Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi Makusanyiko Matatu Yalivyobadili Maisha Yangu

Jinsi Makusanyiko Matatu Yalivyobadili Maisha Yangu

Jinsi Makusanyiko Matatu Yalivyobadili Maisha Yangu

Limesimuliwa na George Warienchuck

JE, UMEWAHI kuguswa moyo sana na jambo fulani ulilosikia katika moja ya makusanyiko yetu na likakuchochea kufanya mabadiliko makubwa maishani? Ilikuwa hivyo kwangu. Ninakumbuka makusanyiko matatu hasa ambayo yalibadili maisha yangu. Kusanyiko la kwanza lilinisaidia kushinda woga; la pili, likanisaidia kuwa na uradhi; la tatu, likanisaidia kujitoa zaidi. Hata hivyo, kabla sijawaeleza kuhusu mabadiliko hayo, acheni niwaeleze mambo fulani ambayo yalitukia miaka mingi kabla ya makusanyiko hayo kufanywa, yaani, mambo yanayohusu maisha yangu ya utotoni.

Nilizaliwa mwaka wa 1928, nikiwa mtoto wa mwisho katika familia yenye watoto watatu. Mimi na dada zangu, Margie na Olga, tulilelewa huko South Bound Brook, New Jersey, Marekani, wakati huo mji huo ulikuwa na wakaaji 2,000 hivi. Ingawa tulikuwa maskini, Mama alikuwa mkarimu. Kila mara aliponunua na kupika chakula cha pekee, aliwagawia majirani. Nilipokuwa na umri wa miaka tisa, Mama alitembelewa na Shahidi aliyekuwa akizungumza lugha ya Kihungaria, lugha ya asili ya mama yangu, na hilo lilimfanya asikilize ujumbe wa Biblia. Baadaye, Bertha, dada aliyekuwa na umri wa miaka 20 hivi aliendeleza funzo hilo la Biblia na akamsaidia Mama kuwa mtumishi wa Yehova.

Tofauti na mama yangu, mimi nilikuwa mwoga na sikujiamini. Mama alifanya mambo yawe mabaya zaidi kwa sababu alinichambua sana. Nilimuuliza hivi huku nikitokwa na machozi: “Kwa nini sikuzote unanichambua-chambua?” akaniambia kwamba ananipenda lakini hakutaka kuniharibu kwa kunisifu-sifu. Mama alikuwa na nia nzuri, lakini nilijihisi kwamba sifai kwa sababu sikupongezwa.

Siku moja, jirani yetu ambaye kwa kawaida alizungumza nami kwa fadhili aliniomba niende pamoja na watoto wake wa kiume kwenye shule ya Jumapili (Siku ya Yenga) katika kanisa lao. Nilijua kwamba ikiwa ningeenda, ningemkasirisha Yehova, lakini niliogopa kumkasirisha jirani huyo mwenye fadhili. Kwa hiyo, kwa miezi kadhaa nilienda kanisani ingawa niliona aibu. Vilevile, nikiwa shuleni niliipuuza dhamiri yangu kwa sababu ya kuwaogopa mwanadamu. Mwalimu mkuu shuleni alikuwa mkali sana, na alihakikisha kwamba walimu waliwalazimisha watoto wote kusalimu bendera. Mimi pia nilisalimu bendera. Nilifanya hivyo kwa mwaka mmoja hivi, kisha nikafanya mabadiliko.

Nilijifunza Kuwa Jasiri

Mwaka wa 1939 kikundi cha funzo la kitabu kilianza kukutana nyumbani kwetu. Ben Mieszkalski, ndugu kijana aliyekuwa painia ndiye aliyeongoza kikundi hicho. Tulimwita Big Ben (Ben Mkubwa), na kwa kweli alikuwa mkubwa. Kwa maoni yangu, alikuwa na urefu na upana kama wa mlango wa mbele wa nyumba yetu. Ingawa umbo lake liliogopesha, alikuwa mwenye fadhili sana, na alitabasamu kwa uchangamfu na hivyo kunifanya nistarehe. Hivyo, Ben aliponiomba nishiriki naye katika utumishi wa shambani, nilikubali kwa furaha. Nasi tukawa marafiki. Niliposhuka moyo, alizungumza nami kama ndugu mkubwa mwenye kujali anavyozungumza na ndugu yake mdogo. Hilo lilinigusa moyo sana, nami nikampenda kwelikweli.

