Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ayubu Alilitukuza Jina la Yehova

Ayubu Alilitukuza Jina la Yehova

Ayubu Alilitukuza Jina la Yehova

“Jina la Yehova na liendelee kubarikiwa.”—AYU. 1:21.

1. Huenda ni nani aliyeandika kitabu cha Ayubu, na alikiandika wakati gani?

MUSA alikuwa na umri wa miaka 40 hivi alipokimbia kutoka Misri ili kuepuka ghadhabu ya Farao, akakimbilia Midiani. (Mdo. 7:23) Alipokuwa katika nchi hiyo, huenda alisikia habari kuhusu majaribu ya Ayubu, ambaye alikuwa akiishi karibu katika nchi ya Usi. Miaka mingi baadaye, Musa na taifa la Israeli walipokuwa karibu na Usi mwishoni mwa safari yao ya nyikani, huenda Musa alipata habari kuhusu miaka ya mwisho-mwisho ya maisha ya Ayubu. Kulingana na mapokeo ya Wayahudi, Musa aliandika kitabu cha Ayubu miaka michache baada ya kifo cha Ayubu.

2. Kitabu cha Ayubu kinawatia moyo watumishi wa Yehova leo katika njia gani?

2 Kitabu cha Ayubu kinatia nguvu imani ya watumishi wa Mungu leo. Katika njia gani? Masimulizi hayo yanatusaidia kuelewa mambo yaliyotukia mbinguni ambayo ni ya maana sana kwetu na yanakazia suala la maana sana la enzi kuu ya Mungu ya ulimwengu wote. Pia, masimulizi ya Ayubu yanapanua uelewaji wetu kuhusu mambo yanayohusika katika kudumisha utimilifu na yanatusaidia kuelewa kwa nini nyakati nyingine Yehova anaruhusu watumishi wake wateseke. Zaidi ya hayo, kitabu cha Ayubu kinamtambulisha Shetani Ibilisi kuwa Adui mkuu wa Yehova na wanadamu. Pia, kitabu hicho kinaonyesha kwamba wanadamu wasio wakamilifu kama Ayubu wanaweza kubaki washikamanifu kwa Yehova hata wakijaribiwa vikali. Acheni tuchunguze matukio fulani yanayoelezwa katika kitabu cha Ayubu.

Ayubu Ajaribiwa na Shetani

3. Tunajua nini kumhusu Ayubu, na kwa nini alikuwa shabaha ya Shetani?

3 Ayubu alikuwa tajiri na mtu mashuhuri sana, mzee wa ukoo mwenye sifa nzuri. Alikuwa mshauri mwenye kuheshimiwa sana ambaye aliwasaidia watu wenye uhitaji. Jambo la maana hata zaidi ni kwamba Ayubu alimwogopa Mungu. Ayubu anaelezwa kuwa mtu ambaye ‘hakuwa na lawama na mnyoofu, na aliyemwogopa Mungu na kujiepusha na ubaya.’ Ayubu alikuwa shabaha ya mashambulizi ya Shetani Ibilisi kwa sababu ya kujitoa kwake kwa Mungu, bali si kwa sababu ya mali na umashuhuri wake.—Ayu. 1:1; 29:7-16; 31:1.

4. Utimilifu ni nini?

4 Utangulizi wa masimulizi ya kitabu cha Ayubu unaeleza kuhusu mkutano uliokuwa mbinguni ambapo malaika walisimama mbele za Yehova. Shetani pia alikuwepo, na alitoa mashtaka kumhusu Ayubu. (Soma Ayubu 1:6-11.) Ingawa Shetani alitaja mali za Ayubu, shabaha yake ilikuwa hasa kupinga utimilifu wa Ayubu. Neno “utimilifu” linamaanisha kuwa mnyoofu, asiye na lawama, mwadilifu, na bila kosa. Kulingana na Biblia, utimilifu wa wanadamu unamaanisha kujitoa kwa moyo kamili kwa Yehova.

