Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kupata Hazina Zilizofichwa

Kupata Hazina Zilizofichwa

Kupata Hazina Zilizofichwa

JE, UMEWAHI kupata hazina iliyofichwa mahali ambapo hukutarajia kuipata? Ndivyo ilivyokuwa Machi 27, 2005 (27/3/2005), kwa Ivo Laud, Shahidi wa Yehova anayeishi huko Estonia. Alikuwa akimsaidia Alma Vardja, Shahidi mwenzake aliyezeeka, kubomoa banda fulani lililokuwa limezeeka. Walipokuwa wakiondoa ukuta wa nje, waliona ubao uliokuwa umefunika upande mmoja wa nguzo. Baada ya kuuondoa ubao huo, waliona shimo lenye upana wa karibu sentimita 10, urefu wa mita 1.2, na kina cha sentimita 10. Shimo hilo lilikuwa limefunikwa na ubao uliopakwa rangi ya nguzo hiyo. (1) Kulikuwa na hazina zilizofichwa ndani ya shimo hilo! Ni hazina gani hizo? Ni nani aliyezificha humo?

Katika shimo hilo, walipata vifurushi vilivyokuwa vimefunikwa kabisa na karatasi ngumu. (2) Vifurushi hivyo vilikuwa na vichapo vya Mashahidi wa Yehova, hasa makala za funzo za Mnara wa Mlinzi, kutia ndani makala fulani za mwaka wa 1947. (3) Zilikuwa zimeandikwa kwa mkono kwa uangalifu katika Kiestonia. Vifurushi fulani vilikuwa na maelezo ya siri kuhusu ni nani aliyekuwa amevificha vichapo hivyo. Maelezo hayo yalikuwa ni rekodi za kuhojiwa kwa Villem Vardja, mume wa Alma. Pia, walipata habari kuhusu miaka aliyokuwa amefungwa gerezani. Kwa nini alifungwa?

Villem Vardja alitumika akiwa Shahidi mwenye madaraka katika Kutaniko la Tartu na baadaye katika Kutaniko la Otepää huko Estonia, nchi ambayo ilikuwa sehemu ya Jamhuri za Kisoshalisti za Sovieti. Inaelekea kwamba alijifunza kweli ya Biblia muda fulani kabla ya Vita vya Pili vya Ulimwengu. Miaka michache baadaye, mnamo Desemba 24, 1948 (24/12/1948), utawala wa Kikomunisti uliamuru Ndugu Vardja akamatwe kwa sababu ya kujihusisha na shughuli za kidini. Alihojiwa na kuteswa na polisi wa siri walipokuwa wakijaribu kumlazimisha awape majina ya waamini wenzake. Baada ya kunyimwa nafasi ya kujitetea katika mahakama, alihukumiwa kifungo cha miaka kumi katika kambi za magereza za Urusi.

Villem Vardja aliendelea kuwa mwaminifu kwa Yehova hadi alipokufa Machi 6, 1990. Mke wake hakujua kwamba bado kulikuwa na vichapo vilivyokuwa vimefichwa. Inaelekea kwamba mume wake hakumwambia kuhusu vichapo hivyo ili amlinde iwapo angehojiwa na polisi. Kwa nini mume wake alivificha vichapo hivyo? Alifanya hivyo kwa sababu mara nyingi askari wa Shirika la Usalama wa Kitaifa la Sovieti (KGB), walipekua kwa ghafula nyumba za Mashahidi wa Yehova, wakitafuta vichapo vya kidini. Huenda Ndugu Vardja alificha vichapo hivyo ili kuhakikisha kwamba waamini wenzake wangeendelea kupata chakula cha kiroho ikiwa askari wa KGB wangechukua vichapo vingine vyote. Mahali pengine ambapo vichapo vilikuwa vimefichwa palipatikana hapo mbeleni, wakati wa kiangazi mwaka wa 1990. Kwa mfano, vichapo vilifichwa huko Tartu, eneo lililo kusini mwa Estonia. Vichapo hivyo vilevile vilikuwa vimefichwa na Villem Vardja.

Kwa nini tunaviita vichapo hivyo hazina? Kwa sababu vichapo hivyo vilivyokuwa vimeandikwa kwa mkono na kufichwa kwa uangalifu vinaonyesha waziwazi jinsi Mashahidi walivyothamini sana chakula cha kiroho ambacho kilipatikana wakati huo. (Mt. 24:45) Je, unathamini chakula cha kiroho ambacho unaweza kupata sasa katika eneo lenu? Kati ya chakula hicho cha kiroho ni Mnara wa Mlinzi katika Kiestonia na lugha nyingine zaidi ya 170.