Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Unapaswa Kuwa Wapi Mwisho Unapokuja?

Unapaswa Kuwa Wapi Mwisho Unapokuja?

Unapaswa Kuwa Wapi Mwisho Unapokuja?

YEHOVA atakapoleta mwisho wa mfumo huu mwovu wa mambo kwenye Har–Magedoni, ni nini kitakachotukia kwa watu wanyoofu? Andiko la Methali 2:21, 22 linajibu: “Wanyoofu ndio watakaokaa duniani, na wasio na lawama ndio watakaobaki ndani yake. Nao waovu, watakatiliwa mbali kutoka duniani; nao wenye hila, watang’olewa kutoka ndani yake.”

Lakini, watu wasio na lawama watabaki ndani ya dunia jinsi gani? Je, kutakuwa na mahali pa makimbilio kwa ajili yao? Wanyoofu wanapaswa kuwa wapi mwisho unapokuja? Masimulizi manne ya Biblia kuhusu watu waliookolewa yanatusaidia kuelewa habari hizo.

Walikuwa Mahali Panapofaa

Tunasoma hivi kwenye 2 Petro 2:5-7 kuhusu kuokolewa kwa wazee wa ukoo, Noa na Loti: “[Mungu] hakujizuia kuuadhibu ulimwengu wa kale, bali alimlinda Noa, mhubiri wa uadilifu, akiwa salama pamoja na wengine saba alipoleta gharika juu ya ulimwengu wa watu wasiomwogopa Mungu; na kwa kuyageuza majiji ya Sodoma na Gomora kuwa majivu aliyahukumia adhabu, akiweka kielelezo kwa watu wasiomwogopa Mungu juu ya mambo yatakayokuja; naye alimkomboa Loti mwadilifu, aliyetaabishwa sana na kule kujitia mno katika mwenendo mpotovu kwa watu wanaokaidi sheria.”

Noa aliokoka Gharika jinsi gani? Mungu alimwambia Noa hivi: “Mwisho wa wote wenye mwili umekuja mbele zangu, kwa maana dunia imejaa jeuri kwa sababu yao; na tazama mimi ninawaharibu pamoja na dunia. Jifanyie safina ya mti wenye utomvu.” (Mwa. 6:13, 14) Noa alijenga safina kama vile tu Yehova alivyomwagiza. Siku saba kabla ya Gharika kuanza, Yehova alimwagiza aingize wanyama ndani ya safina hiyo, kisha Noa angeingia ndani pamoja na washiriki wote wa familia yake. Siku ya saba, mlango ulifungwa, “na hiyo mvua kubwa juu ya dunia ikaendelea kwa siku 40, mchana na usiku.” (Mwa. 7:1-4, 11, 12, 16) Noa na familia yake “walichukuliwa salama kupitia maji.” (1 Pet. 3:20) Kuokolewa kwao kulitegemea wao kuwa ndani ya safina. Hakuna mahali pengine duniani ambapo pangekuwa salama.—Mwa. 7:19, 20.

Katika kisa cha Loti, maagizo yalikuwa tofauti kidogo. Malaika wawili walimjulisha Loti mahali ambapo hakupaswa kuwa. Malaika hao wawili walimwambia Loti hivi: ‘Wote walio wako katika jiji hili la Sodoma, watoe nje ya mahali hapa! Kwa maana sisi tutapaharibu mahali hapa.’ Walipaswa ‘kukimbilia eneo lenye milima.’—Mwa. 19:12, 13, 17.

Mambo ambayo Noa na Loti walijionea yanathibitisha kwamba “Yehova anajua jinsi ya kuwakomboa watu wenye ujitoaji-kimungu kutoka katika jaribu, lakini kuwaweka akiba watu wasio waadilifu kwa ajili ya ile siku ya hukumu.” (2 Pet. 2:9) Katika visa vyote viwili, waliokolewa ikitegemea mahali walipokuwa. Noa alipaswa kuingia ndani ya safina; Loti alipaswa kutoka nje ya Sodoma. Lakini je, inakuwa hivyo sikuzote? Je, Yehova anaweza kuwaokoa waadilifu mahali popote walipo, bila kuhitaji kuwahamisha? Ili kujibu swali hilo, ona masimulizi mengine mawili ya watu waliookolewa.

Je, Sikuzote Kuokoka Kunategemea Kuwa Mahali Fulani?

