Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

‘Yehova Ameufanya Uso Wake Ung’ae Kuwaelekea’

‘Yehova Ameufanya Uso Wake Ung’ae Kuwaelekea’

‘Yehova Ameufanya Uso Wake Ung’ae Kuwaelekea’

USO wa mwanadamu una misuli zaidi ya 30. Ili utabasamu tu, unahitaji kutumia misuli 14! Hebu wazia jinsi ambavyo mazungumzo yangekuwa bila misuli hiyo. Je, yangevutia? Hapana. Zaidi ya kufanya mazungumzo yavutie, misuli ya uso inawasaidia viziwi kwa njia nyingine. Misuli hiyo inapotumiwa kutoa ishara za mwili, inasaidia sana kuonyesha mawazo na fikira. Watu wengi wameshangaa sana kuona jinsi lugha ya ishara inavyoweza kuonyesha hata mawazo magumu pamoja na tofauti ndogo-ndogo katika maana ya maneno.

Hivi karibuni, viziwi ulimwenguni pote wameuona uso ambao unaonyesha hisia na mawazo mbalimbali kuliko uso wa mwanadamu yeyote yule. Wameuona “uso wa Yehova” kwa njia ya mfano. (Omb. 2:19) Hilo halikutokea kimuujiza. Kwa muda mrefu Yehova amewaonyesha viziwi upendo mkubwa. Alifanya hivyo hata zamani katika taifa la kale la Israeli. (Law. 19:14) Leo pia, upendo wake kwa viziwi umeonekana wazi kabisa. “Mapenzi [ya Mungu] ni kwamba watu wa namna zote waokolewe na kupata ujuzi sahihi wa kweli.” (1 Tim. 2:4) Kwa kupata ujuzi sahihi wa kweli kumhusu Mungu, ni kana kwamba viziwi wengi wamepata kuuona uso wake. Wamepata ujuzi huo jinsi gani ingawa hawawezi kusikia? Kabla ya kujibu swali hilo, acheni tuone kwa nini lugha ya ishara ni ya maana kwa viziwi.

Kuona Ni Kusikia

Kuna maoni mengi yasiyo ya kweli kuhusu viziwi na lugha ya ishara. Acheni turekebishe baadhi ya maoni hayo yasiyo ya kweli. Viziwi wanaweza kuendesha magari. Ni vigumu sana kwao kusoma midomo. Lugha ya ishara haihusiani hata kidogo na maandishi ya vipofu, wala si kuigiza tu. Kuna lugha nyingi za ishara ulimwenguni pote. Zaidi ya hayo, viziwi kutoka sehemu mbalimbali wanatumia ishara zinazotofautiana.

Je, viziwi wanaweza kusoma? Ingawa wengine wanasoma vizuri, ukweli ni kwamba wengi wao wana matatizo ya kusoma. Kwa nini? Kwa sababu maneno yanayoandikwa yanategemea lugha inayozungumzwa. Fikiria jinsi mtoto aliye na uwezo wa kusikia anavyojifunza lugha. Kuanzia wakati anapozaliwa, anazungukwa na watu wanaozungumza lugha fulani. Baada ya muda mfupi, anaweza kuunganisha maneno na kuunda sentensi. Hilo linatukia kiasili tu kwa kusikia lugha hiyo ikizungumzwa. Hivyo, unaposikia watoto wakijifunza kusoma, utagundua kwamba wamejifunza kupatanisha maneno yaliyoandikwa, pamoja na sauti na maneno ambayo tayari wanajua.

Sasa jiwazie ukiwa katika nchi ya kigeni ndani ya chumba cha vioo ambamo huwezi kusikia sauti yoyote. Hujawahi kamwe kusikia lugha ya nchi hiyo ikizungumzwa. Kila siku, watu wa nchi hiyo wanakuja na kujaribu kuzungumza na wewe wakiwa nje ya chumba hicho cha vioo. Huwezi kusikia wanachosema. Unaona tu wakifumbua-fumbua midomo yao. Wanapotambua kwamba huwaelewi, wanaandika kwenye karatasi maneno wanayosema na kukuonyesha kwenye kioo. Wanafikiri kwamba utaelewa maandishi hayo. Je, unafikiri unaweza kuyaelewa? Utagundua kwamba si rahisi kuwasiliana nao katika hali hiyo. Kwa nini? Kwa sababu maneno wanayoandika ni ya lugha ambayo hujawahi kamwe kuisikia ikizungumzwa. Viziwi wengi wanakabili hali kama hiyo.

