Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, ‘Umetia Mizizi na Kuimarishwa Juu ya Ule Msingi’?

Je, ‘Umetia Mizizi na Kuimarishwa Juu ya Ule Msingi’?

Je, ‘Umetia Mizizi na Kuimarishwa Juu ya Ule Msingi’?

JE, UMEWAHI kuona mti mkubwa ukiyumba-yumba katika upepo wenye nguvu? Mti huo unakabili mkazo mwingi, lakini unastahimili. Kwa nini? Kwa sababu una mizizi yenye nguvu iliyopenya ndani ya udongo. Tunaweza kuwa kama mti huo. Tunapokabiliana na majaribu makali yaliyo kama dhoruba maishani, sisi pia tunaweza kustahimili ikiwa tutabaki tukiwa ‘tumetia mizizi na kuimarishwa juu ya ule msingi.’ (Efe. 3:14-17) Msingi huo ni nini?

Neno la Mungu linasema kwamba ‘Kristo Yesu mwenyewe ndiye jiwe la msingi la pembeni’ katika kutaniko la Kikristo. (Efe. 2:20; 1 Kor. 3:11) Sisi tukiwa Wakristo, tunatiwa moyo ‘tuendelee kutembea katika muungano na yeye, tukiwa tumetia mizizi na kujengwa katika yeye na kuimarishwa katika imani.’ Tukifanya hivyo, tutaweza kustahimili mashambulizi yote yanayolenga imani yetu, kutia ndani mashambulizi yanayotokana na “hoja zenye kushawishi” zinazotegemea “udanganyifu mtupu” wa wanadamu.—Kol. 2:4-8.

“Upana na Urefu na Kimo na Kina”

Hata hivyo, tunaweza jinsi gani ‘kutia mizizi’ na “kuimarishwa katika imani”? Njia moja kuu ya kutia mizizi yetu ndani kabisa ya udongo kwa njia ya mfano, ni kwa kujifunza kwa bidii Neno la Mungu lilioongozwa na roho yake. Yehova anataka ‘tufahamu kabisa akilini pamoja na watakatifu wote, upana na urefu na kimo na kina’ cha ile kweli. (Efe. 3:18) Kwa hiyo, hakuna Mkristo ambaye anapaswa kutosheka tu na uelewaji wa kijuu-juu, akiridhika kwa kujua tu “mambo ya msingi” yaliyo katika Neno la Mungu. (Ebr. 5:12; 6:1) Tofauti na hilo, kila mmoja wetu anapaswa kuwa na hamu ya kuongeza uelewaji wake wa kweli za Biblia.—Met. 2:1-5.

Bila shaka, hilo halimaanishi kwamba tunahitaji tu kuwa na ujuzi mwingi ili ‘tutie mizizi na kuimarishwa’ katika kweli. Kwa kweli, hata Shetani mwenyewe anajua mambo yaliyoandikwa katika Biblia. Kuna jambo lingine ambalo tunahitaji. Tunahitaji “kuujua upendo wa Kristo ambao unazidi ujuzi.” (Efe. 3:19) Hata hivyo, tunapojifunza kwa sababu tunampenda Yehova na tunapenda kweli, kuongeza ujuzi sahihi wa Neno la Mungu kutatia nguvu imani yetu.—Kol. 2:2.

Pima Uelewaji Wako

Kwa sasa, kwa nini usipime uelewaji wako wa kweli fulani za maana sana zilizo katika Biblia? Huenda kufanya hivyo kutakuchochea kuwa na bidii zaidi katika funzo lako la kibinafsi la Biblia. Kwa mfano, soma mistari ya kwanza ya barua ya mtume Paulo kwa Waefeso. (Ona sanduku lenye kichwa  “Kwa Waefeso.”) Baada ya kusoma mistari hiyo, jiulize, ‘Je, ninaelewa maana ya maneno yaliyo katika kifungu hicho cha Biblia ambayo yameandikwa kwa maandishi yaliyolazwa katika sanduku hilo?’ Acheni tuchunguze maneno hayo hatua kwa hatua.

