Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kudumisha Urafiki Katika Ulimwengu Usio na Upendo

Kudumisha Urafiki Katika Ulimwengu Usio na Upendo

Kudumisha Urafiki Katika Ulimwengu Usio na Upendo

“Mambo haya ninawaamuru ninyi, kwamba mpendane.”—YOH. 15:17.

1. Kwa nini Wakristo wa karne ya kwanza walihitaji kuendelea kuwa marafiki wa karibu?

KATIKA usiku wake wa mwisho duniani, Yesu aliwatia moyo wanafunzi wake washikamanifu waendelee kuwa marafiki. Mapema jioni hiyo, alisema kwamba upendo ambao wangeonyeshana ungewatambulisha kuwa wafuasi wake. (Yoh. 13:35) Mitume walihitaji kuendelea kuwa marafiki wa karibu ikiwa wangevumilia majaribu ambayo yalikuwa mbele yao na kutimiza kazi ambayo Yesu angewakabidhi baada ya muda mfupi. Kwa kweli, Wakristo wa karne ya kwanza walijulikana kwa sababu ya ujitoaji wao wa moyo wote kwa Mungu na kwa waamini wenzao.

2. (a) Tumeazimia kufanya nini, na kwa nini? (b) Tutachunguza maswali gani?

2 Leo, inafurahisha kama nini kushirikiana na tengenezo la ulimwenguni pote ambalo washiriki wake wanafuata kielelezo kilichowekwa na Wakristo wa karne ya kwanza! Tumeazimia kutii amri ya Yesu ya kuonyeshana upendo wa kweli. Hata hivyo, katika siku hizi za mwisho, watu kwa ujumla si washikamanifu na hawaonyeshi upendo wa asili. (2 Tim. 3:1-3) Mara nyingi urafiki wao ni wa kijuu-juu tu na wa kichoyo. Ili tuendelee kutambuliwa kuwa Wakristo wa kweli, ni lazima tuepuke mitazamo kama hiyo. Acheni basi tuchunguze maswali yafuatayo: Ni nini msingi wa urafiki mzuri? Tunaweza kupata jinsi gani marafiki wazuri? Ni wakati gani tunapohitaji kukomesha urafiki? Na tunaweza kudumisha jinsi gani urafiki wenye kujenga?

Ni Nini Msingi wa Urafiki Mzuri?

3, 4. Ni nini msingi wa urafiki wenye nguvu zaidi, na kwa nini?

3 Urafiki wenye nguvu zaidi unajengwa juu ya msingi wa upendo kwa Yehova. Mfalme Sulemani aliandika hivi: “Mtu akiweza kumshinda nguvu mmoja aliye peke yake, wawili wakiwa pamoja wataweza kusimama dhidi yake. Nayo kamba yenye nyuzi tatu haiwezi kukatika upesi.” (Mhu. 4:12) Yehova anapokuwa uzi wa tatu katika urafiki, urafiki huo utadumu.

4 Ni kweli kwamba wale wasiompenda Yehova wanaweza pia kuanzisha urafiki mzuri. Lakini watu wanapokuwa marafiki kwa sababu wote wawili wanampenda Mungu, urafiki wao utakuwa imara kabisa. Wanapokosa kuelewana, marafiki wa kweli wanatendeana kwa njia ambayo inampendeza Yehova. Ikiwa wapinzani wa Mungu wanajaribu kusababisha migawanyiko, maadui hao wanagundua kwamba urafiki kati ya Wakristo wa kweli hauwezi kuvunjwa. Katika historia yote, watumishi wa Yehova wamethibitisha kwamba wako tayari kufa badala ya kuwasaliti waabudu wenzao.—Soma 1 Yohana 3:16.

