Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutambua Daraka la Musa Mkuu Zaidi

Kutambua Daraka la Musa Mkuu Zaidi

Kutambua Daraka la Musa Mkuu Zaidi

“Yehova Mungu atawainulia kutoka kati ya ndugu zenu nabii kama mimi. Msikilizeni huyo.”—MDO. 3:22.

1. Yesu Kristo amekuwa na uvutano gani katika historia?

MIAKA 2,000 iliyopita, mtoto fulani wa kiume alizaliwa, na malaika wengi sana walipoona hilo wakamsifu Mungu, na wachungaji fulani waliwasikia wakimsifu. (Luka 2:8-14) Miaka 30 baadaye, mtoto huyo, ambaye sasa alikuwa mtu mzima, alianza huduma ambayo ilidumu kwa miaka mitatu na nusu tu lakini ilibadili kabisa historia ya wanadamu. Philip Schaff, mwanahistoria mashuhuri wa karne ya 19, alichochewa kusema hivi kuhusu mwanamume huyo kijana: “Ingawa hakuandika chochote, watu wengi wamechochewa kuandika juu yake, na mambo aliyosema na kufanya yamezungumziwa sana katika hotuba, mazungumzo ya watu, vitabu, kazi za usanii, na nyimbo za sifa, kuliko mambo yote yaliyofanywa na watu wote mashuhuri wa zamani na wa kisasa.” Bila shaka, mwanamume huyo wa pekee ni Yesu Kristo.

2. Mtume Yohana alisema nini kumhusu Yesu na huduma Yake?

2 Mtume Yohana aliandika masimulizi ya huduma ya Yesu, akasema hivi mwishoni mwa masimulizi hayo: “Kwa kweli, kuna mambo mengine mengi pia aliyofanya Yesu, ambayo, kama yangeandikwa kirefu, nadhani ulimwengu wenyewe haungeweza kuwa na nafasi ya kuviweka vitabu vya kukunjwa ambavyo vingeandikwa.” (Yoh. 21:25) Yohana alijua kwamba angeweza kuandika mambo machache tu kati ya mambo yote ambayo Yesu alisema na kufanya katika miaka hiyo mitatu na nusu yenye matukio mengi. Hata hivyo, matukio ya kihistoria ambayo Yohana aliripoti katika Injili yake ni yenye thamani kubwa sana.

3. Tunapaswa kufanya nini ili tuelewe zaidi daraka la Yesu katika kusudi la Mungu?

3 Zaidi ya yale masimulizi manne muhimu ya Injili, maandiko mengine ya Biblia yanaeleza mambo mengi yenye kuimarisha imani kuhusu maisha ya Yesu. Kwa mfano, masimulizi ya Biblia kuhusu watu fulani waaminifu walioishi kabla ya Yesu yana habari ambazo zinatusaidia kuelewa zaidi daraka la Yesu katika kusudi la Mungu. Acheni tuchunguze masimulizi machache.

Watu wa Mungu Ambao Walimfananisha Kristo

4, 5. Ni nani waliomfananisha Yesu, na kwa njia gani?

4 Yohana na waandikaji wengine watatu wa Injili wanamtaja Musa, Daudi, na Sulemani kuwa watu waliomfananisha Yesu akiwa Mtiwa-Mafuta wa Mungu na Mfalme aliyechaguliwa. Watumishi hao wa zamani wa Mungu walimfananisha Yesu kwa njia gani, na tunaweza kujifunza nini katika masimulizi hayo?

5 Kwa ufupi, Biblia inatuambia kwamba Musa alikuwa nabii, mpatanishi, na mkombozi. Yesu pia ni nabii, mpatanishi, na mkombozi. Daudi alikuwa mchungaji na mfalme ambaye aliwashinda maadui wa Israeli. Yesu pia ni mchungaji na mfalme anayeshinda. (Eze. 37:24, 25) Sulemani alipokuwa mwaminifu, alikuwa mfalme mwenye hekima, na chini ya ufalme wake Waisraeli walifurahia amani. (1 Fal. 4:25, 29) Yesu pia ana hekima isiyo na kifani naye anaitwa “Mkuu wa Amani.” (Isa. 9:6) Ni wazi kwamba daraka la Kristo Yesu linalingana na lile la wanaume hao wa zamani lakini daraka la Yesu katika kusudi la Mungu halina kifani hata kidogo. Kwanza, acheni tumlinganishe Yesu na Musa tuone jinsi kufanya hivyo kunavyotusaidia kuelewa zaidi daraka la Yesu katika kusudi la Mungu.