Kuagizwa Kimbele “Kabla ya Kuwekwa Msingi wa Ulimwengu”

Paulo aliwaandikia waamini wenzake hivi: “[Mungu] alituagiza kimbele ili tufanywe kuwa wana kwake kupitia Yesu Kristo.” Kwa kweli, Yehova alikusudia kwamba angewafanya wanadamu fulani kuwa sehemu ya familia yake kamilifu ya kimbingu. Watu hao waliofanywa kuwa wana wa Mungu wangetawala wakiwa wafalme na makuhani pamoja na Kristo. (Rom. 8:19-23; Ufu. 5:9, 10) Hapo mwanzo, Shetani alipoipinga enzi kuu ya Yehova, alidokeza kwamba wanadamu walioumbwa na Mungu wana kasoro. Basi, inafaa kama nini kwamba Yehova alichagua washiriki wa familia hiyohiyo ya kibinadamu washiriki katika kuondoa uovu wote ulimwenguni mwishowe, kutia ndani chanzo cha uovu, Shetani Ibilisi! Hata hivyo, Yehova hakuamua kimbele ni wanadamu gani hususa ambao angewafanya kuwa wana. Badala yake, Mungu aliamua kimbele kwamba kungekuwa na kikundi, au wanadamu waliochaguliwa ambao wangetawala pamoja na Kristo mbinguni.—Ufu. 14:3, 4.

Ni “ulimwengu” gani ambao Paulo alimaanisha alipowaandikia Wakristo wenzake kwamba wakiwa kikundi, walichaguliwa “kabla ya kuwekwa msingi wa ulimwengu”? Hakuwa akizungumza kuhusu wakati ambapo Mungu hakuwa ameumba dunia au wanadamu. Hilo lingevunja kanuni ya msingi ya haki. Adamu na Hawa wangekuwa na hatia jinsi gani kwa sababu ya matendo yao ikiwa Mungu tayari alikuwa ameamua kwamba wangefanya dhambi hata kabla hawajaumbwa? Hivyo basi, ni wakati gani ambapo Mungu aliamua kwamba angerekebisha hali ambayo ilitokea wakati Adamu na Hawa walipomuunga mkono Shetani katika kuasi enzi kuu ya Mungu? Yehova alifanya hivyo baada tu ya wazazi wetu wa kwanza kuasi lakini kabla ya kutokea kwa ulimwengu wa wanadamu wasio wakamilifu ambao wangeweza kukombolewa.

“Kulingana na Utajiri wa Fadhili Zake Zisizostahiliwa”

Kwa nini Paulo alisema kwamba mipango inayotajwa katika mistari ya kwanza ya Waefeso ilifanywa ‘kulingana na utajiri wa fadhili za Mungu zisizostahiliwa’? Alisema hivyo ili kukazia kwamba Yehova hakulazimika kuwakomboa wanadamu wenye dhambi.

Tangu tunapozaliwa, hakuna hata mmoja wetu anayestahili kukombolewa. Hata hivyo, kwa kuchochewa na upendo wake mwingi kwa familia ya wanadamu, Yehova alifanya mipango ya pekee ili kutuokoa. Kwa sababu ya hali yetu ya kutokamilika na yenye dhambi, kwa kweli kama Paulo alivyosema, kukombolewa kwetu ni kwa fadhili zisizostahiliwa.

Siri Takatifu ya Kusudi la Mungu

Mwanzoni, Mungu hakufunua jinsi ambavyo angeondoa madhara yaliyoletwa na Shetani. Ilikuwa “siri takatifu.” (Efe. 3:4, 5) Baadaye, wakati kutaniko la Kikristo lilipoanzishwa, Yehova alifunua habari kuhusu vile ambavyo angetimiza kusudi lake la mwanzoni kuelekea wanadamu na dunia. “Kwenye kikomo kamili cha nyakati zilizowekwa rasmi,” akaeleza Paulo, Mungu alianzisha “usimamizi wa mambo,” yaani, mfumo wa kusimamia mambo ambao utaleta muungano kati ya viumbe wake wote wenye akili.

