Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutambua Daraka la Yesu Akiwa Daudi Mkuu Zaidi na Sulemani Mkuu Zaidi

Kutambua Daraka la Yesu Akiwa Daudi Mkuu Zaidi na Sulemani Mkuu Zaidi

Kutambua Daraka la Yesu Akiwa Daudi Mkuu Zaidi na Sulemani Mkuu Zaidi

“Tazama! mtu mkuu kuliko Sulemani yuko hapa.”—MT. 12:42.

1, 2. Kwa maoni ya wanadamu, kwa nini inashangaza kwamba Samweli aliagizwa amtie mafuta Daudi kuwa mfalme?

HAKUONEKANA kuwa mfalme. Badala yake, nabii Samweli alimwona kama mvulana mdogo tu mchungaji. Zaidi ya hayo, alitoka katika mji wa Bethlehemu ambao haukujulikana sana. Mji huo ulisemwa kuwa “mdogo sana kuwa kati ya maelfu ya Yuda.” (Mika 5:2) Hata hivyo, muda si muda, kijana huyo ambaye hakujulikana sana kutoka katika mji mdogo angetiwa mafuta na nabii Samweli ili awe mfalme wa Israeli.

2 Yese, hakuagiza Daudi, mwana wake aliyekuwa kivulana tu, awe wa kwanza kuletwa kwa Samweli ili atiwe mafuta; wala hakuwa wa pili wala wa tatu. Daudi, aliyekuwa mvulana wa mwisho kati ya wavulana wanane wa Yese, hata hakuwapo wakati Samweli alipokuja kwenye nyumba ya mwanamume mwaminifu, Yese, ili kumtia mafuta mmoja kati ya wana wake kuwa mfalme anayefuata wa nchi hiyo. Lakini jambo la maana ni kwamba Yehova alikuwa amemchagua Daudi.—1 Sam. 16:1-10.

3. (a) Yehova anaona jambo gani kuwa la maana zaidi anapomchunguza mtu? (b) Daudi alipotiwa mafuta, ni nini kilichoanza kutenda kazi juu yake?

3 Yehova aliona mambo ambayo Samweli hangeweza kuona. Mungu alitambua mambo yaliyokuwa katika moyo wa Daudi, na yalimpendeza. Mungu hatazami sura ya nje tu; anatazama utu wa ndani. (Soma 1 Samweli 16:7.) Kwa hiyo, Samweli alipotambua kwamba Yehova hakuwa amemchagua yeyote kati ya wale wana wengine saba wa Yese ambao walikuwa wakubwa, aliagiza mwana mdogo zaidi aletwe kutoka malishoni. Simulizi hilo linasema hivi: “Basi [Yese] akatuma watu, naye [Daudi] akaletwa. Naye alikuwa mwekundu, kijana mwenye macho yenye kupendeza na mwenye sura nzuri. Ndipo Yehova akasema: ‘Simama, mtie mafuta, kwa maana huyu ndiye!’ Basi Samweli akachukua ile pembe ya mafuta, akamtia mafuta katikati ya ndugu zake. Na roho ya Yehova ikaanza kutenda kazi juu ya Daudi kuanzia siku hiyo na kuendelea.”—1 Sam. 16:12, 13.

Daudi Alimfananisha Kristo

4, 5. (a) Yesu na Daudi wanalingana katika njia gani mbalimbali? (b) Kwa nini Yesu anaweza kuitwa Daudi Mkuu Zaidi?

4 Yesu alizaliwa Bethlehemu kama Daudi, miaka 1,100 hivi baada ya Daudi kuzaliwa. Yesu pia hakuonwa na wengi kuwa mfalme. Yaani, watu wengi katika Israeli hawakutarajia mfalme wa aina hiyo. Hata hivyo, Yehova alikuwa amemchagua Yesu kama alivyomchagua Daudi. Na kama Daudi, Yesu alipendwa na Yehova. * (Luka 3:22) ‘Roho ya Yehova ilianza kutenda kazi juu’ ya Yesu kama ilivyotenda juu ya Daudi.

