Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Iweni Wenye Kufanya Amani na Watu Wote”

“Iweni Wenye Kufanya Amani na Watu Wote”

“Iweni Wenye Kufanya Amani na Watu Wote”

“Ikiwezekana, kwa kadiri inavyowategemea ninyi, iweni wenye kufanya amani na watu wote.”—ROM. 12:18.

1, 2. (a) Yesu aliwapa wafuasi wake onyo gani? (b) Tunaweza kupata wapi mashauri yanayoonyesha jinsi ya kukabiliana na upinzani?

YESU aliwaonya wafuasi wake kwamba wangepingwa na mataifa ya ulimwengu, na jioni iliyotangulia kifo chake, aliwaeleza sababu. Aliwaambia mitume wake hivi: “Kama mngekuwa sehemu ya ulimwengu, ulimwengu ungependa kilicho chake. Sasa kwa sababu ninyi si sehemu ya ulimwengu, bali nimewachagua ninyi kutoka ulimwenguni, kwa sababu hiyo ulimwengu unawachukia ninyi.”—Yoh. 15:19.

2 Mtume Paulo alijionea ukweli wa maneno hayo ya Yesu. Katika barua yake ya pili kwa Timotheo, kijana aliyeambatana naye, Paulo aliandika hivi: “Wewe umefuata kwa ukaribu fundisho langu, mwendo wangu wa maisha, kusudi langu, imani yangu, ustahimilivu wangu, upendo wangu, uvumilivu wangu, mateso yangu, masumbufu yangu.” Kisha Paulo akaongezea hivi: “Kwa kweli, wote wanaotamani kuishi kwa ujitoaji-kimungu katika ushirika na Kristo Yesu watateswa pia.” (2 Tim. 3:10-12) Katika sura ya 12 ya barua yake kwa Wakristo huko Roma, Paulo alitoa mashauri yenye hekima yaliyoonyesha jinsi walivyopaswa kukabiliana na upinzani. Maneno yake yanaweza kutupatia mwongozo katika wakati huu wa mwisho.

“Fanyeni Mambo Mema”

3, 4. Shauri la Waroma 12:17 linaweza kutumiwa jinsi gani (a) katika familia iliyogawanyika kidini? (b) tunaposhughulika na majirani?

3 Soma Waroma 12:17. Paulo alieleza kwamba tunapochukiwa, hatupaswi kulipiza kisasi. Ni jambo la maana sana kwa washiriki wa familia zilizogawanyika kidini kutii shauri hilo la Paulo. Mwenzi wa ndoa Mkristo anapinga kishawishi cha kulipiza kisasi kwa kuepuka kusema maneno yasiyo ya fadhili au kutenda bila fadhili. Hakuna faida yoyote ya ‘kulipa uovu kwa uovu.’ Badala yake, mtazamo kama huo unaweza tu kufanya hali iwe mbaya zaidi.

4 Paulo anapendekeza jambo bora la kufanya: “Fanyeni mambo mema machoni pa watu wote.” Ikiwa mume asiye mwamini anasema mambo mabaya kuhusu imani ya mke wake ambaye ni mwamini, mke huyo anaweza kuzuia ugomvi mbaya sana usitokee nyumbani kwa kumwonyesha mume wake fadhili za kweli. (Met. 31:12) Carlos, ambaye sasa ni mshiriki wa familia ya Betheli, anasimulia jinsi ambavyo mama yake alishinda upinzani mkali sana kutoka kwa baba yake kwa kuendelea kuonyesha fadhili na kuitunza nyumba vizuri. “Alitutia moyo sisi watoto tumheshimu baba sikuzote. Alisisitiza kwamba nicheze na baba mchezo wa Kifaransa wa kuviringisha mipira chini (boules) hata ingawa sikupenda mchezo huo. Lakini hilo lilimfurahisha baba.” Mwishowe alianza kujifunza Biblia kisha akabatizwa. Kuhusu ‘kufanya mambo mema machoni pa watu wote,’ mara nyingi Mashahidi wa Yehova wameshinda chuki kwa kuwasaidia majirani wao wakati wa misiba.