5. Kwa nini urafiki kati ya Ruthu na Naomi ulikuwa wenye kudumu?

5 Bila shaka, tunaweza kufurahia urafiki ulio mzuri zaidi pamoja tu na wale ambao wanampenda Yehova. Fikiria mfano wa Ruthu na Naomi. Wanawake hao walijenga urafiki ambao ni kati ya urafiki wenye kuvutia zaidi katika Biblia. Kwa nini urafiki wao ulikuwa wenye nguvu na wenye kudumu? Ruthu alifunua sababu alipomwambia Naomi hivi: “Watu wako watakuwa watu wangu, na Mungu wako Mungu wangu. . . . Yehova na anitende hivyo na kuzidi ikiwa chochote isipokuwa kifo kitatutenganisha mimi na wewe.” (Rut. 1:16, 17) Ni wazi kwamba Ruthu na Naomi wote wawili walimpenda sana Mungu, na waliacha upendo huo uongoze jinsi walivyotendeana. Kwa sababu hiyo, wanawake hao wawili walibarikiwa na Yehova.

Jinsi ya Kupata Marafiki Wazuri

6-8. (a) Urafiki wenye kudumu unategemea nini? (b) Unaweza kuchukua jinsi gani hatua ya kwanza ili upate marafiki?

6 Mfano wa Ruthu na Naomi unaonyesha kwamba urafiki mzuri haujitokezi wenyewe tu. Msingi wa kweli wa urafiki ni kwamba marafiki wote wawili wanapaswa kumpenda Yehova. Lakini ni lazima tujitahidi sana na kujidhabihu ili tuwe na urafiki wenye kudumu. Hata ndugu na dada wa kimwili wanaomwabudu Yehova katika familia za Kikristo wanahitaji kujitahidi sana ili kuwa marafiki wa karibu. Hivyo basi, unaweza kuanzisha jinsi gani urafiki mzuri?

7 Chukua hatua ya kwanza. Mtume Paulo aliwatia moyo marafiki wake katika kutaniko la Roma ‘wafuate mwendo wa ukaribishaji-wageni.’ (Rom. 12:13) Kufuata kihalisi njia fulani kunatia ndani kupiga hatua mbalimbali, moja baada ya nyingine. Vivyo hivyo, kuwa mkaribishaji-wageni kunatia ndani kuchukua hatua fulani ndogo-ndogo, kwa ukawaida. Hakuna mtu mwingine anayeweza kufuata njia au mwendo wa ukaribishaji-wageni kwa niaba yako. (Soma Methali 3:27.) Njia moja ya kuwa mkaribishaji-wageni ni kuwaalika watu mbalimbali katika kutaniko ili wale chakula chepesi pamoja nawe. Je, unaweza kufanya ukaribishaji-wageni uwe zoea lako kwa kuwaalika washiriki wa kutaniko lenu?

8 Njia nyingine ambayo unaweza kutumia ili kupata marafiki ni kuwaalika watu mbalimbali washiriki pamoja nawe katika kazi ya kuhubiri. Unaposimama kwenye mlango wa mwenye nyumba na kumsikia yule ambaye unahubiri naye akizungumza kutoka moyoni kuhusu upendo wake kwa Yehova, utachochewa kuwa na uhusiano wa karibu zaidi na mtu huyo.

9, 10. Paulo alituwekea mfano gani, na tunaweza kumwiga namna gani?

9 Panuka katika upendo wako. (Soma 2 Wakorintho 6:12, 13.) Je, umewahi kuhisi kwamba hakuna mtu yeyote katika kutaniko lenu anayeweza kuwa rafiki yako? Ikiwa ndivyo, je, inaweza kuwa kwamba una matakwa makali kuhusu ni nani anayeweza kuwa rafiki yako? Mtume Paulo aliweka mfano mzuri wa kupanuka katika upendo. Pindi moja, hangewazia kamwe kuwa na urafiki wa karibu na watu wasio Wayahudi. Hata hivyo, alikuja kuwa “mtume kwa mataifa.”—Rom. 11:13.

