Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nilipata Kusudi Maishani

Nilipata Kusudi Maishani

Nilipata Kusudi Maishani

Limesimuliwa na Gaspar Martínez

Kwa njia fulani, maisha yangu ni kama hadithi ya kijana maskini aliyetoka mashambani akaenda mjini na kupata utajiri. Hata hivyo, utaona kwamba utajiri niliopata ni tofauti na utajiri niliokuwa nikitafuta.

NILILELEWA katika eneo la mashambani lenye ukame miaka ya 1930 huko Rioja kaskazini mwa Hispania. Nilipokuwa na umri wa miaka kumi, nililazimika kuacha shule ingawa kufikia wakati huo nilikuwa nimejifunza kusoma na kuandika. Nikiwa pamoja na ndugu na dada zangu sita, nilitumia muda wangu malishoni nikichunga kondoo au kulima mashamba yetu madogo.

Kwa sababu ya umaskini, tuliona pesa na mali kuwa vitu vya maana sana. Tuliwaonea wivu watu waliokuwa na vitu vingi kuliko sisi. Hata hivyo, wakati mmoja askofu alisema kwamba ‘kijiji chetu ndicho kilichokuwa na watu waliompenda Mungu sana katika dayosisi yake.’ Hakujua kwamba baada ya muda, watu wengi wangeiacha dini ya Katoliki.

Kutafuta Kitu Bora

Nilimwoa msichana kutoka katika kijiji chetu aliyeitwa Mercedes. Baada ya muda mfupi, tulipata mtoto wa kiume. Mnamo 1957 tulihamia kwenye jiji lililokuwa karibu la Logroño, na mwishowe familia yangu yote pia ilihamia huko. Baada ya muda nilitambua kwamba kwa sababu sikuwa na ustadi wowote wa kazi, haingekuwa rahisi kwangu kupata kazi yenye mshahara mzuri. Sikujua ningepata wapi mwongozo. Nilianza kufanya utafiti kwenye maktaba ya eneo hilo, ingawa sikujua nifanye utafiti kuhusu jambo gani hasa.

Baadaye, nilisikia kuhusu kipindi cha redio ambacho kilitoa mafunzo ya Biblia kwa njia ya barua. Mara tu nilipomaliza mafunzo hayo, washiriki fulani wa Kanisa la Kiinjilisti la Kiprotestanti waliwasiliana nami. Baada ya kwenda mahali pao pa ibada mara kadhaa, nilitambua kwamba kulikuwa na uadui kati ya viongozi wa kikundi hicho. Sikurudi huko tena, nikafikia uamuzi wa kwamba lazima dini zote zinafanana.

Magamba Yaanguka Kutoka Kwenye Macho Yangu

Mwaka wa 1964, kijana aliyeitwa Eugenio alitutembelea nyumbani. Alikuwa Shahidi wa Yehova, dini ambayo sikuwa nimewahi kamwe kusikia habari zake. Lakini nilitaka sana kuzungumza naye kuhusu Biblia. Nilifikiri kwamba nilijua Maandiko vizuri. Nilimjibu kwa kutumia maandiko machache ya Biblia ambayo nilikuwa nimejifunza kutokana na yale mafunzo yangu ya Biblia. Ingawa nilijaribu kutetea mafundisho fulani ya Waprotestanti, sikuyaamini kabisa.

Baada ya kuwa na vipindi viwili virefu vya mazungumzo, nilikubali kwamba Eugenio alilitumia Neno la Mungu kwa ustadi sana. Nilishangaa kuona jinsi alivyofungua maandiko na kuonyesha jinsi yalivyotumika, ingawa kiwango chake cha elimu kilikuwa kidogo kuliko changu. Akitumia Biblia, Eugenio alinionyesha kwamba tunaishi katika siku za mwisho na kwamba hivi karibuni Ufalme wa Mungu utaleta paradiso duniani. Nilishangaa sana.—Zab. 37:11, 29; Isa. 9:6, 7; Mt. 6:9, 10.