5 Daudi na Yesu wanalingana katika mambo mengine mengi. Kwa mfano, Daudi alisalitiwa na mshauri wake Ahithofeli, naye Yesu alisalitiwa na mtume wake Yuda Iskariote. (Zab. 41:9; Yoh. 13:18) Daudi na Yesu walikuwa na bidii nyingi sana kwa ajili ya mahali pa ibada ya Yehova. (Zab. 27:4; 69:9; Yoh. 2:17) Yesu alikuwa pia mrithi wa Daudi. Kabla ya Yesu kuzaliwa, malaika alimwambia mama yake hivi: “Yehova Mungu atampa kiti cha ufalme cha Daudi baba yake.” (Luka 1:32; Mt. 1:1) Hata hivyo, Yesu ni mkuu zaidi kuliko Daudi kwa sababu ahadi zote kumhusu Masihi zingetimizwa na Yesu. Yeye ndiye Daudi Mkuu Zaidi, yule Mfalme wa Kimasihi aliyetazamiwa kwa muda mrefu.—Yoh. 7:42.

Mfuate Yule Mfalme-Mchungaji

6. Daudi alikuwa mchungaji mzuri katika njia gani?

6 Yesu ni mchungaji pia. Mchungaji mwema ana sifa gani? Analitunza, analilisha, na kulilinda kundi lake kwa uaminifu na kwa ujasiri. (Zab. 23:2-4) Daudi alipokuwa kijana alikuwa mchungaji, naye aliwatunza vizuri sana kondoo wa baba yake. Alitenda kwa ujasiri wakati kondoo hao walipokabili hatari na alihatarisha uhai wake ili kuwalinda kutokana na simba na dubu.—1 Sam. 17:34, 35.

7. (a) Ni nini kilichomtayarisha Daudi kutimiza madaraka yake akiwa mfalme? (b) Yesu alionyesha jinsi gani kwa matendo kwamba yeye ndiye Mchungaji Mwema?

7 Miaka ambayo Daudi alikaa mashambani na milimani akiwatunza kondoo ilimtayarisha kutimiza wajibu na madaraka mazito zaidi ya kulichunga taifa la Israeli. * (Zab. 78:70, 71) Yesu pia ameonyesha kwa matendo kwamba yeye ni mchungaji bora kabisa. Yehova anamwongoza na kumpa nguvu za kulichunga ‘kundi lake dogo’ na pia “kondoo wengine.” (Luka 12:32; Yoh. 10:16) Hivyo, Yesu ndiye yule Mchungaji Mwema. Anajua kundi lake vizuri sana hivi kwamba anamwita kila kondoo kwa jina. Anawapenda sana kondoo wake hivi kwamba alipokuwa duniani alijitoa kwa kupenda kwa ajili yao. (Yoh. 10:3, 11, 14, 15) Akiwa Mchungaji Mwema, Yesu anatimiza mambo ambayo Daudi hangeweza kamwe kutimiza. Fidia au dhabihu yake ya ukombozi iliwapa wanadamu nafasi ya kuokolewa kutoka katika kifo. Hakuna kitu kinachoweza kumzuia asilichunge ‘kundi lake dogo’ ili lipate uhai usioweza kufa mbinguni na kuwaongoza ‘kondoo wake wengine’ kupata uzima wa milele katika ulimwengu mpya wenye uadilifu usio na watu hatari ambao ni kama mbwa-mwitu.—Soma Yohana 10:27-29.

Mfuate Yule Mfalme Anayeshinda

8. Daudi alithibitika jinsi gani kuwa mfalme anayeshinda?

8 Akiwa mfalme, Daudi alikuwa shujaa mwenye ujasiri ambaye aliilinda nchi ya watu wa Mungu, na “Yehova akaendelea kumwokoa Daudi popote alipoenda.” Chini ya uongozi wa Daudi, mipaka ya taifa hilo ilipanuka kutoka mto wa Misri mpaka mto Efrati. (2 Sam. 8:1-14) Kwa uwezo wa Yehova, Daudi alikuja kuwa mtawala mwenye nguvu zaidi. Biblia inasema: “Sifa ya Daudi ikaanza kuenea katika nchi zote, na Yehova akatia hofu yake juu ya mataifa yote.”—1 Nya. 14:17.

9. Eleza jinsi Yesu alivyoshinda akiwa Mfalme Aliyechaguliwa.

9 Kama Mfalme Daudi, Yesu pia hakuwa mwoga alipokuwa mwanadamu. Akiwa Mfalme Aliyechaguliwa, alionyesha mamlaka yake juu ya roho waovu, na kuwaokoa watu kutoka kwa uvutano wao. (Marko 5:2, 6-13; Luka 4:36) Hata adui wake mkuu, Shetani Ibilisi, hana uwezo juu yake. Kwa uwezo wa Yehova, Yesu aliushinda ulimwengu, ambao unakaa katika nguvu za Shetani.—Yoh. 14:30; 16:33; 1 Yoh. 5:19.