10 Zaidi ya hayo, Paulo hakuanzisha urafiki na watu wa umri wake tu. Kwa mfano, yeye na Timotheo walikuja kuwa marafiki wa karibu ingawa walikuwa na umri na malezi tofauti. Leo, vijana wengi wanathamini sana kuanzisha urafiki na washiriki wenye umri mkubwa kutanikoni. Vanessa, mwenye umri wa miaka 20 na kitu, anasema hivi: “Nina rafiki mpendwa sana ambaye ana umri wa miaka zaidi ya 50. Ninaweza kumweleza kila jambo ambalo ninaweza kumweleza rafiki wa umri wangu. Ananijali sana.” Walianzisha urafiki huo jinsi gani? Vanessa anasema: “Nilijitahidi sana kuanzisha urafiki huo, sikungoja urafiki huo ujianzishe tu.” Je, uko tayari kuanzisha urafiki pamoja na watu wasio wa umri wako? Bila shaka, Yehova atakuthawabisha kwa sababu ya jitihada zako.

11. Tunaweza kujifunza nini kutokana na mfano wa Yonathani na Daudi?

11 Uwe mshikamanifu. Sulemani aliandika hivi: “Rafiki wa kweli anapenda nyakati zote, naye ni ndugu aliyezaliwa kwa ajili ya wakati wa taabu.” (Met. 17:17) Alipokuwa akiandika maneno hayo, huenda Sulemani alikuwa akifikiria urafiki ambao baba yake, Daudi, alikuwa nao pamoja na Yonathani. (1 Sam. 18:1) Mfalme Sauli alitaka mwana wake Yonathani awe mrithi wa kiti cha ufalme wa Israeli. Lakini Yonathani alikubali uhakika wa kwamba Yehova alimchagua Daudi kwa ajili ya pendeleo hilo. Tofauti na Sauli, Yonathani hakumwonea wivu Daudi. Hakuchukizwa na pongezi ambazo Daudi alipewa, wala hakuamini uchongezi ambao Sauli alieneza kumhusu Daudi. (1 Sam. 20:24-34) Je, sisi ni kama Yonathani? Marafiki wetu wanapopata mapendeleo, je, tunafurahi pamoja nao? Wanapopatwa na matatizo, je, tunawafariji na kuwategemeza? Tukisikia porojo zenye kuumiza zikienezwa kumhusu rafiki yetu, je, tunafanya haraka kuziamini? Au, kama Yonathani, tunamtetea rafiki yetu kwa ushikamanifu?

Wakati Urafiki Unapohitaji Kukomeshwa

12-14. Ni tatizo gani ambalo wanafunzi fulani wa Biblia wanakabili, na tunaweza kuwasaidia jinsi gani?

12 Mwanafunzi wa Biblia anapoanza kufanya mabadiliko katika maisha yake, anaweza kukabili matatizo kuhusiana na marafiki. Anaweza kuwa na marafiki ambao anafurahia kushirikiana nao lakini ambao hawaishi kulingana na viwango vya Biblia vya maadili. Zamani, huenda alishirikiana nao kwa ukawaida. Lakini, sasa anaona kwamba mambo ambayo wanafanya yanaweza kuwa na uvutano mbaya juu yake, na anahisi kwamba anahitaji kupunguza wakati ambao anashirikiana na marafiki kama hao. (1 Kor. 15:33) Hata hivyo, huenda akahisi kwamba asiposhirikiana nao, ataonekana si mshikamanifu.

13 Ikiwa wewe ni mwanafunzi wa Biblia ambaye anakabili tatizo hilo, kumbuka kwamba rafiki wa kweli atafurahi kuona kuwa unajitahidi kuboresha maisha yako. Huenda akataka kujiunga nawe katika kujifunza kumhusu Yehova. Kwa upande mwingine, marafiki wa uwongo ‘watakutukana’ kwa sababu huendi nao kwenye “dimbwi lilelile la chini la upotovu.” (1 Pet. 4:3, 4) Kwa kweli, marafiki hao ndio wasio washikamanifu kwako, bali si wewe.

14 Wanafunzi wa Biblia wanapoachwa na marafiki wao wa zamani ambao hawampendi Mungu, washiriki wa kutaniko wanaweza kujaza pengo hilo. (Gal. 6:10) Je, unawajua kibinafsi wale wanaohudhuria mikutano yenu ambao wanajifunza Biblia? Je, unaweza pindi fulani kuwa na ushirika wenye kujenga pamoja nao?

