Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Hekima ya Yehova Inaonekana Katika Uumbaji

Hekima ya Yehova Inaonekana Katika Uumbaji

Hekima ya Yehova Inaonekana Katika Uumbaji

“Sifa zake ambazo hazionekani . . . zinaeleweka kwa vitu vilivyofanywa.”—ROM. 1:20.

1. Hekima ya ulimwengu imekuwa na uvutano gani juu ya watu wengi leo?

MARA nyingi, neno “hekima” linatumiwa kwa njia isiyofaa. Watu fulani wanasema kwamba mtu ana hekima ikiwa ana ujuzi mwingi sana. Hata hivyo, watu wanaoitwa eti wenye hekima katika ulimwengu hawatoi mwongozo wowote wenye kutegemeka kuhusu kupata kusudi la kweli maishani. Badala yake, wale wanaowafuata watu hao, mwishowe ‘wanarushwa huku na huku kama kwa mawimbi na kuchukuliwa huku na huku na kila upepo wa fundisho.’—Efe. 4:14.

2, 3. (a) Kwa nini Yehova ndiye “mwenye hekima peke yake”? (b) Kuna tofauti gani kati ya hekima ya Mungu na hekima ya ulimwengu?

2 Wale wanaopata hekima ya kweli wako tofauti kama nini, kwa kuwa hekima hiyo inatoka kwa Yehova Mungu! Biblia inatuambia kwamba Yehova ndiye “mwenye hekima peke yake.” (Rom. 16:27) Anajua mambo yote kuhusu ulimwengu, kutia ndani jinsi ulivyoumbwa na historia yake. Sheria za asili, ambazo wanadamu wanategemea ili kufanya utafiti wao, zilitungwa na Yehova. Kwa hiyo, Yehova hastaajabishwi na vitu ambavyo wanadamu wametengeneza wala hababaishwi na falsafa za wanadamu ambazo zinaonekana kuwa za hali ya juu sana. “Hekima ya ulimwengu huu ni upumbavu kwa Mungu.”—1 Kor. 3:19.

3 Biblia inatuambia kwamba Yehova “anatoa hekima” kwa watumishi wake. (Met. 2:6) Tofauti na falsafa za wanadamu, hekima inayotoka kwa Mungu inaeleweka waziwazi. Inakazia ufahamu unaotegemea ujuzi sahihi na uelewaji. (Soma Yakobo 3:17.) Mtume Paulo alistaajabia hekima ya Yehova. Aliandika hivi: “Lo! Jinsi kilivyo kina cha utajiri wa Mungu na hekima na ujuzi! Jinsi hukumu zake zisivyochunguzika na njia zake zisivyotafutika!” (Rom. 11:33) Kwa sababu Yehova ndiye mwenye hekima yote, tuna hakika kwamba sheria zake zinatuongoza kufuata njia bora zaidi ya maisha. Kwa kweli, Yehova tu ndiye anayejua vizuri zaidi mambo tunayohitaji ili kuwa wenye furaha.—Met. 3:5, 6.

Yesu—“Stadi wa Kazi”

4. Tunaweza kutambua hekima ya Yehova kupitia njia gani moja?

4 Hekima ya Yehova, na sifa zake nyingine zisizo na kifani, zinaweza kuonekana katika vitu alivyoumba. (Soma Waroma 1:20.) Kazi za uumbaji za Yehova, kuanzia zile kubwa zaidi mpaka zile ndogo zaidi, zinafunua sifa zake. Hata tutazame wapi—iwe juu mbinguni au kwenye udongo—tunaona mambo mengi yanayoonyesha kwamba kuna Muumba mwenye hekima yote na mwenye upendo. Tunaweza kujifunza mengi kumhusu kwa kuchunguza vitu ambavyo ameumba.—Zab. 19:1; Isa. 40:26.

5, 6. (a) Zaidi ya Yehova, ni nani aliyehusika katika uumbaji? (b) Tutachunguza nini, na kwa nini?

