Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Ninyi Ni Rafiki Zangu”

“Ninyi Ni Rafiki Zangu”

“Ninyi Ni Rafiki Zangu”

“Ninyi ni rafiki zangu ikiwa mnafanya ninalowaamuru ninyi.”—YOH. 15:14.

1, 2. (a) Marafiki wa Yesu walitoka katika malezi gani mbalimbali? (b) Kwa nini ni jambo la maana kwetu kuwa marafiki wa Yesu?

WANAUME wanaoketi na Yesu kwenye chumba cha juu walitoka katika malezi mbalimbali. Petro na Andrea ambao ni ndugu wa kimwili walikuwa wavuvi. Zamani, Mathayo alikuwa mkusanya-kodi, kazi ambayo ilidharauliwa na Wayahudi. Wengine wao, kama vile Yakobo na Yohana, inaelekea walimjua Yesu tangu alipokuwa mvulana mdogo. Na wengine, kama vile Nathanaeli, huenda walikuwa wamemjua kwa miaka michache tu. (Yoh. 1:43-50) Hata hivyo, wote waliokuwepo usiku huo wakati wa Pasaka hiyo ya pekee huko Yerusalemu walisadiki kwamba Yesu alikuwa ndiye yule Masihi aliyeahidiwa, Mwana wa Mungu aliye hai. (Yoh. 6:68, 69) Bila shaka, walitiwa moyo sana walipomsikia Yesu akiwaambia: “Nimewaita ninyi rafiki, kwa sababu mambo yote ambayo nimeyasikia kutoka kwa Baba yangu nimewajulisha ninyi.”—Yoh. 15:15.

2 Maneno hayo ambayo Yesu aliwaambia mitume wake waaminifu yanawahusu kimsingi Wakristo wote watiwa-mafuta leo, na kwa kuongezea yanawahusu waandamani wao wa “kondoo wengine.” (Yoh. 10:16) Hata iwe tumetoka katika malezi gani, tunaweza kuwa na pendeleo la kuwa marafiki wa Yesu. Urafiki wetu pamoja naye ni wa maana sana kwa sababu tunapokuwa marafiki wake tunakuwa pia marafiki wa Yehova. Kwa kweli, hatuwezi kumkaribia Yehova bila kumkaribia kwanza Kristo. (Soma Yohana 14:6, 21.) Hivyo basi, ni lazima tufanye nini ili tuwe marafiki wa Yesu na kudumisha urafiki huo? Kabla ya kuzungumzia habari hiyo ya maana sana, acheni tuchunguze mfano wa Yesu akiwa rafiki mzuri na tuone jambo tunaloweza kujifunza kutokana na jinsi wanafunzi wake walivyohisi kuhusu urafiki huo.

Mfano wa Yesu Akiwa Rafiki Mzuri

3. Yesu alijulikana kwa sababu gani?

3 Mfalme Sulemani mwenye hekima aliandika hivi: “Tajiri ana rafiki wengi.” (Met. 14:20) Maneno hayo yanaonyesha mwelekeo wa wanadamu wasio wakamilifu, wa kufanya urafiki kwa msingi wa kile wanachoweza kupata badala ya kile wanachoweza kutoa. Yesu hakuwa na udhaifu huo. Hakushawishiwa kufanya urafiki na mtu kwa sababu ya uwezo wa mtu huyo wa kiuchumi au cheo chake katika jamii. Ni kweli kwamba Yesu alimpenda mtawala mmoja kijana na akamwalika amfuate ili awe mfuasi wake. Hata hivyo, Yesu alimwambia mwanamume huyo auze vitu alivyokuwa navyo na kuwapa maskini. (Marko 10:17-22; Luka 18:18, 23) Yesu alijulikana kwa sababu alikuwa rafiki ya watu wa hali ya chini na waliodharauliwa, bali si kwa sababu alishirikiana na watu matajiri na mashuhuri.—Mt. 11:19.