Musa Alikuwa Mtangulizi wa Yesu

6. Mtume Petro alieleza namna gani uhitaji wa kumsikiliza Yesu?

6 Muda mfupi baada ya Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K., mtume Petro alinukuu unabii wa Musa uliotimizwa na Yesu Kristo. Petro alikuwa amesimama mbele ya umati wa waabudu ndani ya hekalu. Watu hao ‘walipotewa na akili kwa sababu ya mshangao’ wakati Petro na Yohana walipomponya mtu fulani aliyekuwa kilema tangu kuzaliwa, ambaye alikuwa akiombaomba, na wote wakakimbia ili kuona lililotukia. Petro alieleza kwamba tendo hilo lenye kustaajabisha lilifanywa kwa uwezo wa roho takatifu ya Yehova iliyotenda kupitia Yesu Kristo. Kisha, akinukuu Maandiko ya Kiebrania, akasema hivi: “Kwa kweli, Musa alisema, ‘Yehova Mungu atawainulia kutoka kati ya ndugu zenu nabii kama mimi. Msikilizeni huyo kulingana na mambo yote anayowaambia ninyi.’”—Mdo. 3:11, 22, 23; soma Kumbukumbu la Torati 18:15, 18, 19.

7. Kwa nini watu waliomsikiliza Petro walielewa maneno yake kuhusu nabii aliye mkuu zaidi kuliko Musa?

7 Inaelekea kwamba watu waliokuwa wakimsikiliza Petro walijua maneno hayo ya Musa. Kwa kuwa watu hao walikuwa Wayahudi, walimheshimu sana Musa. (Kum. 34:10) Walitazamia kwa hamu sana kuja kwa nabii aliye mkuu zaidi kuliko Musa. Nabii huyo hangekuwa mtiwa-mafuta tu wa Mungu kama Musa, bali angekuwa yule Masihi, “Kristo wa Mungu, Yule Aliyechaguliwa” na Yehova.—Luka 23:35; Ebr. 11:26.

Jinsi Yesu na Musa Wanavyolingana

8. Maisha ya Musa yanalingana kwa njia gani na maisha ya Yesu?

8 Maisha ya Yesu duniani yanalingana na maisha ya Musa katika mambo fulani. Kwa mfano, wakiwa watoto wachanga, Musa na Yesu waliokoka kuuawa na wafalme wakatili. (Kut. 1:22–2:10; Mt. 2:7-14) Kwa kuongezea, wote wawili ‘waliitwa kutoka Misri.’ Nabii Hosea alisema hivi: “Israeli alipokuwa mvulana, ndipo nikampenda, na kutoka Misri nilimwita mwanangu.” (Hos. 11:1) Maneno hayo ya Hosea yanahusu wakati ambapo Musa, kiongozi aliyewekwa rasmi na Mungu, alipoliongoza taifa la Israeli kutoka Misri. (Kut. 4:22, 23; 12:29-37) Hata hivyo, maneno ya Hosea hayakuhusu tu tukio la zamani bali pia tukio la wakati ujao. Maneno yake yalikuwa unabii ambao ulitimia wakati Yosefu na Maria waliporudi na Yesu kutoka Misri baada ya kifo cha Mfalme Herode.—Mt. 2:15, 19-23.

9. (a) Musa na Yesu walifanya miujiza gani? (b) Taja njia nyingine zinazoonyesha jinsi Yesu alivyolingana na Musa. (Ona sanduku lenye kichwa  “Njia Nyingine Ambazo Yesu Alilingana na Musa,” kwenye ukurasa wa 26.)

9 Musa na Yesu walifanya miujiza, hivyo wakathibitisha kwamba Yehova alikuwa akiwategemeza. Kulingana na Biblia, Musa ndiye mwanadamu wa kwanza kufanya miujiza. (Kut. 4:1-9) Kwa mfano, Musa alifanya miujiza iliyohusu maji wakati alipotoa amri na maji ya Nile na madimbwi yake yenye matete yakawa damu, Bahari Nyekundu ikatenganishwa, na maji yakabubujika kutoka kwenye mwamba jangwani. (Kut. 7:19-21; 14:21; 17:5-7) Yesu pia alifanya miujiza iliyohusu maji. Muujiza wake wa kwanza kabisa ulikuwa kugeuza maji yawe divai katika karamu ya arusi. (Yoh. 2:1-11) Baadaye, alituliza Bahari ya Galilaya yenye msukosuko. Na pindi moja, hata alitembea juu ya maji! (Mt. 8:23-27; 14:23-25) Sanduku lililo kwenye ukurasa wa 26 linataja njia nyingine zinazoonyesha jinsi Musa alivyolingana na Yesu, yule Musa Mkuu Zaidi.