5 Yehova hakuwa peke yake ‘alipoumba mbingu na dunia.’ (Mwa. 1:1) Biblia inaonyesha kwamba muda mrefu kabla ya vitu vinavyoonekana kuumbwa, alimuumba mtu wa roho ambaye alimtumia kuumba “vitu vingine vyote.” Kiumbe huyo wa roho ni Mwana mzaliwa-pekee wa Mungu—“mzaliwa wa kwanza wa viumbe vyote”—ambaye baadaye aliishi duniani akiwa mwanadamu Yesu. (Kol. 1:15-17) Kama Yehova, Yesu pia ana hekima. Katika Methali sura ya 8, anawakilishwa na hekima iliyo na utu. Sura hiyo ya Biblia pia inamtaja Yesu kuwa “stadi wa kazi” wa Mungu.—Met. 8:12, 22-31.

6 Hivyo, uumbaji unaoonekana unafunua hekima ya Yehova na ya Stadi wake wa Kazi, Yesu. Uumbaji unatufundisha mambo ya maana. Acheni tuzungumzie mifano minne ya vitu vilivyoumbwa vinavyotajwa katika Methali 30:24-28 kuwa “vina hekima ya kisilika.” *

Anatufunza Kuwa na Bidii

7, 8. Ni mambo gani kuhusu chungu yanayokuvutia?

7 Tunapochunguza jinsi ambavyo vitu “vilivyo vidogo zaidi duniani” viliumbwa na utendaji wake, tunaweza kujifunza mengi. Kwa mfano, fikiria hekima ya kisilika ya wadudu wanaoitwa chungu.—Soma Methali 30:24, 25.

8 Watafiti fulani wanaamini kwamba kwa kila mtu mmoja kuna chungu 200,000, na chungu hao wote wanafanya kazi kwa bidii katika udongo. Chungu wanaishi katika vikundi mbalimbali, na katika vikundi vingi kuna aina tatu za chungu: malkia, chungu wa kiume, na wafanyakazi. Kila aina ya chungu inafanya kazi fulani ili kutunza mahitaji ya kikundi kizima. Chungu fulani wa Amerika Kusini anayekata majani, anafanya kazi kama mkulima stadi. Mdudu huyo mdogo anatia mbolea, anang’oa na kupanda, na kupalilia mimea ya kuvu katika mashamba yake ili kutokeza kuvu nyingi sana. Watafiti wamegundua kwamba “mkulima” huyo hodari anafanya kazi kulingana na kiasi cha chakula kinachohitajiwa na chungu walio katika kikundi chake. *

9, 10. Tunaweza kuiga bidii ya chungu jinsi gani?

9 Tunaweza kujifunza kutokana na chungu. Wanatufundisha kwamba tunahitaji kufanya jitihada nyingi ili tupate matokeo mazuri. Biblia inatuambia hivi: “Mwendee chungu, ewe mvivu; zitazame njia zake upate kuwa na hekima. Ijapokuwa hana kiongozi, ofisa wala mtawala, yeye hutayarisha chakula chake wakati wa kiangazi; amekusanya akiba ya chakula chake wakati wa mavuno.” (Met. 6:6-8) Yehova na Stadi wake wa Kazi, Yesu, ni wenye bidii. Yesu alisema hivi: “Baba yangu anaendelea kufanya kazi mpaka sasa, na mimi ninaendelea kufanya kazi.”—Yoh. 5:17.

10 Tukiwa waigaji wa Mungu na wa Kristo, sisi pia tunapaswa kuwa wenye bidii. Hata tuwe na mgawo gani katika tengenezo la Mungu, sote tunapaswa kuwa na “mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana.” (1 Kor. 15:58) Hivyo, tunapaswa kufuata himizo ambalo Paulo aliwapa Wakristo huko Roma: “Msiwe wavivu katika kazi zenu. Wakeni roho. Mtumikieni Yehova.” (Rom. 12:11) Jitihada zetu za kufanya mapenzi ya Yehova si za bure, kwa kuwa Biblia inatuhakikishia hivi: “Mungu hakosi kuwa mwadilifu hivi kwamba asahau kazi yenu na upendo mlioonyesha kwa ajili ya jina lake.”—Ebr. 6:10.

