Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Upendo wa Kristo Unatuchochea Kupenda

Upendo wa Kristo Unatuchochea Kupenda

Upendo wa Kristo Unatuchochea Kupenda

“Yesu, akiwa amewapenda walio wake mwenyewe waliokuwa ulimwenguni, akawapenda mpaka mwisho.”—YOH. 13:1.

1, 2. (a) Kwa nini upendo ambao Yesu alionyesha ni wa pekee sana? (b) Ni mambo gani kuhusu upendo ambayo tutazungumzia katika habari hii?

YESU aliweka kielelezo kikamilifu cha upendo. Alionyesha upendo katika kila jambo alilofanya, yaani, usemi wake, mwenendo wake, mafundisho yake, na kifo chake cha kidhabihu. Mpaka kufikia mwisho wa maisha yake duniani, Yesu aliwaonyesha upendo wale aliokutana nao na hasa wanafunzi wake.

2 Mfano bora zaidi wa Yesu wa upendo uliwawekea wafuasi wake kiwango cha juu cha kufuata katika kuonyesha upendo. Mfano huo unatuchochea pia kuwapenda vivyo hivyo ndugu na dada zetu wa kiroho, na pia watu wengine wote. Katika habari hii, tutachunguza mambo ambayo wazee wa kutaniko wanaweza kujifunza kutokana na Yesu kuhusu kuwaonyesha upendo wale wanaofanya makosa, hata makosa mazito. Pia, tutazungumzia jinsi upendo wa Yesu unavyowachochea Wakristo kuwasaidia ndugu zao wanapokabili matatizo ya kiuchumi, misiba, na magonjwa.

3. Ingawa Petro alifanya makosa mazito, Yesu alimtendea jinsi gani?

3 Usiku uliotangulia kifo cha Yesu, mtume wake Petro alimkana mara tatu. (Marko 14:66-72) Hata hivyo, mara tu Petro alipokuwa amerudi, kama Yesu alivyotabiri, Yesu alimsamehe. Yesu alimkabidhi Petro madaraka mazito. (Luka 22:32; Mdo. 2:14; 8:14-17; 10:44, 45) Tunajifunza nini kutokana na mtazamo wa Yesu kuelekea watu wanaofanya makosa mazito?

Onyesha Mtazamo wa Akili wa Kristo Kuwaelekea Wakosaji

4. Tunahitaji kuonyesha mtazamo wa akili wa Kristo katika hali gani hasa?

4 Moja kati ya hali nyingi ambazo zinahitaji tuonyeshe mtazamo wa akili wa Kristo ni hali ambayo inaweza hasa kufadhaisha sana, yaani, wakati wengine wanapofanya makosa mazito, iwe ni katika familia au katika kutaniko. Inasikitisha kwamba siku za mwisho za mfumo wa Shetani zinapofikia kilele chake, roho ya ulimwengu inazidi kuwa mbaya zaidi kiadili. Mitazamo mibaya ya ulimwengu kuhusu yaliyo mabaya inaweza kuwa na uvutano juu ya yeyote kati yetu, na kudhoofisha azimio letu la kutembea kwenye njia nyembamba. Katika karne ya kwanza, watu fulani walitengwa na ushirika wa kutaniko la Kikristo, na wengine wakakaripiwa. Ndivyo ilivyo leo. (1 Kor. 5:11-13; 1 Tim. 5:20) Hata hivyo, wazee wanaoshughulikia mambo hayo wanapoonyesha upendo kama wa Kristo, wanaweza kumsaidia sana mkosaji.

5. Wazee wanapaswa kuiga jinsi gani mtazamo wa Kristo kuelekea wakosaji?

5 Kama Yesu, ni lazima wazee wategemeze viwango vya uadilifu vya Yehova nyakati zote. Wanapofanya hivyo, wanaonyesha upole, fadhili, na upendo wa Yehova. Mtu anapotubu kikweli, ‘anapovunjika moyo’ na ‘kupondeka roho’ kwa sababu ya kosa lake, huenda isiwe vigumu kwa wazee “kumrekebisha upya mtu huyo katika roho ya upole.” (Zab. 34:18; Gal. 6:1) Lakini namna gani wanaposhughulika na mtu mwasi ambaye anaonyesha huzuni kidogo au haonyeshi huzuni yoyote?

