Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ibada ya Familia Ni ya Maana Ili Kuokoka!

Ibada ya Familia Ni ya Maana Ili Kuokoka!

Ibada ya Familia Ni ya Maana Ili Kuokoka!

WAZIA jinsi “vita vya ile siku kuu ya Mungu Mweza-Yote” vitakavyokuwa vyenye kuogopesha! (Ufu. 16:14) Akizungumza waziwazi kwa kutumia mifano, nabii Mika aliandika hivi: “Milima itayeyuka . . . , na nchi tambarare za chini zitapasuka, kama nta kwa sababu ya moto, kama maji yanayomwagwa kwenye mteremko mkali.” (Mika 1:4) Watu ambao hawamtumikii Yehova watapatwa na matokeo gani mabaya? Neno la Mungu linasema: “Wale waliouawa na Yehova siku hiyo hakika watakuwa kutoka mwisho mmoja wa dunia mpaka mwisho wa pili wa dunia.”—Yer. 25:33.

Wakikumbuka maonyo kama hayo, vichwa vya familia, ambao wengi wao ni wazazi wasio na wenzi, wanapaswa kujiuliza swali hili kuhusu watoto wao ambao wana umri wa kutosha kufikiria, ‘Je, wataokoka Har–Magedoni?’ Biblia inatuhakikishia kwamba wataokoka ikiwa watakuwa na uhusiano wa karibu sana pamoja na Yehova kadiri inavyotegemea umri wao.—Mt. 24:21.

Umuhimu wa Kutenga Wakati wa Ibada ya Familia

Ukiwa mzazi, hakikisha kwamba unafanya yote unayoweza ili kuwalea watoto wako “katika nidhamu na mwongozo wa akilini wa Yehova.” (Efe. 6:4) Kujifunza Biblia pamoja na watoto wako ni jambo la maana sana. Tungependa vijana wetu wawe kama Wakristo huko Filipi, ambao walipongezwa na Paulo kwa sababu walimtii Yehova kwa kupenda. Aliandika hivi: “Wapendwa wangu, kwa jinsi ambavyo mmekuwa mkitii sikuzote, si wakati wa kuwapo kwangu tu, bali kwa utayari zaidi sasa wakati wa kutokuwapo kwangu, endeleeni kuufanyia kazi wokovu wenu wenyewe kwa kuogopa na kutetemeka.”—Flp. 2:12.

Je, watoto wako wanatii sheria za Yehova wanapokuwa peke yao? Namna gani wanapokuwa shuleni? Unaweza kuwasaidia jinsi gani watoto wako wasadiki hekima iliyo katika sheria za Yehova ili wazifuate wanapokuwa peke yao?

Ibada ya familia inaweza kusaidia sana katika kujenga imani ya mtoto wako ili amtii Yehova hata anapokuwa peke yake. Hivyo basi, tutazungumzia mambo matatu ya maana katika kufanikisha funzo lenu la Biblia la familia.

Ongoza Funzo la Familia kwa Ukawaida

Biblia inaonyesha kwamba wana wa Mungu wa kimalaika wanaalikwa mbele yake wakati fulani uliowekwa. (Ayu. 1:6) Fanya vivyo hivyo pamoja na watoto wako. Tenga siku na wakati hususa kwa ajili ya jioni ya Ibada yenu ya Familia na uhakikishe kwamba unafuata kabisa ratiba hiyo. Kwa kuongezea, tenga wakati mwingine ambao mnaweza kujifunza ratiba yenu inapovurugwa na jambo lisilotazamiwa.

Kadiri miezi inavyopita, msiwe kamwe na mtazamo wa kwamba ni sawa tu kukosa funzo la Biblia la familia mara kwa mara. Kumbuka kwamba, watoto wako ndio wanafunzi wako wa Biblia wa maana zaidi. Hata hivyo, Shetani angependa kuwawinda. (1 Pet. 5:8) Usipotumia jioni hiyo ya maana sana kwa ajili ya Ibada ya Familia na badala yake iwe ya kutazama televisheni au kufanya mambo mengine yasiyo ya maana sana, Shetani atakuwa ameshinda.—Efe. 5:15, 16; 6:12; Flp. 1:10.