10, 11. Yesu ana daraka gani akiwa Mfalme-Shujaa wa Vita huko mbinguni?

10 Miaka 60 hivi baada ya Yesu kufa na kufufuliwa kwenye uhai mbinguni, mtume Yohana alipata maono ya kinabii kuhusu Yesu akitimiza daraka Lake akiwa Mfalme-Shujaa wa Vita huko mbinguni. Yohana anaandika hivi: “Tazama! farasi mweupe; na yule anayeketi juu yake alikuwa na upinde; naye akapewa taji, naye akaenda akishinda na kukamilisha ushindi wake.” (Ufu. 6:2) Yesu ndiye anayepanda farasi huyo mweupe. ‘Alipewa taji’ mwaka wa 1914 wakati alipowekwa kuwa Mfalme katika Ufalme wa mbinguni. Baada ya hapo, “akaenda akishinda.” Ndiyo, kama Daudi, Yesu ni mfalme anayeshinda. Muda mfupi baada ya kuwekwa kuwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu, alimshinda Shetani katika vita na kumtupa duniani pamoja na roho wake waovu. (Ufu. 12:7-9) Ataendelea kupanda farasi na kushinda mpaka ‘atakapokamilisha ushindi wake,’ na kuuharibu kabisa mfumo mwovu wa Shetani.—Soma Ufunuo 19:11, 19-21.

11 Hata hivyo, kama Daudi, Yesu ni mfalme mwenye huruma, naye ataulinda “umati mkubwa” ili uokoke Har-Magedoni. (Ufu. 7:9, 14) Zaidi ya hayo, chini ya utawala wa Yesu na wale warithi wenzake 144,000 waliofufuliwa, kutakuwa na “ufufuo wa waadilifu na wasio waadilifu pia.” (Mdo. 24:15) Wale watakaofufuliwa duniani watakuwa na tumaini la kuishi milele. Watakuwa na maisha mazuri ajabu wakati ujao! Sote na tuazimie kuendelea ‘kufanya yaliyo mema,’ ili tuishi wakati ambapo dunia itajaa raia waadilifu na wenye furaha wa yule Daudi Mkuu Zaidi.—Zab. 37:27-29.

Sala ya Sulemani ya Kuomba Hekima Yajibiwa

12. Sulemani aliomba nini katika sala?

12 Sulemani mwana wa Daudi alimfananisha pia Yesu. * Sulemani alipokuwa mfalme, Yehova alimtokea katika ndoto na kumwambia kwamba Angempa kitu chochote ambacho angeomba. Sulemani angeweza kuomba utajiri zaidi, mamlaka, au maisha marefu zaidi. Badala yake, alimwomba hivi Yehova bila ubinafsi: “Sasa unipe hekima na ujuzi ili nitoke mbele ya watu hawa na ili niingie ndani, kwa maana ni nani anayeweza kuwahukumu hawa watu wako walio wengi?” (2 Nya. 1:7-10) Yehova alijibu sala ya Sulemani.—Soma 2 Mambo ya Nyakati 1:11, 12.

13. Sulemani alikuwa na hekima isiyo na kifani jinsi gani, na ilitoka wapi?

13 Maadamu Sulemani alikuwa mwaminifu kwa Yehova, alisema maneno yenye hekima kuliko watu wote katika siku zake. Sulemani alisema “methali elfu tatu.” (1 Fal. 4:30, 32, 34) Methali zake nyingi ziliandikwa na bado zinathaminiwa sana na watu wanaotafuta hekima. Malkia wa Sheba alisafiri umbali wa kilomita 2,400 ili kuijaribu hekima ya Sulemani kwa “maswali yenye kutatanisha.” Alivutiwa sana na mambo ambayo Sulemani alisema na pia ufanisi wa ufalme wake. (1 Fal. 10:1-9) Biblia inafunua Chanzo cha hekima ya Sulemani inaposema hivi: “Watu wote wa dunia walikuwa wakiutafuta uso wa Sulemani ili wasikie hekima yake ambayo Mungu alikuwa ametia moyoni mwake.”—1 Fal. 10:24.