5. Shetani alidai nini kumhusu Ayubu?

5 Shetani alidai kwamba Ayubu alimwabudu Mungu kwa sababu ya uchoyo, wala si kwa sababu ya utimilifu. Shetani alidai kwamba Ayubu angekuwa mshikamanifu kwa Yehova ikiwa tu Mungu angeendelea kumthawabisha na kumlinda. Ili kujibu dai la Shetani, Yehova alimruhusu Shetani amshambulie mwanamume huyo mwaminifu. Kwa hiyo, kwa siku moja tu, Ayubu alijulishwa kwamba mifugo yake iliibiwa au kuangamizwa, watumishi wake waliuawa, na watoto wake kumi wakafa. (Ayu. 1:13-19) Je, mashambulizi ya Shetani yalivunja utimilifu wa Ayubu? Maandiko yaliyoongozwa na roho ya Mungu yanaeleza maoni ya Ayubu kuhusu misiba yake: “Yehova ametoa, na Yehova amechukua. Jina la Yehova na liendelee kubarikiwa.”—Ayu. 1:21.

6. (a) Ni jambo gani lililotukia katika mkutano mwingine huko mbinguni? (b) Shetani alikuwa akimfikiria nani alipotilia shaka utimilifu wa Ayubu kwa Yehova?

6 Baadaye, kulikuwa na mkutano mwingine mbinguni. Kwa mara nyingine tena Shetani alimshtaki Ayubu, akisema: “Ngozi kwa ngozi, na kila kitu alicho nacho mtu atakitoa kwa ajili ya nafsi yake. Ili kuwe na badiliko, tafadhali nyoosha mkono wako, uguse kufikia mfupa wake na nyama yake, uone kama hatakulaani wewe mbele za uso wako.” Ona kwamba Shetani alihusisha watu wengine katika mashtaka yake. Kwa kusema, “Kila kitu alicho nacho mtu atakitoa kwa ajili ya nafsi yake,” Ibilisi hakutilia shaka utimilifu wa Ayubu tu, bali pia wa “mtu” yeyote yule anayemwabudu Yehova. Baadaye, Mungu alimruhusu Shetani kumpiga Ayubu kwa ugonjwa wenye maumivu makali. (Ayu. 2:1-8) Lakini huo haukuwa mwisho wa majaribu ya Ayubu.

Mambo Tunayojifunza Kutokana na Msimamo wa Ayubu

7. Ayubu alisongwa sana katika njia gani na mke wake na pia wageni waliomtembelea?

7 Mwanzoni, mke wa Ayubu aliumia moyoni kwa sababu ya mapigo yaliyompata mume wake. Bila shaka, alifadhaika kwa sababu ya vifo vya watoto wake na kupoteza mali ya familia yake. Inaonekana, aliumia moyoni kuona mume wake akikabiliana na ugonjwa wenye maumivu makali. Alimwambia Ayubu hivi: “Je, bado unashikilia sana utimilifu wako? Mlaani Mungu, ufe!” Kisha, wanaume watatu wakafika, yaani, Elifazi, Bildadi, na Sofari, inaelekea walikuja kumfariji Ayubu. Hata hivyo, walitumia mawazo ya udanganyifu na hivyo wakathibitika kuwa “wafariji wasumbufu.” Kwa mfano, Bildadi alidai kwamba watoto wa Ayubu walitenda dhambi na hivyo walistahili madhara yaliyowapata. Elifazi alidai kwamba mateso ya Ayubu yalikuwa adhabu kwa sababu ya dhambi alizotenda wakati uliopita. Hata alitilia shaka ikiwa wale wanaoshika utimilifu wana thamani yoyote machoni pa Mungu! (Ayu. 2:9, 11; 4:8; 8:4; 16:2; 22:2, 3) Chini ya hali hizo ngumu sana, Ayubu aliendelea kuwa mtimilifu. Ni kweli kwamba alikosea ‘alipoitangaza nafsi yake mwenyewe kuwa adilifu badala ya Mungu.’ (Ayu. 32:2) Hata hivyo, alibaki mwaminifu mpaka mwisho.