Kuyeyusha Upinzani kwa “Makaa Yenye Moto”

5, 6. (a) Ni katika maana gani “makaa yenye moto” yanakusanywa juu ya kichwa cha adui? (b) Simulia jambo la kwenu lililoonwa ambalo linaonyesha jinsi kufuata shauri la Waroma 12:20 kunavyoweza kuwa na matokeo mazuri.

5 Soma Waroma 12:20. Bila shaka, Paulo alipochagua maneno yaliyo katika mstari huo, alikuwa akifikiria yale tunayosoma kwenye Methali 25:21, 22: “Ikiwa mtu anayekuchukia ana njaa, mpe mkate ale; na ikiwa ana kiu, mpe maji anywe. Kwa maana unakusanya makaa ya moto juu ya kichwa chake, na Yehova mwenyewe atakupa thawabu.” Paulo alipotoa shauri lililo katika Waroma sura ya 12, hakumaanisha kwamba makaa hayo ya mfano ni ya kumwadhibu au kumwaibisha mpinzani. Badala yake, inaonekana kwamba maneno ya methali hiyo pamoja na yale ambayo Paulo aliwaandikia Waroma, yalihusu njia iliyotumiwa zamani ya kuyeyusha mawe yenye chuma. Msomi Mwingereza wa karne ya 19, Charles Bridges alisema hivi: “Funika kabisa chuma kigumu juu na chini kwa kukusanya makaa yenye moto juu yake, na ukiweke chuma hicho juu ya moto. Ni mioyo michache sana iliyo migumu hivyo, ambayo haiwezi kuyeyushwa na nguvu nyingi sana za upendo wenye subira, unaojinyima, na wenye kuchoma.”

6 Sawa na “makaa yenye moto,” matendo ya fadhili yanaweza kuchochea mioyo ya wapinzani na labda kuyeyusha chuki yao. Matendo ya fadhili yanaweza kuwavutia watu na kuwafanya wawe na mtazamo mzuri kuelekea watu wa Yehova na ujumbe wa Biblia ambao wanahubiri. Mtume Petro aliandika hivi: “Dumisheni mwenendo wenu ukiwa mzuri katikati ya mataifa, ili, katika jambo ambalo wanasema juu yenu ya kuwa ninyi ni watenda-maovu, waweze, likiwa tokeo la matendo yenu mazuri ambayo wameshuhudia kwa macho, kumtukuza Mungu katika siku ya ukaguzi wake.”—1 Pet. 2:12.

‘Fanya Amani na Watu Wote’

7. Amani ambayo Kristo anawaachia wanafunzi wake ni nini, na inapaswa kutuchochea kufanya nini?

7 Soma Waroma 12:18. Katika jioni ya mwisho ambayo Yesu alikuwa pamoja na mitume wake, aliwaambia hivi: “Ninawaachia ninyi amani, ninawapa amani yangu.” (Yoh. 14:27) Amani ambayo Kristo anawaachia wanafunzi wake ni utulivu wa moyoni ambao wanapata wakati wanapohisi kwamba wanapendwa na kukubaliwa na Yehova Mungu na Mwana wake mpendwa. Amani hiyo ya moyoni inapaswa kutuchochea kuishi na wengine kwa amani. Wakristo wa kweli ni wapenda-amani na wafanya-amani.—Mt. 5:9.