Mtambue Kristo Akiwa Nabii

10. Nabii wa kweli ana daraka gani, na kwa nini Musa alikuwa nabii wa kweli?

10 Watu wengi wanafikiri kwamba nabii ni mtu ambaye anatabiri kuhusu wakati ujao, lakini hiyo ni sehemu moja tu ya daraka la nabii. Nabii wa kweli ni msemaji wa Yehova anayeongozwa na roho takatifu, ambaye anatangaza “mambo makuu ya Mungu.” (Mdo. 2:11, 16, 17) Kati ya mambo mengine, anaweza kutabiri matukio ya wakati ujao, na kufunua mambo fulani yanayohusu kusudi la Yehova, au kutangaza hukumu za Mungu. Musa alikuwa nabii wa aina hiyo. Alitabiri mapigo yote kumi yaliyopata Misri. Alitangaza agano la Sheria katika Sinai. Naye alifundisha taifa la Israeli kuhusu mapenzi ya Mungu. Hata hivyo, mwishowe, nabii aliye mkuu zaidi kuliko Musa angekuja.

11. Yesu alitimiza jinsi gani daraka lake akiwa nabii mkuu zaidi kuliko Musa?

11 Baadaye, katika karne ya kwanza, Zekaria alitenda kama nabii alipofunua kusudi la Mungu kuhusu mwana wake, Yohana. (Luka 1:76) Mwana huyo alikuwa Yohana Mbatizaji, aliyetangaza kuja kwa Yesu Kristo, yule nabii mkuu zaidi kuliko Musa aliyekuwa akitazamiwa kwa muda mrefu. (Yoh. 1:23-36) Akiwa nabii, Yesu alitabiri mambo mengi. Kwa mfano, alizungumza kuhusu kifo chake, akitabiri jinsi ambavyo angekufa, mahali ambapo angefia, na wale ambao wangemuua. (Mt. 20:17-19) Wasikilizaji walishangaa sana Yesu alipotabiri pia kuhusu uharibifu wa Yerusalemu na hekalu lake. (Marko 13:1, 2) Unabii wake unahusu pia siku zetu.—Mt. 24:3-41.

12. (a) Yesu aliweka namna gani msingi wa kampeni ya kuhubiri ulimwenguni pote? (b) Kwa nini tunafuata mfano wa Yesu leo?

12 Zaidi ya kuwa nabii, Yesu alikuwa mhubiri na mwalimu. Alihubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu, na hakuna mtu aliyezungumza kwa ujasiri mkubwa kama yeye. (Luka 4:16-21, 43) Alikuwa mwalimu asiye na kifani. Watu fulani waliomsikiliza walisema hivi: “Mtu mwingine hajapata kamwe kusema kama huyu.” (Yoh. 7:46) Yesu alieneza habari njema kwa bidii sana, naye aliwachochea wafuasi wake wawe na bidii kama yake kwa ajili ya Ufalme. Hivyo, aliweka msingi wa kampeni ya kuhubiri na kufundisha ulimwenguni pote ambayo inaendelea mpaka leo. (Mt. 28:18-20; Mdo. 5:42) Mwaka uliopita, wafuasi milioni saba hivi wa Kristo walitumia karibu saa 1,500,000,000 katika kazi ya kuhubiri habari njema ya Ufalme na kuwafundisha kweli za Biblia watu wanaopendezwa. Je, unashiriki kwa bidii katika kazi hiyo?

13. Ni nini kitakachotusaidia ‘kukaa macho’?

13 Hakuna shaka kwamba Yehova alitimiza unabii wa kumwinua nabii aliye kama Musa. Ujuzi huo unakuchochea jinsi gani? Je, unakuhakikishia zaidi kwamba unabii mbalimbali ulioongozwa na roho takatifu ambao unahusu wakati wetu ujao utatimia hivi karibuni? Ndiyo, kutafakari mfano wa yule Musa Mkuu Zaidi kunatuchochea ‘kukaa macho na kutunza akili zetu’ ili kuona mambo ambayo Mungu atafanya hivi karibuni.—1 The. 5:2, 6.