8. Elihu aliwawekea mfano gani mzuri wale wanaotoa mashauri leo?

8 Kisha, tunasoma kuhusu Elihu, ambaye pia alikuja kumtembelea Ayubu. Kwanza, Elihu alisikiliza hoja zilizotolewa na Ayubu na marafiki wake watatu. Ingawa alikuwa kijana kuliko wale wanaume wengine wanne, Elihu alionyesha hekima kubwa zaidi. Alizungumza na Ayubu kwa heshima, akitumia jina lake. Elihu alimpongeza Ayubu kwa unyoofu wake. Lakini pia alisema kwamba Ayubu alijaribu sana kuthibitisha kwamba hakuwa na kosa. Kisha, Elihu alimhakikishia Ayubu kwamba sikuzote ni jambo la maana sana kumtumikia Mungu kwa uaminifu. (Soma Ayubu 36:1, 11.) Ni mfano mzuri kama nini kwa wote wanaotoa mashauri leo! Elihu alionyesha subira, alisikiliza kwa makini, alipongeza ilipowezekana, na alitoa mashauri yenye kujenga.—Ayu. 32:6; 33:32.

9. Yehova alimsaidia Ayubu jinsi gani?

9 Mwishowe, Yehova aliongea na Ayubu! Masimulizi hayo yanasema hivi: “Yehova akaanza kumjibu Ayubu kutoka katika dhoruba ya upepo.” Akitumia mfululizo wa maswali, Yehova alimsaidia Ayubu kwa fadhili lakini kwa uthabiti kurekebisha mawazo yake. Ayubu alikubali kutoka moyoni karipio hilo, na akakiri hivi: “Nimekuwa kitu kisicho na maana . . . Ninatubu katika mavumbi na majivu.” Baada ya kuzungumza na Ayubu, Yehova aliwakaripia wale marafiki watatu wa Ayubu kwa sababu hawakusema “mambo ya kweli.” Ayubu alipaswa kusali kwa ajili yao. Kisha, “Yehova akaigeuza hali ya mateka ya Ayubu aliposali kwa ajili ya wale rafiki zake, na Yehova akaanza kumpa na kumwongezea Ayubu vyote vilivyokuwa vyake, kiasi cha mara mbili.”—Ayu. 38:1; 40:4; 42:6-10.

Tunampenda Sana Yehova Kadiri Gani?

10. Kwa nini Yehova hakumpuuza au kumharibu Shetani?

10 Yehova ni Muumba wa ulimwengu wote, Mwenye Enzi Kuu ya uumbaji wote. Kwa nini hakupuuza tu mashtaka ya Ibilisi? Mungu alijua kwamba kumpuuza au kumharibu Shetani hakungesuluhisha suala ambalo lilitokezwa. Ibilisi alidai kwamba Ayubu, mtumishi mtimilifu wa Yehova, hangeendelea kuwa mshikamanifu ikiwa angepoteza mali yake yote. Ayubu alibaki mshikamanifu katika majaribu. Kisha, Shetani alidai kwamba mwanadamu yeyote angemwacha Mungu ikiwa angeteseka kimwili. Ayubu aliteseka, lakini utimilifu wake haukuvunjwa. Hivyo, Shetani alithibitika kuwa mwongo katika kisa cha mwanamume huyo mwaminifu, lakini asiye mkamilifu. Namna gani waabudu wengine wa Mungu?

11. Yesu alionyesha waziwazi jinsi gani kwamba Shetani ni mwongo?

11 Kwa kweli, kila mtumishi wa Mungu anayeendelea kushika utimilifu wake hata anapojaribiwa kwa njia yoyote ile na Shetani anaonyesha kibinafsi kwamba mashtaka ya adui huyo asiye na huruma ni ya uwongo. Yesu alikuja duniani na akaonyesha waziwazi kwamba Shetani ni mwongo. Yesu alikuwa mtu mkamilifu kama baba yetu wa kwanza, Adamu. Uaminifu wa Yesu mpaka kifo ulionyesha wazi kabisa kwamba Shetani ni mwongo na kwamba mashtaka yake ni ya uwongo.—Ufu. 12:10.

