Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Malaika—“Roho kwa Ajili ya Utumishi wa Watu Wote”

Malaika—“Roho kwa Ajili ya Utumishi wa Watu Wote”

Malaika—“Roho kwa Ajili ya Utumishi wa Watu Wote”

“Je, wao wote si roho kwa ajili ya utumishi wa watu wote, waliotumwa kuhudumu kwa ajili ya wale watakaorithi wokovu?”—EBR. 1:14.

1. Andiko la Mathayo 18:10 na Waebrania 1:14 linatufariji jinsi gani?

YESU KRISTO aliwaonya hivi watu ambao wangewakwaza wafuasi wake: “Angalieni msimdharau mmoja wa hawa wadogo; kwa maana ninawaambia ninyi kwamba malaika zao mbinguni sikuzote huuona uso wa Baba yangu aliye mbinguni.” (Mt. 18:10) Mtume Paulo aliandika hivi kuhusu malaika waadilifu: “Je, wao wote si roho kwa ajili ya utumishi wa watu wote, waliotumwa kuhudumu kwa ajili ya wale watakaorithi wokovu?” (Ebr. 1:14) Maneno hayo yanatuhakikishia kwamba Mungu anatumia viumbe wake wa roho kuwasaidia wanadamu. Biblia inatuambia nini kuwahusu malaika? Wanatusaidia jinsi gani? Tunaweza kujifunza nini kutokana na mfano wao?

2, 3. Viumbe wa roho walio mbinguni wana majukumu gani?

2 Kuna mamilioni ya malaika waaminifu mbinguni. Wote wana ‘uwezo katika nguvu, wakilitenda neno lake.’ (Zab. 103:20; soma Ufunuo 5:11.) Wana hao wa roho wa Mungu wana utu, sifa kama za Mungu, na uhuru wa kuchagua. Wamepangwa vizuri na wana vyeo vya juu katika mpango wa Mungu, na malaika mkuu ni Mikaeli (jina la Yesu la mbinguni). (Dan. 10:13; Yuda 9) Huyo “mzaliwa wa kwanza wa viumbe vyote” ni “Neno,” au Msemaji wa Mungu, na alitumiwa na Yehova kuumba vitu vingine vyote.—Kol. 1:15-17; Yoh. 1:1-3.

3 Maserafi wako chini ya yule malaika mkuu, nao wanatangaza utakatifu wa Yehova na wanawasaidia watu wake kuendelea kuwa safi kiroho. Pia, kuna makerubi, ambao ni wahudumu wa kutetea ukuu wa Mungu. (Mwa. 3:24; Isa. 6:1-3, 6, 7) Malaika wengine, au wajumbe, wana migawo mbalimbali katika kutimiza mapenzi ya Mungu.—Ebr. 12:22, 23.

4. Malaika walitenda jinsi gani msingi wa dunia ulipowekwa, na matokeo yangekuwa nini ikiwa wanadamu wangetumia uhuru wa kuchagua kwa njia inayofaa?

4 Malaika wote walishangilia ‘msingi wa dunia ulipowekwa’ na wakashiriki kwa furaha katika kazi waliyopewa wakati dunia yetu ambayo ni ya pekee sana ilipotayarishwa kuwa makao ya wanadamu. (Ayu. 38:4, 7) Yehova alimuumba mwanadamu kuwa “mdogo kidogo kuliko malaika” lakini akamfanya katika “mfano” Wake, na hivyo kuwawezesha wanadamu kuwa na sifa za pekee kama za Muumba. (Ebr. 2:7; Mwa. 1:26) Kwa kutumia zawadi ya uhuru wa kuchagua kwa njia inayofaa, Adamu na Hawa na wazao wao wangeweza kufurahia maisha katika paradiso wakiwa sehemu ya familia ya Yehova ya ulimwenguni pote ya viumbe wenye akili.

5, 6. Ni uasi gani uliotokea mbinguni, na Mungu alitenda jinsi gani?