4. Kwa nini tunaweza kusema kwamba marafiki wa Yesu walikuwa watu wasio wakamilifu?

4 Bila shaka, marafiki wa Yesu walikuwa watu wasio wakamilifu. Pindi moja Petro alikosa kuona mambo kwa njia ya kiroho. (Mt. 16:21-23) Yakobo na Yohana walionyesha roho ya kujitakia makuu walipomwomba Yesu awape vyeo vikubwa katika Ufalme. Tendo lao liliwakasirisha mitume wengine, na suala hilo la kutafuta ukubwa lilifanya wagombane mara kwa mara. Hata hivyo, Yesu alijitahidi kwa subira kurekebisha mawazo ya marafiki wake naye hakuwa mwepesi kukasirika.—Mt. 20:20-28.

5, 6. (a) Kwa nini Yesu alidumisha urafiki na wengi kati ya mitume wake? (b) Kwa nini Yesu alikomesha urafiki wake pamoja na Yuda?

5 Yesu hakudumisha urafiki na watu hao wasio wakamilifu kwa kupuuza tu au kuachilia udhaifu wao. Badala yake, aliamua kukazia fikira nia yao nzuri na sifa zao nzuri. Kwa mfano, Petro, Yakobo, na Yohana walilala usingizi badala ya kumtegemeza Yesu alipokabili wakati mgumu zaidi. Yesu alivunjwa moyo na jambo hilo. Hata hivyo, aliona kwamba nia yao ilikuwa nzuri, akasema hivi: “Bila shaka, roho inataka, lakini mwili ni dhaifu.”—Mt. 26:41.

6 Kinyume chake, Yesu alikomesha urafiki wake na Yuda Iskariote. Hata ingawa kwa nje Yuda alionekana kuwa rafiki mzuri, Yesu aligundua kwamba rafiki huyo wa zamani alikuwa ameruhusu moyo wake upotoshwe. Kwa sababu Yuda alikuwa sasa rafiki ya ulimwengu, alijifanya mwenyewe kuwa adui ya Mungu. (Yak. 4:4) Kwa hiyo, Yesu alikuwa tayari amemfukuza Yuda wakati alipotangaza urafiki Wake pamoja na mitume wake waaminifu 11 waliobaki.—Yoh. 13:21-35.

7, 8. Yesu alionyesha jinsi gani upendo wake kwa marafiki wake?

7 Yesu hakukazia fikira makosa ya marafiki wake washikamanifu bali alichukua hatua ya kuwasaidia. Kwa mfano, alisali ili Baba yake awalinde wakati wa majaribu. (Soma Yohana 17:11.) Yesu alitilia maanani udhaifu wao wa kimwili. (Marko 6:30-32) Na hakupendezwa tu kuwaeleza yale aliyofikiri bali pia alisikiliza na kuelewa yale waliyofikiri na kuhisi.—Mt. 16:13-16; 17:24-26.

8 Yesu aliishi na kufa kwa ajili ya marafiki wake. Kwa kweli, alijua kwamba kulingana na sheria ilikuwa lazima atoe uhai wake ili kutimiza kiwango cha haki cha Baba yake. (Mt. 26:27, 28; Ebr. 9:22, 28) Lakini Yesu alionyesha upendo kwa kutoa uhai wake. Alisema hivi: “Hakuna aliye na upendo mkuu kuliko huu, kwamba mtu aitoe nafsi yake kwa ajili ya rafiki zake.”—Yoh. 15:13.

Wanafunzi Walihisi Jinsi Gani Kuhusu Urafiki wa Yesu?

9, 10. Watu waliitikia jinsi gani ukarimu wa Yesu?

