Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Tunajifunza somo gani kwenye andiko la Methali 24:27?

Akimshauri kijana mwanamume, mwandikaji wa Methali anasema hivi: “Tayarisha kazi yako huko nje, uifanye tayari kwa ajili yako shambani. Kisha ujenge nyumba yako.” Methali hiyo iliyoongozwa na roho ya Mungu inazungumzia jambo gani? Kwamba mwanamume anapaswa kujitayarisha vizuri kabla hajafunga ndoa na kuanzisha familia, akitambua madaraka ambayo yanatokana na kufunga ndoa.

Wakati uliopita, mstari huo ulielezwa kuwa nyakati nyingine unamaanisha kwamba ni lazima mume ambaye pia ni baba afanye kazi ya kimwili na pia ajitahidi kujenga, au kuitia moyo familia yake, kama vile kuifundisha familia yake mambo ya kiroho. Ingawa bila shaka wazo hilo ni la kweli na linapatana na Maandiko, inaonekana kwamba hilo si jambo kuu ambalo linakaziwa na mstari huo. Kwa nini? Hebu chunguza sababu mbili.

Kwanza, mstari huo unapotaja kujenga haumaanishi kutia moyo au kuimarisha familia ambayo tayari imeanzishwa. Badala yake, unatokeza wazo la kujenga nyumba kihalisi. Neno linalotafsiriwa “ujenge” linaweza pia kutumiwa kwa njia ya mfano, kumaanisha kujenga, au kuanzisha familia, yaani, kuoa na kupata watoto.

Pili, mstari huo unakazia kufanya mambo kwa utaratibu unaofaa, ni kama kusema, “Kwanza fanya jambo hili; kisha ufanye jambo lile.” Basi, je, inawezekana kwamba methali hiyo inasema kuwa madaraka ya kimwili yanapaswa kutangulizwa kabla ya mambo ya kiroho? Bila shaka hapana!

Katika nyakati za Biblia, ikiwa mwanamume alitaka ‘kujenga nyumba yake,’ au kuanzisha familia kwa kufunga ndoa, alihitaji kujiuliza, ‘Je, niko tayari kumtunza na kumtegemeza mke na watoto wowote ambao huenda tukapata baadaye?’ Kabla hajaanzisha familia, alifanya kazi ya kutunza mimea au mashamba yake. Hivyo, Biblia ya Today’s English Version inatafsiri mstari huo waziwazi hivi: “Usijenge nyumba yako na kuanzisha familia mpaka mashamba yako yawe tayari na uwe na hakika kwamba unaweza kutimiza mahitaji ya lazima ya maisha.” Je, kanuni hiyo inatumika leo?

Ndiyo. Mwanamume ambaye anataka kuoa anahitaji kujitayarisha vizuri kwa ajili ya daraka hilo. Ikiwa ana afya nzuri, ni lazima afanye kazi. Bila shaka, kazi ngumu ya mwanamume ya kutunza familia yake haipaswi kuwa tu kuandaa vitu vya kimwili. Neno la Mungu linaonyesha kwamba mwanamume ambaye hatimizi mahitaji ya kimwili, kihisia, na ya kiroho ya familia yake ni mbaya kuliko mtu asiye na imani! (1 Tim. 5:8) Kwa hiyo, mwanamume kijana anapojitayarisha kufunga ndoa na kuanza maisha ya familia anapaswa kujiuliza maswali kama haya: ‘Je, niko tayari kwa kadiri inayofaa kuiandalia familia kimwili? Je, niko tayari kuiongoza familia katika mambo ya kiroho? Je, nitatimiza daraka la kuongoza kwa ukawaida funzo la Biblia pamoja na mke na watoto wangu?’ Kwa kweli, Neno la Mungu linakazia madaraka hayo ya maana sana.—Kum. 6:6-8; Efe. 6:4.

Kwa hiyo, kijana mwanamume ambaye anatafuta mke anapaswa kufikiria kwa makini kanuni iliyo kwenye andiko la Methali 24:27. Vivyo hivyo, kijana mwanamke anapaswa kujiuliza ikiwa yuko tayari kutimiza madaraka ya mama na mke. Wenzi wa ndoa ambao ni vijana wanaweza kujiuliza maswali kama hayo wanapofikiria uwezekano wa kulea watoto. (Luka 14:28) Kufuata mwongozo huo ambao umeongozwa na roho ya Mungu kunaweza kuwasaidia watu wa Mungu waepuke matatizo mengi na wafurahie maisha ya familia yenye kuthawabisha.

[Blabu katika ukurasa wa 12]

Ni maswali gani kuhusu ndoa ambayo kijana mwanamume anapaswa kujiuliza?