8. Tunaweza jinsi gani kuwa wafanya-amani nyumbani na katika kutaniko letu?

8 Njia moja ya kuwa mfanya-amani katika familia ni kutatua haraka iwezekanavyo hali yoyote ya kutoelewana badala ya kuruhusu hali hizo ziwe mbaya zaidi. (Met. 15:18; Efe. 4:26) Hilo linahusu pia kutaniko la Kikristo. Mtume Petro anaonyesha kwamba kufuatia amani kunahusiana na kuuzuia ulimi. (1 Pet. 3:10, 11) Yakobo pia, baada ya kutoa shauri kali kuhusu kuutumia vizuri ulimi na uhitaji wa kuepuka wivu na ugomvi, aliandika hivi: “Hekima inayotoka juu kwanza kabisa ni safi kiadili, kisha yenye kufanya amani, yenye usawaziko, tayari kutii, yenye kujaa rehema na matunda mema, haifanyi tofauti zenye ubaguzi, si ya kinafiki. Zaidi ya hayo, mbegu ya tunda la uadilifu hupandwa chini ya hali zenye amani kwa wale wanaofanya amani.”—Yak. 3:17, 18.

9. Tunapaswa kukumbuka nini tunapojitahidi “kufanya amani na watu wote”?

9 Katika maneno yake yaliyo kwenye Waroma 12:18, Paulo anaonyesha kwamba haitoshi tu kufanya amani katika familia na katika kutaniko. Anasema kwamba tunapaswa “kufanya amani na watu wote.” Hilo linatia ndani majirani, wafanyakazi wenzetu, wanashule wenzetu, na watu tunaokutana nao katika huduma yetu ya hadharani. Hata hivyo, mtume Paulo anafafanua zaidi shauri lake kwa kusema hivi: “Ikiwezekana, kwa kadiri inavyowategemea ninyi.” Hilo linamaanisha kujitahidi kadiri tunavyoweza ili “kufanya amani na watu wote” lakini hatupaswi kulegeza kanuni za Mungu za uadilifu.

Kisasi Ni cha Yehova

10, 11. ‘Tunaiachia nafasi ghadhabu’ katika maana gani, na kwa nini hilo linafaa?

10 Soma Waroma 12:19. Hata tunaposhughulika na “wale wasio na mwelekeo unaofaa” kuhusu kazi yetu na ujumbe wetu, kutia ndani wale wanaotupinga moja kwa moja, tutaendelea “kujizuia chini ya uovu” na kutenda kwa “upole.” (2 Tim. 2:23-25) Paulo anawashauri Wakristo wasijilipizie kisasi lakini ‘waiachie nafasi ghadhabu.’ Paulo anazungumzia ghadhabu gani? Hakumaanisha kamwe kwamba tunapaswa kumwaga ghadhabu yetu wenyewe. Kwa wazi, tunaiachia nafasi ghadhabu ya Mungu. Tukiwa Wakristo, tunajua kwamba si daraka letu kulipiza kisasi. Mtunga-zaburi aliandika hivi: “Acha hasira na uache ghadhabu; usijionyeshe umewaka hasira ili tu kufanya uovu.” (Zab. 37:8) Naye Sulemani alishauri hivi: “Usiseme: ‘Nitalipiza uovu!’ Mtumaini Yehova, naye atakuokoa.”—Met. 20:22.

11 Jambo la hekima la kufanya wakati wapinzani wanapotuumiza ni kumwacha Yehova aamue ikiwa atawaadhibu na pia aamue wakati unaofaa wa kufanya hivyo. Ili kuonyesha kwamba alikuwa akizungumza kuhusu ghadhabu ya Yehova, Paulo aliongezea hivi: “Imeandikwa: ‘Kisasi ni changu; mimi nitalipa, asema Yehova.’” (Linganisha na Kumbukumbu la Torati 32:35.) Ikiwa tungejaribu kujilipizia kisasi, tungekuwa tukitenda kwa kimbelembele, na kuchukua daraka la Yehova. Kwa kuongezea, tukifanya hivyo tutakuwa tukionyesha kwamba hatuamini ahadi hii ya Yehova: “Mimi nitalipa.”