Nilikubali funzo la Biblia bila kusitasita. Karibu kila jambo nililojifunza lilikuwa jipya na lilinigusa moyo. Nilipata tumaini ambalo lilifanya maisha yangu yawe na kusudi. Nilipata nilichokuwa nikitafuta. Sasa niliona jitihada za kuboresha hali yangu katika jamii kuwa za bure, na sikuona tena haja ya kutafuta kazi nzuri zaidi. Hata magonjwa na kifo vitaondolewa.—Isa. 33:24; 35:5, 6; Ufu. 21:4.

Bila kupoteza wakati nilianza kuwaambia watu wangu wa ukoo kuhusu mambo niliyokuwa nikijifunza, na kuwaeleza kwa uchangamfu kwamba Mungu ameahidi kuleta paradiso duniani ambamo wanadamu waaminifu wataishi milele.

Familia Yangu Inakubali Kweli ya Biblia

Muda si muda, tukiwa kikundi cha watu 12 hivi, tuliamua kukutana kila Jumapili (Siku ya Yenga) alasiri katika nyumba ya mjomba wangu ili kuzungumzia ahadi za Biblia. Kila juma tulitumia saa mbili au tatu katika mazungumzo hayo. Eugenio alipoona kwamba wengi kati ya watu wangu wa ukoo walitaka kujifunza Biblia, alipanga ili kujifunza na kila familia.

Nilikuwa na watu wengine wa ukoo huko Durango, mji mdogo uliokuwa umbali wa kilomita 120 hivi, ambako hakukuwa na Mashahidi. Kwa hiyo, miezi mitatu baadaye, nilichukua likizo ya siku chache ili niwatembelee na kuwaeleza kuhusu imani yangu mpya. Wakati huo, tulikutana tukiwa watu kumi hivi kila jioni, na nilizungumza nao mpaka usiku wa manane. Wote walifurahi kusikiliza. Likizo yangu ilipokwisha, niliwaachia Biblia kadhaa na vichapo vya Biblia. Baada ya hapo, tuliendelea kuwasiliana.

Mashahidi walipofika huko Durango, ambako hakuna yeyote aliyekuwa amehubiri hapo mbeleni, walikuta watu 18 wakisubiri kwa hamu kuanza funzo la Biblia. Mashahidi hao walifanya mpango ili kila familia iwe na funzo.

Kufikia wakati huo, Mercedes hakutaka kujifunza kweli, hasa kwa sababu aliogopa wanadamu bali si kwa sababu hakukubaliana na mafundisho ya Biblia. Wakati huo, kazi ya Mashahidi wa Yehova ilikuwa imepigwa marufuku huko Hispania, hivyo, alidhani kwamba wenye mamlaka wangewafukuza watoto wetu wawili kutoka shuleni na kwamba sote tungetengwa na jamii. Lakini alipoona kwamba familia yetu yote ilikuwa ikikubali kweli ya Biblia, yeye pia alitaka kujifunza.

Katika muda wa miaka miwili, watu 40 wa familia yangu walikubali kuwa Mashahidi na wakabatizwa ili kuonyesha kwamba wamejiweka wakfu kumtumikia Mungu. Ndiyo, sasa familia yangu ilikuwa na lengo na kusudi kama langu maishani. Nilihisi kwamba nilikuwa nimetimiza jambo lenye thamani sana. Tulikuwa tumebarikiwa na utajiri mwingi wa kiroho.

Maisha Yaliendelea Kuridhisha Kadiri Nilivyoendelea Kuzeeka

Kwa miaka 20 iliyofuata, nilikazia fikira kuwalea wavulana wetu wawili na kulisaidia kutaniko letu. Mimi na Mercedes tulipohamia Logroño, kulikuwa na Mashahidi 20 hivi tu katika jiji hilo lenye wakaaji karibu 100,000. Baada ya muda, nilipata madaraka mengi kutanikoni.

