Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Unathamini Yale Ambayo Yehova Amefanya Ili Kukukomboa?

Je, Unathamini Yale Ambayo Yehova Amefanya Ili Kukukomboa?

Je, Unathamini Yale Ambayo Yehova Amefanya Ili Kukukomboa?

“Na abarikiwe Yehova Mungu wa Israeli, kwa sababu ameelekeza uangalifu wake na kufanya ukombozi kuelekea watu wake.”—LUKA 1:68.

1, 2. Ni mfano gani ambao unaonyesha uzito wa hali tunayokabili sasa, na tutazungumzia maswali gani?

HEBU wazia kwamba umelazwa hospitalini. Umelazwa katika chumba chenye watu walio na ugonjwa fulani hatari ambao hauna dawa. Unapopata habari kwamba daktari fulani anaongoza jitihada za kutafuta dawa ya ugonjwa huo, unakuwa na tumaini. Unangoja kwa hamu sana habari zozote mpya kuhusu utafiti wa daktari huyo. Siku moja, unapata habari kwamba dawa imepatikana! Yule daktari aliyekuwa anatafuta dawa amejidhabihu kabisa ili kuweza kupata dawa hiyo. Ungehisi namna gani? Bila shaka, ungemheshimu sana na kumthamini kutoka moyoni daktari huyo aliyekuokoa wewe na wengine wengi kutoka katika kifo.

2 Huenda simulizi hilo lisionekane kuwa halisi, lakini kwa kweli sote tuko katika hali kama hiyo. Kila mmoja wetu yuko katika hali hatari zaidi kuliko hali inayoelezwa hapo juu. Tunahitaji sana mtu anayeweza kutuokoa. (Soma Waroma 7:24.) Yehova amejidhabihu sana ili kutukomboa. Mwana wake pia amejidhabihu kwa njia kubwa sana. Basi, acheni tuchunguze maswali manne ya msingi. Kwa nini tunahitaji ukombozi? Yesu alijidhabihu kadiri gani ili tukombolewe? Yehova amejidhabihu kwa kadiri gani ili kutukomboa? Nasi tunaweza kuonyesha namna gani kwamba tunathamini kukombolewa na Mungu?

Kwa Nini Tunahitaji Ukombozi?

3. Dhambi inalingana jinsi gani na ugonjwa hatari unaoenea?

3 Kulingana na kadirio la hivi karibuni, homa ya Kihispania ya mwaka wa 1918 ambayo iliangamiza makumi ya mamilioni ya watu ilikuwa kati ya magonjwa mabaya zaidi katika historia ya wanadamu. Kuna magonjwa mengine mabaya zaidi ambayo pia yanaweza kusababisha kifo. Hata ingawa huenda yakawaambukiza watu wachache, yanasababisha vifo vya watu wengi zaidi ambao wanaambukizwa. * Hata hivyo, acheni tulinganishe dhambi na ugonjwa kama huo hatari ambao unaenea. Kumbuka maneno ya Waroma 5:12: “Kupitia mtu mmoja dhambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia dhambi, na hivyo kifo kikaenea kwa watu wote kwa sababu wote walikuwa wamefanya dhambi.” Kila mtu duniani ameambukizwa dhambi, kwa kuwa wanadamu wote wasio wakamilifu wanatenda dhambi. (Soma Waroma 3:23.) Ni watu wangapi wanaokufa kwa sababu ya dhambi? Paulo aliandika kwamba dhambi inawaletea “watu wote” kifo.

4. Yehova ana maoni gani kuhusu urefu wa maisha yetu, na maoni yake yanatofautiana jinsi gani na maoni ya watu wengi leo?

4 Watu wengi leo wanaona kwamba dhambi na kifo ni mambo ya kawaida tu. Wanaogopa kifo cha ghafula, lakini wanapuuza kifo cha “asili” ambacho kinawanyemelea wanadamu hatua kwa hatua wanapozeeka. Ni rahisi sana kwa wanadamu kusahau maoni ya Muumba. Maisha yetu ni mafupi sana kuliko vile Mungu alivyokusudia. Kwa kweli, kulingana na maoni ya Yehova, hakuna mwanadamu ambaye ameishi “siku moja.” (2 Pet. 3:8) Hivyo, Neno la Mungu linasema kwamba maisha yetu ni mafupi sana kama majira ya majani yanayomea na kunyauka haraka au kama pumzi inayotoka. (Zab. 39:5; 1 Pet. 1:24) Tunahitaji kukumbuka jambo hilo. Kwa nini? Tukielewa hatari ya “ugonjwa” tunaokabili, tunaweza kuthamini zaidi umuhimu wa “matibabu,” yaani, ukombozi wetu.

