Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Endelea Kuwa na Mtazamo wa Akili wa Kristo Ndani Yako

Endelea Kuwa na Mtazamo wa Akili wa Kristo Ndani Yako

Endelea Kuwa na Mtazamo wa Akili wa Kristo Ndani Yako

‘Ninyi kati yenu wenyewe muwe na mtazamo uleule wa akili ambao Kristo Yesu alikuwa nao.’—ROM. 15:5.

1. Kwa nini tunapaswa kujitahidi kuwa na mtazamo wa akili wa Kristo?

YESU KRISTO alisema hivi: “Njooni kwangu . . . mjifunze kutoka kwangu, kwa maana mimi ni mwenye tabia-pole na mnyenyekevu moyoni, nanyi mtapata burudisho kwa ajili ya nafsi zenu.” (Mt. 11:28, 29) Mwaliko huo mchangamfu unaonyesha vizuri mtazamo wa akili wa Yesu wenye upendo. Hakuna mwanadamu yeyote anayeweza kuweka mfano bora wa kufuatwa kama Yesu alivyofanya. Ingawa alikuwa Mwana mwenye nguvu wa Mungu, Yesu aliwaonyesha huruma na upendo mwororo, hasa wale waliokuwa wakiteseka.

2. Ni mambo gani kuhusu mtazamo wa akili wa Yesu tutakayochunguza?

2 Katika makala hii na zile mbili zinazofuata, tutachunguza jinsi tunavyoweza kusitawisha na kudumisha mtazamo wa akili kama wa Yesu na kuonyesha “akili ya Kristo” katika maisha yetu. (1 Kor. 2:16) Tutachunguza mambo matano hasa: Upole na unyenyekevu wa Yesu, fadhili zake, utii wake kwa Mungu, ujasiri wake, na upendo wake usioshindwa.

Jifunze Kutokana na Tabia-Pole ya Kristo

3. (a) Ni somo gani la unyenyekevu ambalo Yesu aliwafundisha wanafunzi wake? (b) Yesu alisema nini wanafunzi wake walipoonyesha udhaifu?

3 Yesu, Mwana mkamilifu wa Mungu, alikuja duniani kwa kupenda kwake ili kutumikia katikati ya wanadamu wasio wakamilifu na wenye dhambi. Baadaye, wengine wao wangemuua. Hata hivyo, sikuzote Yesu alijizuia na kudumisha shangwe yake. (1 Pet. 2:21-23) ‘Kutazama kwa makini’ mfano wa Yesu kunaweza pia kutusaidia kufanya vivyo hivyo tunapohuzunishwa na makosa na kutokamilika kwa wengine. (Ebr. 12:2) Yesu aliwaalika wanafunzi wake waje chini ya nira yake na hivyo kujifunza kutoka kwake. (Mt. 11:29) Wangeweza kujifunza nini? Kwanza, Yesu alikuwa mwenye tabia-pole, na alikuwa mvumilivu kwa wanafunzi wake ingawa walifanya makosa. Usiku uliotangulia kifo chake, Yesu aliwaosha miguu, na hivyo akawafundisha somo la kuwa ‘wanyenyekevu moyoni,’ somo ambalo hawangesahau kamwe. (Soma Yohana 13:14-17.) Baadaye, Petro, Yakobo, na Yohana waliposhindwa ‘kuendelea kukesha,’ kwa huruma Yesu alitambua udhaifu wao. Aliuliza hivi: “Simoni, unalala usingizi? . . . Endeleeni kukesha na kusali, ili msiingie katika jaribu. Bila shaka, roho inataka, lakini mwili ni dhaifu.”—Marko 14:32-38.

4, 5. Mfano wa Yesu unaweza kutusaidia jinsi gani kushughulikia udhaifu wa wengine?