12. Ghadhabu ya Yehova itafunuliwa wakati gani, na jinsi gani?

12 Mapema katika barua yake kwa Waroma, Paulo alisema hivi: “Ghadhabu ya Mungu inafunuliwa kutoka mbinguni juu ya watu wote wasiomwogopa Mungu na wasio waadilifu ambao wanaikandamiza kweli katika njia isiyo ya uadilifu.” (Rom. 1:18) Ghadhabu ya Yehova itafunuliwa kutoka mbinguni kupitia Mwana wake wakati wa “ile dhiki kuu.” (Ufu. 7:14) Hilo litakuwa “uthibitisho wa hukumu ya uadilifu ya Mungu,” kama Paulo alivyoeleza katika moja ya barua zake zilizoongozwa na roho takatifu: “Hii inazingatia kwamba ni jambo la uadilifu kwa upande wa Mungu kuwalipa dhiki wale wanaowafanyia ninyi dhiki, lakini, kwenu ninyi mnaopata dhiki, kitulizo pamoja nasi wakati wa ufunuo wa Bwana Yesu kutoka mbinguni pamoja na malaika zake wenye nguvu katika mwali wa moto, anapoleta kisasi juu ya wale wasiomjua Mungu na wale wasiotii habari njema juu ya Bwana wetu Yesu.”—2 The. 1:5-8.

Kuushinda Uovu kwa Wema

13, 14. (a) Kwa nini hatushangai tunapopata upinzani? (b) Tunaweza kuwabariki jinsi gani wale wanaotutesa?

13 Soma Waroma 12:14, 21. Tukiwa na uhakika kabisa kwamba Yehova atatimiza ahadi zake, tunaweza bila wasiwasi kutumia nguvu zetu zote katika kazi ambayo ametupatia, kazi ya kuhubiri ‘habari njema ya ufalme katika dunia yote inayokaliwa.’ (Mt. 24:14) Tunajua kwamba utendaji huo wa Kikristo utaamsha hasira ya maadui wetu, kwa kuwa Yesu alituonya hivi: “Mtachukiwa na mataifa yote kwa sababu ya jina langu.” (Mt. 24:9) Kwa hiyo, hatushangai wala kuvunjika moyo tunapopata upinzani. Mtume Petro aliandika hivi: “Wapendwa, msishangazwe juu ya moto unaowaka katikati yenu, unaowapata ninyi ili kuwa jaribu, kana kwamba jambo geni linawapata. Kinyume chake, endeleeni kushangilia kwa maana ninyi ni washiriki katika mateso ya Kristo.”—1 Pet. 4:12, 13.

14 Badala ya kuwachukia wale wanaotutesa, tunajitahidi kuwafundisha, huku tukitambua kwamba huenda wengine wao wanatenda hivyo kwa kutojua. (2 Kor. 4:4) Tunajitahidi kutii shauri hili la Paulo: “Endeleeni kuwabariki wale wanaowatesa; muwe mkibariki wala msiwe mkilaani.” (Rom. 12:14) Njia moja ya kuwabariki wapinzani wetu ni kusali kwa ajili yao. Yesu alisema hivi katika Mahubiri yake ya Mlimani: “Endeleeni kuwapenda adui zenu, kuwafanyia mema wale wanaowachukia, kuwabariki wale wanaowalaani, kusali kwa ajili ya wale wanaowatusi.” (Luka 6:27, 28) Mtume Paulo alijua kutokana na maisha yake mwenyewe kwamba mtesaji anaweza kugeuka na kuwa mwanafunzi mwaminifu wa Kristo na mtumishi mwenye bidii wa Yehova. (Gal. 1:13-16, 23) Katika barua nyingine, Paulo alisema: “Tunapotukanwa, tunabariki; tunapoteswa, tunavumilia; tunapoharibiwa sifa, tunasihi.”—1 Kor. 4:12, 13.

