Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Endelea Kukua Katika Upendo wa Kindugu

Endelea Kukua Katika Upendo wa Kindugu

Endelea Kukua Katika Upendo wa Kindugu

“Endeleeni kutembea katika upendo, kama vile Kristo pia alivyowapenda ninyi.”—EFE. 5:2.

1. Yesu alisema wafuasi wake wangekuwa na sifa gani ya maana?

MASHAHIDI WA YEHOVA wanatambuliwa kwa sababu ya kazi yao ya kuhubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu nyumba kwa nyumba. Hata hivyo, Kristo Yesu alichagua sifa tofauti ya Ukristo ambayo ingewatambulisha wanafunzi wake wa kweli. Alisema hivi: “Ninawapa ninyi amri mpya, kwamba mpendane; kama vile ambavyo nimewapenda ninyi, ninyi nanyi mpendane vivyo hivyo. Kwa jambo hili wote watajua kwamba ninyi ni wanafunzi wangu, mkiwa na upendo kati yenu wenyewe.”—Yoh. 13:34, 35.

2, 3. Upendo wetu wa kindugu una matokeo gani mazuri kwa wale wanaohudhuria mikutano yetu ya Kikristo?

2 Upendo ambao unaonyeshwa katika undugu wa kweli wa Kikristo ni wa pekee sana katika jamii ya wanadamu. Kama vile sumaku inavyovuta chuma, ndivyo upendo unavyowavuta pamoja watumishi wa Yehova kwa umoja na kuwavuta watu wanyoofu kwenye ibada ya kweli. Kwa mfano, mfikirie mwanamume anayeitwa Marcelino huko Kamerun ambaye alipofuka macho akiwa kazini. Baada ya kupata msiba huo, uvumi ulienea kwamba alipofuka kwa sababu alikuwa mchawi. Badala ya kumfariji, kasisi na washiriki wengine wa kanisa lao walimfukuza kutoka kanisani. Shahidi wa Yehova alipomwalika kwenye mkutano, Marcelino alisitasita. Aliogopa kufukuzwa tena.

3 Marcelino alishangazwa na kilichotukia kwenye Jumba la Ufalme. Alikaribishwa kwa uchangamfu, na akafarijiwa na mafundisho ya Biblia ambayo alisikia. Alianza kuhudhuria mikutano yote ya kutaniko, akafanya maendeleo katika funzo lake la Biblia, kisha akabatizwa mwaka wa 2006. Sasa anawafundisha majirani na watu wa familia yake kweli na ameanzisha mafunzo mengi ya Biblia. Marcelino anataka watu ambao anawafundisha Biblia wafurahie upendo uleule ambao amefurahia kati ya watu wa Mungu.

4. Kwa nini tunapaswa kutii shauri la Paulo la ‘kuendelea kutembea katika upendo’?

4 Upendo wetu wa kindugu unavutia sana, lakini tunapaswa kujitahidi kuudumisha. Hebu wazia jinsi moto unaong’aa nje wakati wa usiku unavyowavutia watu wanaotaka kuota moto. Watu ambao wanafurahia moto huo wasipoongeza kuni, utazimika. Vivyo hivyo, kifungo kizuri ajabu cha upendo katika kutaniko kitadhoofika tusipojitahidi kukitia nguvu tukiwa Mkristo mmoja-mmoja. Tunaweza kufanya hivyo jinsi gani? Mtume Paulo anajibu hivi: “Endeleeni kutembea katika upendo, kama vile Kristo pia alivyowapenda ninyi na kujitoa mwenyewe kwa ajili yenu kuwa toleo na dhabihu kwa Mungu ili kuwa harufu tamu.” (Efe. 5:2) Swali ambalo tunataka kuchunguza ni hili, Ninaweza kuendelea kutembea katika upendo kwa njia gani?

“Ninyi, Pia, Panukeni”

5, 6. Kwa nini Paulo aliwahimiza Wakristo Wakorintho ‘wapanuke’?