4 Tunatenda jinsi gani mwamini mwenzetu anapokuwa na roho ya kushindana, anapokasirika kwa urahisi, au anapokosa kufuata haraka mashauri ya wazee au ya “mtumwa mwaminifu na mwenye busara”? (Mt. 24:45-47) Huenda tukawa tayari kuwasamehe watu wa ulimwengu wa Shetani udhaifu wao wa kimwili na kuuona kuwa wa kawaida, lakini ndugu zetu wanapokuwa na udhaifu huo inaweza kuwa vigumu kuwasamehe. Ikiwa makosa ya wengine yanatuudhi kwa urahisi, tunahitaji kujiuliza wenyewe, ‘Ninaweza jinsi gani kuonyesha vizuri zaidi “akili ya Kristo”?’ Jaribu kukumbuka kwamba Yesu hakuwakasirikia wanafunzi wake, hata wakati walipoonyesha udhaifu wa kiroho kwa kadiri fulani.

5 Fikiria kisa cha mtume Petro. Yesu alipomwita Petro atoke ndani ya mashua na kumjia huku akitembea juu ya maji, kwa kweli Petro alitembea kwa muda fulani juu ya maji. Kisha Petro akaangalia dhoruba ya upepo naye akaanza kuzama. Je, Yesu alikasirika na kumwambia: “Unastahili hilo! Na hilo liwe somo kwako”? Hapana! “Mara moja Yesu akaunyoosha mkono wake, akamshika na kumwambia: ‘Wewe mwenye imani kidogo, kwa nini umekuwa na shaka?’” (Mt. 14:28-31) Ikiwa tunashughulika na ndugu ambaye anaonekana hana imani, je, tunaweza kwa njia ya mfano kuunyoosha mkono wetu na kumsaidia kuwa na imani zaidi? Bila shaka, tunaweza kujifunza mengi kutokana na jinsi Yesu alivyomtendea Petro kwa upole.

6. Yesu aliwafundisha wanafunzi wake jambo gani kuhusu kutafuta umashuhuri?

6 Petro pia alishiriki katika mabishano ya mitume yaliyokuwa yakiendelea kuhusu ni nani kati yao aliyekuwa mkuu zaidi. Yakobo na Yohana walitaka kuketi mmoja kwenye mkono wa kuume wa Yesu na mwingine kwenye mkono wa kushoto katika Ufalme wake. Petro na mitume wengine waliposikia hilo, walikasirika. Yesu alijua kwamba inaelekea walijifunza mtazamo huo wa kushindana kutoka katika jamii ambamo walilelewa. Aliwaita na kuwaambia: “Mnajua kwamba watawala wa mataifa hupiga ubwana juu yao na wakuu hutumia mamlaka juu yao. Hivyo sivyo ilivyo katikati yenu; bali yeyote anayetaka kuwa mkubwa katikati yenu lazima awe mhudumu wenu, na yeyote anayetaka kuwa wa kwanza katikati yenu lazima awe mtumwa wenu.” Kisha Yesu akataja mfano wake mwenyewe: “Kama vile Mwana wa binadamu alivyokuja, si kuhudumiwa, bali kuhudumu na kutoa nafsi yake kuwa fidia badala ya wengi.”—Mt. 20:20-28.

7. Kila mmoja wetu anaweza jinsi gani kuchangia umoja katika kutaniko?

7 Kutafakari kuhusu mtazamo wa unyenyekevu wa akili wa Yesu kunaweza kutusaidia ‘kujiendesha kama walio wadogo zaidi’ kati ya ndugu zetu. (Luka 9:46-48) Kufanya hivyo kunachangia umoja. Yehova, kama baba mwenye familia kubwa, anataka watoto wake ‘wakae pamoja kwa umoja’ na waelewane. (Zab. 133:1) Yesu alisali kwa Baba yake kwamba Wakristo wote wa kweli wawe na umoja, ili “ulimwengu upate kujua kwamba wewe ulinituma na kwamba uliwapenda wao kama vile ulivyonipenda mimi.” (Yoh. 17:23) Hivyo, umoja wetu unasaidia kututambulisha kuwa wafuasi wa Kristo. Ili tufurahie umoja huo, tunapaswa kuona udhaifu wa wengine kama Kristo alivyouona. Yesu alikuwa mwenye kusamehe, na alifundisha kwamba tunaweza pia kusamehewa ikiwa tu tunawasemehe wengine.—Soma Mathayo 6:14, 15.