12. Kila mtumishi wa Yehova ana nafasi na daraka gani?

12 Hata hivyo, Shetani anaendelea kuwajaribu waabudu wa Yehova. Kupitia utimilifu wetu, kila mmoja wetu ana nafasi na daraka la kuonyesha kwamba anamtumikia Yehova kwa sababu anampenda, bali si kwa sababu za kichoyo. Tuna maoni gani kuhusu daraka hilo? Tunaona kwamba ni pendeleo kuwa washikamanifu kwa Yehova. Pia tunafarijiwa tunapojua kwamba Yehova anatupa nguvu za kuvumilia na, kama katika kisa cha Ayubu, Hataruhusu tujaribiwe kupita uwezo wetu.—1 Kor. 10:13.

Shetani Ni Adui Mkaidi na Mwasi-Imani

13. Kitabu cha Ayubu kinafunua mambo gani kumhusu Shetani?

13 Maandiko ya Kiebrania yanaeleza kwa undani jinsi ambavyo Shetani amempinga Yehova bila aibu na kuwapotosha wanadamu. Katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, tunapata habari zaidi kuhusu upinzani wa Shetani kumwelekea Yehova, na katika kitabu cha Ufunuo, tunajifunza kuhusu kutetewa kwa enzi kuu ya Yehova, na kuharibiwa kwa Shetani milele. Kitabu cha Ayubu kinaongeza ujuzi wetu kuhusu uasi wa Shetani. Shetani alipohudhuria mikutano mbinguni, hakuhudhuria akiwa na kusudi la kumsifu Yehova. Ibilisi alikuwa na mtazamo mwovu na nia mbaya. Baada ya kumshtaki Ayubu na kuruhusiwa amjaribu, ‘Shetani aliondoka mbele za uso wa Yehova.’—Ayu. 1:12; 2:7.

14. Shetani alionyesha mtazamo gani kumwelekea Ayubu?

14 Hivyo, kitabu cha Ayubu kinamtambulisha Shetani kuwa adui wa wanadamu asiye na huruma. Kipindi cha wakati kisichojulikana kilipita kati ya mkutano wa mbinguni unaotajwa kwenye Ayubu 1:6 na ule unaotajwa kwenye Ayubu 2:1, na wakati huo Ayubu alijaribiwa kikatili. Uaminifu wa Ayubu ulimwezesha Yehova kumwambia Shetani: “Hata sasa bado [Ayubu] anashikilia sana utimilifu wake, ingawa wewe unanichochea juu yake nimmeze bila sababu.” Lakini Shetani hakukubali kwamba madai yake kumhusu Ayubu yalikuwa yamethibitishwa kuwa ya uwongo. Badala yake, aliomba kwamba Ayubu ajaribiwe tena vikali. Hivyo, Ibilisi alimjaribu Ayubu wakati alipokuwa tajiri na wakati ambapo hakuwa na chochote. Kwa wazi, Shetani hawahurumii watu wenye uhitaji au wale wanaopatwa na misiba. Anachukia watu watimilifu. (Ayu. 2:3-5) Hata hivyo, uaminifu wa Ayubu ulionyesha kwamba Shetani ni mwongo.

15. Waasi-imani wa siku zetu wanafanana jinsi gani na Shetani?

15 Shetani alikuwa kiumbe wa kwanza kuasi imani. Waasi-imani wa siku hizi wanaonyesha sifa mbaya kama zile za Ibilisi. Huenda wakawa na mwelekeo mbaya wa kuwachambua-chambua watu fulani katika kutaniko, wazee Wakristo, au Baraza Linaloongoza. Waasi-imani fulani wanapinga kutumiwa kwa jina la Mungu, Yehova. Hawataki kujifunza kumhusu Yehova au kumtumikia. Kama baba yao, Shetani, waasi-imani wanalenga watu watimilifu. (Yoh. 8:44) Haishangazi kwamba watumishi wa Yehova wanaepuka kabisa kushirikiana na waasi-imani!—2 Yoh. 10, 11.