Mthamini Kristo Akiwa Mpatanishi

14. Musa alikuwa mpatanishi kati ya Waisraeli na Mungu jinsi gani?

14 Yesu alikuwa mpatanishi kama Musa. Mpatanishi ni kama daraja linalounganisha pande mbili. Musa alikuwa mpatanishi wa agano la Sheria kati ya Yehova na Waisraeli. Ikiwa wana wa Yakobo wangetii sheria za Mungu, wangeendelea kuwa mali ya pekee ya Mungu, kutaniko lake. (Kut. 19:3-8) Agano hilo lilitumika kuanzia 1513 K.W.K. mpaka karne ya kwanza W.K.

15. Yesu ni mpatanishi bora zaidi jinsi gani?

15 Mwaka wa 33 W.K., Yehova alifanya agano bora zaidi pamoja na taifa jipya la Israeli, “Israeli wa Mungu,” ambalo lilikuja kuwa kutaniko la ulimwenguni pote la Wakristo watiwa-mafuta. (Gal. 6:16) Ingawa agano ambalo Musa alikuwa mpatanishi wake lilitia ndani sheria zilizoandikwa na Mungu kwenye mawe, agano ambalo Yesu alikuwa mpatanishi ni bora zaidi. Mungu ameandika sheria za agano hilo katika mioyo ya wanadamu. (Soma 1 Timotheo 2:5; Waebrania 8:10.) Hivyo, sasa “Israeli wa Mungu” ni mali yake ya pekee, “taifa lenye kuzaa matunda” ya Ufalme wa Kimasihi. (Mt. 21:43) Washiriki wa taifa hilo la kiroho wanashiriki katika agano hilo jipya. Hata hivyo, agano hilo haliwanufaishi hao peke yao. Watu wengi sana, kutia ndani wengi ambao sasa wamelala katika kifo, watapata baraka za milele kwa sababu ya agano hilo bora zaidi.

Mheshimu Kristo Akiwa Mkombozi

16. (a) Yehova alimtumia Musa katika njia gani kuwakomboa Waisraeli? (b) Kulingana na Kutoka 14:13, ni nani aliye Chanzo cha wokovu?

16 Usiku wa mwisho kabla ya kutoka Misri, wazao fulani wa Israeli walikabili hatari kubwa. Muda si muda, malaika wa Mungu angepita katika nchi ya Misri na kuwaua wazaliwa wote wa kwanza. Yehova alimwambia Musa kwamba wazaliwa wa kwanza wa Israeli wangeokolewa ikiwa Waisraeli wangechukua damu ya mwana-kondoo wa Pasaka na kuipaka juu ya miimo na sehemu ya juu ya milango. (Kut. 12:1-13, 21-23) Ndivyo walivyofanya. Baadaye, taifa lote zima lilikabili hatari kubwa sana. Walijikuta wamenaswa kati ya Bahari Nyekundu na magari ya kivita ya Wamisri yaliyokuwa yakiwafuata mbio. Kwa mara nyingine tena Yehova aliwakomboa kupitia Musa, ambaye alitenganisha kimuujiza maji ya bahari hiyo.—Kut. 14:13, 21.

17, 18. Yesu ni mkombozi mkuu zaidi kuliko Musa katika njia gani?

17 Ingawa matendo hayo ya ukombozi yalikuwa makuu, ukombozi ambao Yehova aliandaa kupitia Yesu ni mkuu hata zaidi. Yesu ndiye anayetumiwa kuwakomboa wanadamu wanaotii kutoka katika utumwa wa dhambi. (Rom. 5:12, 18) Na ukombozi huo ni “ukombozi wa milele.” (Ebr. 9:11, 12) Jina Yesu linamaanisha “Yehova Ni Wokovu.” Yesu, akiwa Mkombozi au Mwokozi wetu, hatukomboi tu kutoka katika dhambi tulizofanya wakati uliopita bali pia anatufungulia njia ya kupata maisha bora ya wakati ujao. Kwa kuwakomboa kutoka katika utumwa wa dhambi, Yesu anawaokoa wafuasi wake kutokana na hasira ya Mungu na kuwawezesha kuwa na uhusiano wenye upendo pamoja na Yehova.—Mt. 1:21.

