Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuonyesha Adabu Tukiwa Wahudumu wa Mungu

Kuonyesha Adabu Tukiwa Wahudumu wa Mungu

Kuonyesha Adabu Tukiwa Wahudumu wa Mungu

“Iweni waigaji wa Mungu.”—EFE. 5:1.

1, 2. (a) Kwa nini ni jambo la maana kuwa na adabu? (b) Ni nini kitakachozungumziwa katika habari hii?

MWANDISHI wa vitabu, Sue Fox aliandika hivi kuhusu kujiendesha kwa heshima: “Hatuwezi kuchukua likizo katika kuonyesha adabu. Kuonyesha adabu kuna matokeo mazuri kila mahali na kila wakati.” Watu wanapozoea kuonyesha adabu, matatizo kati yao na wengine yanapungua na mara nyingi yanatoweka. Lakini wasipozoea kuonyesha adabu matatizo yanaongezeka. Kuwatendea wengine bila adabu kunasababisha migogoro, chuki, na huzuni.

2 Kwa ujumla, washiriki wa kutaniko la kweli la Kikristo ni watu wenye adabu. Hata hivyo, ni lazima tujilinde ili tusiige ukosefu wa adabu ambao umeenea katika ulimwengu leo. Acheni tuone jinsi kutumia kanuni za Biblia zinazohusu adabu kunavyoweza kutulinda katika jambo hilo na kuwavuta watu kwenye ibada ya kweli. Ili uelewe mambo yanayohusika katika kuonyesha adabu, fikiria mfano wa Yehova Mungu na Mwana wake.

Yehova na Mwana Wake Ni Mifano Mizuri Katika Kuonyesha Adabu

3. Yehova Mungu ameweka mfano gani katika kuonyesha adabu?

3 Yehova Mungu anaweka mfano mkamilifu katika kuonyesha adabu. Hata ingawa ana cheo kikubwa akiwa Mwenye Enzi Kuu wa ulimwengu wote, anawatendea wanadamu kwa fadhili na heshima kubwa. Yehova alipozungumza na Abrahamu na Musa, alitumia neno la Kiebrania ambalo mara nyingi linatafsiriwa “tafadhali.” (Mwa. 13:14; Kut. 4:6) Watumishi wake wanapotenda makosa, Yehova ni “mwenye rehema na mwenye neema, si mwepesi wa hasira na ni mwingi wa fadhili zenye upendo na ukweli.” (Zab. 86:15) Yuko tofauti kabisa na wanadamu fulani ambao wanafoka kwa hasira wengine wanapowakosea.

4. Tunaweza kumwiga Yehova jinsi gani wengine wanapoongea na sisi?

4 Mungu anaonyesha pia adabu katika njia anayowasikiliza wanadamu. Abrahamu alipouliza maswali kuhusu watu wa Sodoma, Yehova alijibu kila swali kwa subira. (Mwa. 18:23-32) Hakuona kwamba mahangaiko ya Abrahamu yalimpotezea wakati. Yehova anasikiliza sala za watumishi wake na vilio vya watenda-dhambi wanaotubu. (Soma Zaburi 51:11, 17.) Je, hatupaswi kumwiga Yehova kwa kuwasikiliza wengine wanapoongea na sisi?

5. Kumwiga Yesu katika kuonyesha adabu kunaweza kuboresha jinsi gani uhusiano wetu na wengine?

5 Kati ya mambo mengi ambayo Yesu Kristo alijifunza kutoka kwa Baba yake ni kuonyesha adabu. Ingawa nyakati nyingine Yesu alihitaji kutumia nguvu na wakati wake mwingi katika huduma, sikuzote alikuwa mwenye subira na mwenye fadhili. Watu wenye ukoma, vipofu waliokuwa wakiomba-omba msaada, na wengine wenye uhitaji waliona kwamba Yesu alikuwa tayari na alipenda kuwasaidia. Hakuwapuuza, ingawa walikuja kumwona bila kumjulisha mapema. Mara nyingi, alikatisha shughuli zake ili amsaidie mtu aliyekuwa akiteseka. Yesu aliwajali kwa njia ya pekee sana watu waliomwamini. (Marko 5:30-34; Luka 18:35-41) Tukiwa Wakristo, tunafuata mfano wa Yesu kwa kuwa wenye fadhili na tayari kusaidia. Watu wetu wa ukoo, majirani, na watu wengine wanaona tunapojiendesha kwa njia hiyo. Zaidi ya hayo, tunapojiendesha hivyo tunamletea Yehova utukufu nasi tunapata furaha.

6. Yesu aliweka mfano gani katika kuonyesha uchangamfu na urafiki?

6 Pia, Yesu aliwaheshimu watu kwa kuwaita kwa majina yao. Je, viongozi wa dini ya Kiyahudi waliwaheshimu wengine kwa njia hiyo? Hapana. Waliwaona watu ambao hawakujua Sheria kuwa “watu waliolaaniwa” na waliwatendea hivyo. (Yoh. 7:49) Mwana wa Mungu hakuwatendea hivyo. Martha, Maria, Zakayo, na wengine wengi walimsikia akiwaita kwa majina yao. (Luka 10:41, 42; 19:5) Ingawa huenda utamaduni na hali zikaamua jinsi tunavyozungumza na watu leo, watumishi wa Yehova wanajitahidi kuwaonyesha wengine uchangamfu. * Hawaruhusu tofauti za kijamii ziwazuie kuwaonyesha waamini wenzao na watu wengine heshima wanayostahili.—Soma Yakobo 2:1-4.