Kulindwa Kiroho

11. Eleza sifa fulani za wibari.

11 Wibari ni kiumbe mwingine mdogo anayeweza kutufundisha mambo ya maana. (Soma Methali 30:26.) Wibari ni mnyama anayefanana na sungura mkubwa, lakini ana masikio mafupi ya mviringo na miguu mifupi. Mnyama huyo mdogo anaishi kwenye miamba. Wibari ana macho makali yanayomsaidia sana, na pia mashimo na nyufa zilizo kwenye makao yake ya miamba zinamlinda kutokana na wanyama wanaowinda. Wibari wanaishi pamoja katika vikundi na wanashirikiana sana, na hivyo wanapata ulinzi na joto wakati wa baridi kali. *

12, 13. Tunajifunza mambo gani kutokana na wibari?

12 Tunaweza kujifunza nini kutokana na wibari? Kwanza, mnyama huyo anajitahidi kuepuka hatari. Anatumia macho yake makali kuona wanyama wanaowinda wakiwa mbali, naye anakaa karibu na mashimo na nyufa ili akimbilie humo na kuokoa uhai wake. Sisi pia tunahitaji kuwa macho kabisa kiroho ili kuona hatari zilizo katika ulimwengu wa Shetani. Mtume Petro aliwahimiza Wakristo hivi: “Tunzeni akili zenu, iweni wenye kulinda. Adui yenu, Ibilisi, anatembea huku na huku kama simba anayenguruma, akitafuta kummeza mtu.” (1 Pet. 5:8) Alipokuwa duniani, Yesu aliendelea kuwa macho ili kujilinda kutokana na jitihada zote za Shetani za kuvunja utimilifu Wake. (Mt. 4:1-11) Yesu aliwawekea wafuasi wake mfano mzuri!

13 Njia moja ya kuwa macho ni kutumia ulinzi wa kiroho ambao Yehova anatupa. Hatupaswi kupuuza kujifunza Neno la Mungu na kuhudhuria mikutano ya Kikristo. (Luka 4:4; Ebr. 10:24, 25) Zaidi ya hayo, kama vile wibari wanavyopata faida kwa kushirikiana sana, sisi pia tunahitaji kuendelea kushirikiana kwa ukaribu na Wakristo wenzetu ili kuwe na “ubadilishanaji wa kitia-moyo.” (Rom. 1:12) Tunapokubali kulindwa na Yehova, tunaonyesha kwamba tunakubaliana na mtunga-zaburi Daudi, aliyeandika hivi: “Yehova ni mwamba wangu na ngome yangu na Mwokoaji wangu. Mungu wangu ni mwamba wangu. Nitamkimbilia.”—Zab. 18:2.

Kuvumilia Upinzani

14. Ingawa huenda tusimstaajabie nzige mmoja, tunaweza kusema nini kuhusu kundi la nzige?

14 Tunaweza pia kujifunza mambo fulani kutokana na nzige. Huenda tusimstaajabie nzige mmoja tu, ambaye kwa kawaida ana urefu wa sentimita tano hivi, lakini kwa hakika kundi la nzige linastaajabisha. (Soma Methali 30:27.) Kwa kuwa nzige wanakula chakula kingi sana, kundi la wadudu hao wasiochoka linaweza kuharibu haraka shamba lililo tayari kuvunwa. Katika Biblia, sauti ya kundi la wadudu wanaovamia, kutia ndani nzige, inalinganishwa na sauti ya magari ya vita na sauti ya miali ya moto ambayo inateketeza majani makavu. (Yoe. 2:3, 5) Watu wanawasha moto ili kujaribu kuzuia kundi la nzige, lakini kwa kawaida moto unashindwa kuwazuia. Kwa nini? Miili ya nzige waliokufa inazima moto huo, kisha nzige wanaobaki wanasonga mbele bila kizuizi chochote. Hata bila mfalme au kiongozi, kundi la nzige linasonga kama jeshi lililojipanga vizuri, na kushinda kizuizi chochote kile. *Yoe. 2:25.