5 Kwa hakika, malaika watakatifu walishangaa sana walipoona uasi ukianza katika familia ya Mungu. Mmoja wa malaika hao hakutosheka kumsifu Yehova lakini alitamani kuabudiwa. Alijifanya kuwa Shetani (jina linalomaanisha “Mpinzani”) kwa kutilia shaka haki ya Yehova ya kutawala na kujaribu kwa kimbelembele kuanzisha utawala wake pinzani. Shetani aliposema uwongo kwa mara ya kwanza, aliwachochea wale wenzi wa kwanza wa ndoa wajiunge naye kumwasi Muumba wao mwenye upendo.—Mwa. 3:4, 5; Yoh. 8:44.

6 Yehova alitangaza haraka hukumu juu ya Shetani kwa kusema hivi katika unabii wa kwanza wa Biblia: “Nitaweka uadui kati yako na yule mwanamke na kati ya uzao wako na uzao wake. Yeye atakuponda kichwa nawe utamtia jeraha kwenye kisigino.” (Mwa. 3:15) Uadui ungeendelea kuwapo kati ya Shetani na “mwanamke” wa Mungu. Ndiyo, Yehova aliliona tengenezo la mbinguni la viumbe wa roho waaminifu kuwa mwanamke wake mpendwa aliyeunganishwa naye akiwa Mume. Unabii huo uliweka msingi hakika wa tumaini, ingawa ulibaki ukiwa “siri takatifu” ambayo ilipaswa kufunuliwa hatua kwa hatua. Mungu alikusudia kwamba mmoja wa wana wa tengenezo lake la mbinguni angewaponda waasi wote na kwamba kupitia kwa mwana huyo “vitu vilivyo mbinguni na vitu vilivyo duniani” vingeunganishwa.—Efe. 1:8-10.

7. Malaika fulani walifanya nini katika siku za Noa, na matokeo yalikuwa nini?

7 Katika siku za Noa, malaika fulani waliacha “makao yao wenyewe yanayofaa” na kuvaa miili ya nyama ili kufuatia raha za kichoyo duniani. (Yuda 6; Mwa. 6:1-4) Yehova aliwatupa waasi hao katika giza zito, hivyo wakajiunga na Shetani na kuwa “majeshi ya roho waovu” na maadui hatari wa watumishi wa Mungu.—Efe. 6:11-13; 2 Pet. 2:4.

Malaika Wanatusaidia Jinsi Gani?

8, 9. Yehova amewatumia malaika jinsi gani kuwasaidia wanadamu?

8 Abrahamu, Yakobo, Musa, Yoshua, Isaya, Danieli, Yesu, Petro, Yohana, na Paulo ni kati ya wale waliohudumiwa na malaika. Malaika waadilifu walitekeleza hukumu za Mungu na kuwapa watu unabii na maagizo, kutia ndani Sheria ya Musa. (2 Fal. 19:35; Dan. 10:5, 11, 14; Mdo. 7:53; Ufu. 1:1) Kwa kuwa sasa tuna Neno la Mungu lililo kamili, malaika hawahitaji kutuletea ujumbe wa Mungu. (2 Tim. 3:16, 17) Hata ingawa hatuwezi kuwaona, malaika wanajitahidi sana kufanya mapenzi ya Mungu na kuwasaidia watumishi wake.

9 Biblia inatuhakikishia hivi: “Malaika wa Yehova anapiga kambi pande zote kuwazunguka wanaomwogopa, na yeye huwaokoa.” (Zab. 34:7; 91:11) Kwa sababu ya suala la utimilifu, Yehova anamruhusu Shetani atuletee majaribu ya kila aina. (Luka 21:16-19) Hata hivyo, Mungu anajua ikiwa tumevumilia jaribu kwa muda mrefu vya kutosha kuonyesha kwamba tutabaki washikamanifu kwake. (Soma 1 Wakorintho 10:13.) Sikuzote malaika wako macho kuingilia kati ili kutusaidia kulingana na mapenzi ya Mungu. Walimwokoa Shadraki, Meshaki, Abednego, Danieli, na Petro lakini hawakuzuia maadui wasiwaue Stefano na Yakobo. (Dan. 3:17, 18, 28; 6:22; Mdo. 7:59, 60; 12:1-3, 7, 11) Hali na masuala yaliyohusika yalikuwa tofauti. Vivyo hivyo, ndugu zetu fulani katika kambi za mateso za Wanazi waliuawa, lakini Yehova aliwasaidia wengi wao kuokoka.