Kabla ya Yehova kuiharibu Misri kwa mapigo kumi katika siku za Musa, Aliwaagiza Waisraeli wapake damu ya mnyama wa Pasaka kwenye vizingiti na miimo ya nyumba zao. Kwa nini? Ili kwamba ‘wakati Yehova angepita katikati ili kuwaletea pigo Wamisri na kuiona damu kwenye sehemu ya juu ya mlango na kwenye ile miimo miwili ya mlango, Yehova angepita juu ya mlango, naye hangeruhusu uharibifu uingie ndani ya nyumba zao na kuwaletea pigo.’ Usiku huohuo, “Yehova akampiga kila mzaliwa wa kwanza katika nchi ya Misri, kuanzia mzaliwa wa kwanza wa Farao anayeketi juu ya kiti cha ufalme kufikia mzaliwa wa kwanza wa mateka aliye gerezani, na kila mzaliwa wa kwanza wa mnyama.” Wazaliwa wa kwanza wa Waisraeli waliokolewa bila kuhamia mahali pengine.—Kut. 12:22, 23, 29.

Pia, fikiria kisa cha Rahabu, kahaba aliyeishi katika jiji la Yeriko. Waisraeli walikuwa karibu kuanza vita vya kuimiliki Nchi ya Ahadi. Rahabu alipotambua kwamba jiji la Yeriko lingeharibiwa, aliwaambia wapelelezi wawili Waisraeli kwamba wakaaji wa jiji walikuwa wamevunjika moyo kwa kuwa waliogopa Waisraeli waliokuwa wakikaribia sana. Aliwaficha wapelelezi hao na kuwaomba wamwapie kuwa wangemlinda hai yeye na familia yake yote wakati ambapo jiji la Yeriko lingeharibiwa. Wapelelezi hao walimwagiza Rahabu akusanye pamoja watu wa familia yake ndani ya nyumba yake, iliyokuwa imejengwa kwenye ukuta wa jiji. Ikiwa wangetoka nje ya nyumba wangeharibiwa pamoja na watu wengine wa jiji hilo. (Yos. 2:8-13, 15, 18, 19) Hata hivyo, baadaye Yehova alimwambia Yoshua hivi: “Ukuta wa jiji utaanguka chini.” (Yos. 6:5) Sasa mahali ambapo wapelelezi walisema kuwa pangekuwa salama palionekana kuwa hatari. Rahabu na watu wa familia yake wangeokolewa jinsi gani?

Wakati ulipofika wa kuteka Yeriko, Waisraeli walipiga kelele nao wakaanza kupuliza pembe. Andiko la Yoshua 6:20 linasema hivi: “Ikawa kwamba mara tu watu [wa Israeli] walipoisikia sauti ya pembe na watu wakapaaza kelele kubwa za vita, ndipo ukuta ukaanza kuanguka chini kabisa.” Hakuna mwanadamu yeyote angeweza kuuzuia ukuta huo usianguke. Hata hivyo, kwa muujiza, ukuta wa jiji hilo haukuendelea kuanguka ulipofika kwenye nyumba ya Rahabu. Yoshua akawaamuru wale wapelelezi wawili: “Ingieni katika nyumba ya yule mwanamke, yule kahaba, mkamtoe nje mwanamke huyo na wote walio wake, kama vile mlivyomwapia.” (Yos. 6:22) Watu wote waliokuwa ndani ya nyumba ya Rahabu waliokolewa.

Kuokoka Kulitegemea Nini Hasa?

Tunaweza kujifunza nini kutokana na kuokoka kwa Noa, Loti, Rahabu, na Waisraeli katika siku za Musa? Masimulizi hayo yanatusaidia jinsi gani kujua ni wapi tunapopaswa kuwa mwisho wa mfumo huu mwovu wa mambo unapokuja?

Ni kweli kwamba, kuokoka kwa Noa kulitegemea kuwa ndani ya safina. Lakini kwa nini aliingia ndani ya safina? Ni kwa sababu alikuwa na imani na alikuwa mtiifu. Biblia inasema hivi: “Noa akafanya kulingana na yote ambayo Mungu alikuwa amemwamuru. Alifanya vivyo hivyo.” (Mwa. 6:22; Ebr. 11:7) Namna gani sisi? Je, tunafanya yote ambayo Mungu ametuamuru? Noa alikuwa pia “mhubiri wa uadilifu.” (2 Pet. 2:5) Kama Noa, je, sisi ni wenye bidii katika kazi ya kuhubiri, hata ikiwa watu wa eneo letu hawataki kutusikiliza?