15, 16. Ni kwa njia gani wahubiri wa Ufalme leo ni kama kundi la nzige?

15 Nabii Yoeli alilinganisha utendaji wa watumishi wa Yehova na utendaji wa nzige. Aliandika hivi: “Wanakimbia kama wanaume wenye nguvu. Wanapanda ukuta kama wanaume wa vita. Nao huenda kila mmoja katika njia zake, nao hawabadili mapito yao. Wala hawasukumani. Wanasonga mbele kama mwanamume katika mwendo wake; na baadhi yao wakianguka katikati ya silaha, wale wengine hawageuzi mwendo wao.”—Yoe. 2:7, 8.

16 Unabii huo unaeleza vizuri sana kuhusu wahubiri wa Ufalme wa Mungu leo! Hakuna “ukuta” wa upinzani ambao umeweza kusimamisha kazi yao ya kuhubiri. Badala yake, wanamwiga Yesu, ambaye aliendelea kufanya mapenzi ya Mungu hata ingawa wengi walimdharau. (Isa. 53:3) Ni kweli kwamba Wakristo fulani ‘wameanguka katikati ya silaha’ kwa kuuawa kwa sababu ya imani yao. Hata hivyo, kazi ya kuhubiri imeendelea, na idadi ya wahubiri wa Ufalme inaendelea kuongezeka. Kwa kweli, mara nyingi mateso yamesaidia habari njema iwafikie watu ambao hawangesikia kamwe ujumbe wa Ufalme. (Mdo. 8:1, 4) Katika huduma yako, je, unaonyesha uvumilivu kama wa nzige hata unapopata watu wasiopendezwa au wapinzani?—Ebr. 10:39.

“Shikamaneni na Mema”

17. Kwa nini miguu ya mjusi inaweza kushika kabisa sehemu laini?

17 Ni kana kwamba mjusi ana uwezo kuliko nguvu za uvutano. (Soma Methali 30:28.) Kwa kweli, wanasayansi wanashangazwa na uwezo wa kiumbe huyo mdogo wa kupanda kuta na hata kutembea kwenye madari laini bila kuanguka. Ni nini kinachomwezesha mjusi kufanya hivyo? Mjusi hana gundi fulani ya pekee au vidude vya kufyonza hewa. Badala yake, kwenye kila kidole cha mguu wake kuna sehemu zilizoinuka ambazo zina maelfu ya vitu kama nywele. Vitu hivyo vina mamia ya nyuzinyuzi ambazo zina ncha zenye umbo la sahani ndogo. Nguvu za molekuli za nyuzi hizo zote zinaweza kutegemeza uzito unaozidi uzito wa mwili wa mjusi, hata anapotembea tumbo juu kwenye kioo! Watafiti wameshangazwa na uwezo huo wa mjusi, nao wanasema kwamba gundi zenye nguvu zinaweza kutengenezwa kwa kuiga miguu ya mjusi. *