5. Kila mmoja wetu amepoteza nini kwa sababu ya dhambi?

5 Ili kuelewa matokeo mabaya ya dhambi na madhara yake, ni lazima tujitahidi kuelewa hasara ambayo dhambi imetuletea. Huenda ikawa vigumu mwanzoni kuelewa hilo kwa sababu dhambi ilitupotezea kitu fulani ambacho hatujawahi kamwe kuwa nacho. Hapo mwanzo, Adamu na Hawa walifurahia uhai mkamilifu wa kibinadamu. Walikuwa wakamilifu katika akili na mwili, wangeweza kuelekeza mawazo, hisia, na matendo yao jinsi walivyotaka. Hivyo, walikuwa na uhuru wa kufanya maendeleo wakiwa watumishi wa Yehova Mungu na kusitawisha sifa nzuri sana. Badala yake, walipoteza zawadi hiyo yenye thamani. Walipochagua kumwasi Yehova, walipoteza aina ya maisha ambayo Yehova alikusudia wao na wazao wao wawe nayo. (Mwa. 3:16-19) Wakati huohuo, walijiletea na kutuletea sisi “ugonjwa” mbaya sana ambao tumekuwa tukizungumzia. Yehova aliwapa hukumu waliyostahili. Lakini anatupa sisi tumaini la ukombozi.—Zab. 103:10.

Yesu Alijidhabihu Kadiri Gani Ili Tukombolewe?

6, 7. (a) Yehova alionyesha jinsi gani mwanzoni kwamba ukombozi wetu ungehitaji dhabihu yenye thamani kubwa sana? (b) Tunaweza kujifunza nini kutokana na dhabihu zilizotolewa na Abeli na wazee wa ukoo walioishi kabla ya Sheria ya Musa kutolewa?

6 Yehova alijua kwamba dhabihu ya kuwakomboa wazao wa Adamu na Hawa ingekuwa yenye thamani kubwa sana. Katika unabii ulioandikwa kwenye Mwanzo 3:15, tunajifunza jambo fulani kuhusu thamani ya ukombozi. Yehova angetokeza “uzao,” mwokozi, ambaye siku moja angemharibu Shetani na kumponda kabisa ili asiwepo. Hata hivyo, mwokozi huyo angeteseka na kutiwa jeraha la mfano kwenye kisigino. Inaonekana kwamba jeraha hilo lingekuwa pigo kubwa lenye maumivu makali, lakini lingemaanisha nini? Mchaguliwa wa Yehova angevumilia hali gani?

7 Ili kuwaokoa wanadamu kutoka katika dhambi, mwokozi huyo angehitaji kutokeza njia ya kuwapatanisha wanadamu na Mungu kwa kuondoa matokeo ya dhambi. Hilo lingehusisha nini? Matukio fulani ya zamani yalionyesha kwamba dhabihu ingehitajiwa. Mwanadamu wa kwanza mwaminifu, Abeli, alipomtolea Yehova dhabihu za wanyama, alipata kibali cha Mungu. Baadaye, wazee wa ukoo waliomwogopa Mungu kama vile Noa, Abrahamu, Yakobo, na Ayubu walitoa dhabihu kama hizo, ambazo zilimpendeza Mungu. (Mwa. 4:4; 8:20, 21; 22:13; 31:54; Ayu. 1:5) Karne nyingi baadaye, Sheria ya Musa iliwasaidia watu kuelewa vizuri zaidi mpango wa kutoa dhabihu.

8. Kuhani mkuu alifanya nini katika Siku ya Upatanisho kila mwaka?

8 Kati ya dhabihu za maana sana ambazo ziliamriwa na Sheria zilitia ndani dhabihu zilizotolewa kila mwaka katika Siku ya Upatanisho. Siku hiyo, kuhani mkuu alifanya mambo mbalimbali ya mfano. Alitoa dhabihu kwa Yehova ili kufanya upatanisho wa dhambi, kwanza dhambi za jamii ya makuhani, kisha dhambi za makabila yasiyo ya kikuhani. Kuhani mkuu aliingia mahali Patakatifu Zaidi ndani ya maskani au katika hekalu, ambamo ni yeye peke yake angeweza kuingia siku hiyo moja tu kwa mwaka. Akiwa humo, alinyunyiza damu ya dhabihu mbele ya sanduku la agano. Nyakati nyingine, wingu jangavu lenye kung’aa lilionekana juu ya sanduku hilo takatifu. Wingu hilo liliwakilisha kuwapo kwa Yehova Mungu.—Kut. 25:22; Law. 16:1-30.