9 Yesu alikuwa mkarimu katika kutumia wakati wake, kuonyesha upendo, na kutoa vitu vya kimwili. Kwa sababu hiyo, watu walijihisi huru kumkaribia na walifurahi pia kumpa vitu. (Luka 8:1-3) Kutokana na mambo aliyojionea mwenyewe, Yesu alisema hivi: “Muwe na mazoea ya kuwapa watu, na watu watawapa ninyi. Watawamwagia katika mfuko wa nguo zenu kipimo kizuri, kilichoshindiliwa, kilichotikiswa pamoja na kufurika. Kwa maana kwa kipimo mnachopimia, watawapimia ninyi pia.”—Luka 6:38.

10 Bila shaka, watu wengine walijaribu kushirikiana na Yesu kwa sababu tu ya vitu ambavyo wangepata kutoka kwake. Marafiki hao wa uwongo walimwacha Yesu walipoelewa kimakosa jambo fulani alilosema. Badala ya kumwamini Yesu wakati walipokosa kuelewa alilosema, walifanya haraka kukata kauli yenye kosa na kuacha kumfuata. Lakini mitume walikuwa washikamanifu. Mara nyingi, urafiki wao pamoja na Kristo ulijaribiwa, lakini walifanya yote waliyoweza ili kumtegemeza katika nyakati nzuri na mbaya pia. (Soma Yohana 6:26, 56, 60, 66-68.) Katika usiku wake wa mwisho duniani akiwa mwanadamu, Yesu alieleza jinsi alivyowathamini sana marafiki wake kwa kusema hivi: “Ninyi ndio mmeshikamana nami katika majaribu yangu.”—Luka 22:28.

11, 12. Yesu aliwahakikishia wanafunzi wake nini, nao waliitikia namna gani?

11 Muda mfupi baada ya Yesu kuwapongeza wanafunzi wake kwa sababu ya ushikamanifu wao, walimwacha. Kwa muda mfupi, waliruhusu woga wa wanadamu ushinde upendo wao kwa Kristo. Kwa mara nyingine tena, Yesu aliwasamehe. Baada ya kufa na kufufuliwa, aliwatokea na kuwahakikishia tena urafiki wake. Zaidi ya hilo, aliwakabidhi kazi takatifu, yaani, kufanya wanafunzi kutoka kwa “watu wa mataifa yote” na kuwa mashahidi wake “mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.” (Mt. 28:19; Mdo. 1:8) Wanafunzi hao waliitikia jinsi gani?

12 Wanafunzi hao walijitoa kwa moyo na nafsi yao yote kueneza ujumbe wa Ufalme. Kwa msaada wa roho takatifu ya Yehova, walijaza Yerusalemu mafundisho yao baada ya muda mfupi. (Mdo. 5:27-29) Hata vitisho vya kuwaua havingeweza kuwazuia wasitii amri ya Yesu ya kufanya wanafunzi. Makumi machache tu ya miaka baada ya Yesu kuwapa amri hiyo, mtume Paulo aliandika kwamba habari njema ilikuwa imehubiriwa “katika uumbaji wote ulio chini ya mbingu.” (Kol. 1:23) Bila shaka, wanafunzi hao walithibitisha kwamba walithamini urafiki wao pamoja na Yesu!

13. Wanafunzi wa Yesu waliruhusu mafundisho yake yabadili maisha yao katika njia gani?

13 Pia, wale waliogeuka na kuwa wanafunzi waliruhusu mafundisho ya Yesu yabadili maisha yao. Kwa wengi, hilo lilimaanisha kufanya mabadiliko makubwa katika mwenendo na utu wao. Kabla ya hapo, wanafunzi fulani wapya walikuwa walawiti, wazinzi, walevi, au wezi. (1 Kor. 6:9-11) Wengine walihitaji kubadili mtazamo wao kuelekea watu wa jamii nyingine. (Mdo. 10:25-28) Hata hivyo, walimtii Yesu. Walivua utu wao wa zamani na kuvaa utu mpya. (Efe. 4:20-24) Walipata kujua “akili ya Kristo,” wakaelewa na kuiga njia yake ya kufikiri na kutenda.—1 Kor. 2:16.

