Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Wakeni Roho”

“Wakeni Roho”

“Wakeni Roho”

“Msiwe wavivu katika kazi zenu. Wakeni roho. Mtumikieni Yehova.”—ROM. 12:11.

1. Kwa nini Waisraeli walitoa dhabihu za wanyama na matoleo mengine?

YEHOVA anathamini sana kuona watumishi wake wakijidhabihu kutoka moyoni ili kuonyesha kwamba wanampenda na wanajitiisha kwake ili kufanya mapenzi yake. Katika nyakati za zamani, Yehova alikubali dhabihu mbalimbali za wanyama na matoleo mengine. Waisraeli walitoa dhabihu na matoleo hayo kulingana na Sheria ya Musa ili wasamehewe dhambi zao na pia ilikuwa njia ya kuonyesha shukrani. Katika kutaniko la Kikristo, Yehova hajatuwekea takwa la kutoa dhabihu halisi kama hizo za kidesturi. Hata hivyo, katika sura ya 12 ya barua yake kwa Wakristo huko Roma, mtume Paulo anaonyesha kwamba bado tunatazamiwa kutoa dhabihu. Acheni tuone jinsi tunavyoweza kufanya hivyo.

Dhabihu Iliyo Hai

2. Tukiwa Wakristo, tunaishi maisha ya aina gani, na hilo linahusisha nini?

2 Soma Waroma 12:1, 2Katika sehemu ya kwanza ya barua yake, Paulo alionyesha waziwazi kwamba Wakristo waliotiwa mafuta, Wayahudi na wasio Wayahudi, walitangazwa kuwa waadilifu mbele za Mungu kwa imani, bali si kwa matendo. (Rom. 1:16; 3:20-24) Katika sura ya 12, Paulo anaeleza kwamba Wakristo wanapaswa kuonyesha shukrani kwa kuishi maisha ya kujidhabihu. Ili tufanikiwe, ni lazima tufanye upya akili zetu. Kwa sababu ya hali ya kutokamilika ambayo tumerithi, tumetiishwa chini ya “sheria ya dhambi na kifo.” (Rom. 8:2) Kwa hiyo, tunahitaji kugeuzwa, yaani, “kufanywa upya katika nguvu zinazoendesha akili [zetu],” kwa kubadili kabisa mielekeo yetu. (Efe. 4:23) Tunaweza tu kufanya badiliko hilo kamili kwa msaada wa Mungu na roho yake. Ni lazima pia tujitahidi kabisa, tukitumia ‘nguvu zetu za kufikiri.’ Inamaanisha kwamba tunapaswa kujitahidi kadiri tunayoweza ili ‘tusifanyizwe kulingana na mfumo huu wa mambo,’ pamoja na maadili yake mapotovu, burudani yake chafu, na mawazo yake yaliyopotoka.—Efe. 2:1-3.

3. Kwa nini tunashiriki katika utendaji wa Kikristo?

3 Pia, Paulo anatutia moyo tutumie ‘nguvu zetu za kufikiri’ ili kujihakikishia wenyewe “mapenzi ya Mungu yaliyo mema na yenye kukubalika na makamilifu.” Kwa nini tunasoma Biblia kila siku, kutafakari kuhusu yale tunayosoma, kusali, kuhudhuria mikutano ya Kikristo, na kushiriki katika kazi ya kuhubiri habari njema ya Ufalme? Je, ni kwa sababu wazee wa kutaniko wanatuhimiza tufanye hivyo? Bila shaka, tunashukuru kwamba wazee wanatutolea vikumbusho vinavyotusaidia. Lakini tunashiriki katika utendaji wa Kikristo kwa sababu tunachochewa na roho ya Mungu kuonyesha kwamba tunampenda Yehova kutoka moyoni. Zaidi ya hayo, sisi binafsi tunasadiki kwamba ni mapenzi ya Mungu tushiriki katika utendaji huo. (Zek. 4:6; Efe. 5:10) Pia, tunapata shangwe na uradhi mwingi tunapotambua kwamba kwa kuishi maisha kamili ya Kikristo tunaweza kukubaliwa na Mungu.