10. Zaidi ya malaika kutusaidia, tunaweza pia kupata msaada gani?

10 Maandiko hayafundishi kwamba kila mtu duniani ana malaika anayemlinda. Tunasali tukiwa na uhakika kwamba “hata tukiomba nini kulingana na mapenzi yake, [Mungu] hutusikia.” (1 Yoh. 5:14) Bila shaka, Yehova anaweza kumtuma malaika atusaidie, lakini anaweza pia kutumia njia tofauti ili kutusaidia. Wakristo wenzetu wanaweza kuchochewa kutusaidia na kutufariji. Mungu anaweza kutupa hekima na nguvu za ndani tunazohitaji ili kukabiliana na “mwiba katika mwili” ambao unatufanya tuhisi kana kwamba tunapigwa makofi na “malaika wa Shetani.”—2 Kor. 12:7-10; 1 The. 5:14.

Mwige Yesu

11. Malaika walitumiwa jinsi gani kumsaidia Yesu, naye alitimiza nini kwa kubaki mwaminifu kwa Mungu?

11 Fikiria jinsi Yehova alivyowatumia malaika katika kisa cha Yesu. Walitangaza kuzaliwa na kufufuliwa kwake, nao walimhudumia alipokuwa duniani. Malaika wangeweza kuzuia asikamatwe na asiuawe kikatili. Badala yake, malaika alitumwa ili amtie nguvu. (Mt. 28:5, 6; Luka 2:8-11; 22:43) Kupatana na kusudi la Yehova, Yesu alikufa kifo cha kidhabihu na kuthibitisha kwamba mwanadamu mkamilifu anaweza kuendelea kuwa mtimilifu kwa Mungu hata anapoteswa kikamili. Hivyo, Yehova alimfufua Yesu na kumpa uhai wa mbinguni usioweza kufa, na pia akampa “mamlaka yote” na kuwatiisha malaika chini yake. (Mt. 28:18; Mdo. 2:32; 1 Pet. 3:22) Hivyo, Yesu alithibitika kuwa sehemu ya msingi ya “uzao” wa “mwanamke” wa Mungu.—Mwa. 3:15; Gal. 3:16.

12. Tunaweza kuiga jinsi gani mfano wa Yesu wa kuishi kwa utimamu wa akili?

12 Yesu alijua kwamba hakupaswa kumjaribu Yehova kwa kutazamia malaika wamwokoe ikiwa angetenda bila hekima. (Soma Mathayo 4:5-7.) Basi, acheni tumwige Yesu kwa kuishi kwa “utimamu wa akili,” bila kujihatarisha ovyoovyo, lakini tukikabili mateso tukiwa na ujasiri.—Tito 2:12.

Mambo Tunayoweza Kujifunza Kutokana na Malaika Waaminifu

13. Tunaweza kujifunza nini kutokana na mfano wa malaika waadilifu wanaotajwa kwenye 2 Petro 2:9-11?

13 Mtume Petro anataja mfano mzuri wa malaika waadilifu anapowakemea wale ‘wanaowatukana’ watumishi wa Yehova waliotiwa mafuta. Ingawa malaika wana nguvu nyingi, kwa unyenyekevu wanaepuka kuwashtaki-shtaki wengine “kwa sababu ya kumheshimu Yehova.” (Soma 2 Petro 2:9-11.) Acheni sisi pia tuepuke kuwahukumu-hukumu wengine isivyofaa, tuwaheshimu wale waliopewa mamlaka ya kusimamia kutaniko, na kuacha mambo katika mikono ya Yehova, ambaye ni Mwamuzi Mkuu Zaidi.—Rom. 12:18, 19; Ebr. 13:17.