Urafiki Pamoja na Kristo Leo

14. Yesu aliahidi kufanya nini wakati wa “umalizio wa mfumo wa mambo”?

14 Wengi kati ya Wakristo hao wa karne ya kwanza walimjua Yesu kibinafsi au walimwona baada ya ufufuo wake. Kwa wazi, sisi hatuna pendeleo hilo. Basi, tunaweza kuwa marafiki wa Kristo jinsi gani? Njia moja ni kutii mwongozo unaotolewa na jamii ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara, ambayo inafanyizwa na ndugu watiwa-mafuta wa Yesu ambao wangali hai duniani. Yesu aliahidi kwamba wakati wa “umalizio wa mfumo wa mambo,” atamweka rasmi mtumwa huyo “juu ya mali zake zote.” (Mt. 24:3, 45-47) Leo, wengi wa wale ambao wanataka kuwa marafiki wa Kristo si washiriki wa jamii hiyo ya mtumwa. Kukubali kwao mwongozo wanaopata kutoka kwa jamii ya mtumwa mwaminifu kuna uvutano gani juu ya urafiki wao pamoja na Kristo?

15. Ni nini kitakachoamua ikiwa mtu atawekwa upande wa kondoo au wa mbuzi?

15 Soma Mathayo 25:31-40. Yesu aliwaita wale ambao wangefanyiza jamii ya mtumwa mwaminifu kuwa ndugu zake. Katika mfano unaohusu kutenganishwa kwa kondoo na mbuzi, Yesu anasema waziwazi kwamba jinsi watu wanavyowatendea ndugu zake ni kana kwamba wanamtendea yeye binafsi. Kwa kweli, alisema kwamba jambo kuu ambalo lingetofautisha kondoo na mbuzi ni jinsi ambavyo mtu angemtendea hata yule aliye ‘mdogo zaidi wa ndugu zake.’ Kwa hiyo, njia kuu ambayo wale walio na tumaini la kuishi duniani wanaonyesha tamaa yao ya kuwa marafiki wa Kristo ni kwa kuiunga mkono jamii ya mtumwa mwaminifu.

16, 17. Tunaweza kuonyesha jinsi gani urafiki wetu kuwaelekea ndugu za Kristo?

16 Ikiwa unatumaini kuishi duniani chini ya Ufalme wa Mungu, unaweza kuonyesha jinsi gani urafiki wako kuwaelekea ndugu za Kristo? Acheni tuchunguze njia tatu tu. Kwanza, kwa kushiriki kwa moyo wote katika kazi ya kuhubiri. Kristo aliwaamuru ndugu zake wahubiri habari njema ulimwenguni pote. (Mt. 24:14) Hata hivyo, ingekuwa vigumu sana kwa mabaki ya ndugu za Kristo walio duniani leo kutimiza daraka hilo bila msaada wa waandamani wao wa kondoo wengine. Kwa kweli, kila mara washiriki wa jamii ya kondoo wengine wanaposhiriki katika kazi ya kuhubiri, wanawasaidia ndugu za Kristo kutimiza kazi yao takatifu. Kristo na jamii ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara wanathamini sana tendo hilo la urafiki.

17 Njia ya pili ambayo wale wa jamii ya kondoo wengine wanaweza kuwasaidia ndugu za Kristo ni kwa kutegemeza kifedha kazi ya kuhubiri. Yesu aliwatia moyo wafuasi wake wajifanyie marafiki na “mali zisizo za uadilifu.” (Luka 16:9) Si kwamba tunaweza kununua kwa pesa urafiki wa Yesu au Yehova. Badala yake, tunapotumia vitu vyetu vya kimwili ili kutegemeza kazi ya Ufalme, tunathibitisha urafiki na upendo wetu, si kwa maneno tu, bali pia “kwa tendo na kweli.” (1 Yoh. 3:16-18) Tunatoa utegemezo huo wa kifedha kwa kushiriki katika kazi ya kuhubiri, kwa kutoa michango ya pesa ili kujenga na kutunza mahali petu pa ibada, na pia wakati tunapotoa michango ya pesa kwa ajili ya kazi ya kuhubiri ya ulimwenguni pote. Iwe kiasi cha pesa tunachotoa ni kidogo au ni kikubwa, bila shaka Yehova na Yesu wanathamini tunapotoa kwa uchangamfu.—2 Kor. 9:7.

