Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Songa Mbele Kuelekea Ukomavu—“Ile Siku Kuu ya Yehova Iko Karibu”

Songa Mbele Kuelekea Ukomavu—“Ile Siku Kuu ya Yehova Iko Karibu”

Songa Mbele Kuelekea Ukomavu—“Ile Siku Kuu ya Yehova Iko Karibu”

“Tusonge mbele kuelekea ukomavu.”—EBR. 6:1.

1, 2. Wakristo wa karne ya kwanza huko Yerusalemu na Yudea walipata jinsi gani nafasi ya “kukimbilia milimani”?

YESU alipokuwa duniani, wanafunzi wake walimkaribia na kumuuliza: “Ni nini itakayokuwa ishara ya kuwapo kwako na ya umalizio wa mfumo wa mambo?” Unabii ambao Yesu aliwapa alipojibu swali lao ulitimizwa kwa mara ya kwanza katika karne ya kwanza. Yesu alitaja tukio lisilo la kawaida ambalo lingeonyesha kwamba mwisho umekaribia. Wakati wangeona tukio hilo, ‘wale walio katika Yudea wangepaswa kuanza kukimbilia milimani.’ (Mt. 24:1-3, 15-22) Je, wanafunzi wa Yesu wangetambua ishara hiyo na kufuata maagizo yake?

2 Karibu miaka 30 baadaye, katika mwaka wa 61 W.K., mtume Paulo aliwaandikia Wakristo Waebrania waliokuwa wakiishi Yerusalemu na maeneo ya karibu ujumbe wenye nguvu na wa moja kwa moja. Paulo na waamini wenzake hawakujua kwamba ishara ya kipindi cha kwanza cha “dhiki kuu” ingetukia baada tu ya miaka mitano hivi. (Mt. 24:21) Katika mwaka wa 66 W.K., Sesho Galo aliwaongoza wanajeshi Waroma kushambulia Yerusalemu, na walikuwa karibu kuliteka jiji hilo. Lakini kwa ghafula waliondoka, na hivyo wale waliokuwa hatarini wakapata nafasi ya kukimbilia mahali salama.

3. Paulo aliwahimiza jinsi gani Wakristo Waebrania, na kwa nini?

3 Wakristo hao walihitaji utambuzi makini na ufahamu wa kiroho ambao ungewasaidia kutambua matukio yaliyotabiriwa ili waweze kukimbia. Hata hivyo, wengine wao sasa walikuwa “wazito katika kusikia.” Walikuwa kama watoto wachanga wa kiroho wanaohitaji “maziwa.” (Soma Waebrania 5:11-13.) Hata wengine ambao walikuwa wametembea katika njia ya kweli kwa miaka mingi walianza kuonyesha ishara za “kujiondoa kwa Mungu aliye hai.” (Ebr. 3:12) Wengine walikuwa na “desturi” ya kukosa mikutano ya Kikristo ‘siku hiyo ya msiba ilipokuwa inakaribia.’ (Ebr. 10:24, 25) Paulo aliwahimiza kwa wakati unaofaa, aliposema hivi: “Kwa kuwa sasa tumeliacha fundisho la msingi juu ya Kristo, na tusonge mbele kuelekea ukomavu.”—Ebr. 6:1.

4. Kwa nini ni jambo la maana kukaa macho kiroho, na ni nini kitakachotusaidia kufanya hivyo?

4 Tunaishi wakati wa utimizo wa mwisho wa unabii wa Yesu. “Ile siku kuu ya Yehova iko karibu.” Mfumo wote wa Shetani utaharibiwa katika siku hiyo. (Sef. 1:14) Ni lazima tukae macho kabisa kiroho kuliko wakati mwingine wowote ule. (1 Pet. 5:8) Je, kweli tunafanya hivyo? Ukomavu wa Kikristo utatusaidia kukazia macho nyakati tunamoishi.

Ukomavu wa Kikristo Unamaanisha Nini?

