kweli, huenda baadhi ya vitabu hivyo vilikuwa sehemu ya Biblia lakini vilipewa tu majina ambayo wasomaji wa leo hawajui. Kwa mfano, andiko la 1 Mambo ya Nyakati 29:29 linataja “maneno ya Samweli mwonaji,” “maneno ya nabii Nathani,” na “maneno ya Gadi mwonaji.” Huenda maneno hayo yote yanafanyiza kitabu ambacho tunakiita leo Samweli cha Kwanza na cha Pili, au labda kitabu cha Waamuzi.

Huenda vingine ni vitabu ambavyo vina majina sawa na vitabu vya Biblia lakini kwa kweli si sehemu ya Biblia. Kwa mfano, tunaweza kuthibitisha jambo hilo kwa kutumia vitabu hivi vinne vya zamani: “Kitabu cha mambo ya nyakati za wafalme wa Yuda,” “Kitabu cha Wafalme wa Yuda na wa Israeli,” “Kitabu cha Wafalme wa Israeli,” na “Kitabu cha Wafalme wa Israeli na wa Yuda.” Ingawa huenda majina ya vitabu hivyo yanafanana na majina ya vitabu vya Biblia vya 1 Wafalme na 2 Wafalme, vitabu hivyo vinne havikuandikwa kwa mwongozo wa roho takatifu, wala si sehemu ya vitabu vya Biblia. (1 Fal. 14:29; 2 Nya. 16:11; 20:34; 27:7) Inaelekea kwamba ni maandishi ya kihistoria yaliyoandikwa wakati ambapo nabii Yeremia na Ezra waliandika masimulizi yao yaliyo katika Biblia.

Ndiyo, waandikaji fulani wa Biblia walirejelea au kuchunguza hati au maandishi ya kihistoria yaliyokuwapo lakini ambayo hayakuandikwa kwa mwongozo wa roho takatifu. Andiko la Esta 10:2 linataja “Kitabu cha mambo ya nyakati ya wafalme wa Umedi na Uajemi.” Vivyo hivyo, alipokuwa akiandika Injili yake, Luka ‘alifuata kwa uangalifu mambo yote tangu mwanzo kwa usahihi.’ Labda alimaanisha kwamba alichunguza vitabu vilivyokuwapo wakati huo alipokuwa akiandika orodha ya ukoo wa Yesu ambayo tunaweza kusoma katika kitabu chake cha Injili. (Luka 1:3; 3:23-38) Ingawa rekodi ambazo Luka alichunguza hazikuandikwa kwa mwongozo wa roho ya Mungu, bila shaka kitabu chake cha Injili kiliongozwa na roho ya Mungu. Na kitabu hicho cha Injili ni chenye thamani kwetu pia.

Inaonekana kwamba vitabu viwili vinavyotajwa kwenye swali letu, yaani, “kitabu cha Yashari” na “kitabu cha Vita vya Yehova,” havikuandikwa kwa mwongozo wa roho lakini vilikuwapo kwa muda mrefu. Kwa sababu hiyo, Yehova hakuvihifadhi. Kutajwa kwa vitabu hivyo viwili katika Biblia, kumefanya wasomi fulani wakate kauli kwamba vilikuwa vitabu vya mashairi au nyimbo za vita kati ya Waisraeli na maadui wao. (2 Sam. 1:17-27) Kitabu kimoja cha utafiti wa Biblia kinadokeza kwamba huenda habari zilizokuwa katika vitabu hivyo zilikuwa “mashairi na nyimbo zilizokusanywa kwa ukawaida na waimbaji stadi katika Israeli la kale ambao walihifadhi desturi za pekee na nyimbo za Israeli.” Hata wanaume ambao Mungu alitumia wakati fulani kama manabii au waonaji waliandika vitabu ambavyo havikuongozwa na roho ya Yehova wala hakuamua viwe sehemu ya Maandiko ambayo ni yenye “faida kwa kufundisha, kwa kukaripia, kwa kunyoosha mambo” katika siku zetu.—2 Tim. 3:16; 2 Nya. 9:29; 12:15; 13:22.

Uhakika wa kwamba vitabu fulani vinatajwa katika Biblia na vilitumiwa kama vyanzo vya habari haupaswi kutufanya tukate kauli kwamba viliandikwa kwa mwongozo wa roho ya Mungu. Hata hivyo, Yehova Mungu amehifadhi maandishi yote yenye “neno la Mungu wetu,” na neno hilo “litadumu mpaka wakati usio na kipimo.” (Isa. 40:8) Ndiyo, habari ambazo Yehova aliamua ziandikwe katika vile vitabu 66 vya Biblia ndizo tunazohitaji tu ili ‘tuwe na uwezo kamili, na vifaa kamili kwa ajili ya kila kazi njema.’—2 Tim. 3:16, 17.