8. Tunaweza kujifunza nini kutokana na mfano wa watumishi wa Mungu ambao wametumika kwa miaka mingi?

8 Tunaweza pia kujifunza mengi kwa kuiga imani ya wale ambao wamekuwa wakimwiga Kristo kwa miaka mingi. Kama Yesu, kwa kawaida watumishi hao wa Mungu wanajitahidi kuelewa udhaifu wa wengine. Wamejifunza kwamba kuonyesha huruma kama ya Kristo kunatusaidia “kuchukua udhaifu wa wale wasio na nguvu” na pia kunachangia umoja. Zaidi ya hayo, kunalitia moyo kutaniko lote kuonyesha mtazamo wa akili wa Kristo. Wanataka ndugu zao waonyeshe mtazamo huohuo wa akili kama vile mtume Paulo alivyotaka Wakristo wa Roma wafanye: “Mungu anayetoa uvumilivu na faraja na awawezeshe ninyi kati yenu wenyewe kuwa na mtazamo uleule wa akili ambao Kristo Yesu alikuwa nao, ili kwa umoja na kwa kinywa kimoja mpate kumtukuza Mungu na Baba ya Bwana wetu Yesu Kristo.” (Rom. 15:1, 5, 6) Ndiyo, ibada yetu yenye umoja inamletea Yehova sifa.

9. Kwa nini tunahitaji roho takatifu ili kuiga mfano wa Yesu?

9 Yesu alihusianisha kuwa “mnyenyekevu moyoni” na upole, ambao ni sehemu ya matunda ya roho takatifu ya Mungu. Hivyo, pamoja na kujifunza mfano wa Yesu, tunahitaji roho takatifu ya Yehova ili tuweze kuiga mfano huo kwa njia inayofaa. Tunapaswa kusali ili tupewe roho takatifu ya Mungu na kujitahidi kusitawisha matunda yake, yaani, “upendo, shangwe, amani, ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole, kujizuia.” (Gal. 5:22, 23) Hivyo, tukifuata kielelezo cha unyenyekevu na upole ambacho Yesu aliweka, tutampendeza Baba yetu wa mbinguni, Yehova.

Yesu Aliwatendea Wengine kwa Fadhili

10. Yesu alionyesha fadhili jinsi gani?

10 Pia, fadhili ni sehemu ya matunda ya roho takatifu. Sikuzote Yesu aliwatendea wengine kwa fadhili. Wote ambao walimtafuta Yesu kwa unyoofu waliona kwamba ‘aliwapokea kwa fadhili.’ (Soma Luka 9:11.) Tunaweza kujifunza nini kutokana na fadhili ambazo Yesu alionyesha? Mtu mwenye fadhili ni mwenye urafiki, mpole, mwenye huruma na rehema. Yesu alikuwa hivyo. Aliwasikitikia watu “kwa sababu walikuwa wamechunwa ngozi na kutupwa huku na huku kama kondoo wasio na mchungaji.”—Mt. 9:35, 36.

11, 12. (a) Eleza kisa kimoja kinachoonyesha jinsi Yesu alivyotenda kwa huruma. (b) Unaweza kujifunza nini kutokana na mfano huo?

11 Yesu alionyesha pia kwamba aliwasikitikia na kuwahurumia watu kwa kuwasaidia. Fikiria kisa kimoja. Kwa miaka 12, mwanamke mmoja aliteseka kwa sababu ya kutokwa na damu isivyo kawaida. Alijua kwamba chini ya Sheria ya Musa, hali yake ilimfanya kuwa najisi na pia mtu mwingine yeyote ambaye angemgusa. (Law. 15:25-27) Hata hivyo, inaonekana kwamba sifa nzuri ya Yesu na jinsi alivyowatendea watu ilimsadikisha mwanamke huyo kwamba Yesu angemponya. Aliendelea kusema: “Nikiyagusa tu mavazi yake ya nje nitapona.” Kwa ujasiri, alifanya hivyo na papo hapo akahisi kwamba ameponywa.