18 Ukombozi ambao Yesu anaandaa kutoka katika dhambi utatia ndani uhuru kutoka katika matokeo mabaya ya dhambi, yaani, magonjwa na hata kifo. Ili uwazie jinsi hali itakavyokuwa, fikiria jambo lililotukia wakati Yesu alipoenda katika nyumba ya mtu fulani aliyeitwa Yairo, ambaye binti yake wa miaka 12 alikuwa amekufa. Yesu alimhakikishia hivi Yairo: “Usiogope, uwe tu na imani, naye ataokolewa.” (Luka 8:41, 42, 49, 50) Binti huyo alifufuka kama Yesu alivyosema! Je, unaweza kuwazia shangwe ya wazazi wake? Hivyo ndivyo tutakavyoshangilia sana wakati “wale wote waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho wataisikia sauti [ya Yesu] na kutoka” wakati wa ufufuo. (Yoh. 5:28, 29) Kwa kweli, Yesu ni Mwokozi, Mkombozi wetu!—Soma Matendo 5:31; Tito 1:4; Ufu. 7:10.

19, 20. (a) Kutafakari kuhusu daraka la Yesu akiwa Musa Mkuu Zaidi kunatusaidia jinsi gani? (b) Habari inayofuata itazungumzia nini?

19 Kujua kwamba tunaweza kuwasaidia watu wafaidike na matendo ya Yesu ya kuokoa kunatuchochea tushiriki katika kazi ya kuhubiri na kufundisha. (Isa. 61:1-3) Zaidi ya hayo, kutafakari kuhusu daraka la Yesu akiwa Musa Mkuu Zaidi kunatufanya tuwe na uhakika zaidi kwamba atawakomboa wafuasi wake wakati atakapokuja kutekeleza hukumu juu ya waovu.—Mt. 25:31-34, 41, 46; Ufu. 7:9, 14.

20 Ndiyo, Yesu ndiye Musa Mkuu Zaidi. Alifanya mambo mengi ya ajabu ambayo Musa hangeweza kamwe kufanya. Maneno ya Yesu akiwa nabii na matendo yake akiwa mpatanishi yanawafaidi wanadamu wote. Akiwa Mkombozi, Yesu atawaletea wanadamu watakaokombolewa wokovu wa milele bali si wa muda mfupi. Hata hivyo, kuna mengi ya kujifunza kumhusu Yesu kutokana na wanaume waaminifu wa kale. Habari inayofuata itazungumzia jinsi alivyokuwa Daudi Mkuu Zaidi na Sulemani Mkuu Zaidi.

Unaweza Kueleza?

Ni kwa njia gani Yesu ni mkuu zaidi kuliko Musa akiwa

• nabii?

• mpatanishi?

• mkombozi?

[Maswali ya Funzo]

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 26]

 Njia Nyingine Ambazo Yesu Alilingana na Musa

□ Wote waliacha vyeo vya juu ili wamtumikie Yehova na watu wake.—2 Kor. 8:9; Flp. 2:5-8; Ebr. 11:24-26.

□ Wote walikuwa watiwa-mafuta, au ‘kristo.’—Marko 14:61, 62; Yoh. 4:25, 26; Ebr. 11:26.

□ Wote walikuja katika jina la Yehova.—Kut. 3:13-16; Yoh. 5:43; 17:4, 6, 26.

□ Wote walikuwa wapole.—Hes. 12:3; Mt. 11:28-30.

□ Wote waliwalisha watu wengi.—Kut. 16:12; Yoh. 6:48-51.

□ Wote walikuwa mahakimu na watoa-sheria.—Kut. 18:13; Mal. 4:4; Yoh. 5:22, 23; 15:10.

□ Wote walikabidhiwa ukichwa juu ya nyumba ya Mungu.—Hes. 12:7; Ebr. 3:2-6.

□ Wote wanaitwa mashahidi waaminifu wa Yehova.—Ebr. 11:24-29; 12:1; Ufu. 1:5.

□ Baada ya kifo cha Musa na cha Yesu akiwa mwanadamu, Mungu aliondoa miili yao.—Kum. 34:5, 6; Luka 24:1-3; Mdo. 2:31; 1 Kor. 15:50; Yuda 9.