Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi ya Kupata Shangwe Kutokana na Zawadi ya Useja

Jinsi ya Kupata Shangwe Kutokana na Zawadi ya Useja

Jinsi ya Kupata Shangwe Kutokana na Zawadi ya Useja

“WAKAFUNGA ndoa, kisha wakaishi raha mustarehe.” Hadithi nyingi za watoto zinamalizia kwa maneno kama hayo. Sinema na vitabu vya mapenzi mara nyingi vinakazia ujumbe huohuo wa kwamba huwezi kupata furaha usipofunga ndoa! Zaidi ya hayo, tamaduni nyingi zinawashinikiza sana vijana wafunge ndoa. Debby alisema hivi alipokuwa na umri wa miaka 20 na kitu: “Watu wanakufanya uhisi kwamba mradi wa pekee wa msichana ni kuolewa. Wanaeneza wazo la kwamba maisha yanaanza baada ya kufunga ndoa.”

Mtu wa kiroho haoni mambo kwa njia hiyo isiyo na usawaziko. Ingawa ndoa ilikuwa jambo la kawaida katika maisha ya Waisraeli, Biblia inawataja wanaume na wanawake waseja ambao waliishi maisha yenye kuthawabisha sana. Leo, Wakristo fulani wanachagua maisha ya useja, na wengine wengi wanabaki waseja kwa sababu ya hali. Hata wawe na sababu gani za kubaki waseja, swali la maana ni hili: Mkristo anaweza kufanya nini ili afanikiwe akiwa mseja?

Yesu mwenyewe hakufunga ndoa, na tunaelewa wazi ni kwa sababu ya mgawo aliopewa. Aliwaambia wanafunzi wake kwamba wengine kati ya wafuasi wake pia ‘wangeupa nafasi’ useja. (Mt. 19:10-12) Hivyo, Yesu alionyesha kwamba ili tuwe na maisha ya useja yenye mafanikio, ni lazima tukubali, au kuipa nafasi njia hii ya maisha katika akili na moyo wetu.

Je, shauri la Yesu linamhusu tu yule ambaye ameamua kimakusudi kubaki mseja maishani ili akazie fikira zake zote migawo ya kitheokrasi? (1 Kor. 7:34, 35) Si lazima. Fikiria hali ya Mkristo ambaye angependa kufunga ndoa lakini kwa sasa hajapata mwenzi anayefaa. Dada mseja mwenye umri wa miaka 30 na kitu anayeitwa Ana alisema: “Hivi karibuni, mfanyakazi mwenzangu ambaye si Shahidi aliniomba nifunge ndoa naye, jambo ambalo sikutazamia. Kwa kadiri fulani nilivutiwa naye, lakini niliondoa haraka hisia hizo kwa sababu ninataka tu kufunga ndoa na mtu ambaye atanisaidia nimkaribie Yehova zaidi.”

Tamaa ya kuolewa “katika Bwana tu” inawasaidia dada wengi kama Ana kuepuka kuolewa na mtu asiye mwamini. * (1 Kor. 7:39; 2 Kor. 6:14) Kwa sababu wanaheshimu shauri la Mungu, wanaupa nafasi useja, angalau kwa wakati huu. Wanaweza kufanya nini ili wafanikiwe?

Jifunze Kuwa na Mtazamo Mzuri

Mtazamo wetu unaweza kutusaidia sana kukubali hali yoyote, hata ikiwa si hali tunayofurahia. Carmen, dada mseja mwenye umri wa miaka 40 hivi anasema: “Ninafurahia hali yangu jinsi ilivyo, sioti ndoto kuhusu mambo nisiyokuwa nayo.” Ni kweli kwamba nyakati nyingine tunahisi upweke au tunavunjika moyo. Lakini kukumbuka kwamba wengine wengi katika ushirika mzima wa ndugu zetu ulimwenguni wanakabili hali kama hizo kunaweza kututia moyo kuendelea mbele tukiwa na uhakika. Yehova amewasaidia wengi kuupa nafasi useja na kukabiliana na magumu mengine.—1 Pet. 5:9, 10.

Ndugu na dada wengi Wakristo wametambua kwamba useja una faida zake. Ester, dada mseja mwenye umri wa miaka 30 na kitu anasema hivi: “Ninafikiri siri ya kupata furaha ni kukazia fikira mambo mazuri katika hali yoyote unayokabili.” Carmen anaongezea hivi: “Ninaamini kwamba hata nikiolewa au nisipoolewa, nikitanguliza mambo ya Ufalme, Yehova hataninyima jambo lolote jema.” (Zab. 84:11) “Huenda maisha yangu hayako kama vile nilivyopanga, lakini nina furaha na nitaendelea kuwa na furaha.”

Mifano ya Waseja Katika Biblia

Binti ya Yeftha hakuwa amepanga kubaki mseja. Lakini nadhiri ya baba yake ilimlazimisha kutumikia patakatifu tangu akiwa kijana na kuendelea. Mgawo huo ambao hakutazamia bila shaka ulibadili mipango aliyokuwa nayo na ulikuwa kinyume cha hisia zake za asili. Aliomboleza kwa miezi miwili alipotambua kwamba hangeolewa na kuwa na familia. Hata hivyo, alikubali hali yake mpya na akatumika kwa moyo wote katika maisha yake yote. Wanawake wengine Waisraeli walimpongeza kila mwaka kwa sababu ya roho yake ya kujidhabihu.—Amu. 11:36-40.