Lugha ya ishara ni njia bora kabisa inayowasaidia viziwi kuwasiliana. Mtu anatumia ishara za mwili ili kuonyesha mawazo fulani. Ishara anazoonyesha pamoja na ishara za uso zinafuata sheria za lugha ya ishara. Kwa kufanya hivyo, mtu anaweza kutoa ujumbe akitumia lugha ya ishara.

Kwa kweli, karibu kila ishara ambayo kiziwi anatoa kwa mikono, mwili, na uso wake anapotumia lugha ya ishara ina maana. Ishara za uso hazitolewi ili kuwavutia tu watu. Ishara za uso ni sehemu muhimu ya sheria za lugha ya ishara. Kwa mfano: Kuuliza swali ukiwa umeinua nyusi za macho kunaweza kuonyesha kwamba unauliza swali la kumsaidia kufikiri au swali ambalo linahitaji jibu la ndiyo au hapana. Ikiwa nyusi zimeshuka, huenda unauliza ni nani, ni nini, ni wapi, kwa nini, au namna gani. Ishara fulani za mdomo zinaweza kuonyesha ukubwa wa kifaa fulani au ukubwa wa tendo fulani. Jinsi kiziwi anavyotikisa kichwa chake, kuinua mabega yake, kufanya ishara kwa mashavu, na kupepesa macho yake kunakazia maana kamili ya mawazo yanayotolewa.

Ishara hizo zote zinamsaidia mtazamaji kuelewa habari kwa njia yenye kufurahisha. Kwa kutumia njia hiyo bora ya kuwasiliana, viziwi ambao wanajua vizuri lugha ya ishara wanaweza kutoa wazo lolote, iwe ni wazo la kishairi au wazo gumu, mawazo ya kimapenzi au ya kuchekesha, mambo yanayoonekana au yasiyoonekana.

Vichapo vya Lugha ya Ishara Vina Faida

Ujuzi kumhusu Yehova unapotolewa kwa lugha ya ishara, ni kana kwamba kiziwi anasikia ujumbe huo na ‘kumwamini’ Mwanzilishi wa ujumbe huo. Hivyo, Mashahidi wa Yehova wamejitahidi sana kuwahubiria viziwi ulimwenguni pote na kutayarisha vifaa vya kuwasaidia. (Rom. 10:14) Kwa sasa, kuna vikundi 58 vya kutafsiri lugha ya ishara ulimwenguni pote, na vichapo vya lugha ya ishara vinapatikana kwenye DVD katika lugha 40 za ishara. Je, kazi hiyo yote imekuwa na matokeo yoyote mazuri?

Jeremy, ambaye wazazi wake wote ni viziwi, anasema hivi: “Ninakumbuka jinsi baba yangu alivyotumia saa nyingi akisoma na kujaribu kuelewa mafungu machache tu ya makala ya Mnara wa Mlinzi katika chumba chake cha kulala. Kwa ghafula, alitoka katika chumba chake na kusema hivi kwa msisimuko kwa lugha ya ishara: ‘Nimeelewa! Nimeelewa!’ Kisha alianza kunieleza maana ya mafungu aliyosoma. Wakati huo nilikuwa na umri wa miaka 12 tu. Niliyatazama kwa haraka mafungu hayo na kumwambia hivi kwa lugha ya ishara: ‘Baba, sidhani hiyo ndiyo maana. Yanamaanisha . . .’ Aliniambia kwa ishara niache kumweleza, kisha alirudi katika chumba chake ili kujaribu kuelewa maana ya mafungu hayo. Sitasahau kamwe jinsi alivyoonekana amekata tamaa na jinsi nilivyoguswa moyo nilipomtazama akirudi katika chumba chake cha kulala. Hata hivyo, sasa anaweza kuelewa habari hizo vizuri zaidi kwa sababu ana vichapo vya lugha ya ishara kwenye DVD. Ninafurahi sana kuona uso wake uking’aa anapoeleza jinsi anavyohisi kumhusu Yehova.”