Mfuate Yule Mfalme Mwenye Hekima

14. Ni katika njia gani Yesu alikuwa “mtu mkuu kuliko Sulemani”?

14 Ni mwanadamu mmoja tu aliyekuwa na hekima nyingi sana kuliko Sulemani. Mwanadamu huyo ni Yesu Kristo, ambaye alisema kwamba alikuwa “mtu mkuu kuliko Sulemani.” (Mt. 12:42) Yesu alisema “maneno ya uzima wa milele.” (Yoh. 6:68) Kwa mfano, Mahubiri ya Mlimani yanaeleza kindani kanuni za methali fulani za Sulemani. Sulemani alieleza mambo mbalimbali yanayomletea furaha mwabudu wa Yehova. (Met. 3:13; 8:32, 33; 14:21; 16:20) Yesu alikazia kwamba furaha ya kweli inatokana na mambo yanayohusiana na ibada ya Yehova na kutimia kwa ahadi za Mungu. Alisema hivi: “Wenye furaha ni wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho, kwa kuwa ufalme wa mbinguni ni wao.” (Mt. 5:3) Wale wanaofuata kanuni zilizo katika mafundisho ya Yesu wanakuwa na uhusiano wa karibu zaidi pamoja na Yehova, “chemchemi ya uzima.” (Zab. 36:9; Met. 22:11; Mt. 5:8) Kristo anawakilisha “hekima ya Mungu.” (1 Kor. 1:24, 30) Akiwa Mfalme wa Kimasihi, Yesu Kristo ana “roho ya hekima.”—Isa. 11:2.

15. Tunaweza kufaidika namna gani kutokana na hekima inayotoka kwa Mungu?

15 Tukiwa wafuasi wa yule Sulemani Mkuu Zaidi, tunaweza kufaidika namna gani kutokana na hekima inayotoka kwa Mungu? Kwa kuwa hekima ya Yehova inafunuliwa katika Neno lake, ni lazima tujitahidi sana kuipata kwa kujifunza Biblia kwa makini, hasa maneno ya Yesu yaliyoandikwa, na kutafakari mambo tunayosoma. (Met. 2:1-5) Kwa kuongezea, tunahitaji kuendelea kumwomba Mungu hekima bila kuchoka. Neno la Mungu linatuhakikishia kwamba sala zetu za kutoka moyoni za kuomba msaada zitajibiwa. (Yak. 1:5) Kwa msaada wa roho takatifu, tutapata hazina za hekima katika Neno la Mungu ambazo zinaweza kutusaidia kupambana na matatizo na kufanya maamuzi yenye hekima. (Luka 11:13) Sulemani aliitwa pia “mkutanishaji” ambaye “aliendelea kuwafundisha watu ujuzi.” (Mhu. 12:9, 10) Yesu, akiwa Kichwa cha kutaniko la Kikristo, pia ni mkutanishaji wa watu wake. (Yoh. 10:16; Kol. 1:18) Kwa hiyo, tunapaswa kuhudhuria mikutano ya kutaniko, ambamo ‘tunaendelea kufundishwa.’

16. Sulemani na Yesu wanalingana katika njia gani?

16 Sulemani alikuwa mfalme mwenye bidii sana. Alipanga programu ya ujenzi katika taifa lote, alisimamia ujenzi wa majumba ya kifalme, barabara, mifereji ya maji, majiji yenye maghala, majiji ya magari ya vita, na majiji ya wapanda-farasi. (1 Fal. 9:17-19) Miradi yake ya ujenzi ilinufaisha ufalme wake wote. Yesu pia ni mjenzi. Alijenga kutaniko lake juu ya “mwamba.” (Mt. 16:18) Yeye pia atasimamia kazi ya ujenzi itakayofanywa katika ulimwengu mpya.—Isa. 65:21, 22.

Mfuate Yule Mfalme wa Amani

17. (a) Utawala wa Sulemani ulikuwa na sifa gani ya pekee? (b) Sulemani hangeweza kufanya nini?