12 Yesu alijua kwamba kuna mtu aliyemgusa, na aliangalia huku na huku ili aone ni nani aliyemgusa. Inaelekea akiogopa kukemewa kwa sababu alikuwa amevunja Sheria, mwanamke huyo alianguka kwenye miguu ya Yesu huku akitetemeka, kisha akamwambia ukweli wote. Je, Yesu alimkemea mwanamke huyo maskini aliyekuwa ameteseka sana? Hapana! Alimtia moyo kwa kumwambia hivi: “Binti yangu, imani yako imekuponya. Nenda kwa amani.” (Marko 5:25-34) Alifarijika kama nini aliposikia maneno hayo yenye fadhili!

13. (a) Mtazamo wa Yesu ulikuwa tofauti jinsi gani na ule wa Mafarisayo? (b) Yesu aliwatendea watoto namna gani?

13 Tofauti na Mafarisayo wenye mioyo migumu, Kristo hakutumia kamwe mamlaka yake ili kuwaongezea wengine mizigo. (Mt. 23:4) Badala yake, aliwafundisha wengine njia za Yehova kwa fadhili na subira. Yesu alikuwa rafiki mwenye upendo kwa wafuasi wake, sikuzote aliwaonyesha upendo na fadhili, alikuwa rafiki wa kweli. (Met. 17:17; Yoh. 15:11-15) Hata watoto walistarehe sana kuwa pamoja na Yesu, na ni wazi kwamba yeye pia alihisi vivyo hivyo akiwa pamoja nao. Ingawa alikuwa na shughuli nyingi sana alipata wakati wa kuwa pamoja na watoto. Pindi moja, wanafunzi wake ambao walikuwa bado wakijifikiria wenyewe kuwa bora kama viongozi wa kidini wa eneo lao, walijaribu kuwazuia watu wasilete watoto wao wachanga kwa Yesu ili awaguse. Yesu hakufurahia kuona wanafunzi wake wakifanya hivyo. Aliwaambia hivi: “Waacheni watoto wachanga waje kwangu; msijaribu kuwazuia, kwa maana ufalme wa Mungu ni wa wale walio kama hao.” Kisha, akitumia mtoto ili kuwafundisha somo, alisema hivi: “Kwa kweli ninawaambia ninyi, Yeyote yule asiyeupokea ufalme wa Mungu kama mtoto mchanga hataingia kamwe ndani yake.”—Marko 10:13-15.

14. Watoto wanapata faida gani wanapohangaikiwa kikweli?

14 Fikiria kidogo jinsi ambavyo baadhi ya watoto hao wangehisi miaka mingi baadaye wakiwa wanaume na wanawake wazima, wangekumbuka kwamba Yesu Kristo ‘aliwachukua mikononi mwake na akawabariki.’ (Marko 10:16) Leo pia watoto watawakumbuka kwa upendo wazee na wengine ambao wanapendezwa nao kikweli bila uchoyo. Jambo la maana zaidi ni kwamba kuanzia umri mchanga, watoto ambao wanaonyeshwa upendo huo wa kweli kutanikoni wanajifunza kwamba roho ya Yehova iko juu ya watu wake.

Onyesha Fadhili Katika Ulimwengu Usio na Fadhili

15. Kwa nini hatupaswi kushangaa watu wanapokosa kuonyesha fadhili leo?

15 Watu wengi leo wanahisi kwamba hawana wakati wa kuwaonyesha wengine fadhili. Kwa hiyo, kila siku shuleni, kazini, wanaposafiri, na wanapohubiri, watu wa Yehova wanakabili roho ya ulimwengu. Huenda mitazamo isiyo ya fadhili ikatuvunja moyo, lakini hilo halipaswi kutushangaza. Yehova alimwongoza Paulo kutuonya mapema kwamba maisha katika ‘siku hizi za mwisho’ zilizo ngumu yangewafanya Wakristo wa kweli wachangamane na watu “wenye kujipenda wenyewe, . . . wasio na upendo wa asili.”—2 Tim. 3:1-3.