15, 16. (a) Tunapaswa kutenda jinsi gani rafiki yetu akiacha kumtumikia Yehova? (b) Tunaweza kuthibitisha jinsi gani kwamba tunampenda Mungu?

15 Namna gani ikiwa rafiki yako katika kutaniko anaamua kumwacha Yehova, na labda anatengwa na ushirika? Hali hiyo inaweza kuwa yenye kufadhaisha sana. Dada mmoja alisema hivi kuhusu alivyohisi wakati rafiki yake wa karibu alipoacha kumtumikia Yehova: “Nilihisi ni kana kwamba sehemu fulani ya mwili wangu ilikuwa imekufa. Nilifikiri kwamba rafiki yangu alikuwa imara katika kweli, lakini hakuwa imara. Nilijiuliza ikiwa alikuwa akimtumikia Yehova ili aifurahishe tu familia yake. Kisha nikaanza kuchunguza nia yangu. Je, nilikuwa nikimtumikia Yehova kwa sababu zinazofaa?” Dada huyo alikabiliana jinsi gani na hali hiyo? Anasema hivi: “Nilimtupia Yehova mzigo wangu. Nimeazimia kumwonyesha Yehova kwamba ninampenda kwa sababu ya sifa zake, bali si kwa sababu ananipa marafiki katika tengenezo lake.”

16 Hatuwezi kutazamia kwamba tutaendelea kuwa marafiki wa Mungu ikiwa tunawaunga mkono wale ambao wanachagua kuwa marafiki wa ulimwengu. Mwanafunzi Yakobo aliandika hivi: “Je, hamjui kwamba urafiki na ulimwengu ni uadui na Mungu? Kwa hiyo, yeyote anayetaka kuwa rafiki ya ulimwengu anajifanya kuwa adui ya Mungu.” (Yak. 4:4) Tunaweza kuthibitisha kwamba tunampenda Mungu kwa kutumaini kwamba ikiwa sisi ni washikamanifu kwake, atatusaidia kukabiliana na uchungu wa kupoteza rafiki. (Soma Zaburi 18:25.) Dada aliyetajwa mapema anasema hivi kwa ufupi: “Nilijifunza kwamba hatuwezi kumfanya mtu ampende Yehova au kutupenda sisi. Kwa wazi, ni uamuzi wa mtu binafsi.” Hivyo basi, tunaweza kufanya nini ili kudumisha urafiki wenye kujenga pamoja na wale wanaobaki katika kutaniko?

Kudumisha Urafiki Mzuri

17. Marafiki wazuri wanazungumza jinsi gani?

17 Mawasiliano mazuri yanadumisha uhusiano wa karibu kati ya marafiki. Unaposoma masimulizi ya Biblia kuhusu Ruthu na Naomi, Daudi na Yonathani, na Paulo na Timotheo, utaona kwamba marafiki wazuri wanazungumza kwa uhuru lakini kwa heshima. Kuhusu jinsi tunavyopaswa kuzungumza na wengine, Paulo aliandika hivi: “Maneno yenu na yawe yenye neema sikuzote, yenye kukolezwa chumvi.” Paulo alikuwa akisema hasa kuhusu jinsi tunavyopaswa kuzungumza na wale “walio nje,” yaani, wale ambao si ndugu zetu Wakristo. (Kol. 4:5, 6) Bila shaka, ikiwa tunapaswa kuwaheshimu watu wasio waamini tunapozungumza nao, tunapaswa kuwaheshimu hata zaidi marafiki wetu katika kutaniko!

18, 19. Tunapaswa kuwa na maoni gani kuhusu shauri lolote tunalopewa na rafiki yetu Mkristo, na wazee wa Efeso walituwekea mfano gani?