6. Wazee wanapaswa kuepuka nini wanaposhughulika na wakosaji, na kwa nini?

6 Mkosaji anapokataa shauri la Kimaandiko au anapojaribu kuwalaumu wengine kwa sababu ya kosa lake, huenda wazee na wengine wakakasirika. Wanapojua hasara ambayo mtu huyo tayari amesababisha, huenda wakajaribu kutoa maoni yao kuhusu matendo na mtazamo wake. Hata hivyo, hasira inasababisha madhara na haionyeshi “akili ya Kristo.” (1 Kor. 2:16; soma Yakobo 1:19, 20.) Yesu aliwaonya waziwazi watu fulani katika siku zake, lakini hakuwahi kamwe kusema jambo lolote lenye kuchukiza au lenye kuumiza. (1 Pet. 2:23) Badala yake, aliacha njia ikiwa wazi ili wakosaji watubu na kupata tena kibali cha Yehova. Kwa kweli, sababu moja kuu iliyomfanya Yesu aje ulimwenguni ilikuwa “kuwaokoa watenda-dhambi.”—1 Tim. 1:15.

7, 8. Ni nini kinachopaswa kuwaongoza wazee wanaposhughulikia mambo ya kihukumu?

7 Mfano wa Yesu katika kushughulika na wakosaji unapaswa kufinyanga jinsi gani mtazamo wetu kuelekea wale ambao wanatiwa nidhamu na kutaniko? Kumbuka kwamba mpango wa Kimaandiko wa kuwachukulia hatua ya kihukumu wakosaji katika kutaniko unalinda kundi na unaweza kumchochea mkosaji aliyetiwa nidhamu atubu. (2 Kor. 2:6-8) Inahuzunisha kwamba wengine hawatubu na hivyo wanatengwa na ushirika, hata hivyo inatia moyo kujua kwamba idadi kubwa ya watu hao baadaye wanamrudia Yehova na pia kutaniko lake. Wazee wanapoonyesha mtazamo kama wa Kristo, wanafanya iwe rahisi zaidi kwa mtu huyo kubadili moyo wake na mwishowe kurudi. Wakati ujao, huenda wengine kati ya watu hao waliofanya makosa zamani hawatakumbuka mashauri yote ya Kimaandiko ambayo wazee waliwapa, lakini bila shaka watakumbuka kwamba wazee waliwaheshimu na kuwatendea kwa upendo.

8 Kwa hiyo, ni lazima wazee waonyeshe “matunda ya roho,” hasa upendo kama wa Kristo, hata ikiwa wakosaji hawakubali mashauri ya Kimaandiko. (Gal. 5:22, 23) Hawapaswi kamwe kukimbilia kumtenga mkosaji na ushirika wa kutaniko. Wanapaswa kuonyesha kwamba wanataka wakosaji wamrudie Yehova. Hivyo, baadaye mtenda-dhambi anapobadili moyo wake, kama vile wengi wanavyofanya, huenda akamshukuru sana Yehova na pia “zawadi katika wanadamu” ambao walifanya iwe rahisi zaidi kwake kurudi katika kutaniko.—Efe. 4:8, 11, 12.