5 Mtume Paulo aliwaandikia hivi Wakristo katika jiji la kale la Korintho: “Kinywa chetu kimefunguliwa kwenu, enyi Wakorintho, moyo wetu umepanuka. Ninyi hamjasongwa mkakosa nafasi ndani yetu, lakini mmesongwa mkakosa nafasi katika upendo wenu mwororo. Kwa hiyo, yakiwa kama malipo—mimi nasema kana kwamba ni kwa watoto—ninyi, pia, panukeni.” (2 Kor. 6:11-13) Kwa nini Paulo aliwahimiza Wakorintho wapanuke katika upendo wao?

6 Fikiria jinsi kutaniko katika jiji la kale la Korintho lilivyoanza. Paulo alikuja Korintho mwishoni mwa mwaka wa 50 W.K. Ingawa mtume huyo alikabili matatizo alipoanza kuhubiri katika jiji hilo, hakukata tamaa. Baada ya muda mfupi, watu wengi katika jiji hilo waliamini habari njema. Kwa “mwaka mmoja na miezi sita,” Paulo alijitoa kabisa katika kufundisha na kulitia nguvu kutaniko hilo jipya. Ni wazi kwamba aliwapenda sana Wakristo Wakorintho. (Mdo. 18:5, 6, 9-11) Walikuwa na kila sababu ya kumpenda na kumheshimu Paulo pia. Hata hivyo, watu fulani katika kutaniko hilo walijitenga naye. Labda watu wachache hawakupenda mashauri yake ya waziwazi. (1 Kor. 5:1-5; 6:1-10) Huenda wengine walisikiliza uchongezi wa wale ‘mitume walio bora sana.’ (2 Kor. 11:5, 6) Paulo alitaka ndugu na dada zake wote wampende kikweli. Kwa hiyo, aliwasihi ‘wapanuke’ kwa kuwa na uhusiano wa karibu pamoja naye na waamini wenzao.

7. Tunaweza ‘kupanuka’ jinsi gani katika kuonyesha upendo wa kindugu?

7 Namna gani sisi? Tunaweza ‘kupanuka’ jinsi gani katika kuonyesha upendo wa kindugu? Kwa kawaida, huenda watu wenye umri mmoja au wa kabila moja wakapendana. Na mara nyingi watu wanaopenda tafrija ileile wanatumia wakati mwingi pamoja. Lakini ikiwa mapendezi yetu pamoja na Wakristo fulani yanatutenganisha na Wakristo wengine, tunahitaji ‘kupanuka.’ Ni jambo la hekima kujiuliza hivi: ‘Je, mara nyingi ninaepuka kuhubiri au kushiriki katika tafrija na ndugu na dada ambao si marafiki wangu wa karibu? Kwenye Jumba la Ufalme, je, ninaepuka kushirikiana sana na watu wapya kwa sababu ninaamini kwamba ili wawe marafiki wangu ni lazima muda mrefu upite? Je, ninawasalimu watu wenye umri mkubwa na pia wale wenye umri mdogo katika kutaniko?’

8, 9. Shauri la Paulo katika Waroma 15:7 linaweza kutusaidia namna gani kusalimiana kwa njia ambayo itaboresha upendo wetu wa kindugu?

8 Kuhusu kusalimiana, maneno ya Paulo kwa Waroma yanaweza kutusaidia kusitawisha maoni yanayofaa kuelekea waabudu wenzetu. (Soma Waroma 15:7.) Neno la Kigiriki ambalo linatafsiriwa ‘karibisha’ linamaanisha “kumpokea mtu kwa fadhili au kwa ukarimu, kumruhusu ajiunge na kikundi chako na awe rafiki yako.” Katika nyakati za Biblia, mtu mkarimu alipowakaribisha marafiki katika nyumba yake, aliwaeleza jinsi alivyofurahi sana kuwaona. Kwa njia ya mfano, Kristo ametukaribisha hivyo katika kutaniko, na tunahimizwa tumwige katika kuwakaribisha waabudu wenzetu.