5, 6. (a) Ukomavu wa kiroho unatia ndani nini? (b) Ili tusonge mbele kuelekea ukomavu tunahitaji kujitahidi katika sehemu gani mbili?

5 Paulo aliwatia moyo Wakristo Waebrania wa karne ya kwanza wasonge mbele kufikia ukomavu na pia akawaambia kile ambacho ukomavu wa kiroho unamaanisha. (Soma Waebrania 5:14.) “Watu wakomavu” hawatosheki tu na “maziwa.” Wanakula “chakula kigumu.” Kwa hiyo, wanajua “mambo ya msingi” na “mambo mazito” ya ile kweli. (1 Kor. 2:10) Zaidi ya hayo, nguvu zao za ufahamu zimezoezwa kwa kutumia mambo wanayojua ili kuwasaidia kutofautisha yaliyo sawa na yaliyo makosa. Wanapohitaji kufanya uamuzi, mazoezi hayo yanawawezesha kutambua kanuni za Kimaandiko zinazohusika na jinsi ya kuzitumia.

6 Paulo aliandika hivi: “Ni lazima kwetu kuyakazia uangalifu zaidi kuliko ilivyo kawaida mambo tuliyosikia, ili tusipeperushwe kamwe.” (Ebr. 2:1) Tunaweza kupeperuka kutoka katika imani bila sisi kutambua. Tunaweza kuepuka hali hiyo kwa kukazia “uangalifu zaidi kuliko ilivyo kawaida” kweli za kiroho tunazojifunza. Kwa hiyo, kila mmoja wetu anahitaji kujiuliza hivi: ‘Je, bado ninajifunza mambo ya msingi tu? Je, inawezekana kwamba ninafuata upepo tu na kufanya mambo kidesturi, lakini sithamini kweli kwa moyo wangu wote? Ninaweza kufanya maendeleo ya kiroho yanayofaa jinsi gani?’ Ili tusonge mbele kuelekea ukomavu ni lazima tujitahidi angalau katika sehemu mbili. Ni lazima tulifahamu vizuri Neno la Mungu. Na tunahitaji kujifunza kutii.

Lifahamu Vizuri Neno la Mungu

7. Tunaweza kufaidika jinsi gani kwa kulifahamu vizuri Neno la Mungu?

7 Paulo aliandika hivi: “Kila mtu anayetumia maziwa hafahamu neno la uadilifu, kwa maana yeye ni mtoto mchanga.” (Ebr. 5:13) Ili kufikia ukomavu, ni lazima tulifahamu vizuri Neno la Mungu, yaani, ujumbe ambao ametupa. Kwa kuwa ujumbe huo uko katika Neno lake, Biblia, tunapaswa kuwa wanafunzi wenye bidii wa Maandiko na wa vichapo vya “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” (Mt. 24:45-47) Kujifunza kwa njia hiyo kutatusaidia kuelewa mawazo ya Mungu na kuzoeza nguvu zetu za ufahamu. Fikiria mfano wa mwanamke Mkristo anayeitwa Orchid. * Anasema hivi: “Kikumbusho ambacho kimebadili kabisa maisha yangu ni kikumbusho kuhusu kusoma Biblia kwa ukawaida. Ilinichukua miaka miwili hivi kusoma Biblia yote, lakini nilihisi ni kana kwamba ndipo tu nilianza kumjua Muumba wangu. Nilijifunza kuhusu njia zake, mambo anayopenda na yale anayochukia, wingi wa nguvu zake, na kina cha hekima yake. Kusoma Biblia kila siku kumenisaidia kukabiliana na hali fulani ngumu sana katika maisha yangu.”

8. Neno la Mungu linaweza kutupa nguvu za kufanya nini?

8 Kusoma kwa ukawaida sehemu fulani ya Neno la Mungu kunaruhusu ujumbe wake ‘uwe na nguvu’ katika maisha yetu. (Soma Waebrania 4:12.) Kusoma kwa ukawaida Neno la Mungu kunaweza kufinyanga utu wetu wa ndani na kutufanya tumpendeze Yehova zaidi. Je, unahitaji kuongeza wakati unaotumia katika kusoma Biblia na kutafakari kuhusu mambo inayosema?