Kuonyesha Upendo Kama wa Kristo Wakati wa Mwisho

9. Toa mfano kuhusu jinsi Yesu alivyowaonyesha wanafunzi wake upendo kwa njia yenye kutokeza.

9 Luka anaeleza kuhusu wakati fulani ambapo Yesu alionyesha upendo kwa njia yenye kutokeza. Huku akijua mapema kwamba askari-jeshi Waroma wangezingira jiji la Yerusalemu ambalo lilihukumiwa maangamizi, na hivyo ingekuwa vigumu kukimbia, kwa upendo, Yesu aliwaonya wanafunzi wake hivi: “Mtakapoona Yerusalemu limezingirwa na majeshi yaliyopiga kambi, ndipo jueni kwamba kufanywa ukiwa kwake kumekaribia.” Walipaswa kufanya nini? Yesu alitoa mapema maagizo hususa yaliyo wazi. “Ndipo wale walio katika Yudea waanze kukimbilia milimani, na wale walio katikati yake na waondoke, nao wale walio katika sehemu za mashambani wasiingie ndani; kwa sababu hizi ni siku za kupatiliza haki, ili mambo yote yaliyoandikwa yatimizwe.” (Luka 21:20-22) Baada ya majeshi ya Roma kuzingira Yerusalemu mwaka wa 66 W.K., watu watiifu walifuata maagizo hayo.

10, 11. Kuchunguza kukimbia kwa Wakristo wa mapema kutoka Yerusalemu kunaweza kutusaidia jinsi gani kujitayarisha kwa ajili ya ile “dhiki kuu”?

10 Walipokuwa wakikimbia kutoka Yerusalemu, Wakristo walihitaji kuonyeshana upendo kama wa Kristo, jinsi tu Kristo alivyokuwa amewaonyesha upendo. Bila shaka, walihitaji kushiriki pamoja chochote walichokuwa nacho. Zaidi ya kuharibiwa kwa jiji hilo la kale, unabii wa Yesu ungetimizwa kwa njia iliyo kubwa zaidi. Alitabiri hivi: ‘Kutakuwa na dhiki kuu ya namna ambayo haijapata kutukia tangu mwanzo wa ulimwengu mpaka sasa, hapana, wala haitatukia.’ (Mt. 24:17, 18, 21) Kabla na wakati wa “dhiki kuu” hiyo ambayo iko mbele, sisi pia huenda tukakabili wakati mgumu na shida nyingi. Kuwa na mtazamo wa akili wa Kristo kutatusaidia kukabiliana na hali hizo.

11 Wakati huo, tutahitaji kufuata mfano wa Yesu, kuonyesha upendo usio wa kichoyo. Kupatana na hilo, Paulo alitoa shauri hili: “Kila mmoja wetu na ampendeze jirani yake katika yaliyo mema kwa ajili ya kujengwa kwake. Kwa maana hata Kristo hakujipendeza mwenyewe . . . Sasa Mungu anayetoa uvumilivu na faraja na awawezeshe ninyi kati yenu wenyewe kuwa na mtazamo uleule wa akili ambao Kristo Yesu alikuwa nao.”—Rom. 15:2, 3, 5.

12. Ni upendo wa aina gani ambao tunahitaji kusitawisha sasa, na kwa nini?

12 Petro, ambaye alionyeshwa upendo na Yesu, aliwahimiza vivyo hivyo Wakristo wasitawishe “upendo wa kindugu usio na unafiki” na kuonyesha ‘utii kwa ile kweli.’ Wanapaswa ‘kupendana sana kutoka moyoni.’ (1 Pet. 1:22) Leo, kuliko wakati mwingine wowote, tunahitaji kusitawisha hata zaidi sifa kama hizo za Kristo. Tayari, mikazo inaongezeka juu ya watu wote wa Mungu. Hakuna anayepaswa kuitumaini sehemu yoyote ya ulimwengu huu wa kale, kama msukosuko wa hivi karibuni wa kiuchumi ulimwenguni unavyoonyesha waziwazi. (Soma 1 Yohana 2:15-17.) Badala yake, mwisho wa mfumo huu unapokaribia sana tunahitaji kumkaribia zaidi Yehova na kuwakaribia waamini wenzetu, kwa kusitawisha urafiki wa kweli katika kutaniko. Paulo alishauri hivi: “Katika upendo wa kindugu iweni na upendo mwororo kwa mtu na mwenzake. Katika kuonyeshana heshima iweni wa kwanza.” (Rom. 12:10) Na Petro alikazia jambo hilo zaidi, aliposema: “Zaidi ya mambo yote, iweni na upendo mkubwa ninyi kwa ninyi, kwa sababu upendo hufunika dhambi nyingi.”—1 Pet. 4:8.