Watu fulani waliokuwa matowashi kimwili wakati wa Isaya huenda walivunjika moyo kwa sababu ya hali yao. Biblia haisemi ni nini kilichowafanya wawe matowashi. Kwa hiyo, hawangeweza kuwa washiriki kamili wa kutaniko la Israeli, wala hawangeweza kuoa na kupata watoto. (Kum. 23:1) Hata hivyo, Yehova alielewa hisia zao, na aliwapongeza kwa sababu walitii agano lake kwa nafsi yote. Aliwaambia kwamba angewapa “ukumbusho” na “jina mpaka wakati usio na kipimo” katika nyumba yake. Yaani, matowashi hao waaminifu wangekuwa na tumaini hakika la kufurahia uzima wa milele chini ya utawala wa Kimasihi wa Yesu. Yehova hangewasahau kamwe.—Isa. 56:3-5.

Hali za Yeremia zilikuwa tofauti sana. Baada ya Mungu kumpa Yeremia mgawo wa kuwa nabii, alimwagiza abaki mseja kwa sababu aliishi katika nyakati ngumu na pia kwa sababu ya mgawo wake. Yehova alimwambia hivi: “Usijichukulie mke, wala usiwe na wana na mabinti mahali hapa.” (Yer. 16:1-4) Biblia haifunui jinsi Yeremia alivyohisi kuhusu maagizo hayo, hata hivyo, inatuhakikishia kwamba alikuwa mtu aliyependezwa na neno la Yehova. (Yer. 15:16) Katika miaka iliyofuata, Yeremia alipovumilia hali mbaya sana ya kuzingirwa kwa Yerusalemu kwa miezi 18, bila shaka aliona hekima ya kutii amri ya Yehova ya kubaki mseja.—Omb. 4:4, 10.

Jinsi ya Kufanikisha Maisha Yako

Watu hao wanaotajwa katika Biblia walikuwa waseja, lakini walitegemezwa na Yehova na wakamtumikia kikamili. Vivyo hivyo leo, tunaweza kufanikisha sana maisha yetu kwa kushiriki katika utendaji wenye maana. Biblia ilitabiri kwamba wanawake wanaotangaza habari njema wangekuwa jeshi kubwa. (Zab. 68:11) Maelfu ya dada waseja wako miongoni mwa umati huo. Huduma yao imezaa matunda, na wengi wao wamebarikiwa kuwa na wana na mabinti wa kiroho.—Marko 10:29, 30; 1 The. 2:7, 8.

Loli ambaye ametumikia akiwa painia kwa miaka 14 anasema hivi: “Upainia unanisaidia kuwa na kusudi maishani. Nikiwa dada mseja, ninatumika kwa bidii na nina shughuli nyingi maishani. Na hilo linanisaidia kuepuka upweke. Mwishoni mwa siku ninahisi nimetosheka kwa sababu ninaweza kuona kwamba huduma yangu inawasaidia sana watu. Hilo linaniletea shangwe nyingi sana.”

Dada wengi wamejifunza lugha mpya, na wamepanua huduma yao kwa kuwahubiria watu wanaozungumza lugha za kigeni. Ana, aliyetajwa mwanzoni anasema hivi: “Katika mji ambamo ninaishi, kuna maelfu ya wageni.” Anafurahia kuwahubiria watu wanaozungumza Kifaransa. “Kujifunza lugha ambayo ninaweza kuitumia kuzungumza na wengi wao kumenifungulia njia ya kutumika katika eneo jipya na hilo limefanya kazi yangu ya kuhubiri ipendeze sana.”

Kwa kuwa mara nyingi waseja hawana madaraka mengi, wengine wao wamejitolea kutumika katika maeneo yenye uhitaji mkubwa zaidi wa wahubiri. Lidiana, dada mseja mwenye umri wa miaka 30 na kitu, ambaye ametumikia katika nchi zenye uhitaji mkubwa zaidi anasema: “Ninaamini kabisa kwamba kadiri unavyofanya mengi zaidi katika utumishi wa Yehova, ndivyo inavyokuwa rahisi zaidi kupata marafiki wa karibu na kuhisi unapendwa. Nimepata marafiki wengi wa karibu kutoka katika nchi na malezi mbalimbali, na marafiki hao wamefanikisha sana maisha yangu.”

Biblia inamtaja Filipo, yule mweneza-injili aliyekuwa na binti wanne waseja ambao walitoa unabii. (Mdo. 21:8, 9) Inaonekana walikuwa na bidii katika utumishi kama baba yao. Je, inawezekana kwamba walitumia zawadi yao ya kutoa unabii kwa faida ya Wakristo wenzao huko Kaisaria? (1 Kor. 14:1, 3) Leo, dada wengi waseja wanawajenga wengine vivyo hivyo kwa kuhudhuria mikutano ya Kikristo kwa ukawaida na kushiriki.