17 Jina Sulemani linatokana na neno linalomaanisha “amani.” Mfalme Sulemani alitawala akiwa Yerusalemu. Jina Yerusalemu linamaanisha “Umilikaji wa Amani Mara Mbili.” Utawala wake wa miaka 40 ulikuwa na amani isiyo na kifani katika taifa la Israeli. Biblia inasema hivi kuhusu miaka hiyo: “Yuda na Israeli wakaendelea kukaa salama, kila mtu chini ya mzabibu wake mwenyewe na chini ya mtini wake mwenyewe, kuanzia Dani mpaka Beer-sheba, siku zote za Sulemani.” (1 Fal. 4:25) Hata hivyo, ingawa Sulemani alikuwa na hekima nyingi sana hakuweza kuwaweka huru raia wake kutoka katika utumwa wa magonjwa, dhambi, na kifo. Lakini, yule Sulemani Mkuu Zaidi, atawaweka huru raia wake kutoka katika utumwa huo wote.—Soma Waroma 8:19-21.

18. Tunafurahia hali gani katika kutaniko la Kikristo?

18 Hata sasa tunafurahia amani katika kutaniko la Kikristo. Kwa hakika, tunafurahia paradiso ya kiroho iliyo ya kweli. Tuna amani pamoja na Mungu na wanadamu wenzetu. Ona kwamba Isaya alitabiri kuhusu baraka ambazo tunafurahia leo: “Nao watafua panga zao ziwe majembe na mikuki yao iwe miundu. Taifa halitainua upanga juu ya taifa, wala hawatajifunza vita tena.” (Isa. 2:3, 4) Tunapotenda kupatana na roho ya Mungu, tunachangia umaridadi wa paradiso hiyo ya kiroho.

19, 20. Tuna sababu gani za kushangilia?

19 Hata hivyo, hali zitakuwa bora hata zaidi wakati ujao. Wanadamu watiifu watakapofurahia amani isiyo na kifani chini ya utawala wa Yesu, ‘watawekwa huru kutoka katika utumwa wa uharibifu’ hatua kwa hatua mpaka watakapofikia ukamilifu wa kibinadamu. (Rom. 8:21) Baada ya kupita mtihani wa mwisho mwishoni mwa utawala wa Miaka Elfu Moja, “wapole wataimiliki dunia, nao watapata furaha yao tele katika wingi wa amani.” (Zab. 37:11; Ufu. 20:7-10) Kwa kweli, utawala wa Kristo Yesu utakuwa bora zaidi kuliko utawala wa Sulemani kwa njia ambazo hatuwezi kamwe kuwazia!

20 Kama Waisraeli walivyoshangilia chini ya uongozi wa Musa, Daudi, na Sulemani, tutashangilia hata zaidi chini ya utawala wa Kristo. (1 Fal. 8:66) Tunamshukuru sana Yehova kwa kutupa Mwana wake mzaliwa wa pekee—ambaye ni Musa, Daudi, na Sulemani Mkuu Zaidi!

[Maelezo ya chini]

^ fu. 4 Huenda jina Daudi linamaanisha “Mpendwa.” Wakati Yesu alipobatizwa na wakati alipogeuka umbo, Yehova alizungumza kutoka mbinguni akimwita “mwanangu, mpendwa.”—Mt. 3:17; 17:5.

^ fu. 7 Daudi alikuwa pia kama mwana-kondoo anayemtumaini mchungaji wake. Alimtegemea yule Mchungaji Mkuu Zaidi, Yehova, ili amlinde na kumwongoza. Alisema hivi akiwa na uhakika kabisa: “Yehova ni Mchungaji wangu. Sitakosa chochote.” (Zab. 23:1) Yohana Mbatizaji alimtambulisha Yesu kuwa “Mwana-Kondoo wa Mungu.”—Yoh. 1:29.

^ fu. 12 Inapendeza kwamba jina la pili la Sulemani lilikuwa Yedidia, ambalo linamaanisha “Mpendwa wa Yah.”—2 Sam. 12:24, 25.

Je, Unaweza Kueleza?

• Yesu ni Daudi Mkuu Zaidi jinsi gani?

• Yesu ni Sulemani Mkuu Zaidi jinsi gani?

• Ni jambo gani unalothamini kumhusu Daudi Mkuu Zaidi, ambaye pia ni Sulemani Mkuu Zaidi?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 31]

Hekima ambayo Sulemani alipewa na Mungu ilionyesha mapema hekima ya yule Sulemani Mkuu Zaidi

[Picha katika ukurasa wa 32]

Utawala wa Yesu utakuwa bora zaidi kuliko utawala wa Sulemani na wa Daudi kwa njia ambazo hatuwezi kamwe kuwazia!