Zawadi Mbalimbali

4, 5. Wazee Wakristo wanapaswa kutumia zawadi zao jinsi gani?

4 Soma Waroma 12:6-8, 11. Paulo anaeleza kwamba “tuna zawadi zinazotofautiana kulingana na fadhili zisizostahiliwa tulizopewa.” Zawadi fulani ambazo Paulo anataja kama vile, kuhimiza na kusimamia, zinawahusu hasa wazee Wakristo, ambao wanahimizwa wasimamie “kwa bidii ya kweli.”

5 Paulo anasema kwamba waangalizi wanapaswa kuonyesha bidii hiyohiyo wakati wanapotumikia wakiwa walimu na wanapotimiza “huduma” yao. Inaonekana kwamba mistari mingine katika sura hiyo inaonyesha kwamba Paulo alikuwa akizungumza kuhusu “huduma” inayofanywa ndani ya kutaniko, au katika ule “mwili mmoja.” (Rom. 12:4, 5) Huduma hiyo ni sawa na ile inayotajwa katika Matendo 6:4, wakati ambapo mitume walitangaza hivi: “Tutajitoa kwa sala na kwa huduma ya neno.” Huduma hiyo inatia ndani nini? Wazee Wakristo wanatumia zawadi zao kuwajenga washiriki wa kutaniko. Wanaonyesha kwamba ‘wako katika huduma hiyo’ wakati wanapotoa kwa bidii mwongozo na maagizo kwa kutaniko kutoka katika Neno la Mungu kwa kusali na kujifunza, kufanya utafiti, kufundisha, na kulichunga kutaniko. Waangalizi wanapaswa kutumia zawadi zao kwa uangalifu na kuwatunza kondoo “kwa uchangamfu.”—Rom. 12:7, 8; 1 Pet. 5:1-3.

6. Tunaweza kufuata jinsi gani shauri la Waroma 12:11 ambalo ni andiko la msingi la habari hii?

6 Paulo anaongezea hivi: “Msiwe wavivu katika kazi zenu. Wakeni roho. Mtumikieni Yehova.” Tukigundua kwamba tuna mwelekeo wa kuwa wavivu katika huduma yetu, huenda tukahitaji kuchunguza tena mazoea yetu ya kujifunza kisha tusali kwa bidii zaidi na mara nyingi zaidi ili tupate roho ya Yehova, ambayo inaweza kutusaidia kuondoa uzembe wowote na kuwa tena wenye bidii. (Luka 11:9, 13; Ufu. 2:4; 3:14, 15, 19) Roho takatifu iliwatia nguvu Wakristo wa zamani ili waseme juu ya “mambo makuu ya Mungu.” (Mdo. 2:4, 11) Vivyo hivyo leo, roho hiyo inaweza kutuchochea tuwe na bidii katika huduma, wenye ‘kuwaka roho.’

Unyenyekevu na Kiasi

7. Kwa nini tunapaswa kuwa wanyenyekevu na wenye kiasi katika utumishi wetu?

7 Soma Waroma 12:3, 16. Zawadi ambazo huenda tunazo zinategemea “fadhili zisizostahiliwa” za Yehova. Paulo anasema hivi katika andiko lingine: “Kuwa kwetu na sifa za kustahili vya kutosha hutoka kwa Mungu.” (2 Kor. 3:5) Kwa hiyo, hatupaswi kujitukuza. Tunapaswa kutambua kwa unyenyekevu kwamba matokeo yoyote mazuri tunayopata katika huduma yetu yanatokana na baraka za Mungu, bali hayategemei uwezo wetu wenyewe. (1 Kor. 3:6, 7) Kuhusu jambo hilo, Paulo alisema hivi: “Namwambia kila mtu hapo kati yenu asijifikirie mwenyewe zaidi kuliko ilivyo lazima kufikiri.” Ni jambo la maana sana kwetu kujiheshimu, kuridhika na kupata shangwe katika utumishi wetu wa Ufalme. Hata hivyo, kuwa na kiasi, au kutambua mipaka yetu, kutatuzuia kushikilia sana maoni yetu. Badala yake, tunapaswa ‘kufikiri ili tuwe na akili timamu.’