16. Tunaweza kuwachochea wengine jinsi gani katika kutaniko ili wawe wenye fadhili kama Kristo?

16 Kwa upande mwingine, hali katika kutaniko la kweli la Kikristo inaburudisha tofauti na hali katika ulimwengu usio na fadhili. Kwa kumwiga Yesu, kila mmoja wetu anaweza kuchangia hali hiyo nzuri. Tunaweza kufanya hivyo jinsi gani? Kwanza, walio wengi katika kutaniko wanahitaji msaada wetu na kitia-moyo kwa sababu wanakabili matatizo ya afya au hali nyingine ngumu. Katika ‘siku hizi za mwisho,’ huenda matatizo kama hayo yakaongezeka, lakini kwa vyovyote vile si mapya. Katika nyakati za Biblia, Wakristo walipata matatizo kama hayo. Kwa hiyo, leo ni jambo linalofaa kuwasaidia wengine kama Wakristo walioishi zamani walivyofanya. Kwa mfano, Paulo aliwahimiza Wakristo ‘waseme kwa kuzifariji nafsi zilizohuzunika, wategemeze walio dhaifu, wawe wenye ustahimilivu kuelekea wote.’ (1 The. 5:14) Hilo linamaanisha kwamba wanahitaji kutenda kwa fadhili kama Kristo.

17, 18. Tunaweza kuiga fadhili za Yesu katika njia gani?

17 Wakristo wana wajibu wa ‘kuwapokea ndugu zao kwa fadhili,’ kuwatendea jinsi ambavyo Yesu angewatendea, kuwajali kikweli wale ambao huenda tumewajua kwa miaka mingi na wale ambao hatujawahi kukutana nao. (3 Yoh. 5-8) Kama vile Yesu alivyochukua hatua ya kwanza kuwaonyesha wengine huruma, sisi pia, tunapaswa sikuzote kuwaburudisha wengine.—Isa. 32:2; Mt. 11:28-30.

18 Kila mmoja wetu anaweza kuonyesha fadhili kwa kupendezwa kikweli na hali ya wengine. Tafuta njia na nafasi za kufanya hivyo. Wasaidie! Paulo alihimiza hivi: “Katika upendo wa kindugu iweni na upendo mwororo kwa mtu na mwenzake,” kisha akaongezea hivi: “Katika kuonyeshana heshima iweni wa kwanza.” (Rom. 12:10) Hilo linamaanisha kufuata mfano wa Kristo, kuwatendea wengine kwa shauku na fadhili, kujifunza kuonyesha “upendo usio na unafiki.” (2 Kor. 6:6) Paulo alieleza upendo huo wa Kristo kwa njia hii: “Upendo ni wenye ustahimilivu na wenye fadhili. Upendo hauna wivu, haujigambi, haujivuni.” (1 Kor. 13:4) Badala ya kuwawekea kinyongo ndugu na dada zetu, na tutii himizo hili: “Iweni wenye fadhili ninyi kwa ninyi, wenye huruma nyororo, mkisameheana kwa hiari kama vile Mungu pia kupitia Kristo alivyowasamehe ninyi kwa hiari.”—Efe. 4:32.

19. Tunapata matokeo gani mazuri tunapoonyesha fadhili kama Kristo?

19 Tukijitahidi sana kusitawisha na kuonyesha fadhili kama Kristo nyakati zote na katika hali zote tutathawabishwa sana. Roho ya Yehova itatenda kazi kwa uhuru katika kutaniko, na hivyo kila mtu ataweza kutokeza matunda ya roho. Zaidi ya hayo, tunapofuata kielelezo cha Yesu na kuwasaidia wengine kufanya hivyo, ibada yetu yenye furaha na umoja itamletea Mungu shangwe. Kwa hiyo, acheni sikuzote tujitahidi kabisa kuonyesha upole na fadhili kama Yesu tunaposhughulika na wengine.

Je, Unaweza Kueleza?

• Yesu alionyesha jinsi gani kwamba alikuwa “mwenye tabia-pole na mnyenyekevu moyoni”?

• Yesu alionyesha fadhili jinsi gani?

• Tunaonyesha katika njia gani upole na fadhili kama Kristo katika ulimwengu huu usiokamilika?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 8]

Imani ya ndugu ikidhoofika kama imani ya Petro ilivyodhoofika, je, tutamsaidia?

[Picha katika ukurasa wa 10]

Unaweza kufanya nini ili fadhili ienee katika kutaniko?