9 Tunapowasalimu ndugu zetu kwenye Jumba la Ufalme na sehemu nyinginezo, tunaweza kuwakazia uangalifu wale ambao hatujawaona au kuzungumza nao karibuni. Kwa nini usitumie dakika chache kuzungumza nao? Katika mkutano unaofuata, tunaweza kuzungumza na wengine. Baada ya muda mfupi, tutakuwa tumefurahia kuzungumza na karibu ndugu na dada zetu wote. Hakuna haja ya kuhangaika ikiwa hatuwezi kuzungumza na kila mtu siku ileile. Hakuna mtu anayepaswa kukasirika ikiwa hatuwezi kumsalimu katika kila mkutano.

10. Watu wote katika kutaniko wana nafasi gani bora sana, na tunaweza kuitumia kikamili jinsi gani?

10 Kuwasalimu wengine ni hatua ya kwanza ya kuwakaribisha. Ni hatua inayoweza kuongoza kwenye mazungumzo yenye kufurahisha na urafiki wa kudumu. Kwa mfano, wale wanaohudhuria makusanyiko mbalimbali wanapojitambulisha kwa wengine na kuanza kuzungumza nao, wanatamani kuonana tena. Wale wanaojitolea kujenga Majumba ya Ufalme na pia wale wanaoshiriki katika kazi ya kutoa misaada, mara nyingi wanakuwa marafiki wazuri kwa sababu baada ya muda wanajua sifa nzuri za wenzao wanapozungumza kuhusu mambo ambayo wamejionea katika maisha. Katika tengenezo la Yehova kuna nafasi nyingi sana za kuanzisha urafiki wa kudumu. ‘Tukipanuka,’ tutapata marafiki wengi zaidi, na upendo ambao unatuunganisha katika ibada ya kweli utaongezeka.

Tafuta Wakati wa Kuzungumza na Wengine

11. Kama andiko la Marko 10:13-16 linavyoonyesha, Yesu aliweka mfano gani?

11 Wakristo wote wanaweza kujitahidi kuwa wenye urafiki na rahisi kufikiwa na wengine, kama Yesu alivyokuwa. Fikiria jinsi Yesu alivyosema wakati wanafunzi wake walipojaribu kuwazuia wazazi wasimletee watoto wao. Alisema hivi: “Waacheni watoto wachanga waje kwangu; msijaribu kuwazuia, kwa maana ufalme wa Mungu ni wa wale walio kama hao.” Kisha “akachukua watoto akawakumbatia na kuanza kuwabariki, akiweka mikono yake juu yao.” (Marko 10:13-16) Hebu wazia jinsi watoto hao walivyosisimka walipoonyeshwa upendo na Yesu, yule Mwalimu Mkuu!

12. Ni nini kinachoweza kutuzuia tusizungumze na wengine?

12 Kila Mkristo anapaswa kujiuliza, ‘Je, ninajitahidi kuzungumza na wengine, au mara nyingi ninaonekana kuwa mwenye shughuli nyingi sana?’ Nyakati nyingine, mazoea ambayo si mabaya yanaweza kuzuia mazungumzo. Kwa mfano, ikiwa tunapokuwa na wengine tunatumia kwa ukawaida simu ya mkononi au tunavaa masikioni vifaa vya kusikiliza habari iliyorekodiwa, tunaweza kuwafanya wafikiri kwamba hatupendi kushirikiana nao. Ikiwa mara nyingi wengine wanatuona tukikaza akili zetu zote kwenye redio au kompyuta ya mkononi, huenda wakakata kauli kwamba hatupendi kuzungumza nao. Bila shaka, kuna “wakati wa kukaa kimya.” Lakini kwa kawaida, tunapokuwa na wengine, huo ni “wakati wa kusema.” (Mhu. 3:7) Huenda wengine wakasema, “Ninapenda kukaa peke yangu” au “Sipendi kuongea asubuhi.” Hata hivyo, tunapozungumza kwa urafiki na wengine hata wakati ambapo hatupendi kuzungumza, tunathibitisha kwamba tuna upendo ambao “hautafuti faida zake wenyewe.”—1 Kor. 13:5.

13. Paulo alimtia moyo Timotheo awe na maoni gani kuhusu ndugu na dada zake Wakristo?

13 Paulo alimtia moyo kijana Timotheo awaheshimu washiriki wote wa kutaniko. (Soma 1 Timotheo 5:1, 2.) Sisi pia tunapaswa kuwatendea Wakristo waliozeeka kama mama na baba zetu, na watoto kama ndugu na dada zetu wa kimwili. Tukiwa na mtazamo huo, hakuna ndugu wala dada yetu mpendwa ambaye ataogopa kuzungumza na sisi.