9. (a) Katika Siku ya Upatanisho, kuhani mkuu alimfananisha nani, na dhabihu alizotoa ziliwakilisha nini? (b) Kuingia kwa kuhani mkuu ndani ya Patakatifu Zaidi kuliwakilisha nini?

9 Mtume Paulo aliongozwa na roho ya Mungu kufunua maana ya matendo hayo ya mfano. Alionyesha kwamba kuhani mkuu alimfananisha Masihi, Yesu Kristo, na kutolewa kwa dhabihu hizo kulifananisha kifo cha Kristo cha kidhabihu. (Ebr. 9:11-14) Dhabihu hiyo kamilifu ingefanya upatanisho wa kweli kwa ajili ya vikundi viwili vya watu, yaani, jamii ya makuhani ya ndugu watiwa-mafuta wa Kristo 144, 000 na “kondoo wengine.” (Yoh. 10:16) Kuhani mkuu alipoingia Patakatifu Zaidi, alifananisha kimbele jinsi ambavyo Yesu angeingia ndani ya mbingu zenyewe ili atoe mbele za Yehova Mungu thamani ya dhabihu yake ya fidia au ukombozi.—Ebr. 9:24, 25.

10. Unabii wa Biblia ulionyesha kwamba Masihi angepatwa na nini?

10 Ni wazi kwamba kukombolewa kwa wazao wa Adamu na Hawa kungehitaji dhabihu yenye thamani kubwa sana. Masihi angepaswa kudhabihu uhai wake! Manabii walieleza ukweli huo kwa undani zaidi katika Maandiko ya Kiebrania. Kwa mfano, nabii Danieli alisema moja kwa moja kwamba “Masihi aliye Kiongozi . . . atakatiliwa mbali,” au kuuawa, ili “kufanya upatanisho kwa ajili ya kosa.” (Dan. 9:24-26) Isaya alitabiri kwamba Masihi angekataliwa, angeteswa, na kuuawa, au kuchomwa kwa silaha, ili abebe dhambi za wanadamu wasio wakamilifu.—Isa. 53:4, 5, 7.

11. Mwana wa Yehova alionyesha kwa njia gani kwamba alikuwa tayari kujidhabihu ili tukombolewe?

11 Kabla ya kuja duniani, Mwana mzaliwa-pekee wa Mungu alijua mambo ambayo angekabili ili kutukomboa. Angeteswa kabisa na kisha kuuawa. Baba yake alipomfundisha kweli hizo, je, aliogopa au kuasi? Hakufanya hivyo, badala yake, alijitiisha kwa kupenda kwa maagizo ya Baba yake. (Isa. 50:4-6) Vivyo hivyo, alipokuwa duniani, Yesu alifanya mapenzi ya Baba yake kwa utii. Kwa nini? Alitoa jibu kwa maneno haya: “Ninampenda Baba.” Alitoa jibu lingine kwa maneno haya: “Hakuna aliye na upendo mkuu kuliko huu, kwamba mtu aitoe nafsi yake kwa ajili ya rafiki zake.” (Yoh. 14:31; 15:13) Kwa hiyo, kwa sehemu kubwa ukombozi wetu unategemea upendo wa Mwana wa Yehova. Ingawa alidhabihu uhai wake mkamilifu wa kibinadamu, alifurahi kufanya hivyo ili tukombolewe.

Yehova Alijidhabihu Kadiri Gani Ili Kutukomboa?

12. Fidia au dhabihu ya ukombozi inaonyesha mapenzi ya nani, na kwa nini aliitoa?

12 Yesu hakuwa Mwanzilishi au Mkusudiaji wa fidia au dhabihu ya ukombozi. Badala yake, njia hiyo ya ukombozi ilikuwa sehemu ya maana sana ya kutimiza mapenzi ya Yehova. Mtume Paulo alionyesha kwamba madhabahu ya hekalu, ambayo yalitumiwa kutoa dhabihu, yaliwakilisha mapenzi ya Yehova. (Ebr. 10:10) Kwa hiyo, tunapaswa kwanza kabisa kumshukuru Yehova kwa sababu ya ukombozi ambao tunapata kupitia dhabihu ya Kristo. (Luka 1:68) Ukombozi huo unaonyesha mapenzi makamilifu ya Yehova na upendo wake mkubwa sana kwa wanadamu.—Soma Yohana 3:16.