Ayubu Alilitukuza Jina la Yehova

16. Ayubu alionyesha mtazamo gani kumwelekea Yehova?

16 Ayubu alilitumia na kulisifu jina la Yehova. Hata alipoumia sana moyoni kwa sababu ya habari za vifo vya watoto wake, Ayubu hakumhesabia Mungu jambo lolote lisilofaa. Ingawa Ayubu alifikiri kimakosa kwamba Mungu ndiye aliyesababisha vifo hivyo, bado alilitukuza jina la Yehova. Baadaye, katika moja ya maneno yake ya kimethali, Ayubu alisema hivi: “Tazama! Kumwogopa Yehova—hiyo ndiyo hekima, na kuacha ubaya ni uelewaji.”—Ayu. 28:28.

17. Ni nini kilichomsaidia Ayubu kudumisha utimilifu wake?

17 Ni nini kilichomsaidia Ayubu kudumisha utimilifu wake? Ni wazi kwamba kabla ya kupatwa na misiba hiyo, alikuwa tayari amesitawisha uhusiano wa karibu pamoja na Yehova. Ingawa hatuna uthibitisho wa kwamba alijua kwamba Shetani alikuwa ametoa mashtaka fulani kumhusu Yehova, Ayubu aliazimia kubaki mshikamanifu. Alisema hivi: “Mpaka nitakapokata pumzi, sitajiondolea utimilifu wangu!” (Ayu. 27:5) Ayubu alidumisha jinsi gani uhusiano huo wa karibu pamoja na Mungu? Bila shaka, alithamini yale aliyosikia kuhusu jinsi Mungu alivyoshughulika na Abrahamu, Isaka, na Yakobo, ambao walikuwa watu wake wa ukoo. Na kwa kuchunguza uumbaji, Ayubu angeweza kutambua sifa nyingi za Yehova.—Soma Ayubu 12:7-9, 13, 16.

18. (a) Ayubu alionyesha jinsi gani kwamba alijitoa kwa Yehova? (b) Tunaiga mfano mzuri wa Ayubu katika njia gani?

18 Mambo ambayo Ayubu alijifunza yalimchochea kuwa na tamaa ya kumpendeza Yehova. Kwa kuwa huenda washiriki wa familia yake walifanya jambo fulani lisilompendeza Mungu au ‘walimlaani Mungu moyoni mwao,’ Ayubu alitoa dhabihu kwa ukawaida. (Ayu. 1:5) Hata akiwa chini ya majaribu makali, bado Ayubu alisema mambo mazuri kumhusu Yehova. (Ayu. 10:12) Anatuwekea mfano mzuri kama nini! Sisi pia tunapaswa kujifunza kwa ukawaida ili tupate ujuzi sahihi kumhusu Yehova na makusudi yake. Tunapaswa kuwa na mazoea mazuri ya kiroho, kama vile kujifunza, kuhudhuria mikutano, kusali, na kuhubiri habari njema. Zaidi ya hayo, tunafanya yote tunayoweza ili kulitangaza jina la Yehova. Na kama vile utimilifu wa Ayubu ulivyompendeza Yehova, ndivyo utimilifu wa watumishi wa Mungu leo unavyofanya moyo wa Yehova ushangilie. Habari hiyo itazungumziwa katika makala inayofuata.

Je, Unakumbuka?

• Kwa nini Shetani Ibilisi alimkazia fikira Ayubu?

• Ayubu alivumilia majaribu gani, naye aliitikia jinsi gani?

• Ni nini kitakachotusaidia kudumisha utimilifu kama alivyofanya Ayubu?

• Tunajifunza nini kumhusu Shetani katika kitabu cha Ayubu?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 4]

Masimulizi ya Ayubu yanatusaidia kuelewa suala la maana sana la enzi kuu ya Mungu ya ulimwengu wote

[Picha katika ukurasa wa 6]

Utimilifu wako unaweza kujaribiwa chini ya hali gani?