Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kushirikiana Kunachangia Maendeleo ya Kiroho

Kushirikiana Kunachangia Maendeleo ya Kiroho

Kushirikiana Kunachangia Maendeleo ya Kiroho

ROHO ya kushirikiana ni ya maana kwa wale wanaotaka kufanya maendeleo katika kuwa na familia inayothamini mambo ya kiroho. Yehova alipowaumba wenzi wa ndoa wawili wa kwanza, alikazia uhitaji wa kushirikiana. Hawa alipaswa kushirikiana na Adamu akiwa “kikamilisho” chake. (Mwa. 2:18) Ndoa inapaswa kuwa muungano ambamo mwanamume na mwanamke wanasaidiana. (Mhu. 4:9-12) Ili kutimiza wajibu ambao Yehova amewapa wazazi na watoto ni lazima pia familia ishirikiane.

Ibada ya Familia

Barry na Heidi wana watoto watano. Wametambua kwamba kushirikiana katika kufanya funzo la Biblia la familia kunawasaidia kufanya maendeleo. Barry anaeleza hivi: “Kabla ya funzo la familia, mara kwa mara ninawapa watoto migawo fulani midogo. Ninaweza kuwaomba watayarishe maelezo yanayotegemea habari zilizo katika Amkeni! Pia, sisi huwa na vipindi vya kufanya mazoezi kuhusu mambo ambayo tutasema katika utumishi wa shambani ili kila mtoto awe na utangulizi fulani.” Heidi anaongezea hivi: “Sote tuna orodha ya miradi ya kiroho ambayo tunataka kutimiza, na tukiwa familia tunaipitia miradi hiyo pindi kwa pindi wakati wa funzo la familia ili kuona maendeleo ambayo tunafanya.” Vilevile wenzi hao wa ndoa wametambua kwamba wanapotenga jioni fulani za kutotazama televisheni, familia nzima inapata nafasi ya kusoma kwa utulivu.

Mikutano ya Kutaniko

Mike na Denise walifanikiwa kulea watoto wanne. Familia yao ilifaidika jinsi gani kwa kushirikiana? Mike anasema hivi: “Nyakati nyingine, tulishindwa kufika mikutanoni kwa wakati ingawa tulikuwa tumefanya mipango mizuri. Hata hivyo, tulitambua kwamba tuliposhirikiana tulifaulu kufika mikutanoni kwa wakati.” Denise anaeleza hivi: “Watoto wetu walipokuwa wakikua, kila mtoto alikuwa na kazi za nyumbani za kufanya. Binti yetu Kim, alisaidia katika kazi ya upishi na kutayarisha meza kabla ya mlo.” Michael, mwana wao anakumbuka hivi: “Kila Jumanne (Siku ya 2) jioni tulikuwa na mkutano wa kutaniko nyumbani mwetu. Kwa hiyo, tulisafisha chumba na kupanga viti.” Matthew, mwana wao mwingine, anaongezea hivi: “Jioni tulizokuwa na mkutano, Baba alihakikisha kwamba amerudi nyumbani mapema kutoka kazini ili atusaidie kujitayarisha kwa ajili ya mkutano.” Wamepata matokeo gani?

Jitihada Zote za Kushirikiana Si za Bure

Mike anasimulia hivi: “Mwaka wa 1987, mimi na Denise tulianza kufanya upainia. Wakati huo, watatu kati ya watoto wetu walikuwa bado wanaishi nyumbani. Wawili kati yao pia walianza kufanya upainia na wengine wameshiriki katika miradi ya kujenga Betheli. Shangwe nyingine ambayo tumepata tukiwa familia ni kwamba tumewasaidia watu 40 kufikia hatua ya kujiweka wakfu na kubatizwa. Pia, tumepata pendeleo la kushiriki katika miradi ya ujenzi tukiwa familia, hata katika nchi nyingine.”

Kwa kweli, jitihada zote za kushirikiana katika familia si za bure. Je, mnaweza kufikiria njia nyingine ambazo mnaweza kushirikiana katika familia yenu? Mnaweza kuwa na hakika kwamba kuonyesha roho ya kushirikiana kutaisaidia familia yenu ifanye maendeleo zaidi ya kiroho.

[Picha katika ukurasa wa 28]

Vipindi vya kufanya mazoezi vinasaidia familia kufanya maendeleo katika utumishi wa shambani