Naye Lidia, alikuwa Mkristo wa mapema huko Filipi na Biblia inamsifu kwa sababu ya ukarimu wake. (Mdo. 16:14, 15, 40) Lidia, ambaye huenda alikuwa mseja au mjane, alikuwa mkarimu sana, na kwa sababu ya ukarimu wake alipata thawabu kwa kushirikiana na waangalizi waliosafiri, kama Paulo, Sila, na Luka. Kuonyesha roho kama hiyo ya ukarimu leo kunaleta baraka pia.

Kutosheleza Uhitaji wa Kupendwa

Zaidi ya kutumia maisha yetu katika utendaji wa maana, sote tuna uhitaji wa kupendwa na kuonyeshwa urafiki. Waseja wanaweza kutosheleza uhitaji huo jinsi gani? Kwanza, Yehova yuko tayari sikuzote kutupenda, kututia nguvu, na kutusikiliza. Nyakati nyingine, Mfalme Daudi alihisi akiwa ‘peke yake na mwenye kuteseka,’ hata hivyo, alijua kwamba wakati wowote angeweza kumwomba Yehova amtegemeze. (Zab. 25:16; 55:22) Aliandika hivi: “Hata ikiwa baba yangu na mama yangu wangeniacha, Yehova mwenyewe angenichukua.” (Zab. 27:10) Mungu anawakaribisha watumishi wake wote wamkaribie, wawe marafiki wake wa karibu.—Zab. 25:14; Yak. 2:23; 4:8.

Zaidi ya hilo, katika undugu wetu wa ulimwenguni pote, tunaweza kupata baba, mama, ndugu, na akina dada wa kiroho ambao watatupenda na kufanikisha maisha yetu. (Mt. 19:29; 1 Pet. 2:17) Wakristo wengi waseja wanaridhika sana wanapofuata mfano wa Dorkasi, ambaye “alizidi katika matendo mema na zawadi za rehema.” (Mdo. 9:36, 39) Loli anasema hivi: “Popote ninapoenda, ninatafuta marafiki wa kweli kutanikoni ambao watanipenda na kunitegemeza ninaposhuka moyo. Ili kuimarisha urafiki huo, ninajitahidi kupendezwa na wengine na kuwaonyesha upendo. Nimetumikia katika makutaniko manane, na sikuzote nimepata marafiki wa kweli. Mara nyingi si dada wa umri wangu, nyakati nyingine ni mama waliozeeka au matineja.” Katika kila kutaniko, kuna wale wanaohitaji kupendwa na kuonyeshwa urafiki. Kupendezwa kikweli na watu hao kunaweza kuwasaidia sana na kutosheleza tamaa yetu ya kuwapenda wengine na kupendwa.—Luka 6:38.

Mungu Hatasahau

Biblia inaonyesha kwamba ni lazima Wakristo wote wajidhabihu kwa njia fulani kwa sababu ya nyakati ngumu ambamo tunaishi. (1 Kor. 7:29-31) Wale walio waseja kwa sababu wameazimia kutii amri ya Mungu ya kuoa au kuolewa katika Bwana tu bila shaka wanastahili kuthaminiwa na kuheshimiwa kwa njia ya pekee. (Mt. 19:12) Hata hivyo, haimaanishi kwamba hawawezi kuwa na maisha yenye furaha kwelikweli kwa sababu ya dhabihu yao inayostahili pongezi.

Lidiana anasema: “Ninaishi maisha yenye kuridhisha ambayo yanategemea utumishi wangu na uhusiano wangu pamoja na Yehova. Ninajua watu waliofunga ndoa ambao wana furaha na wengine ambao hawana furaha. Jambo hilo hakika linanisadikisha kwamba furaha yangu haitegemei kuolewa au kutoolewa wakati ujao.” Kama Yesu alivyosema, furaha inategemea hasa kutoa na kutumikia, mambo ambayo Wakristo wote wanaweza kufanya.—Yoh. 13:14-17; Mdo. 20:35.

Bila shaka, jambo linalotuletea shangwe kubwa zaidi ni kujua kwamba Yehova atatubariki kwa sababu ya dhabihu yoyote ile ambayo tunatoa ili tufanye mapenzi yake. Biblia inatuhakikishia hivi: “Mungu hakosi kuwa mwadilifu hivi kwamba asahau kazi yenu na upendo mlioonyesha kwa ajili ya jina lake.”—Ebr. 6:10.

[Maelezo ya chini]

^ fu. 6 Ingawa katika habari hii tunawataja dada Wakristo, kanuni zinazotajwa zinawahusu pia akina ndugu.

[Blabu katika ukurasa wa 25]

“Ninafurahia hali yangu jinsi ilivyo, sioti ndoto kuhusu mambo nisiyokuwa nayo.”—Carmen

[Picha katika ukurasa wa 26]

Loli na Lidiana wanafurahia kutumika katika maeneo yenye uhitaji mkubwa zaidi

[Picha katika ukurasa wa 27]

Mungu anawakaribisha watumishi wake wote wamkaribie