18. Kwa nini tunapaswa kutii mwongozo unaotegemea Biblia ambao unatolewa na wazee wa kutaniko?

18 Njia ya tatu ambayo sote tunaweza kuthibitisha kwamba sisi ni marafiki wa Kristo ni kwa kutii mwongozo unaotolewa na wazee wa kutaniko. Wanaume hao wamewekwa rasmi na roho takatifu chini ya mwongozo wa Kristo. (Efe. 5:23) Mtume Paulo aliandika hivi: “Watiini wale wanaoongoza katikati yenu na mnyenyekee.” (Ebr. 13:17) Nyakati nyingine, huenda tukaliona kuwa jambo gumu kutii mwongozo unaotegemea Biblia ambao tunapewa na wazee wa kutaniko letu. Inaelekea tunajua udhaifu wao, na huenda hilo likapotosha maoni yetu kuhusu mashauri yao. Hata hivyo, bado Kristo, aliye Kichwa cha kutaniko, anapendezwa kuwatumia wanaume hao wasio wakamilifu. Kwa hiyo, urafiki wetu pamoja na Kristo unahusiana moja kwa moja na jinsi tunavyoitikia mamlaka yao. Tunapofuata mwongozo wa wazee kwa furaha badala ya kukazia fikira makosa yao, tunathibitisha kwamba tunampenda Kristo.

Tunaweza Kupata Wapi Marafiki Wazuri?

19, 20. Tunaweza kupata nini katika kutaniko, na tutachunguza nini katika habari inayofuata?

19 Yesu anaendelea kututunza si kupitia tu usimamizi wa wachungaji wenye upendo, bali pia kupitia mama, ndugu, na dada wa kiroho katika kutaniko. (Soma Marko 10:29, 30.) Ulipoanza kwa mara ya kwanza kushirikiana na tengenezo la Yehova, watu wako wa ukoo waliitikia jinsi gani? Labda, walikuunga mkono katika jitihada zako za kumkaribia Mungu na Kristo. Lakini Yesu alionya kwamba wakati fulani “adui za mtu watakuwa watu wa nyumbani kwake mwenyewe.” (Mt. 10:36) Inafariji kama nini kujua kwamba katika kutaniko, tunaweza kupata wale ambao watashikamana nasi kwa ukaribu kuliko ndugu zetu wa kimwili!—Met. 18:24.

20 Kama inavyoonyeshwa na salamu za Paulo mwenyewe mwishoni mwa barua yake kwa kutaniko la Roma, alianzisha urafiki wa karibu sana na watu wengi. (Rom. 16:8-16) Mtume Yohana alimalizia barua yake ya tatu kwa maneno haya: “Wape rafiki salamu zangu kwa jina.” (3 Yoh. 14) Ni wazi kwamba yeye pia alianzisha urafiki wa kudumu na watu wengi. Tunaweza kuiga jinsi gani mfano wa Yesu na wanafunzi wa mapema kwa kuanzisha na kudumisha urafiki mzuri na ndugu na dada zetu wa kiroho? Tutachunguza jibu la swali hilo katika habari inayofuata.

Ungesema Nini?

• Yesu aliweka mfano gani akiwa rafiki mzuri?

• Wanafunzi waliitikia jinsi gani urafiki wa Yesu?

• Tunaweza kuthibitisha namna gani kwamba sisi ni marafiki wa Kristo?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 14]

Yesu alipendezwa kujua maoni ya marafiki wake na jinsi walivyohisi

[Picha katika ukurasa wa 16]

Tunaweza kuonyesha jinsi gani tamaa yetu ya kuwa marafiki wa Kristo?