Mwaka wa 1941, Ben aliomba familia yetu isafiri pamoja naye katika gari lake ili kuhudhuria kusanyiko huko St. Louis, Missouri. Nilisisimuka kwelikweli! Sikuwa nimewahi kusafiri kilomita zaidi ya 80 kutoka nyumbani, lakini sasa ningesafiri kilomita zaidi ya 1,500! Hata hivyo, kulikuwa na matatizo huko St. Louis. Ingawa watu walikuwa wameahidi kuwapa Mashahidi mahali pa kulala, makasisi waliwaamuru wafuasi wa dini zao wafutilie mbali mipango hiyo. Wengi walifanya hivyo. Familia tuliyopangiwa kuishi nayo pia ilikuwa imetishwa. Lakini bado ilitukaribisha. Familia hiyo ilisema kwamba haingevunja ahadi ya kutupatia mahali pa kulala. Nilipendezwa na ujasiri wao.

Dada zangu walibatizwa katika kusanyiko hilo. Siku hiyohiyo, Ndugu Rutherford, kutoka Betheli ya Brooklyn, alitoa hotuba yenye kuchangamsha na aliwaomba watoto wote waliotaka kufanya mapenzi ya Mungu wasimame. Karibu watoto 15,000 walisimama. Nilisimama pia. Kisha akatuomba sisi sote ambao tulitaka kufanya yote tuwezayo katika kazi ya kuhubiri tuseme “Ndiyo.” Nikiwa pamoja na watoto wengine tulisema kwa sauti “Ndiyo!” Wahudhuriaji walipiga makofi kwa sauti kubwa. Hilo lilinichochea kwelikweli.

Baada ya kusanyiko hilo, tulimtembelea ndugu mmoja huko West Virginia. Alitusimulia kwamba siku moja alipokuwa akihubiri, umati wa watu wenye hasira ulimpiga na kumfunika mwili kwa lami na manyoya. Nilisikiliza kwa makini sana. Ndugu huyo akasema, “Lakini nitaendelea kuhubiri.” Tulipoondoka nyumbani kwake, nilijihisi kama Daudi. Nilikuwa tayari kukabiliana na Goliathi, yaani, mwalimu mkuu wa shule yetu.

Niliporudi shuleni, nilienda kuzungumza na mwalimu mkuu. Akanikodolea macho kwa hasira. Nilimwomba Yehova kimyakimya anisaidie. Kisha, nikasema hivi kwa haraka: “Nimehudhuria kusanyiko la Mashahidi wa Yehova. Sitaisalimu bendera tena!” Alinyamaza kwa muda. Kisha, mwalimu mkuu akasimama polepole kutoka kwenye dawati lake akanijia. Uso wake ulikuwa mwekundu kwa sababu ya hasira. Akanifokea: “Salimu bendera au nikufukuze shuleni!” Wakati huu sikulegeza msimamo wangu, na nilihisi shangwe moyoni, shangwe ambayo sikuhisi hapo awali.

Nilitamani sana kumwambia Ben jambo lililotukia. Nilipomwona katika Jumba la Ufalme, nilimwambia hivi kwa sauti: “Nimefukuzwa shuleni! Sikusalimu bendera!” Ben alinishika begani, akatabasamu, kisha akasema: “Kwa kweli, Yehova anakupenda.” (Kum. 31:6) Maneno hayo yalinichochea kwelikweli! Nilibatizwa Juni 15, 1942 (15/6/1942).

Nilijifunza Siri ya Kuridhika

Baada ya Vita vya Pili vya Ulimwengu, kwa ghafula hali ya kiuchumi ya nchi yetu iliimarika, na kila mahali nchini kukawa na vitu vingi vipya vya kununua. Nilikuwa na kazi yenye mshahara mzuri na nilinunua vitu ambavyo hapo mbeleni sikudhani kwamba ningeweza kununua. Baadhi ya marafiki wangu walinunua pikipiki, na wengine wakarekebisha nyumba zao. Nilinunua gari jipya kabisa. Baada ya muda mfupi, tamaa ya kupata vitu vingi vya kimwili ilifanya nipunguze muda niliotumia katika kazi ya Ufalme. Nilijua kwamba nilikuwa nikikazia fikira mambo yasiyofaa. Kwa kupendeza, kusanyiko ambalo lilifanywa huko New York City mwaka wa 1950 lilinisaidia kurekebisha mtazamo wangu.

Katika kusanyiko hilo, msemaji mmoja baada ya mwingine aliwatia moyo wahudhuriaji wasonge mbele katika kazi ya kuhubiri. Msemaji mmoja alituhimiza hivi: “Mtosheke na vitu vya lazima vya maisha, na mkimbie shindano la mbio.” Ni kana kwamba alikuwa akizungumza nami. Pia, nilihudhuria programu ya kuhitimu kwa darasa moja la Gileadi, na programu hiyo ikanifanya nifikirie, ‘Ikiwa Mashahidi hawa wenye umri kama wangu wanaweza kuacha maisha ya starehe ili watumike katika nchi za kigeni, mimi pia ninapaswa kuwa tayari kufanya hivyo hapa nyumbani.’ Mwishoni mwa kusanyiko hilo, niliamua kuwa painia.

