Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Iga Ushikamanifu wa Ittai

Iga Ushikamanifu wa Ittai

Iga Ushikamanifu wa Ittai

“MATENDO yako ni makuu na ya ajabu, Yehova Mungu, Mweza-Yote. Njia zako ni za uadilifu na za kweli, Mfalme wa umilele. Ni nani ambaye kwa kweli hatakuogopa wewe, Yehova, na kulitukuza jina lako, kwa sababu wewe peke yako ni mshikamanifu?” Wimbo huo, unaoimbwa mbinguni na “wale wanaotokea wakiwa washindi kutoka kwa yule mnyama-mwitu na kutoka kwa ile sanamu yake,” unakazia ushikamanifu wa Mungu. (Ufu. 15:2-4) Yehova anataka waabudu wake wamwige katika kuonyesha sifa hiyo yenye kuvutia.—Efe. 4:24.

Kwa upande mwingine, Shetani Ibilisi, anajitahidi anavyoweza kuwatenganisha watumishi wa Mungu walio duniani kutoka kwa upendo wa Mungu wanayemwabudu. Hata hivyo, wengi wameendelea kuwa washikamanifu kwa Mungu, hata chini ya hali ngumu sana. Tunafurahi kama nini kwamba Yehova anathamini sana ushikamanifu huo! Kwa kweli, tunahakikishiwa hivi: “Yehova ni mpenda-haki, naye hatawaacha washikamanifu wake.” (Zab. 37:28) Ili kutusaidia kuendelea kuwa washikamanifu, ametia ndani ya Neno lake masimulizi ya watu wengi washikamanifu. Kwa mfano, kuna simulizi la yule Mgathi aliyeitwa Itai.

‘Mgeni na Mhamishwa’

Inadhaniwa kwamba Itai alikuwa mwenyeji wa jiji maarufu la Ufilisti lililoitwa Gathi, nyumbani kwa lile jitu Goliathi na maadui wengine wenye kuogopesha wa Israeli. Katika Biblia, shujaa huyu wa vita, Itai, anatajwa kwa mara ya kwanza wakati Absalomu anapomwasi Mfalme Daudi. Wakati huo, Itai na wanaume 600 Wafilisti waliokuwa wamemfuata waliishi uhamishoni karibu na Yerusalemu.

Huenda hali ya Itai na wafuasi wake ilimkumbusha Daudi wakati alipokuwa mkimbizi, wakati yeye na mashujaa 600 Waisraeli walipohamia eneo la Ufilisti na kuingia katika milki ya Akishi, mfalme wa Gathi. (1 Sam. 27:2, 3) Itai na wanaume wake wangefanya nini wakati ambapo Daudi angekabiliana na uasi wa mwana wake Absalomu? Je, wangemuunga mkono Absalomu, wangeamua kutounga mkono upande wowote, au wangejiunga na Daudi na wanaume wake?

Wazia hali ilivyokuwa wakati Daudi alipokuwa akikimbia kutoka Yerusalemu na kusimama mahali panapoitwa Beth-merhaki, jina linalomaanisha “Nyumba ya Mbali.” Huenda ndiyo nyumba ya mwisho katika eneo la Mlima wa Mizeituni huko Yerusalemu kabla tu ya kuvuka Bonde la Kidroni. (2 Sam. 15:17) Akiwa hapo, Daudi anakagua tena majeshi yake yanapopita. Tazama! Daudi haandamani tu na Waisraeli washikamanifu bali pia na Wakerethi wote na Wapelethi wote. Zaidi ya hilo, Wagathi wote, yaani, Itai na mashujaa wake wa vita 600 wamefuatana naye.—2 Sam. 15:18.

Daudi anamwambia hivi Itai kwa huruma nyingi: “Kwa nini wewe pia uende pamoja nasi? Rudi, ukae na mfalme [huenda alimaanisha Absalomu]; kwa maana wewe ni mgeni, na tena, wewe ni mhamishwa kutoka mahali pako. Ulikuja jana tu na je, leo nikufanye utange-tange pamoja nasi, uende wakati ninapoenda na popote ninapoenda? Rudi, na uwachukue ndugu zako urudi pamoja nao, na Yehova akuonyeshe fadhili zenye upendo na uaminifu!”—2 Sam. 15:19, 20.