18 Marafiki wazuri wanathamini maoni ya mmoja na mwingine, hivyo mawasiliano kati yao yanapaswa kuwa yenye adabu na yaliyo wazi. Mfalme Sulemani mwenye hekima aliandika hivi: “Mafuta na uvumba ndivyo huufanya moyo ushangilie, ndivyo pia utamu wa rafiki ya mtu kwa sababu ya shauri la nafsi.” (Met. 27:9) Je, hivyo ndivyo unavyoona shauri lolote ambalo unapewa na rafiki yako? (Soma Zaburi 141:5.) Ikiwa rafiki yako anaonyesha hangaiko kuhusu mambo fulani unayofanya, wewe unaitikia jinsi gani? Je, unaona maelezo yake kuwa tendo la fadhili zisizostahiliwa, au unamkasirikia?

19 Mtume Paulo alifurahia uhusiano wa karibu pamoja na wazee wa kutaniko la Efeso. Inaelekea kwamba aliwafahamu wanaume fulani kati yao wakati walipogeuka na kuwa waamini. Hata hivyo, wakati wa mkutano wake wa mwisho pamoja nao, aliwapa mashauri ya waziwazi. Waliitikia jinsi gani? Marafiki wa Paulo hawakukasirika. Badala yake, walithamini jinsi alivyopendezwa nao, na hata walilia aliposema kwamba hawatamwona tena.—Mdo. 20:17, 29, 30, 36-38.

20. Rafiki mwenye upendo atafanya nini?

20 Marafiki wazuri hawakubali tu mashauri mazuri lakini pia wanayatoa. Bila shaka, tunahitaji kutambua wakati wa ‘kukazia akili mambo yetu wenyewe.’ (1 The. 4:11) Na tunapaswa pia kutambua kwamba kila mmoja wetu “atatoa hesabu kwa Mungu kwa ajili yake mwenyewe.” (Rom. 14:12) Lakini inapohitajika, rafiki mwenye upendo atamkumbusha rafiki yake viwango vya Yehova kwa fadhili. (1 Kor. 7:39) Kwa mfano, utafanya nini ikiwa unatambua kwamba rafiki yako ambaye hajafunga ndoa anaanza kuwa na uhusiano wa karibu sana na mtu ambaye si mwamini? Je, utasitasita kumweleza mahangaiko yako kwa sababu unaogopa kuumiza hisia zake? Au utafanya nini ikiwa rafiki yako anapuuza mashauri yako? Rafiki mzuri ni yule anayetafuta msaada wa wachungaji wenye upendo ili kumsaidia rafiki ambaye amejikwaa katika kosa fulani. Kuchukua hatua kama hiyo kunahitaji ujasiri. Hata hivyo, hakuna madhara yoyote ya kudumu ambayo yataharibu urafiki unaotegemea upendo kwa Yehova.

21. Nyakati nyingine sote tutafanya nini, lakini kwa nini ni jambo la maana kudumisha urafiki wenye nguvu katika kutaniko?

21 Soma Wakolosai 3:13, 14. Nyakati nyingine, tutafanya mambo ambayo yatawafanya marafiki wetu wawe na “sababu ya kulalamika” juu yetu, nao pia watatenda au kusema mambo ambayo yatatukasirisha. Yakobo aliandika hivi: “Sisi sote hujikwaa mara nyingi.” (Yak. 3:2) Hata hivyo, kinachoamua ikiwa sisi ni marafiki wa kweli si mara ambazo tunatendeana makosa, bali ni ikiwa tunasameheana kabisa makosa hayo. Ni jambo la maana kama nini kwetu kujenga urafiki wenye nguvu kwa kuzungumza waziwazi na kusameheana kwa hiari! Tukionyesha upendo kama huo, utakuwa “kifungo kikamilifu cha muungano.”

Ungesema Nini?

• Tunaweza kupata jinsi gani marafiki wazuri?

• Huenda urafiki ukahitaji kukomeshwa wakati gani?

• Tunapaswa kufanya nini ili kudumisha urafiki wenye nguvu?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 18]

Ni nini uliokuwa msingi wa urafiki wenye kudumu kati ya Ruthu na Naomi?

[Picha katika ukurasa wa 19]

Je, wewe unaonyesha kwa ukawaida sifa ya ukaribishaji-wageni?