Hatua ya kwanza ya mpango huo wa kuunganisha viumbe wote wenye akili ilianza Pentekoste 33 W.K. wakati Yehova alipoanza kuwakusanya wale ambao wangetawala pamoja na Kristo mbinguni. (Mdo. 1:13-15; 2:1-4) Hatua ya pili ingekuwa kuwakusanya pamoja wale ambao wataishi katika paradiso duniani chini ya Ufalme wa Kimasihi wa Kristo. (Ufu. 7:14-17; 21:1-5) Maneno “usimamizi wa mambo” hayamaanishi Ufalme wa Kimasihi, kwa sababu Ufalme huo haukuwa umesimamishwa kabla ya 1914. Badala yake, maneno hayo yanamaanisha njia ya Mungu ya kushughulikia, au kusimamia mambo ili kutimiza kusudi lake la kurudisha umoja ulimwenguni pote.

“Iweni Watu Wazima Katika Nguvu za Uelewaji”

Bila shaka, mazoea mazuri ya kujifunza kibinafsi yatakusaidia uelewe kikamili “upana na urefu na kimo na kina” cha ile kweli. Hata hivyo, ni kweli kwamba shughuli nyingi katika maisha yetu siku hizi zinafanya iwe rahisi kwa Shetani kudhoofisha, au hata kuharibu mazoea yetu mazuri ya kujifunza. Usimruhusu Shetani afanye hivyo. Tumia “uwezo wa akili” ambao Mungu amekupa ili uwe ‘mtu mzima katika nguvu za uelewaji.’ (1 Yoh. 5:20; 1 Kor. 14:20) Hakikisha kwamba unaelewa ni kwa nini unaamini mambo unayoamini na kwamba sikuzote unaweza kutoa ‘sababu ya tumaini lililo ndani yako.’—1 Pet. 3:15.

Wazia kwamba ulikuwa huko Efeso wakati barua ya Paulo iliposomwa kwa mara ya kwanza. Je, si kweli kwamba maneno yake yangekuchochea utamani kukua “katika ujuzi sahihi wa Mwana wa Mungu”? (Efe. 4:13, 14) Bila shaka! Kwa hiyo, acha maneno ya Paulo yaliyoongozwa na roho ya Mungu yakuchochee ufanye vivyo hivyo leo. Kumpenda Yehova sana na kuwa na ujuzi sahihi wa Neno lake kutakusaidia kubaki ukiwa ‘umetia mizizi na kuimarishwa juu ya ule msingi,’ yaani, Kristo. Ukifanya hivyo, utaweza kuvumilia majaribu yoyote ambayo huenda Shetani atakuletea kabla ya kumalizika kabisa kwa mfumo huu mwovu.—Zab. 1:1-3; Yer. 17:7, 8.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 27]

 “Kwa Waefeso”

“Abarikiwe Mungu na Baba ya Bwana wetu Yesu Kristo, kwa kuwa ametubariki kwa kila aina ya baraka ya kiroho katika mahali pa kimbingu katika muungano na Kristo, kama vile alivyotuchagua katika muungano naye kabla ya kuwekwa msingi wa ulimwengu, ili tuwe watakatifu na bila dosari mbele zake katika upendo. Kwa maana alituagiza kimbele ili tufanywe kuwa wana kwake kupitia Yesu Kristo, kulingana na upendezi mwema wa mapenzi yake, kwa sifa ya fadhili zake zisizostahiliwa zenye utukufu alizotupatia kwa fadhili kwa njia ya mpendwa wake. Kwa njia yake tuna kuachiliwa huru kwa njia ya fidia kupitia damu ya huyo, ndiyo, msamaha wa makosa yetu, kulingana na utajiri wa fadhili zake zisizostahiliwa. Alituzidishia hizo katika hekima yote na akili nzuri, kwa kuwa alitujulisha siri takatifu ya mapenzi yake. Ni kulingana na upendezi wake mwema alioukusudia ndani yake mwenyewe kwa ajili ya usimamizi wa mambo kwenye kikomo kamili cha nyakati zilizowekwa rasmi, yaani, kukusanya tena pamoja vitu vyote katika Kristo, vitu vilivyo mbinguni na vitu vilivyo duniani.”—Efe. 1:3-10.