9, 10. Kulifahamu Neno la Mungu kunatia ndani nini? Toa mfano.

9 Kuifahamu Biblia kunatia ndani mengi zaidi ya kujua tu yale inayosema. Watoto wachanga wa kiroho katika siku za Paulo walifahamu Neno la Mungu lililoongozwa na roho. Hata hivyo, hawakulitumia kibinafsi na kuona faida yake. Hawakuufahamu ujumbe wake kwa kuuruhusu uwaongoze kufanya maamuzi yenye hekima katika maisha yao.

10 Kulifahamu Neno la Mungu kunamaanisha kujua yaliyomo na kuyatumia mambo hayo maishani. Kisa cha dada Mkristo anayeitwa Kyle kinaonyesha jinsi tunavyoweza kufanya hivyo. Kyle aligombana na mfanyakazi mwenzake. Alichukua hatua gani ili kusuluhisha ugomvi huo? Anaeleza: “Nilikumbuka mara moja andiko la Waroma 12:18, linalosema hivi: ‘Kwa kadiri inavyowategemea ninyi, iweni wenye kufanya amani na watu wote.’ Kwa hiyo, nilipanga kuzungumza na mfanyakazi huyo baada ya kazi.” Mazungumzo hayo yalikuwa mazuri sana, na mfanyakazi huyo alifurahi kwamba Kyle alichukua hatua hiyo. Kyle anasema: “Nilijifunza kwamba tukitumia kanuni za Biblia bila shaka tutafanikiwa.”

Jifunze Kutii

11. Ni nini kinachoonyesha kwamba inaweza kuwa vigumu kutii tunapokabili hali ngumu?

11 Inaweza kuwa vigumu kutumia mambo ambayo tumejifunza kutoka katika Maandiko, hasa tunapokabili hali ngumu. Kwa mfano, muda mfupi baada ya Yehova kuwaweka huru wana wa Israeli kutoka utumwani huko Misri, ‘walianza kugombana na Musa’ nao ‘wakaendelea kumjaribu Yehova.’ Kwa nini? Kwa sababu hawakuwa na maji ya kunywa. (Kut. 17:1-4) Katika muda usiozidi miezi miwili baada ya kufanya agano pamoja na Mungu na kukubali kufanya “mambo yote ambayo Yehova [alikuwa] amesema,” walivunja sheria iliyohusu kuabudu sanamu. (Kut. 24:3, 12-18; 32:1, 2, 7-9) Je, waliogopa kwa sababu Musa alikawia kurudi alipokuwa akipewa maagizo kwenye Mlima Horebu? Je, huenda Waisraeli walifikiri kwamba Waamaleki wangewashambulia tena na kuwashinda kwa sababu Musa hakuwapo, yule ambaye mwanzoni aliinua mikono wakashinda? (Kut. 17:8-16) Inawezekana, lakini hata iwe walikuwa na sababu gani, Waisraeli ‘walikataa kutii.’ (Mdo. 7:39-41) Paulo aliwahimiza Wakristo ‘wafanye yote wanayoweza’ ili ‘wasianguke katika kielelezo kilekile cha kutotii’ ambacho Waisraeli walionyesha walipoogopa kuingia katika Nchi ya Ahadi.—Ebr. 4:3, 11.

12. Yesu alijifunza utii jinsi gani, na alipata faida gani?

12 Ili tusonge mbele kuelekea ukomavu tunahitaji kufanya yote tunayoweza ili kumtii Yehova. Kielelezo cha Yesu Kristo kinaonyesha kwamba mara nyingi tunajifunza kutii kutokana na mateso yanayotupata. (Soma Waebrania 5:8, 9.) Kabla ya kuja duniani, Yesu alimtii Baba yake. Hata hivyo, aliteseka kimwili na kiakili alipokuwa akifanya mapenzi ya Baba yake duniani. Kwa kutii chini ya hali ngumu, Yesu ‘alifanywa kuwa mkamilifu’ kwa ajili ya cheo kipya ambacho Mungu alitaka kumpa, cheo cha kuwa Mfalme na Kuhani Mkuu.