14. Malaika wanatuwekea mfano gani kuhusu kutumikia kwa unyenyekevu?

14 Malaika wa Yehova wanatuwekea mfano mzuri wa kutumikia kwa unyenyekevu. Malaika fulani walikataa kuwafunulia wanadamu majina yao. (Mwa. 32:29; Amu. 13:17, 18) Ingawa kuna mamilioni ya viumbe wa roho mbinguni, Biblia inafunua majina ya Mikaeli na Gabrieli tu. Hilo linaweza kutuzuia tusiwape malaika heshima ambayo hawastahili. (Luka 1:26; Ufu. 12:7) Mtume Yohana alipoanguka chini ili kumwabudu malaika, malaika huyo alimpa shauri hili: “Uwe mwangalifu! Usifanye hivyo! Mimi ni mtumwa mwenzako tu na wa ndugu zako.” (Ufu. 22:8, 9) Ibada yetu, kutia ndani sala zetu, zinapaswa kumwendea Mungu peke yake.—Soma Mathayo 4:8-10.

15. Malaika wanatuwekea mfano gani katika kuonyesha subira?

15 Malaika pia wanatuwekea mfano mzuri katika kuonyesha subira. Ingawa wanataka sana kujua siri takatifu za Mungu, hawaambiwi zote. Biblia inasema hivi: “Malaika wanatamani kuchungulia ndani ya mambo hayo.” (1 Pet. 1:12) Kwa hiyo, wanafanya nini? Wanangojea kwa subira wakati unaofaa wa Mungu ‘kujulisha kupitia kutaniko’ ‘hekima yake ya namna nyingi sana.’—Efe. 3:10, 11.

16. Mwenendo wetu unaweza kuwa na uvutano gani juu ya malaika?

16 Wakristo wanaojaribiwa ni ‘tamasha kwa malaika.’ (1 Kor. 4:9) Wakiwa wameridhika sana, malaika wanaona matendo yetu ya uaminifu na hata wanashangilia mtenda-dhambi anapotubu. (Luka 15:10) Malaika wanaona mwenendo unaompendeza Mungu wa wanawake Wakristo. Biblia inasema kwamba “mwanamke anapaswa kuwa na ishara ya mamlaka juu ya kichwa chake kwa sababu ya malaika.” (1 Kor. 11:3, 10) Ndiyo, malaika wanafurahi kuona wanawake Wakristo na watumishi wengine wote wa Mungu duniani wakitii ukichwa na kufuata utaratibu wa kitheokrasi. Utii huo ni kikumbusho kinachofaa kwa wana hao wa mbinguni wa Mungu.

Malaika Wanaunga Mkono kwa Bidii Kazi ya Kuhubiri

17, 18. Kwa nini tunaweza kusema kwamba malaika wanaunga mkono kazi yetu ya kuhubiri?

17 Malaika wanahusika katika mambo fulani ya pekee yanayotukia katika “siku ya Bwana.” Kwa mfano, walihusika wakati Ufalme uliposimamishwa mwaka wa 1914 na wakati “Mikaeli na malaika zake” walipomtupa Shetani na roho wake waovu kutoka mbinguni. (Ufu. 1:10; 11:15; 12:5-9) Mtume Yohana aliona ‘malaika akiruka katikati ya mbingu, naye alikuwa na habari njema ya milele ili aitangaze kuwa habari za furaha kwa wale wanaokaa duniani.’ Malaika huyo alitangaza hivi: “Mwogopeni Mungu na kumpa utukufu, kwa sababu saa ya hukumu yake imefika, na kwa hiyo mwabuduni Yeye aliyezifanya mbingu na dunia na bahari na chemchemi za maji.” (Ufu. 14:6, 7) Hivyo, watumishi wa Yehova wana hakika kwamba watasaidiwa na malaika wanapohubiri habari njema ya Ufalme uliosimamishwa, hata ikiwa wanapingwa vikali na Ibilisi.—Ufu. 12:13, 17.

18 Leo, malaika hawazungumzi nasi ili kutuongoza kwa watu wenye mioyo minyoofu kama vile malaika mmoja alivyozungumza na Filipo na kumwelekeza kwa towashi Mwethiopia. (Mdo. 8:26-29) Hata hivyo, mambo mengi yaliyoonwa katika siku zetu yanaonyesha kwamba malaika wanaunga mkono kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme hata ingawa hatuwaoni, nao wanatuongoza kwa wale ‘wenye mwelekeo unaofaa kwa ajili ya uzima wa milele.’ * (Mdo. 13:48) Ni jambo la maana kama nini kushiriki katika huduma kwa ukawaida ili tutimize sehemu yetu katika kazi ya kuwatafuta wale wanaotaka ‘kumwabudu Baba kwa roho na kweli’!—Yoh. 4:23, 24.