Itai anatangaza ushikamanifu wake usioyumbayumba. Anajibu hivi: “Kama Yehova anavyoishi na kama anavyoishi bwana wangu mfalme, mahali atakapokuwa bwana wangu mfalme, iwe ni kifo ama ni uzima, hapo ndipo mtumishi wako atakapokuwa!” (2 Sam. 15:21) Huenda hilo lilimkumbusha Daudi maneno yaliyosemwa na Ruthu, nyanya ya baba yake. (Rut. 1:16, 17) Daudi aliguswa moyo na maneno hayo ya Itai, hivi kwamba akamwambia hivi Itai: “Nenda uvuke” Bonde la Kidroni. Basi, “Itai Mgathi akavuka, na pia watu wake wote na watoto wadogo wote waliokuwa pamoja naye.”—2 Sam. 15:22.

“Ili Kutufundisha Sisi”

Andiko la Waroma 15:4 linasema hivi: “Mambo yote yaliyoandikwa zamani yaliandikwa ili kutufundisha sisi.” Hivyo, tunapaswa kujiuliza hivi: Tunajifunza nini kutokana na mfano wa Itai? Fikiria mambo ambayo huenda yalimchochea awe mshikamanifu kwa Daudi. Hata ingawa alikuwa mgeni na mhamishwa kutoka Ufilisti, Itai alitambua kwamba Yehova ni Mungu aliye hai na Daudi ni mtiwa-mafuta wa Yehova. Itai hakuchochewa na chuki iliyokuwapo kati ya Waisraeli na Wafilisti. Hakuona tu kwamba Daudi ndiye aliyemuua yule shujaa Mfilisti Goliathi na Wafilisti wengine wengi. (1 Sam. 18:6, 7) Itai alimwona Daudi kuwa mtu aliyempenda Yehova na bila shaka aliona sifa nzuri za Daudi. Hivyo, Daudi akamheshimu sana Itai. Zaidi ya hayo, Daudi aliweka sehemu ya tatu ya majeshi yake “chini ya mkono wa Itai” katika vita vya mwisho juu ya majeshi ya Absalomu!—2 Sam. 18:2.

Sisi pia tunapaswa kujitahidi kuona sifa nzuri za wengine badala ya kukazia fikira tofauti za kitamaduni, kijamii, au kikabila—ubaguzi au chuki yoyote ambayo huenda bado tunayo. Uhusiano mzuri uliositawi kati ya Daudi na Itai unaonyesha kwamba kumjua na kumpenda Yehova kunaweza kutusaidia kushinda vizuizi hivyo.

Tunapotafakari kuhusu mfano wa Itai, tunaweza kujiuliza hivi: ‘Je, ninaonyesha ushikamanifu kama huo kwa Daudi Mkuu Zaidi, Kristo Yesu? Je, ninaonyesha kwamba mimi ni mshikamanifu kwa kushiriki kwa bidii katika kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme na kufanya wanafunzi?’ (Mt. 24:14; 28:19, 20) ‘Niko tayari kuvumilia mambo mengi kadiri gani ili nionyeshe kwamba mimi ni mshikamanifu?’

Vichwa vya familia pia wanafaidika kwa kutafakari kuhusu ushikamanifu wa Itai. Uaminifu wa Itai kwa Daudi na uamuzi wake wa kwenda pamoja na mfalme aliyetiwa mafuta na Mungu uliwachochea wanaume wa Itai. Vivyo hivyo, maamuzi ambayo vichwa vya familia wanafanya ili kutegemeza ibada ya kweli yanaweza kuwa na uvutano kwa familia zao na yanaweza hata kusababisha matatizo ya muda. Hata hivyo, tunahakikishiwa hivi: ‘Kwa mtu mshikamanifu Yehova atatenda kwa ushikamanifu.’—Zab. 18:25.

Baada ya vita kati ya Daudi na Absalomu, Maandiko hayasemi zaidi kuhusu Itai. Hata hivyo, masimulizi hayo mafupi kumhusu katika Neno la Mungu yanatusaidia kufahamu vizuri utu wake wakati wa kipindi kigumu katika maisha ya Daudi. Kwa kuwa Itai anatajwa katika Maandiko, hilo linaonyesha kwamba Yehova anaona na kuwathawabisha watu washikamanifu.—Ebr. 6:10.