Loti aliokoka uharibifu kwa kukimbia kutoka Sodoma. Aliokolewa kwa sababu alikuwa mwadilifu machoni pa Mungu na alitaabishwa sana na mwenendo mpotovu wa watu wa Sodoma na Gomora waliokaidi sheria. Je, kweli tunataabishwa na mwenendo mpotovu unaoenea leo? Au je, tumeuzoea sana hivi kwamba hautusumbui tena? Je, tunafanya yote tunayoweza ili tupatwe ‘bila doa na bila dosari na tukiwa katika amani’?—2 Pet. 3:14.

Kuokoka kwa Waisraeli huko Misri na Rahabu katika jiji la Yeriko, kulitegemea kubaki ndani ya nyumba zao. Hilo lilihitaji imani na utii. (Ebr. 11:28, 30, 31) Fikiria jinsi kila familia ya Waisraeli ilivyoendelea kumkazia macho mzaliwa wao wa kwanza ‘kilio kikubwa kilipoanza kutokea’ katika nyumba moja baada ya nyingine ya Wamisri. (Kut. 12:30) Fikiria jinsi Rahabu alivyojikunyata pamoja na familia yake aliposikia mngurumo wa kuta za Yeriko zilizokuwa zikianguka ukikaribia nyumba yake zaidi na zaidi. Alihitaji kuwa na imani sana ili kubaki mtiifu na kukaa ndani ya nyumba hiyo.

Hivi karibuni mwisho utakuja juu ya ulimwengu huu mwovu wa Shetani. Bado hatujui jinsi Yehova atakavyowalinda watu wake katika ‘siku ya hasira yake’ yenye kuogopesha sana. (Sef. 2:3) Hata hivyo, haidhuru tutakuwa mahali gani au tutakuwa katika hali gani, tunaweza kuwa na hakika kwamba kuokoka kwetu kutategemea imani yetu katika Yehova na utii wetu kumwelekea. Wakati huohuo, tunapaswa kusitawisha mtazamo unaofaa kuelekea kile ambacho unabii wa Isaya unataja kuwa ‘vyumba vyetu vya ndani.’

“Ingia Katika Vyumba Vyako vya Ndani”

Andiko la Isaya 26:20 linasema hivi: “Nendeni, watu wangu, ingia katika vyumba vyako vya ndani, na ufunge milango nyuma yako. Jifiche kwa kitambo kidogo mpaka hukumu itakapopita.” Huenda unabii huo ulitimia kwa mara ya kwanza mwaka wa 539 K.W.K. Wamedi na Waajemi waliposhinda Babiloni. Baada ya kuingia Babiloni, inaonekana kwamba Koreshi yule Mwajemi aliamuru kila mtu abaki ndani ya nyumba kwa sababu askari-jeshi wake waliamuriwa kumuua mtu yeyote aliyepatikana nje.

Katika siku zetu, ‘vyumba vya ndani’ vinavyotajwa katika unabii huo vinaweza kuhusianishwa kwa ukaribu sana na makutaniko zaidi ya 100,000 ya Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote. Makutaniko hayo yanatimiza daraka la maana sana katika maisha yetu. Yataendelea kutimiza daraka hilo wakati wa “ile dhiki kuu.” (Ufu. 7:14) Watu wa Mungu wanaamuriwa waingie katika ‘vyumba vyao vya ndani’ na kujificha “mpaka hukumu itakapopita.” Ni jambo la maana kusitawisha na kudumisha mtazamo mzuri kuelekea kutaniko na kuazimia kabisa kuendelea kushirikiana nalo kwa ukaribu sana. Tunapaswa kutilia maanani himizo hili la Paulo: ‘Acheni tufikiriane ili kuchocheana katika upendo na matendo mazuri, bila kuacha kukusanyika pamoja sisi wenyewe, kama vile wengine walivyo na desturi, bali tutiane moyo, na kufanya hivyo zaidi kwa kadiri tunavyoona siku ile kuwa inakaribia.’—Ebr. 10:24, 25.

[Picha katika ukurasa wa 7]

Tunaweza kujifunza nini kutokana na matendo ya Mungu ya kale ya kuokoa?

[Picha katika ukurasa wa 8]

Huenda ‘vyumba vya ndani’ vikahusianishwa na nini katika siku zetu?