19, 20. Malaika wanatimiza sehemu gani katika matukio ya “umalizio wa mfumo wa mambo”?

19 Akizungumza kuhusu siku zetu, Yesu alisema kwamba “katika umalizio wa mfumo wa mambo” malaika ‘watawatenga waovu kutoka katikati ya waadilifu.’ (Mt. 13:37-43, 49) Malaika wanashiriki katika kukusanywa kwa mwisho na kutiwa muhuri kwa watiwa-mafuta. (Soma Mathayo 24:31; Ufu. 7:1-3) Zaidi ya hilo, Yesu anaandamana na malaika ‘anapotenganisha kondoo na mbuzi.’—Mt. 25:31-33, 46.

20 “Wakati wa ufunuo wa Bwana Yesu kutoka mbinguni pamoja na malaika zake wenye nguvu” wote “wale wasiomjua Mungu na wale wasiotii habari njema juu ya Bwana wetu Yesu” wataharibiwa. (2 The. 1:6-10) Yohana alipoona maono ya tukio hilohilo, alieleza jinsi Yesu na majeshi ya kimbingu ya malaika yanavyosonga yakiwa yamepanda farasi weupe ili kupigana vita kwa uadilifu.—Ufu. 19:11-14.

21. Malaika ‘aliye na ufunguo wa abiso na mnyororo mkubwa mkononi mwake’ atamchukulia hatua gani Shetani na roho wake waovu?

21 Yohana pia ‘aliona malaika akishuka kutoka mbinguni akiwa na ufunguo wa abiso na mnyororo mkubwa mkononi mwake.’ Huyo si mwingine ila yule malaika mkuu Mikaeli, ambaye atamfunga Ibilisi na kumtupa katika abiso pamoja na roho wake waovu. Wataachiliwa kwa muda mfupi mwishoni mwa Utawala wa Kristo wa Miaka Elfu Moja wakati wanadamu wakamilifu watakapokabili jaribu la mwisho. Baadaye, Shetani na waasi wake wote wataharibiwa. (Ufu. 20:1-3, 7-10; 1 Yoh. 3:8) Uasi wote juu ya Mungu utakuwa umeondolewa.

22. Malaika watahusika jinsi gani katika mambo yatakayotukia hivi karibuni, nasi tunapaswa kuwa na maoni gani kuhusu daraka lao?

22 Ukombozi mkubwa kutoka kwa mfumo mwovu wa mambo wa Shetani unakaribia sana. Malaika watatimiza kazi hususa katika matukio hayo ya maana ambayo yatatetea enzi kuu ya Yehova na kutimiza kikamili kusudi lake kwa ajili ya dunia na wanadamu. Kwa kweli, malaika waadilifu ni “roho kwa ajili ya utumishi wa watu wote, waliotumwa kuhudumu kwa ajili ya wale watakaorithi wokovu.” Hivyo, acheni tumshukuru Yehova Mungu kwa sababu anawatumia malaika kutusaidia kufanya mapenzi yake na kupata uzima wa milele.

[Maelezo ya chini]

^ fu. 18 Ona Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu, ukurasa wa 549-551.

Ungesema Nini?

• Viumbe wa roho walio mbinguni wamepangwa jinsi gani?

• Malaika fulani walifanya nini katika siku za Noa?

• Mungu amewatumia malaika jinsi gani kutusaidia?

• Malaika waadilifu wanatimiza daraka gani katika siku zetu?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 21]

Malaika wanashangilia kufanya mapenzi ya Mungu

[Picha katika ukurasa wa 23]

Kama ilivyokuwa katika kisa cha Danieli, malaika wako macho sikuzote kuingilia kati ili kutusaidia kulingana na mapenzi ya Mungu

[Picha katika ukurasa wa 24]

Uwe jasiri, kwa maana malaika wanaunga mkono kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme!

[Hisani]

Globe: NASA photo