Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Umetenga Wakati wa Kujifunza Biblia?

Je, Umetenga Wakati wa Kujifunza Biblia?

Je, Umetenga Wakati wa Kujifunza Biblia?

MWAKA jana, Baraza Linaloongoza lilitangaza badiliko katika ratiba ya mikutano ya kutaniko, ambalo limetuwezesha kupata wakati zaidi wa kujifunza na kuzungumzia Biblia katika familia. Ikiwa wewe ni kichwa cha familia, hakikisha kwamba unaongoza kwa ukawaida funzo la Biblia la familia lenye kujenga pamoja na mke na watoto wako. Wenzi wa ndoa ambao hawana watoto wanaweza kutumia wakati huo kujifunza Biblia pamoja. Ndugu na dada waseja ambao hawana madaraka ya familia wanaweza kutumia wakati huo inavyofaa kwa ajili ya funzo la Biblia la kibinafsi.

Wengi wameshukuru kwa sababu ya mpango wa kuwa na jioni ya Ibada ya Familia. Kwa mfano, Kevin, ambaye ni mzee wa kutaniko, aliandika hivi: “Neno ‘asante’ halitoshi kueleza jinsi tunavyohisi katika kutaniko. Nikiwa pamoja na wazee wenzangu, tumezungumzia jinsi tunavyotumia jioni hiyo ya ziada kufanya jambo ambalo Baraza Linaloongoza lilituomba tufanye, yaani, kujifunza pamoja na familia zetu.”

Jodi, ambaye mume wake ni mzee wa kutaniko, aliandika hivi: “Tuna mabinti watatu walio na umri wa miaka 15, 11, na 2. Hivi majuzi tulihamia kutaniko la lugha ya ishara. Tunatumia muda na jitihada nyingi ili kujitayarisha kwa ajili ya mikutano yote. Sasa, kwa sababu ya badiliko hilo, tuna jioni ya ziada ya kukazia fikira ibada yetu ya familia!”

John na JoAnn, wenzi wa ndoa ambao wanatumika wakiwa mapainia wa kawaida, waliandika hivi: “Mara nyingi, funzo letu la Biblia la familia halikuwa la kawaida kwa sababu tulihitaji kulifanya pamoja na shughuli mbalimbali za kutaniko. Mpango huo mpya ni zawadi kutoka kwa Yehova ambayo inatuburudisha kiroho, tunapotumia wakati huo kufanya jambo ambalo tunapaswa kufanya.”

Tony, ndugu mseja mwenye umri wa miaka 20 na kitu, ametenga Jumanne (Siku ya 2) jioni kuwa wakati wa kujifunza kibinafsi. Anatumia pindi nyingine katika juma kutayarisha mikutano ya kutaniko. Hata hivyo, Tony anasema, “Ninasubiri kwa hamu siku ya Jumanne.” Kwa nini? “Jioni hiyo ni wakati wangu wa pekee wa kuwa na Yehova.” Tony anaeleza hivi: “Kwa karibu saa mbili, ninajifunza mambo ambayo yanaimarisha uhusiano wangu pamoja na Yehova. Ninapokuwa na muda mwingi wa kujifunza, ninakuwa na wakati wa kutafakari mistari ya Biblia ninayosoma.” Matokeo yamekuwa nini? “Mashauri ya Yehova yanapenya ndani zaidi ya moyo wangu kuliko hapo mbeleni.” Je, anaweza kutoa mfano wowote? “Katika kitabu Insight, nilisoma kuhusu urafiki kati ya Daudi na Yonathani. Nilijifunza mengi kutokana na mtazamo wa Yonathani usio wa kichoyo. Mfano wake ulinisaidia kuelewa vizuri zaidi kinachomaanishwa na kuwa rafiki wa kweli. Ninasubiri kwa hamu kupata habari nyingine zenye thamani kama hizo kila siku ya Jumanne jioni!”

Bila shaka, watumishi wote wa Yehova watafaidika sana wakitumia vizuri wakati wa ziada ambao tunao sasa wa kuwa na funzo la Biblia lenye kujenga na ibada ya familia.