Wakati huohuo, nilikuwa nimeanza uchumba na Evelyn Mondak, dada mwenye bidii katika kutaniko letu. Mama ya Evelyn, ambaye alikuwa amewalea watoto sita katika njia za Yehova, alikuwa mwanamke mwenye ujasiri. Alipenda kuhubiri barabarani mbele ya Kanisa moja kubwa la Katoliki. Ingawa mara nyingi kasisi wa kanisa hilo aliyekasirika alimwambia aondoke hapo, hakuondoka hata kidogo. Kama mama yake, Evelyn hakuogopa wanadamu.—Met. 29:25.

Mwaka wa 1951, mimi na Evelyn tulifunga ndoa, tukaacha kazi, na kuanza upainia. Mwangalizi mmoja wa mzunguko alitutia moyo tuhamie huko Amagansett, kijiji kilicho kwenye ufuo wa Bahari ya Atlantiki, karibu kilomita 160 kutoka New York City. Wakati kutaniko la eneo hilo lilipotufahamisha kwamba hawakuwa na mahali ambapo tungeishi, tulitafuta nyumba inayokokotwa na gari (trela) ya bei ya chini lakini hatukupata. Kisha, tukaona trela iliyokuwa imezeeka. Mwenye trela hiyo alikubali kutuuzia trela hiyo kwa dola 900 za Marekani, kiasi kilicholingana kabisa na pesa ambazo tulikuwa tumepokea kama zawadi za arusi. Tulinunua trela hiyo, tukairekebisha, na tukaikokota hadi kwenye eneo letu jipya. Hata hivyo, tulipofika huko hatukuwa na pesa zozote na hatukujua jinsi ambavyo tungejitegemeza tukiwa mapainia.

Evelyn alifanya kazi ya kusafisha nyumba mbalimbali, nami nikapata kazi ya kufanya usafi katika hoteli moja ya Kiitaliano wakati wa usiku. Mwenye hoteli hiyo aliniambia hivi: “Unaweza kumpelekea mke wako chakula chochote kinachobaki.” Kwa hiyo, nilipofika nyumbani saa nane usiku, trela yetu ilijaa harufu nzuri ya piza na tambi za kula. Vyakula hivyo ambavyo tulivipasha moto vilifaa sana hasa wakati wa majira ya baridi kali tulipokuwa tukitetemeka ndani ya trela yetu yenye baridi. Kwa kuongezea, wakati mwingine ndugu wa kutaniko letu walileta na kuacha samaki mkubwa nje ya trela yetu. Katika miaka ambayo tulitumikia pamoja na ndugu wapendwa huko Amagansett, tulijifunza kwamba kutosheka na vitu vya lazima kunafanya maisha yaridhishe. Hiyo ilikuwa miaka ya furaha.

Tunachochewa Kujitoa Zaidi

Mnamo Julai (Mwezi wa 7) 1953, tuliwasalimu mamia ya wamishonari ambao walikuwa wamekuja kutoka katika migawo yao ya nchi za kigeni ili kuhudhuria kusanyiko la kimataifa katika New York City. Walisimulia mambo yaliyoonwa yenye kuchochea. Msisimko wao ulituchochea. Zaidi ya hayo, wakati msemaji katika kusanyiko alipokazia kwamba bado nchi nyingi hazikuwa zimehubiriwa ujumbe wa Ufalme, tulitambua jambo tulilopaswa kufanya, yaani, kujitoa zaidi kwa kupanua huduma yetu. Katika kusanyiko hilohilo, tulijaza fomu ya mazoezi ya umishonari. Mwaka huohuo, tulialikwa kuhudhuria darasa la 23 la Shule ya Gileadi, ambalo lilianza Februari (Mwezi wa 2) 1954. Lilikuwa pendeleo kubwa kama nini!

Tulisisimuka sana tulipotambua kwamba tulipewa mgawo wa kutumika huko Brazili. Kabla ya kuanza safari yetu ya siku 14 kwa meli, ndugu mmoja mwenye madaraka katika Betheli aliniambia hivi: “Dada tisa wamishonari ambao ni waseja watasafiri pamoja na wewe na mke wako kwenda Brazili. Watunze!” Hebu wazia jinsi mabaharia walivyoshangaa waliponiona nikiingia ndani ya meli huku wanawake kumi vijana wakinifuata. Hata hivyo, dada hao hawakuwa na tatizo katika kushughulikia hali hiyo. Ingawa hivyo, nilifurahi tulipofika Brazili tukiwa salama.