13-15. Ndugu fulani wameonyesha jinsi gani upendo kama wa Kristo baada ya misiba kutokea?

13 Ulimwenguni pote, Mashahidi wa Yehova wanajulikana kwa sababu wanaonyesha kwa matendo upendo wa kweli kama wa Kristo. Fikiria Mashahidi waliojitolea kusaidia baada ya dhoruba na vimbunga vilivyoharibu maeneo makubwa kusini mwa Marekani mwaka wa 2005. Wakichochewa na mfano wa Yesu, Mashahidi zaidi ya 20,000 walijitolea, na wengi wao waliacha nyumba nzuri na kazi nzuri ili kuwasaidia ndugu zao waliopatwa na misiba hiyo.

14 Katika eneo fulani, maji ya bahari yalifurika na kuingia umbali wa kilomita 80 kwenye nchi kavu, na kufanyiza ukuta wa maji wenye urefu wa mita 10. Maji yalipopungua, nyumba na majengo mengi katika eneo hilo yalikuwa yameharibiwa kabisa. Mashahidi waliokuwa na ustadi walijitolea kusaidia kutoka nchi nyingi, nao walikuja na vifaa na vyombo vya ujenzi kwenye eneo hilo na walikuwa tayari kufanya kazi yoyote ile iliyohitajiwa. Dada wawili wa kimwili ambao ni wajane, walipakia vitu vyao ndani ya gari dogo la mizigo na kuliendesha kwa umbali wa kilomita zaidi ya 3,000 ili kwenda kusaidia. Mmoja wa akina dada hao alibaki katika eneo hilo, na bado anaendelea kusaidia halmashauri ya kutoa misaada na anatumikia akiwa painia wa kawaida.

15 Nyumba zaidi ya 5,600 za Mashahidi na watu wengine wa eneo hilo zimejengwa upya au kurekebishwa. Mashahidi wa eneo hilo walihisi jinsi gani walipoonyeshwa upendo huo mkubwa sana? Dada mmoja ambaye nyumba yake ilibomolewa alihamia ndani ya gari dogo la kukokotwa lenye paa linalovuja na jiko lililovunjika. Ndugu walimjengea nyumba ndogo lakini maridadi. Akiwa amesimama mbele ya nyumba yake mpya maridadi, alitokwa na machozi ya shukrani kwa Yehova na kwa ndugu zake. Katika visa vingine vingi, Mashahidi wa eneo hilo waliohamishwa walibaki katika makao yao ya muda kwa mwaka mzima au zaidi baada ya nyumba zao kujengwa upya. Kwa nini? Ili wafanyakazi wa kujitolea wakae katika nyumba hizo mpya. Waliweka mfano mzuri kama nini katika kuonyesha mtazamo wa akili wa Kristo!

Kuonyesha Mtazamo wa Kristo Kuwaelekea Wagonjwa

16, 17. Ni katika njia gani tunaweza kuonyesha mtazamo wa akili wa Kristo kuelekea wagonjwa?

16 Ni wachache kati yetu ambao wamepatwa na msiba mkubwa wa kiasili. Hata hivyo, ni wazi kwamba ni lazima kila mmoja wetu akabiliane na matatizo ya afya, iwe ni yeye mwenyewe au washiriki wa familia yake. Mtazamo wa akili wa Yesu kuelekea wagonjwa ni mfano mzuri kwetu. Upendo wake ulimchochea kuwasikitikia. Umati ulipomletea wagonjwa, ‘aliwaponya wote waliokuwa na hali mbaya.’—Mt. 8:16; 14:14.

17 Leo, Wakristo hawana uwezo kama wa Yesu wa kuponya kimuujiza, lakini wanawahurumia wagonjwa kama alivyofanya Yesu. Wanaonyesha hivyo jinsi gani? Kwa mfano, wazee wanaonyesha kwamba wana mtazamo wa akili wa Kristo kwa kufanya mipango na kuhakikisha kwamba wagonjwa wanasaidiwa katika kutaniko, na hivyo kuonyesha kwamba wanafuata kanuni inayotajwa kwenye Mathayo 25:39, 40. * (Soma.)