13, 14. Mfano wa Abrahamu unaweza kutusaidia jinsi gani kuthamini jambo ambalo Yehova amefanya kwa ajili yetu?

13 Yehova alijidhabihu kwa kadiri gani ili aonyeshe upendo wake kwetu? Si rahisi kwetu kuelewa. Hata hivyo, kuna simulizi fulani la Biblia ambalo linaweza kutusaidia kuelewa jambo hilo kwa njia iliyo wazi zaidi. Yehova alimwomba mwanamume mwaminifu Abrahamu afanye jambo gumu sana, yaani, amtoe mwana wake Isaka kuwa dhabihu. Ni wazi kwamba Abrahamu alikuwa baba mwenye upendo. Alipozungumza na Abrahamu kuhusu Isaka, Yehova alimwita Isaka, “mwana wako wa pekee unayempenda sana.” (Mwa. 22:2) Hata hivyo, Abrahamu aliona kwamba kufanya mapenzi ya Yehova lilikuwa jambo la maana zaidi kuliko upendo wake kwa Isaka. Abrahamu alitii bila kusitasita. Lakini, Yehova hakumruhusu Abrahamu afanye jambo ambalo Yeye mwenyewe angefanya siku moja. Mungu alimtuma malaika kumzuia Abrahamu kabla tu ya kumdhabihu mwana wake. Abrahamu aliazimia kabisa kumtii Mungu wake wakati wa jaribu hilo kali hivi kwamba alikuwa na uhakika kuwa tumaini pekee la kumwona kijana huyo tena lilikuwa ni kupitia ufufuo tu. Lakini alikuwa na imani kabisa kwamba Mungu angemfufua Isaka. Kwa kweli, Paulo alisema kwamba Abrahamu alimpokea Isaka tena kupitia ufufuo “kwa njia ya mfano.”—Ebr. 11:19.

14 Je, unaweza kuwazia uchungu ambao Abrahamu alihisi alipokuwa akijitayarisha kumtoa mwana wake? Kwa njia fulani, kisa cha Abrahamu kinaonyesha kwa njia ya mfano jinsi Yehova alivyohisi alipomdhabihu yule ambaye alimwita “Mwanangu, mpendwa.” (Mt. 3:17) Hata hivyo, kumbuka kwamba inaelekea uchungu wa Yehova ulikuwa mwingi zaidi. Yeye na Mwana wake walifurahi kushirikiana kwa mamilioni, labda hata mabilioni ya miaka. Mwana huyo alifanya kazi kwa shangwe pamoja na Baba yake akiwa “stadi wa kazi” mpendwa na pia Msemaji wake, yaani, “Neno.” (Met. 8:22, 30, 31; Yoh. 1:1) Hatuwezi kamwe kuelewa uchungu mwingi ambao Yehova alivumilia alipomwona Mwana wake akiteswa, akidhihakiwa, na kisha kuuawa kama mhalifu. Yehova alijidhabihu kwa njia kubwa kabisa ili atukomboe! Kwa hiyo basi, tunaweza kuonyesha jinsi gani kwamba tunathamini ukombozi huo?

Unaweza Kuonyesha Namna Gani Kwamba Unathamini Ukombozi?

15. Yesu alikamilisha jinsi gani tendo kubwa la upatanisho, na hilo lilifungua njia ya nini?

15 Yesu alikamilisha tendo kubwa la upatanisho baada ya kufufuliwa na kwenda mbinguni. Alipokutana tena na Baba yake mpendwa, alimtolea thamani ya dhabihu yake. Baraka kubwa sana zilifuata. Msamaha kamili ulipatikana, kwanza kwa ajili ya dhambi za ndugu watiwa-mafuta wa Kristo, kisha kwa ajili ya dhambi za “ulimwengu wote.” Kwa sababu ya dhabihu hiyo, leo watu wote wanaotubu kikweli dhambi zao na kuwa wafuasi wa kweli wa Kristo wanaweza kuwa na msimamo safi mbele za Yehova Mungu. (1 Yoh. 2:2) Hilo linakuhusu jinsi gani?