Fikiria kisa cha wenzi fulani wa ndoa Mashahidi ambao walizungumza na Jessenia, mwanamke fulani kijana aliye kiziwi huko Chile. Baada ya kuruhusiwa na mama yake kumwonyesha Jessenia My Book of Bible StoriesOn DVD katika Lugha ya Ishara ya Chile, walisema hivi: “Jessenia alipoanza kutazama hadithi hizo, alianza kucheka kisha akatokwa na machozi. Mama yake alipomuuliza kwa nini analia, alimjibu kwamba ni kwa sababu alifurahia sana mambo aliyokuwa akitazama. Ndipo mama yake alipotambua kwamba alielewa kabisa DVD hiyo.”

Mwanamke kiziwi anayeishi katika eneo la mashambani la Venezuela alikuwa na mtoto mmoja, naye alikuwa anatazamia kujifungua mtoto wa pili. Yeye na mume wake walihisi kwamba hawawezi kumtunza mtoto mwingine kwa sababu ya matatizo ya kiuchumi, kwa hiyo walikuwa wakifikiria kutoa mimba hiyo. Bila kujua hilo, Mashahidi wa Yehova waliwatembelea na kuwaonyesha somo namba 12 katika vidio yenye kichwa Mungu Anataka Tufanye Nini? ya Lugha ya Ishara ya Venezuela. Somo hilo linaeleza maoni ya Mungu kuhusu kutoa mimba na kuua. Baadaye, mwanamke huyo aliwaambia Mashahidi kwamba alishukuru sana kujifunza somo hilo. Alisema kwamba waliamua kutotoa mimba baada ya kujifunza somo hilo. Kwa sababu ya kichapo cha lugha ya ishara kwenye DVD, uhai wa mtoto ambaye hajazaliwa uliokolewa.

Lorraine, Shahidi aliye kiziwi, anaeleza hivi: “Kujifunza Biblia kumekuwa kama kufumbua fumbo kubwa. Singeweza kuelewa kikamili ujumbe wa Biblia kwa sababu sikuwa na habari kamili. Hata hivyo, kweli za Biblia zilipoanza kupatikana katika lugha ya ishara, mapengo hayo yalijazwa.” George, kiziwi ambaye amekuwa Shahidi kwa miaka 38, anasema hivi: “Hakuna shaka kwamba uwezo wa kuelewa jambo wewe mwenyewe unakusaidia kujiheshimu na kujiamini kwa kadiri fulani. Ninahisi kwamba DVD za lugha ya ishara zimenisaidia sana kukua kiroho.”

“Mkutano Ulifanywa Katika Lugha Yangu!”

Zaidi ya kuandaa vichapo vya lugha ya ishara, Mashahidi wa Yehova wamepanga makutaniko ambayo yanafanya mikutano yote katika lugha ya ishara. Kwa sasa, ulimwenguni pote kuna makutaniko zaidi ya 1,100 ya lugha ya ishara. Viziwi wanafurahia mikutano katika lugha ya ishara, kweli za Biblia zinafundishwa kwa lugha ambayo kiziwi anatumia, yaani, lugha ya ishara. Kweli hizo zinafundishwa kwa njia ambayo inaheshimu utamaduni wake na uzoefu wake maishani.

Je, kuanzishwa kwa makutaniko ya lugha ya ishara kumekuwa na faida? Fikiria simulizi la Cyril, ambaye alibatizwa mwaka wa 1955 na kuwa Shahidi wa Yehova. Kwa miaka mingi alijitahidi kujifunza vichapo na kuhudhuria mikutano ya Kikristo kwa uaminifu. Nyakati nyingine, wafasiri walikuwapo na nyakati nyingine hawakuwapo. Wakati hawakuwapo, aliwategemea Mashahidi ambao walijaribu kwa upendo kumsaidia kwa kumwandikia mambo yaliyokuwa yakisemwa jukwaani. Ni mwaka wa 1989 tu, baada ya yeye kuwa Shahidi kwa miaka 34 hivi, ndipo kutaniko la kwanza la lugha ya ishara lilipoanzishwa nchini Marekani katika jiji la New York City. Akiwa mshiriki wa kutaniko hilo, Cyril alihisi namna gani? “Ilikuwa ni kama kutoka ndani ya msitu, ndani ya shimo lenye giza na kuingia katika nuru. Mkutano ulifanywa katika lugha yangu!”