14. Kuna faida gani ya kuwa na mazungumzo yenye kujenga pamoja na wengine?

14 Tunapokuwa na mazungumzo yenye kujenga pamoja na wengine, tunawasaidia kuwa na hali nzuri ya kiroho na ya kihisia. Ndugu fulani anayetumika kwenye ofisi moja ya tawi anafurahi sana anapokumbuka jinsi Wanabetheli fulani wenye umri mkubwa walivyozungumza naye kwa ukawaida alipokuwa mpya Betheli. Maneno yao yenye kutia moyo yalimfanya ahisi kwamba kwa kweli alipendwa na familia ya Betheli. Sasa anajitahidi kuwaiga kwa kuzungumza na Wanabetheli wenzake.

Unyenyekevu Unatusaidia Kufanya Amani

15. Ni nini kinachoonyesha kwamba tunaweza kukosana?

15 Inaonekana kwamba Euodia na Sintike, dada wawili Wakristo katika jiji la kale la Filipi, walishindwa kusuluhisha tatizo fulani la kutoelewana kati yao. (Flp. 4:2, 3) Ubishi mkali kati ya Paulo na Barnaba ulijulikana na watu wengi na uliwafanya watengane kwa muda fulani. (Mdo. 15:37-39) Masimulizi hayo yanaonyesha kwamba waabudu wa kweli wanaweza kukosana. Yehova anatusaidia kutatua hali za kutoelewana na kuanzisha tena urafiki. Lakini anataka tuchukue hatua fulani.

16, 17. (a) Unyenyekevu ni wa maana kadiri gani katika kusuluhisha matatizo ya kutoelewana? (b) Simulizi la jinsi Yakobo alivyotenda alipokutana na Esau linaonyesha namna gani faida ya unyenyekevu?

16 Hebu wazia kwamba wewe na rafiki yako mnataka kusafiri kwa gari. Kabla ya kuanza safari, ni lazima kwanza uwashe gari kwa kutumia ufunguo. Vivyo hivyo, hatua ya kwanza ya kusuluhisha tatizo la kutoelewana ni kutumia ufunguo fulani. Ufunguo huo ni unyenyekevu. (Soma Yakobo 4:10.) Kama mfano unaofuata wa Kimaandiko unavyoonyesha, ufunguo huo unawawezesha wale ambao wamekosana kuanza kutumia kanuni za Biblia.

17 Miaka 20 ilikuwa imepita tangu Esau alipokasirika kwa uchungu kwa sababu ndugu yake pacha, Yakobo, alichukua haki yake ya kuwa mzaliwa wa kwanza, na hivyo alitaka kumuua. Baada ya muda mrefu kupita, mapacha hao walikuwa karibu kukutana tena, “naye Yakobo akaogopa sana, akaanza kuhangaika.” Alihisi kwamba kulikuwa na uwezekano mkubwa wa Esau kumshambulia. Lakini walipokutana, Yakobo alifanya jambo ambalo Esau hakutazamia. “Akaanza kuinama mpaka chini” alipokuwa akimkaribia ndugu yake. Ni nini kilichotukia baada ya hapo? “Esau akaanza kukimbia kwenda kumpokea. Naye akaanza kumkumbatia na kumwangukia shingoni, akambusu, nao wakatokwa na machozi.” Hatari ya vita kutokea kati yao iliepukwa. Unyenyekevu wa Yakobo ulisaidia kuondoa chuki yoyote ambayo huenda Esau alikuwa amefungia moyoni.—Mwa. 27:41; 32:3-8; 33:3, 4.

18, 19. (a) Tunapokosana na wengine, kwa nini ni jambo la maana sisi tuchukue hatua ya kwanza na kufuata mashauri ya Kimaandiko? (b) Kwa nini hatupaswi kukata tamaa wakati mtu tuliyekosana naye anapokosa kuitikia vizuri mwanzoni?