18. Dada wawili walimwonyesha dada mwingine upendo wa kweli jinsi gani, na matokeo yalikuwa nini?

18 Bila shaka, si lazima mtu awe mzee wa kutaniko ili awafanyie wengine mema. Fikiria kisa cha Charlene mwenye umri wa miaka 44, ambaye alikuwa na kansa na aliambiwa kwamba angekufa baada ya siku kumi. Dada wawili wa kiroho, Sharon na Nicolette, walipoona uhitaji wake na jinsi mume wake alivyokuwa na kazi nyingi ya kumtunza, walijitolea kumsaidia wakati wote mpaka alipokufa. Aliendelea kuishi kwa muda wa majuma sita, lakini dada hao wawili walionyesha upendo wao mpaka mwisho. Sharon anasema hivi: “Ni vigumu unapojua kwamba mtu fulani hatapona. Hata hivyo, Yehova alitutia nguvu. Kisa hicho kilitufanya tumkaribie zaidi Yehova na tuwe na uhusiano wa karibu kati yetu.” Mume wa Charlene anasema: “Sikuzote nitakumbuka msaada wenye fadhili na unaofaa kutoka kwa dada hao wawili wapendwa. Nia yao nzuri na mtazamo wao mzuri ulifanya jaribu hilo la mwisho liwe rahisi zaidi kwa mke wangu mwaminifu Charlene na ulinisaidia kupata utulivu wa kimwili na wa kihisia ambao nilihitaji sana. Nitaendelea kuwashukuru milele. Kujidhabihu kwao kuliitia nguvu imani yangu kwa Yehova na upendo wangu kwa ushirika mzima wa ndugu zetu.”

19, 20. (a) Tumechunguza mambo gani matano kuhusu mtazamo wa akili wa Kristo? (b) Umeazimia kufanya nini?

19 Katika mfululizo huu wa makala tatu, tumechunguza mambo matano kuhusu mtazamo wa akili wa Yesu na jinsi tunavyoweza kuiga njia yake ya kufikiri na kutenda. Acheni tuwe ‘wenye tabia-pole na wanyenyekevu moyoni,’ kama Yesu alivyokuwa. (Mt. 11:29) Na tujitahidi pia kuwatendea wengine kwa fadhili hata ikiwa kutokamilika kwao na udhaifu wao unaonekana wazi. Acheni tutii kwa ujasiri matakwa yote ya Yehova, hata tunapokabili majaribu.

20 Mwishowe, acheni tuwaonyeshe ndugu zetu wote upendo “mpaka mwisho” kama Kristo alivyofanya. Upendo huo unatutambulisha kuwa wafuasi wa kweli wa Yesu. (Yoh. 13:1, 34, 35) Ndiyo, “upendo wenu wa kindugu na uendelee.” (Ebr. 13:1) Usisite kufanya hivyo! Tumia maisha yako kumsifu Yehova na kuwasaidia wengine! Yehova atabariki jitihada zako ukifanya hivyo kwa unyoofu.

[Maelezo ya chini]

^ fu. 17 Ona habari yenye kichwa “Fanya Zaidi ya Kusema Tu: ‘Ukaote Moto na Kushiba’” katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Oktoba 15, 1986 (15/10/1986).

Je, Unaweza Kueleza?

• Wazee wanaweza kuonyesha jinsi gani mtazamo wa Kristo kuelekea wakosaji?

• Kwa nini kuiga upendo wa Kristo ni jambo la maana hasa wakati huu wa mwisho?

• Tunaweza kuonyesha jinsi gani mtazamo wa akili wa Kristo kuelekea wagonjwa?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 17]

Wazee wanataka wakosaji wamrudie Yehova

[Picha katika ukurasa wa 18]

Wakristo waliokimbia kutoka Yerusalemu walionyesha mtazamo wa akili wa Kristo jinsi gani?

[Picha katika ukurasa wa 19]

Mashahidi wa Yehova wanajulikana kwa sababu wanaonyesha kwa matendo upendo kama wa Kristo