Makutaniko ya Mashahidi wa Yehova ya lugha ya ishara ni mahali ambapo viziwi wanaweza kukusanyika kwa ukawaida ili kujifunza kumhusu Mungu na kumwabudu. Ni mahali ambapo watu wa Mungu wanaweza kupata marafiki na kutiwa moyo. Katika ulimwengu ambamo viziwi wanatengwa na wengine kwa sababu hawawezi kuwasiliana kwa urahisi, wanapata nafasi ya kuwasiliana na kushirikiana na wengine katika makutaniko hayo. Katika makutaniko hayo, viziwi wanaweza kujifunza, kukua kiroho, na kufanya maendeleo wanapomtumikia Yehova. Mashahidi wengi viziwi wanatumika wakiwa waeneza-injili wa wakati wote. Wengine wamehamia nchi nyingine ili kuwasaidia viziwi kujifunza kumhusu Yehova. Wanaume Wakristo ambao ni viziwi wanajifunza kupanga mambo, kuwa walimu, na wachungaji stadi, na hivyo wengi wao wanastahili kutimiza madaraka katika kutaniko.

Huko Marekani, kuna makutaniko zaidi ya 100 ya lugha ya ishara na vikundi 80 hivi. Huko Brazili, kuna makutaniko 300 hivi ya lugha ya ishara na vikundi zaidi ya 400. Kuna makutaniko karibu 300 ya lugha ya ishara nchini Mexico. Nchi ya Urusi ina makutaniko zaidi ya 30 ya lugha ya ishara na vikundi 113. Hiyo ni mifano michache tu ya maendeleo yanayofanywa ulimwenguni pote.

Mashahidi wa Yehova wanafanya pia makusanyiko katika lugha ya ishara. Mwaka uliopita, makusanyiko ya wilaya zaidi ya 120 yalifanywa ulimwenguni pote katika lugha mbalimbali za ishara. Makusanyiko hayo yanawawezesha Mashahidi viziwi kuona kwamba wao ni sehemu ya undugu wa Kikristo wa ulimwenguni pote ambao unafaidika kutokana na chakula cha kiroho cha wakati unaofaa.

Leonard ni kiziwi naye amekuwa Shahidi wa Yehova kwa miaka zaidi ya 25. Anasema hivi: “Sikuzote nilijua kwamba Yehova ndiye Mungu wa kweli. Hata hivyo, sikuelewa waziwazi kwa nini ameruhusu mateso. Nyakati nyingine, hilo lilinifanya nimkasirikie Mungu. Lakini hotuba fulani iliyotolewa katika kusanyiko la wilaya ilinisaidia mwishowe kuelewa masuala yanayohusika. Hotuba ilipokwisha, mke wangu alinipiga kikumbo na kuniuliza, ‘Umeridhika?’ Kwa unyoofu, nilisema ndiyo! Baada ya miaka 25, ninashukuru kwamba sikumwacha Yehova kamwe. Sikuzote nilimpenda lakini sikumwelewa kikamili. Sasa ninamwelewa!”

Wanashukuru Kutoka Moyoni

Ni “ishara” gani za uso wa Yehova ambazo viziwi wanaona wanapojifunza kumhusu? Upendo, huruma, haki, ushikamanifu, fadhili zenye upendo na sifa nyingine nyingi.

Jamii ya kimataifa ya Mashahidi viziwi inauona uso wa Yehova na itaendelea kufanya hivyo kwa njia iliyo wazi zaidi. Akichochewa na upendo wa kutoka moyoni kwa ajili ya viziwi, ‘Yehova ameufanya uso wake ung’ae kuwaelekea.’ (Hes. 6:25) Viziwi hao wanashukuru kama nini kwamba wamemjua Yehova!

[Picha katika ukurasa wa 24, 25]

Ulimwenguni pote kuna makutaniko zaidi ya 1,100 ya lugha ya ishara

[Picha katika ukurasa wa 26]

Uso wa Yehova umeng’aa kwa uangavu katika eneo la viziwi