18 Biblia ina mashauri mazuri sana kuhusu kusuluhisha matatizo ya kutoelewana. (Mt. 5:23, 24; 18:15-17; Efe. 4:26, 27) * Hata hivyo, tusipofuata kwa unyenyekevu mashauri hayo, itakuwa vigumu kufanya amani. Kumngoja yule mtu mwingine aonyeshe unyenyekevu si suluhisho la matatizo ikiwa sisi pia tuna ufunguo huo mikononi mwetu.

19 Ikiwa hatua ambazo tumechukua mwanzoni za kufanya amani zinaonekana hazifanikiwi kwa sababu fulani, hatupaswi kukata tamaa. Huenda yule mtu mwingine akahitaji wakati wa kuchunguza hisia zake. Ndugu za Yosefu walimtendea kwa hila. Muda mrefu ulipita kabla hawajakutana naye akiwa waziri mkuu wa Misri. Hata hivyo, mwishowe walibadili mioyo yao na kumwomba msamaha. Yosefu aliwasamehe, na wana wa Yakobo wakawa taifa ambalo lilipata pendeleo la kuitwa kwa jina la Yehova. (Mwa. 50:15-21) Tunapodumisha amani pamoja na ndugu na dada zetu, tunachangia umoja na shangwe ya kutaniko.—Soma Wakolosai 3:12-14.

Acheni Tupendane “kwa Tendo na Kweli”

20, 21. Tunajifunza somo gani kutokana na hatua ya Yesu ya kuwaosha miguu mitume wake?

20 Muda mfupi kabla ya kifo chake, Yesu aliwaambia hivi mitume wake: “Niliweka kielelezo kwa ajili yenu, ili, kama vile nilivyowafanyia ninyi, ninyi pia mfanye hivyo.” (Yoh. 13:15) Alikuwa tu amemaliza kuwaosha miguu wanafunzi wake 12. Yesu hakufanya hivyo kama desturi tu au kama tendo la fadhili tu. Kabla ya kueleza simulizi hilo la kuwaosha mitume miguu, Yohana aliandika hivi: “Yesu, akiwa amewapenda walio wake mwenyewe waliokuwa ulimwenguni, akawapenda mpaka mwisho.” (Yoh. 13:1) Yesu alifanya utumishi ambao kwa kawaida ulifanywa na mtumwa kwa sababu alichochewa na upendo kuwaelekea wanafunzi wake. Walipaswa sasa kutendeana kwa upendo na kwa unyenyekevu. Ndiyo, upendo wa kweli wa kindugu unapaswa kutuchochea kuwahangaikia na kuwajali ndugu na dada zetu wote Wakristo.

21 Mtume Petro, ambaye alioshwa miguu na Mwana wa Mungu, alielewa maana ya jambo ambalo Yesu alifanya. Aliandika hivi: “Sasa kwa kuwa mmezitakasa nafsi zenu kwa kuwa watiifu kwa ile kweli tokeo likiwa ni upendo wa kindugu usio na unafiki, pendaneni sana kutoka moyoni.” (1 Pet. 1:22) Mtume Yohana, ambaye pia alioshwa miguu na Bwana, aliandika hivi: “Watoto wadogo, acheni tupendane, si kwa neno wala kwa ulimi, bali kwa tendo na kweli.” (1 Yoh. 3:18) Mioyo yetu na ituchochee kuonyesha upendo wetu wa kindugu kwa matendo.

[Maelezo ya chini]

^ fu. 18 Ona kitabu Tengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova, ukurasa wa 144-150.

Je, Unakumbuka?

• Tunaweza ‘kupanuka’ kwa njia gani katika upendo wetu kwa wenzetu?

• Ni nini kitakachotusaidia kutafuta wakati wa kuzungumza na wengine?

• Unyenyekevu unasaidia jinsi gani katika kufanya amani?

• Ni nini kinachopaswa kutuchochea kuwajali waamini wenzetu?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 21]

Wakaribishe kwa uchangamfu waamini wenzako

[Picha katika ukurasa wa 23]

Usikose kutumia nafasi unazopata za kuzungumza na wengine