8. Tunaweza kuepuka jinsi gani kuwa “wenye busara machoni [petu] wenyewe”?

8 Litakuwa jambo la upumbavu kwetu kujisifu kwa sababu ya mambo tunayotimiza. Ni “Mungu anayeikuza.” (1 Kor. 3:7) Paulo anasema kwamba Mungu amemgawia kila mshiriki wa kutaniko “kipimo cha imani.” Badala ya kujiona kuwa bora, tunapaswa kutambua mambo ambayo wengine wanatimiza kulingana na kipimo chao cha imani. Paulo anasema hivi tena: “Mwafikirie wengine kama vile mnavyojifikiria wenyewe.” Katika barua yake nyingine, mtume huyo anatuambia tusifanye ‘jambo lolote kwa ugomvi au kwa kujisifu, bali kwa unyenyekevu wa akili tukiwaona wengine kuwa ni bora kuliko sisi.’ (Flp. 2:3) Tunahitaji jitihada nyingi na unyenyekevu wa kweli ili kutambua kwamba kila mmoja wa ndugu na dada zetu ni bora kuliko sisi katika njia moja au nyingine. Unyenyekevu utatuzuia kuwa “wenye busara machoni [petu] wenyewe.” Ingawa mapendeleo ya utumishi wa pekee yanaweza kuwafanya wengine wajulikane zaidi, wote watapata shangwe nyingi wakitimiza “mambo ya hali ya chini,” kazi za hali ya chini ambazo mara nyingi zinapuuzwa na watu.—1 Pet. 5:5.

Umoja Wetu wa Kikristo

9. Kwa nini Paulo anawalinganisha Wakristo waliozaliwa kwa roho na viungo vya mwili?

9 Soma Waroma 12:4, 5, 9, 10. Paulo anawalinganisha Wakristo watiwa-mafuta na viungo vya mwili, wanapotumikia kwa umoja chini ya Kichwa chao, Kristo. (Kol. 1:18) Anawakumbusha Wakristo waliozaliwa kwa roho kwamba mwili una viungo vingi, lakini vina kazi tofauti na kwamba ‘ingawa ni wengi, wao ni mwili mmoja katika muungano na Kristo.’ Vivyo hivyo, Paulo aliwahimiza hivi Wakristo watiwa-mafuta huko Efeso: “Na tukue kwa upendo katika mambo yote ndani yake yeye aliye kichwa, Kristo. Kutoka katika yeye mwili wote, kwa kuunganishwa pamoja kwa upatano na kufanywa ushirikiane kupitia kila kiungo ambacho hutoa kile kinachohitajiwa, kulingana na utendaji wa kila kiungo kimoja-kimoja katika kipimo kinachofaa, hutokeza ukuzi wa mwili ili huo ujijenge wenyewe katika upendo.”—Efe. 4:15, 16.

10. “Kondoo wengine” wanapaswa kutambua mamlaka gani?

10 Ingawa “kondoo wengine” si sehemu ya mwili wa Kristo wenye washiriki wengi, wanaweza kujifunza mengi kutokana na mfano huo. (Yoh. 10:16) Paulo anasema kwamba Yehova ‘alivitiisha vitu vyote chini ya miguu ya Kristo, na kumfanya kuwa kichwa juu ya vitu vyote kuhusiana na kutaniko.’ (Efe. 1:22) Leo, kondoo wengine ni sehemu ya “vitu vyote” ambavyo Yehova ameweka chini ya ukichwa wa Mwana wake. Wao pia ni kati ya “mali” ambazo Kristo amemkabidhi ‘mtumwa wake mwaminifu na mwenye busara.’ (Mt. 24:45-47) Kwa hiyo, wale walio na tumaini la kuishi duniani wanapaswa kutambua kwamba Kristo ni Kichwa chao na kujitiisha kwa mtumwa mwaminifu na mwenye busara na Baraza lake Linaloongoza na pia kwa wanaume waliowekwa rasmi kuwa waangalizi katika kutaniko. (Ebr. 13:7, 17) Hilo linachangia umoja wa Kikristo.