Baada ya kujifunza Kireno, nilipewa mgawo wa kuwa mwangalizi wa mzunguko huko Rio Grande do Sul, jimbo lililo kusini mwa Brazili. Mwangalizi wa mzunguko aliyekuwa mseja ambaye ningechukua mahali pake, aliniambia hivi pamoja na mke wangu: “Ninashangaa kwamba wenzi wa ndoa wametumwa huku. Eneo hili lina milima na mabonde.” Makutaniko yalitawanyika katika eneo kubwa la mashambani, na mengine yangefikika tu kwa kutumia lori. Ikiwa ungemnunulia dereva chakula, angekuruhusu upande juu ya lori lake. Tuliketi juu ya mizigo kama wapanda farasi walio juu ya mgongo wa farasi, huku tukiwa tumeshika kwa nguvu kamba zilizokuwa zimefunga mizigo. Kila mara lori lilipopiga kona kali, tulishikilia kamba kwa nguvu ili tusianguke, mizigo ilipoinama tuliangalia chini kwenye mabonde yenye kina kirefu. Hata hivyo, baada ya safari hizo zenye kuchosha za mchana kutwa, tulifurahi sana kuona nyuso zenye furaha za ndugu waliokuwa wakitungoja.

Tuliishi katika nyumba za akina ndugu. Walikuwa maskini sana lakini hilo halikuwazuia kutoa kwa ukarimu. Katika eneo moja la mbali, ndugu wote walikuwa wakifanya kazi katika kiwanda cha kupakia nyama. Kwa kuwa walilipwa mishahara midogo, walikula mara moja tu kwa siku. Walipokosa kufanya kazi kwa siku moja, hawakulipwa. Ingawa hivyo, wakati wa ziara zetu, waliomba ruhusa ya siku mbili kazini ili kuunga mkono utendaji wa kutaniko. Walimtumaini Yehova. Ndugu hao wanyenyekevu walitufunza mambo ambayo hatutawahi kamwe kusahau kuhusu kujidhabihu ili kutanguliza Ufalme wa Mungu. Kwa sababu ya kuishi nao, tulipata elimu ambayo hakuna chuo ambacho kinaweza kufunza. Ninapofikiria miaka hiyo, na kuwakumbuka ndugu hao, bado machozi ya shangwe yananitoka.

Mwaka wa 1976, tulirudi Marekani ili kumtunza mama yangu aliyekuwa mgonjwa. Tulihuzunika sana kuondoka Brazili, lakini tunafurahi kwamba tulijionea ongezeko kubwa la wahubiri na makutaniko katika nchi hiyo. Kila mara tunapopokea barua kutoka Brazili, tunakumbuka mambo mengi yenye kupendeza katika kipindi hicho kizuri ajabu cha maisha yetu.

Kukutana Tena na Marafiki Wapendwa

Tulipokuwa tunamtunza Mama, tulifanya upainia huku tukifanya kazi za usafi. Mwaka wa 1980, Mama alikufa akiwa mwaminifu kwa Yehova. Baada ya hapo, nilipewa mgawo wa kuwa mwangalizi wa mzunguko nchini Marekani. Mwaka wa 1990, mimi na mke wangu tulitembelea kutaniko moja huko Connecticut, na tukakutana na mtu wa pekee sana. Mmoja wa wazee wa kutaniko hilo alikuwa Ben, ndiyo, yuleyule Ben aliyenisaidia miaka 50 hivi mapema kuchukua msimamo upande wa Yehova. Je, unaweza kuwazia shangwe tuliyokuwa nayo tulipokumbatiana?

Tangu 1996, mimi na Evelyn tumetumika tukiwa mapainia wa pekee walio dhaifu kimwili katika kutaniko la Kireno huko Elizabeth, New Jersey. Nina matatizo ya afya, lakini kwa msaada wa mke wangu mpendwa, ninashiriki katika utumishi kadiri ninavyoweza. Pia, Evelyn anamsaidia jirani yetu aliye dhaifu na aliyezeeka. Jina lake ni nani? Bertha, ndiyo, yuleyule Bertha aliyemsaidia mama yangu kuwa mtumishi wa Yehova zaidi ya miaka 70 iliyopita! Tunafurahi kwamba tumepata nafasi ya kumwonyesha shukrani kwa yote aliyofanya katika kuisaidia familia yetu ijifunze kweli.

Ninashukuru kwamba makusanyiko hayo ya zamani yalinichochea kuchukua msimamo upande wa ibada ya kweli, kurahisisha maisha yangu, na kupanua utumishi wangu. Ndiyo, makusanyiko hayo yalinisaidia kuishi maisha mazuri.

[Picha katika ukurasa wa 23]

Mama ya Evelyn (kushoto) na mama yangu

[Picha katika ukurasa wa 23]

Rafiki yangu Ben

[Picha katika ukurasa wa 24]

Tukiwa Brazili

[Picha katika ukurasa wa 25]

Leo nikiwa pamoja na Evelyn