18. Tunaweza kufanya nini ili kuhakikisha kwamba sikuzote ‘tunashikamana na mema’?

18 Tunaweza kujifunza nini kutokana na mjusi? Biblia inatuhimiza hivi: “Chukieni maovu, shikamaneni na mema.” (Rom. 12:9) Uvutano mbaya uliopo katika ulimwengu wa Shetani unaweza kutufanya tuache kushikamana na kanuni za Mungu. Kwa mfano, kushirikiana na watu wasiofuata sheria za Mungu, iwe ni shuleni au kazini au kupitia burudani inayomchukiza Mungu, kunaweza kudhoofisha azimio letu la kutenda mema. Usikubali kamwe hilo likupate! Neno la Mungu linaonya hivi: “Usiwe mwenye hekima machoni pako mwenyewe.” (Met. 3:7) Badala yake, fuata shauri la hekima ambalo Musa aliwapa watu wa Mungu zamani za kale: “Unapaswa kumwogopa Yehova Mungu wako. Unapaswa kumtumikia yeye, nawe unapaswa kushikamana naye.” (Kum. 10:20) Tukishikamana na Yehova, tutakuwa tunamwiga Yesu, ambaye Biblia inasema hivi kumhusu: “Uliupenda uadilifu, nawe ukauchukia uasi-sheria.”—Ebr. 1:9.

Mambo Tunayojifunza Kutokana na Uumbaji

19. (a) Ni sifa gani za Yehova ambazo unaona katika uumbaji? (b) Hekima ya Mungu inaweza kutuletea faida gani?

19 Tumeona kwamba sifa za Yehova zinaonekana wazi kupitia vitu alivyoumba, na uumbaji wake unatufundisha mambo mengi ya maana. Kadiri tunavyojifunza kuhusu kazi za Yehova, ndivyo tunavyostaajabia zaidi hekima yake. Kutilia maanani hekima ya Mungu kutaongeza furaha yetu sasa na kutatulinda wakati ujao. (Mhu. 7:12) Ndiyo, tutajionea ukweli wa uhakikisho huu unaotolewa katika Methali 3:13, 18: “Mwenye furaha ni mtu ambaye amepata hekima, na mtu anayepata utambuzi. Ni mti wa uzima kwa wale wanaoishika, na wale wanaoishika sana wataitwa wenye furaha.”

[Maelezo ya chini]

^ fu. 6 Vijana hasa wanaweza kufurahia kuchunguza marejeo yaliyo katika maelezo ya chini na kueleza kuhusu utafiti wao wakati wa Funzo la Mnara wa Mlinzi la kutaniko.

^ fu. 8 Ili upate habari zaidi kuhusu chungu anayekata majani, ona magazeti ya Amkeni! ya Machi 22, 1997 (22/3/1997), ukurasa wa 31, na Mei 22, 2002 (22/5/2002), ukurasa wa 31.

^ fu. 11 Ili upate habari zaidi kuhusu wibari, ona gazeti la Amkeni! la Mei 8, 1991, ukurasa wa 15-16 au gazeti la Kiingereza au la Kifaransa la Septemba 8, 1990 (8/9/1990), ukurasa wa 15-16.

^ fu. 14 Ili upate habari zaidi kuhusu nzige, ona gazeti la Amkeni! la Kiingereza la Oktoba 22, 1976 (22/10/1976), ukurasa wa 11, au la Kifaransa la Februari 8, 1977 (8/2/1977), ukurasa wa 11.

^ fu. 17 Ili upate habari zaidi kuhusu mjusi, ona gazeti la Amkeni! la Aprili 2008 (4/2008), ukurasa wa 26.

Je, Unakumbuka?

Ni jambo gani lenye faida tunalojifunza kutoka kwa . . .

• chungu?

• wibari?

• nzige?

• mjusi?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 16]

Je, una bidii kama ya chungu anayekata majani?

[Picha katika ukurasa wa 17]

Wibari wanapata ulinzi wanaposhirikiana wakiwa kikundi. Je, wewe pia unafanya hivyo?

[Picha katika ukurasa wa 18]

Wahudumu Wakristo wanaonyesha uvumilivu kama nzige

[Picha katika ukurasa wa 18]

Kama mjusi anavyojishikilia kabisa kwenye sehemu mbalimbali, ndivyo Wakristo wanavyoshikamana na mema

[Hisani]

Stockbyte/Getty Images