15. Ni njia gani bora ya kuushinda uovu kwa wema?

15 Hivyo basi, Mkristo wa kweli anatii maneno ya mstari wa mwisho wa Waroma sura ya 12: “Usiache ushindwe na uovu, bali endelea kuushinda uovu kwa wema.” Chanzo cha uovu wote ni Shetani Ibilisi. (Yoh. 8:44; 1 Yoh. 5:19) Katika ufunuo ambao mtume Yohana alipewa, Yesu alifunua kwamba ndugu zake watiwa-mafuta ‘wamemshinda [Shetani] kwa sababu ya damu ya Mwana-Kondoo na kwa sababu ya neno la kutoa kwao ushahidi.’ (Ufu. 12:11) Hilo linaonyesha kwamba njia bora ya kumshinda Shetani na uvutano wake mwovu juu ya mfumo wa sasa wa mambo ni kwa kufanya mema kupitia kazi yetu ya kutoa ushahidi na kuhubiri habari njema ya Ufalme.

Kushangilia Katika Tumaini

16, 17. Andiko la Waroma sura ya 12 limetufundisha nini kuhusu (a) jinsi tunavyopaswa kutumia maisha yetu? (b) jinsi tunavyopaswa kutenda katika kutaniko? (c) jinsi tunavyopaswa kuwatendea watu ambao wanapinga imani yetu?

16 Mazungumzo yetu mafupi kuhusu sura ya 12 ya barua ya Paulo kwa Wakristo huko Roma yametukumbusha mambo mengi. Tumejifunza kwamba tukiwa watumishi waliojiweka wakfu kwa Yehova, tunapaswa kuwa tayari kujidhabihu. Huku tukichochewa na roho ya Mungu, tunatoa dhabihu hizo kwa kupenda kwa sababu nguvu zetu za kufikiri zimetusadikisha kwamba hayo ni mapenzi ya Mungu. Tunawaka roho na kutumia zawadi zetu mbalimbali kwa bidii. Tunatumika kwa unyenyekevu wote na kiasi, na kufanya yote tunayoweza ili kulinda umoja wetu wa Kikristo. Tunafuata mwendo wa ukaribishaji-wageni na kuonyesha hisia-mwenzi ya kweli.

17 Andiko la Waroma sura ya 12 linatupatia pia mashauri mengi kuhusu jinsi tunavyopaswa kukabiliana na upinzani. Hatupaswi kulipiza kisasi. Tunapaswa kujitahidi kuushinda upinzani kwa matendo ya fadhili. Tunapaswa kujitahidi sana kuishi kwa amani na watu wote kwa kadiri inavyowezekana, bila kuvunja kanuni za Biblia. Tunapaswa kufanya hivyo katika familia, katika kutaniko, kuelekea majirani wetu, kazini, shuleni, na katika huduma yetu ya hadharani. Hata tunapokabili upinzani wa moja kwa moja, tunajitahidi kabisa kuushinda uovu kwa wema, huku tukikumbuka kwamba kisasi ni cha Yehova.

18. Ni mashauri gani matatu yanayotolewa kwenye Waroma 12:12?

18 Soma Waroma 12:12. Kwa kuongezea mashauri hayo yote yenye hekima na yenye faida, Paulo anatoa mashauri mengine matatu. Kwa kuwa hatuwezi kamwe kufanya mambo hayo yote bila msaada wa Yehova, mtume Paulo anatushauri ‘tudumu katika sala.’ Hilo litatuwezesha kufuata shauri lake lingine la ‘kuvumilia chini ya dhiki.’ Mwishowe, tunahitaji kukazia akili zetu wakati ujao ambao Yehova ametuahidi na ‘kushangilia katika tumaini’ la uzima wa milele, iwe ni mbinguni au duniani.

Kwa Kupitia

• Tunapaswa kukabiliana jinsi gani na upinzani?

• Tunapaswa kujitahidi kufanya amani katika sehemu gani, na jinsi gani?

• Kwa nini hatupaswi kujilipizia kisasi?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 8]

Kuwasaidia majirani wetu kunaweza kutusaidia kushinda chuki yao

[Picha katika ukurasa wa 9]

Je, unajitahidi kuwa mfanya-amani katika kutaniko?