Kisha, nilipokuwa na umri wa miaka 56, kwa ghafula kampuni iliyokuwa imeniajiri kazi ilifunga kiwanda nilimokuwa nikifanya kazi, na hivyo nikapoteza kazi. Nilikuwa nimetamani sana kuwa katika utumishi wa wakati wote, hivyo nilitumia nafasi hiyo kuanza upainia. Pesa za malipo ya uzeeni nilizopewa zilikuwa chache sana na hazingeweza kututegemeza. Mercedes alisaidia kwa kufanya kazi mbalimbali za usafi. Tuliweza kuitegemeza familia yetu na hatukukosa vitu vya lazima. Bado mimi ni painia, naye Mercedes anatumikia akiwa painia msaidizi mara kwa mara, na anafurahia sana kazi ya kuhubiri.

Miaka michache iliyopita, Mercedes alikuwa akimwachia kwa ukawaida magazeti yetu mwanamke kijana anayeitwa Merche ambaye alijifunza Biblia alipokuwa mtoto. Merche alipenda sana kusoma vichapo vyetu, na Mercedes alitambua kwamba bado Merche alithamini sana kweli za Biblia. Mwishowe, Merche alikubali funzo la Biblia na akaanza kufanya maendeleo makubwa. Lakini Vicente, mume wake, alikuwa akinywa pombe kupita kiasi na hivyo alipoteza kazi mara nyingi. Hivyo, hakumsaidia kifedha, na ndoa yao ilikuwa karibu kuvunjika kwa sababu ya zoea lake la kunywa pombe kupita kiasi.

Mke wangu alimpendekezea Merche amwambie Vicente aje kuzungumza nami, na mwishowe alikuja. Baada ya kuja mara kadhaa alikubali funzo la Biblia. Vicente alianza kubadilika, akaanza kuacha zoea lake la kunywa pombe kwa siku kadhaa hatua kwa hatua. Kisha alijizuia kunywa pombe kwa juma moja au zaidi. Mwishowe, aliacha kabisa kunywa pombe. Sura yake ilibadilika sana, na familia yake ikawa na umoja. Familia yake yote, kutia ndani mke na binti yake, wanaunga mkono kabisa kutaniko dogo katika Visiwa vya Canary, ambako wanaishi kwa sasa.

Kutafakari Kuhusu Maisha Yangu Yenye Kusudi

Ingawa baadhi ya watu wangu wa ukoo ambao walijifunza mafundisho ya Biblia zamani wamekufa, bado familia yetu imeendelea kukua na Mungu ametubariki sana. (Met. 10:22) Ni jambo lenye kuridhisha kama nini kuona kwamba karibu watu wote walioanza kujifunza Biblia miaka 40 iliyopita, kutia ndani watoto na wajukuu wao, wameendelea kumtumikia Yehova kwa uaminifu!

Sasa, wengi kati ya watu wangu wa ukoo ni Mashahidi wa Yehova na wengi wao wanatumikia wakiwa wazee, watumishi wa huduma, na mapainia. Mwana wangu mkubwa pamoja na mke wake wanatumikia kwenye ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova huko Madrid, Hispania. Nilipoanza kushirikiana na Mashahidi wa Yehova, idadi ya Mashahidi ilikuwa karibu 3,000 nchini Hispania. Sasa idadi yao ni zaidi ya 100,000. Ninafurahia sana utumishi wa wakati wote, na ninamshukuru sana Mungu kwa sababu nimekuwa na maisha mazuri sana katika utumishi wake. Ingawa sikupata elimu nyingi ya kilimwengu, mara kwa mara ninatumikia nikiwa mwangalizi wa mzunguko wa badala.

Miaka michache iliyopita, nilitambua kwamba karibu watu wote walihama kutoka katika kijiji chetu. Mwishowe, umaskini uliwafanya wakaaji wote waache mashamba na nyumba zao ili kutafuta maisha bora. Inafurahisha kuona kwamba idadi kubwa ya wahamaji hao, kutia ndani mimi, wamepata hazina za kiroho. Tulijifunza kwamba maisha yana kusudi na kwamba kumtumikia Yehova kunaleta shangwe kubwa ajabu.

[Picha katika ukurasa wa 32]

Karibu watu wote wa familia ya Ndugu Martínez ambao wako katika kweli