Fanya Funzo Liwe Lenye Faida

Jioni ya Ibada ya Familia haipaswi kuwa tu wakati wa kusoma mambo yaliyoandikwa. Jitahidi kufanya funzo hilo liwe lenye faida. Jinsi gani? Nyakati nyingine, chagua habari inayohusu mambo ambayo mtoto wako atakabili siku au majuma yanayofuata. Kwa mfano, kwa nini usitie ndani vipindi vya kufanya mazoezi ya kuhubiri? Watoto wanafurahia mambo ambayo wanafanya vizuri. Kujizoeza jinsi ya kuanzisha mazungumzo na kufikiria njia za kushughulikia vipingamizi kutawasaidia wawe na uhakika zaidi wanapotumia njia mbalimbali za kuhubiri kuhusu Ufalme.—2 Tim. 2:15.

Pia, mnaweza kuwa na vipindi vya mazoezi ambavyo vitawasaidia watoto wako kukabiliana na shinikizo la marafiki. Sura ya 15 ya kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2, inaweza kutumiwa kama msingi wa mazungumzo ya familia. Sehemu yenye kichwa “Kukabiliana na Mkazo” iliyo kwenye ukurasa wa 132 na 133 inatoa mapendekezo na pia inamruhusu mtoto wako atayarishe majibu ambayo anahisi kwamba yanamfaa. Sentensi iliyo mwishoni mwa ukurasa wa 133 inawahimiza hivi vijana: “Ukiwa na mzazi au rafiki mkomavu, fanya mazoezi naye.” Kwa nini mara kwa mara usifanye vipindi hivyo vya mazoezi viwe sehemu ya Ibada yenu ya Familia?

Ibada ya familia inawapa wazazi nafasi ya kukazia faida za kuwa na miradi ya kiroho. Kuhusu jambo hilo, kitabu Vijana Huuliza, Buku la 2, kina habari nzuri sana kwenye sura ya 38, yenye kichwa “Nitayatumiaje Maisha Yangu?” Mnapozungumzia sura hiyo, msaidie mtoto wako atambue kwamba kukazia fikira utumishi wa Yehova maishani, ndiyo njia bora zaidi ya maisha. Sitawisha katika moyo wa mtoto wako tamaa ya kuwa painia, kutumika Betheli, kuhudhuria Shule ya Mazoezi ya Kihuduma, au kufuatia aina nyingine ya utumishi wa wakati wote.

Onyo: Wazazi fulani ambao wangependa mtoto wao afanikiwe wanakazia fikira sana mambo ambayo wanataka mtoto wao atimize hivi kwamba wanasahau kumpongeza kwa sababu ya mambo ambayo tayari anatimiza. Bila shaka, ni vizuri kuwatia moyo watoto wako wajiwekee miradi inayofaa kama vile utumishi wa Betheli na kazi ya umishonari. Lakini, unapofanya hivyo, uwe mwangalifu ili usimkasirishe mtoto wako kwa sababu ya mambo unayotaka atimize na hivyo kumfanya avunjike moyo. (Kol. 3:21) Sikuzote kumbuka kwamba ni lazima mwishowe mwana au binti yako ampende Yehova kwa moyo wake, bali si moyo wako. (Mt. 22:37) Basi tafuta nafasi za kumpongeza mtoto wako kwa sababu ya mambo anayofanya vizuri, na uepuke mwelekeo wa kukazia fikira mambo ambayo hafanyi. Msaidie athamini mambo yote ambayo Yehova amefanya. Kisha acha moyo wa mtoto wako uchochewe na wema wa Yehova.

Fanya Funzo la Familia Lifurahishe

Jambo la tatu ambalo ni la maana ili kufanikisha jioni ya Ibada ya Familia ni kuifanya iwe yenye kufurahisha. Unaweza kufanya hivyo jinsi gani? Labda pindi fulani mnaweza kusikiliza drama au kutazama na kuzungumzia mojawapo ya video zilizotolewa na Mashahidi wa Yehova. Au mnaweza kusoma pamoja sehemu ya Biblia, na umgawie kila mshiriki wa familia asome sehemu ya mhusika fulani.