16. Tunaweza kutumia mfano gani kuonyesha kwa nini tunapaswa kuthamini ukombozi ambao Yehova ameandaa kwa ajili yetu?

16 Acheni turudie mfano uliotolewa mwanzoni mwa habari hii. Tuseme kwamba yule daktari anayepata dawa ya ugonjwa anawafikia wagonjwa walio katika chumba ambamo umelazwa na kusema hivi: Mgonjwa yeyote anayekubali dawa hii na kuitumia kupatana na maagizo bila shaka atapona. Namna gani ikiwa wengi kati ya wagonjwa wenzako wanakataa kufuata maagizo ya daktari huyo, huku wakidai kwamba ni vigumu sana kufuata maagizo hayo au kutumia dawa hiyo? Je, utawafuata tu, hata ingawa una ushuhuda wenye kusadikisha wa kwamba dawa hiyo kwa kweli inaponya? Hapana! Bila shaka, ungeshukuru kwamba dawa imepatikana, kisha ungefuata maagizo ya daktari huyo kwa uangalifu, labda hata ungewaambia wengine uamuzi wako. Katika njia kubwa zaidi, kila mmoja wetu anapaswa kuwa na tamaa ya kumwonyesha Yehova jinsi tunavyothamini sana ukombozi ambao ameandaa kupitia dhabihu ya fidia ya Mwana wake.—Soma Waroma 6:17, 18.

17. Unaweza kuonyesha katika njia gani kwamba unathamini yale ambayo Yehova amefanya ili kukukomboa?

17 Ikiwa tunathamini yale ambayo Yehova na Mwana wake wamefanya ili kutukomboa kutoka katika dhambi na kifo, tutaonyesha hivyo kwa matendo. (1 Yoh. 5:3) Tutapambana na mwelekeo wetu wa kufanya dhambi. Hatutakuwa kamwe na mazoea ya kutenda dhambi kimakusudi na kuishi maisha ya unafiki ambayo yanahusiana na mazoea hayo. Ikiwa tungeishi maisha ya aina hiyo tungekuwa tukionyesha kwamba hatuthamini hata kidogo dhabihu ya ukombozi. Badala yake, tutaonyesha kwamba tunathamini dhabihu hiyo kwa kujitahidi sana kubaki safi machoni pa Mungu. (2 Pet. 3:14) Tutaonyesha hivyo kwa kuwatangazia wengine tumaini letu zuri la ukombozi, ili wao pia waweze kuwa na msimamo safi mbele za Yehova na kuwa na tumaini la kuishi milele wakati ujao. (1 Tim. 4:16) Bila shaka, ni jambo linalofaa tutumie wakati na nguvu zetu zote kumsifu Yehova na Mwana wake! (Marko 12:28-30) Fikiria hili! Tunaweza kutazamia wakati ambapo tutaponywa kabisa kutokana na dhambi. Tunaweza kuishi kama Mungu alivyokusudia, tukiwa wakamilifu na kwa umilele, kwa sababu tu ya yale ambayo Yehova amefanya ili kutukomboa!—Rom. 8:21.

[Maelezo ya chini]

^ fu. 3 Inasemekana kwamba homa ya Kihispania iliambukiza kati ya asilimia 20 na asilimia 50 ya watu wote ulimwenguni wakati huo. Huenda virusi vya ugonjwa huo vilisababisha vifo vya kati ya asilimia 1 na asilimia 10 ya watu walioambukizwa virusi hivyo. Kinyume chake, virusi vya Ebola haviwaambukizi watu kwa ukawaida, lakini katika visa fulani vimesababisha vifo vya asilimia 90 hivi ya watu walioambukizwa.

Ungesema Nini?

• Kwa nini unahitaji ukombozi haraka?

• Tendo la Yesu la kujidhabihu linakuhusu jinsi gani?

• Unahisi namna gani kuhusu zawadi ya Yehova ya fidia au dhabihu ya ukombozi?

• Unachochewa kufanya nini kwa sababu ya maandalizi ya Yehova ya kukukomboa?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 27]

Katika Siku ya Upatanisho, kuhani mkuu wa Israeli alimfananisha Masihi

[Picha katika ukurasa wa 28]

Utayari wa Abrahamu wa kumtoa mwana wake unatufundisha mengi kuhusu dhabihu kubwa zaidi ya Yehova