11. Umoja wetu unategemea nini, na Paulo alitoa shauri gani lingine?

11 Umoja huo unategemea upendo, ambao ni “kifungo kikamilifu cha muungano.” (Kol. 3:14) Kwenye Waroma sura ya 12, Paulo anakazia hilo anaposema kwamba upendo wetu unapaswa kuwa “bila unafiki” na kwamba “katika upendo wa kindugu” tunapaswa kuwa na “upendo mwororo kwa mtu na mwenzake.” Hilo linatufanya tuheshimiane. Mtume Paulo anasema hivi: “Katika kuonyeshana heshima iweni wa kwanza.” Bila shaka, hatupaswi kufikiri kwamba upendo ni hisia tu ya moyoni. Tunapaswa kufanya yote tunayoweza ili kudumisha usafi wa kutaniko. Anapotoa shauri lake kuhusu upendo, Paulo anaongezea hivi: “Chukieni maovu, shikamaneni na mema.”

Njia au Mwendo wa Ukaribishaji-Wageni

12. Tunajifunza nini kuhusu ukaribishaji-wageni kutokana na Wakristo wa Makedonia ya kale?

12 Soma Waroma 12:13. Kuwapenda ndugu zetu kutatuchochea ‘kushiriki pamoja na watakatifu kulingana na mahitaji yao’ na kulingana na uwezo wetu. Hata ikiwa tuna vitu vichache vya ulimwengu huu, tunaweza kushiriki na wengine vitu tulivyo navyo. Akiandika kuhusu Wakristo wa Makedonia, Paulo alisema hivi: “Wakati wa jaribu kubwa chini ya mateso shangwe yao nyingi na umaskini mkubwa ulifanya utajiri wa ukarimu wao uwe mwingi. Kwa maana hilo lilikuwa kulingana na uwezo wao halisi, ndiyo, mimi nashuhudia, kupita uwezo wao halisi, nao kwa kupenda kwao wenyewe waliendelea kutuomba kwa kusihi sana wapate pendeleo la kutoa kwa fadhili na kushiriki katika huduma iliyokusudiwa watakatifu [huko Yudea].” (2 Kor. 8:2-4) Ingawa Wakristo wa Makedonia walikuwa maskini, walikuwa wakarimu sana. Waliona kuwa ni pendeleo kushiriki vitu vyao vya kimwili pamoja na ndugu zao maskini wa Yudea.

13. Maneno “fuateni mwendo wa ukaribishaji-wageni” yanamaanisha nini?

13 Maneno “fuateni mwendo wa ukaribishaji-wageni” yametafsiriwa kutokana na neno la Kigiriki ambalo linamaanisha kuchukua hatua ya kwanza. Tafsiri ya Biblia ya The New Jerusalem Bible inatafsiri hivi maneno hayo: “Tafuta nafasi za kuwa mkaribishaji-wageni.” Nyakati nyingine ukaribishaji-wageni unaonyeshwa kwa kumwalika mtu fulani kwa ajili ya chakula, na tunastahili pongezi ikiwa tunafanya hivyo kwa upendo. Lakini tukichukua hatua ya kwanza ya kuwaalika wengine, tutagundua njia nyingine nyingi za kuwa wakaribishaji-wageni. Ikiwa hali yetu ya kiuchumi au ya kiafya haituruhusu kuwaalika wengine kwa ajili ya chakula, tunaweza kuwaonyesha ukaribishaji-wageni kwa kuwaalika kwa ajili ya kikombe cha kahawa, cha chai, au kinywaji cha aina nyingine.

14. (a) Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “ukaribishaji-wageni” linatokana na maneno gani? (b) Tunaweza kuonyesha jinsi gani kwamba tunawajali wageni katika huduma?