13. Ni nini kinachoonyesha kwamba tumejifunza kutii?

13 Namna gani sisi? Je, tumeazimia kumtii Yehova hata tunapokabili matatizo yenye kufadhaisha? (Soma 1 Petro 1:6, 7.) Mungu ametoa mashauri ya wazi kuhusu maadili, unyoofu, kutumia ulimi kwa njia inayofaa, kusoma na kujifunza Maandiko kibinafsi, kuhudhuria mikutano ya Kikristo, na kushiriki katika kazi ya kuhubiri. (Yos. 1:8; Mt. 28:19, 20; Efe. 4:25, 28, 29; 5:3-5; Ebr. 10:24, 25) Je, tunamtii Yehova katika mambo hayo hata chini ya hali ngumu? Tunapotii tunaonyesha kwamba tumefanya maendeleo kuelekea ukomavu.

Kwa Nini Ukomavu wa Kikristo una Faida?

14. Toa mfano unaoonyesha jinsi kusonga mbele kuelekea ukomavu kunavyoweza kumlinda mtu.

14 Mkristo aliye na nguvu za ufahamu ambazo zimezoezwa vizuri kutofautisha yaliyo sawa na yasiyo sawa, analindwa kikweli katika ulimwengu ‘ambao umeishiwa na ufahamu wote wa maadili.’ (Efe. 4:19) Kwa mfano, ndugu mmoja anayeitwa James, ambaye alisoma kwa ukawaida vichapo vya Kimaandiko na kutafakari sana, alikubali kufanya kazi katika kampuni ambayo wafanyakazi wenzake wote walikuwa wanawake. James anasema hivi: “Ingawa wengi wao walikuwa na maadili mapotovu, mfanyakazi mmoja alionekana kuwa na maadili mazuri na alipendezwa na kweli ya Biblia. Hata hivyo, tulipokuwa peke yetu katika chumba kimoja kazini, alianza kunitongoza. Nilifikiri alikuwa akicheza tu lakini haikuwa rahisi kumzuia. Papo hapo nilikumbuka jambo lililosimuliwa katika Mnara wa Mlinzi kuhusu ndugu fulani aliyekabili kishawishi kama hicho kazini. Gazeti hilo lilitaja mfano wa Yosefu na mke wa Potifa. * Papo hapo nilimsukuma msichana huyo, akakimbia nje.” (Mwa. 39:7-12) James alishukuru kwamba jambo baya zaidi halikutukia na kwamba alidumisha dhamiri njema.—1 Tim. 1:5.

15. Kusonga mbele kuelekea ukomavu kunaimarisha jinsi gani moyo wetu wa mfano?

15 Ukomavu pia unaleta faida kwa sababu unaimarisha moyo wetu wa mfano na kutulinda ili ‘tusichukuliwe mbali na mafundisho mbalimbali na yaliyo mageni.’ (Soma Waebrania 13:9.) Tunapojitahidi kufanya maendeleo ya kiroho, akili yetu inakazia “mambo yaliyo ya maana zaidi.” (Flp. 1:9, 10) Hilo linatusaidia kumthamini Mungu zaidi na kuthamini mambo yote ambayo ametuandalia kwa faida yetu. (Rom. 3:24) Mkristo ambaye ni ‘mtu mzima katika nguvu za uelewaji’ anasitawisha uthamini mkubwa naye anakuwa na urafiki wa karibu pamoja na Yehova.—1 Kor. 14:20.