Kuna sehemu fulani katika magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! ambazo zina habari nzuri sana za kuzungumzia katika familia. Kwa mfano, mnaweza kutumia sehemu iliyo kwenye ukurasa wa 31 wa kila gazeti la Amkeni! yenye kichwa “Ungejibuje?” Katika matoleo fulani ya gazeti la watu wote la Mnara wa Mlinzi kuna sehemu ya utafiti yenye kichwa “Kwa Ajili ya Vijana Wetu.” Zaidi ya mazoezi hayo ya kufanya utafiti, pia matoleo fulani yana habari kwa ajili ya watoto wenye umri mdogo yenye kichwa “Wafundishe Watoto Wako.”

Katika gazeti la Amkeni! habari zilizo kwenye sehemu yenye kichwa “Vijana Huuliza” zitawafaa zaidi wazazi walio na vijana matineja, kama ilivyo pia na kitabu Vijana Huuliza, Buku la 2. Mnapotumia kitabu hicho, msipuuze sanduku lenye kichwa “Una Maoni Gani?” lililo mwishoni mwa kila sura. Sanduku hilo halikusudiwi tu kurudia mambo makuu. Maswali yaliyo katika sanduku hilo yanaweza kutumiwa kama msingi wa mazungumzo ya familia.

Hata hivyo, uwe mwangalifu ili usibadili funzo la familia kuwa kipindi cha kumhoji mtoto. Kwa mfano, usijaribu kumlazimisha mtoto wako asome kwa sauti mambo ambayo ameandika katika kurasa zenye kichwa “Daftari” au katika sehemu nyingine za kitabu hicho zinazomwomba aandike maoni yake. Katika sehemu iliyo kwenye ukurasa wa 3 yenye kichwa, “Taarifa kwa Wazazi,” kitabu hicho kinasema hivi: “Ili vijana wenu waandike majibu yao kwa unyoofu, acheni walichoandika katika nakala zao kiwe siri yao. Baadaye, huenda wakawa huru kuzungumza nanyi kuhusu mambo ambayo wameandika.”

Ikiwa utaongoza ibada yako ya familia kwa ukawaida, na kuifanya iwe yenye faida, na yenye kufurahisha, Yehova atabariki sana jitihada zako. Wakati huo wa pekee sana katika familia utasaidia wapendwa wako waendelee kuwa hai na wenye nguvu kiroho.

[Sanduku katika ukurasa wa 31]

Tumia Njia Mbalimbali

“Tulipokuwa tukijifunza na mabinti wetu wachanga, mimi na mume wangu tulizungumzia habari ambazo tungetumia katika kutayarisha mikutano ya kutaniko kisha tuliwaomba wasichana wetu wachore picha inayoonyesha mambo makuu ya habari tuliyozungumzia. Nyakati nyingine, tuliigiza matukio yaliyo katika Biblia au tulikuwa na vipindi vya mazoezi ya kuhubiri. Sikuzote tulifanya funzo lifaane na umri wao, lipendeze, liwe lenye kujenga, na lenye kufurahisha.”—J.M., Marekani.

“Ili kumsaidia mwana wa mwanafunzi wangu wa Biblia aelewe jinsi kitabu cha kukunjwa kilivyotumiwa nyakati za Biblia, tulichapisha kitabu cha Isaya bila nambari za sura na mistari. Tuliunganisha kurasa zote na tukaweka bomba dogo kwenye kila mwisho. Kisha mvulana huyo alijaribu kufanya kama Yesu alivyofanya katika sinagogi huko Nazareti. Simulizi lililo kwenye Luka 4:16-21 linasema kwamba Yesu ‘akakifungua [kitabu cha kukunjwa cha Isaya] na kupata’ sehemu aliyokuwa akitafuta. (Isa. 61:1, 2) Hata hivyo, mvulana huyo alipojaribu kufanya kama Yesu alivyofanya, alishindwa kupata Isaya 61 kwenye karatasi hiyo ndefu isiyo na nambari za sura na mistari. Akiwa amependezwa na ustadi wa Yesu wa kufungua vitabu vya kukunjwa, mvulana huyo alisema hivi kwa mshangao: ‘Yesu alikuwa mtu wa ajabu!’”—Y.T., Japani.

[Picha katika ukurasa wa 30]

Vipindi vya mazoezi vinaweza kuwasaidia watoto wako kukabiliana na shinikizo la marafiki

[Picha katika ukurasa wa 31]

Jitahidi kufanya jioni ya Ibada ya Familia iwe yenye kufurahisha