14 Ukaribishaji-wageni unahusisha mtazamo wetu. Neno la Kigiriki ambalo limetafsiriwa “ukaribishaji-wageni” linatokana na maneno mawili ya msingi ambayo yanamaanisha “upendo” na “mgeni.” Tuna maoni gani kuhusu wageni, au watu tusiowajua? Wakristo wanaojitahidi kujifunza lugha nyingine ili wawahubirie habari njema wageni kutoka nchi nyingine ambao wamehamia katika eneo la kutaniko lao wanaweza kwa kweli kuonwa kuwa kati ya watu wanaofuata mwendo wa ukaribishaji-wageni. Bila shaka, wengi wetu hatuwezi kujifunza lugha nyingine. Hata hivyo, sote tunaweza kushiriki kikamilifu katika kuwasaidia wageni kwa kutumia vizuri kijitabu chetu Good News for People of All Nations (Une bonne nouvelle pour des gens de toutes nations), ambacho kina ujumbe wa Biblia katika lugha nyingi. Je, umepata matokeo mazuri kwa kutumia kijitabu hicho katika huduma?

Hisia-Mwenzi

15. Yesu aliweka jinsi gani mfano katika kufuata shauri la Waroma 12:15?

15 Soma Waroma 12:15. Shauri la Paulo katika mstari huo linaweza kuelezwa kwa maneno machache tu: Onyesha hisia-mwenzi. Tunahitaji kujifunza kuelewa na hata kuhisi kama mtu mwingine anavyohisi, iwe ana shangwe au amehuzunika. Ikiwa tunawaka roho, hisia zetu za shangwe au huruma kwa wengine zitaonekana. Wanafunzi 70 wa Kristo waliporudi wakiwa na shangwe baada ya kampeni ya kuhubiri na kuanza kusimulia matokeo mazuri ya kazi yao, Yesu mwenyewe ‘akawa na shangwe sana katika roho takatifu.’ (Luka 10:17-21) Alifurahi pamoja nao. Kwa upande mwingine, Yesu ‘alilia pamoja na watu waliokuwa wakilia’ wakati rafiki yake Lazaro alipokufa.—Yoh. 11:32-35.

16. Tunaweza kuonyesha jinsi gani hisia-mwenzi, na ni nani hasa wanaohitaji kufanya hivyo?

16 Tunataka kufuata mfano wa Yesu katika kuonyesha hisia-mwenzi. Mkristo mwenzetu anaposhangilia, tunataka kushangilia pamoja naye. Vivyo hivyo, tunapaswa kuwahurumia ndugu na dada zetu kwa sababu ya uchungu na maumivu yao. Mara nyingi, tunaweza kuwafariji sana waamini wenzetu ambao wanateseka kihisia ikiwa tutachukua wakati wa kuwasikiliza kwa huruma. Na nyakati nyingine, huenda tukaguswa moyo sana na hivyo kuonyesha hisia-mwenzi zetu za kweli kwa machozi. (1 Pet. 1:22) Wazee, hasa, wanapaswa kufuata shauri ambalo Paulo alitoa kuhusu kuonyesha hisia-mwenzi.

17. Tumejifunza mambo gani kutokana na Waroma sura ya 12, na ni mambo gani yatakayozungumziwa katika habari inayofuata?

17 Katika mistari ambayo tumezungumzia katika andiko la Waroma sura ya 12 tumepata mashauri tunayoweza kutumia katika maisha yetu binafsi tukiwa Wakristo na katika uhusiano wetu pamoja na ndugu zetu. Katika habari inayofuata, tutachunguza mistari inayobaki ya sura hiyo, ambayo inaonyesha jinsi tunavyopaswa kuwaona na kushughulika na watu walio nje ya kutaniko la Kikristo, kutia ndani wapinzani na wale wanaotutesa.

Kwa Kupitia

• Tunaonyesha jinsi gani kwamba ‘tunawaka roho’?

• Kwa nini tunapaswa kumtumikia Mungu kwa unyenyekevu na kiasi?

• Tunaweza kuwaonyesha waamini wenzetu hisia-mwenzi na huruma katika njia gani?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 4]

Kwa nini tunashiriki katika utendaji huu wa Kikristo?

[Picha katika ukurasa wa 6]

Kila mmoja wetu anaweza kushiriki jinsi gani katika kuwasaidia wageni kutoka nchi nyingine kujifunza kuhusu Ufalme?