16. Ni nini kilichomsaidia dada mmoja kusitawisha ‘moyo ulio imara’?

16 Dada anayeitwa Louise alikiri kwamba kwa muda fulani baada ya kubatizwa, alitaka sana kuwapendeza wengine. Alisema hivi: “Sikuwa nikifanya jambo lolote baya, hata hivyo, nilipoteza hamu ya kumtumikia Yehova. Nilitambua kwamba nilihitaji kufanya mabadiliko fulani ili nimtumikie Yehova kwa uwezo wangu wote. Badiliko kubwa zaidi lilikuwa kumwabudu kwa moyo wangu wote.” Louise alipofanya jitihada hizo, alisitawisha ‘moyo ulio imara,’ ambao ulimsaidia sana kukabiliana na tatizo fulani la kiafya lenye kufadhaisha. (Yak. 5:8) Louise alisema, “Nilipambana sana, lakini nilimkaribia Yehova zaidi.”

‘Tii Kutoka Moyoni’

17. Kwa nini utii ulikuwa jambo la maana hasa katika karne ya kwanza?

17 Shauri la Paulo la ‘kusonga mbele kuelekea ukomavu’ liliokoa uhai wa Wakristo wa karne ya kwanza walioishi Yerusalemu na Yudea. Wale waliotii shauri hilo walikuwa na utambuzi mzuri sana wa kiroho uliohitajika ili kutambua ishara ambayo Yesu alikuwa amewapa ya ‘kuanza kukimbilia milimani.’ Walipoona “lile chukizo linalosababisha ukiwa . . . likiwa limesimama katika mahali patakatifu,” yaani, majeshi ya Roma yakizunguka na kuingia Yerusalemu, walijua kwamba ulikuwa wakati wa kukimbia. (Mt. 24:15, 16) Kulingana na mwanahistoria wa mambo ya dini, Eusebius, Wakristo walitii onyo la kinabii la Yesu, nao wakaondoka Yerusalemu kabla ya uharibifu na kwenda kuishi katika jiji la Pela lililokuwa katika eneo lenye milima la Gileadi. Hivyo, waliepuka msiba mbaya zaidi uliowahi kukumba Yerusalemu katika historia yote.

18, 19. (a) Kwa nini kutii ni jambo la maana siku zetu? (b) Habari inayofuata itazungumzia nini?

18 Utii unaotegemea kusonga mbele kuelekea ukomavu utatuokoa sisi pia tunapokabili utimizo mkubwa wa unabii wa Yesu wa kwamba ‘kutakuwa na dhiki kuu’ ambayo haijapata kutukia kamwe. (Mt. 24:21) Je, tutatii mwongozo wowote wa haraka ambao huenda tutapokea wakati ujao kutoka kwa “msimamizi-nyumba mwaminifu”? (Luka 12:42) Ni jambo la maana kama nini kwamba tujifunze ‘kutii kutoka moyoni’!—Rom. 6:17.

19 Ili tufikie ukomavu ni lazima tuzoeze nguvu zetu za ufahamu. Tunafanya hivyo kwa kujitahidi kulifahamu vizuri zaidi Neno la Mungu na kujifunza kutii. Vijana wanakabili matatizo ya pekee wanapokua kufikia ukomavu wa Kikristo. Habari inayofuata inazungumzia jinsi wanavyoweza kukabiliana na matatizo hayo kwa mafanikio.

[Maelezo ya chini]

^ fu. 7 Majina fulani yamebadilishwa.

^ fu. 14 Ona habari yenye kichwa “Tumeimarishwa Kukataa Kutenda Kosa,” katika toleo la Mnara wa Mlinzi la Oktoba 1, 1999 (1/10/1999).

Umejifunza Nini?

• Ukomavu wa kiroho unamaanisha nini, na tunaupata jinsi gani?

• Kulifahamu Neno la Mungu kunatusaidia jinsi gani kusonga mbele kufikia ukomavu?

• Tunajifunza utii kwa njia gani?

• Ukomavu unatuletea faida jinsi gani?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 10]

Kutumia mashauri ya Biblia kunatusaidia kukabiliana na matatizo kwa njia ya ukomavu

[Picha katika ukurasa wa 12, 13]

Kufuata mashauri ya Yesu kuliwaokoa Wakristo wa karne ya kwanza