7. Kanuni za Biblia zinatusaidia jinsi gani kuwatendea kwa adabu wanadamu wenzetu kila mahali?

7 Mungu na Mwana wake wanawatendea watu wa mataifa na makabila yote kwa njia ya neema au fadhili na hilo linaonyesha kwamba wanawaheshimu watu hao na hilo linawavutia wale walio na mtazamo unaofaa kuelekea kweli. Bila shaka, katika sehemu mbalimbali za ulimwengu watu wanaonyesha adabu kwa njia tofauti-tofauti. Kwa hiyo, hatufuati sheria kali kuhusu kuonyesha adabu. Badala yake, tunaruhusu kanuni za Biblia zitusaidie kubadilika kulingana na hali kwa kuwaheshimu wanadamu wenzetu kila mahali. Acheni tuchunguze jinsi tunavyoweza kupata matokeo mazuri katika huduma ya Kikristo kwa kuwatendea watu kwa adabu.

Kuwasalimu Watu na Kuongea Nao

8, 9. (a) Ni mazoea gani yanayoweza kuonwa kuwa yasiyo ya adabu? (b) Kwa nini tunapaswa kuruhusu maneno ya Yesu kwenye Mathayo 5:47 yaongoze jinsi tunavyowatendea wengine?

8 Katika maisha haya yenye shughuli nyingi ambazo ni za kawaida katika sehemu nyingi leo, mara nyingi watu wawili wanapitana bila hata kusema “habari yako” au “hujambo?” Bila shaka, hakuna mtu anayetazamiwa kuongea na kila mtu anayekutana naye kwenye njia iliyojaa watu. Hata hivyo, katika hali nyingine nyingi, ni jambo linalofaa na linalopendeza kuwasalimu wengine. Je, una mazoea ya kuwasalimu watu? Au mara nyingi unawapita tu bila kutabasamu au kuwaambia neno zuri? Bila nia mbaya, mtu anaweza kusitawisha mazoea ambayo kwa kweli hayaonyeshi adabu.

9 Yesu alitukumbusha hivi: “Mkiwasalimu ndugu zenu tu, mnafanya jambo gani linalozidi lile la kawaida? Je, watu wa mataifa pia hawafanyi jambo hilohilo?” (Mt. 5:47) Kuhusu jambo hilo, mshauri Donald Weiss aliandika hivi: “Watu wanachukia kuona wengine wakiwapita bila kusema neno lolote au wakiwapuuza. Kwa kweli, huwezi kutoa sababu yoyote inayoweza kuwatuliza watu ambao umewapuuza. Suluhisho ni rahisi: Salimu watu. Zungumza nao.” Tutapata matokeo mazuri tusipowapuuza wengine au kuwaonyesha ubaridi.

10. Kujiendesha kwa adabu kunaweza kutusaidia jinsi gani kupata matokeo mazuri katika huduma? (Ona sanduku  “Anza kwa Tabasamu Changamfu.”)

10 Fikiria kisa cha Tom na Carol, wenzi wa ndoa Wakristo ambao wanaishi katika mji fulani mkubwa huko Amerika Kaskazini. Kuanzisha mazungumzo ya kirafiki pamoja na majirani wao kumekuwa sehemu ya huduma yao. Wanafanya hivyo jinsi gani? Akitaja andiko la Yakobo 3:18, Tom anasema: “Tunajaribu kuwa wenye urafiki na kufanya amani na watu. Tunazungumza na watu tunaowakuta nje ya nyumba zao na wale wanaofanya kazi katika eneo hilo. Tunatabasamu na kuwasalimu. Tunaongea nao kuhusu mambo yanayowapendeza, kama vile watoto wao, mbwa wao, nyumba zao, na kazi zao. Baada ya muda, wanatuona kuwa marafiki wao.” Carol anaongezea hivi: “Baadaye tunapowatembelea, tunawajulisha majina yetu na kuwauliza majina yao. Tunawaeleza kuhusu shughuli zetu katika eneo hilo lakini tunaongea nao kwa muda mfupi tu. Mwishowe, tunawatolea ushahidi.” Tom na Carol wanapendwa sana na wengi kati ya majirani wao. Wengi wao wamekubali kuchukua vichapo vinavyotegemea Biblia, na wachache wameonyesha kwamba wanapendezwa sana kujifunza kweli.

Kuonyesha Adabu Tunapokabili Hali Ngumu

11, 12. Kwa nini tunapaswa kutazamia kutendewa vibaya tunapohubiri habari njema, na tunapaswa kutenda jinsi gani?

11 Nyakati nyingine, tunatendewa kwa njia isiyo ya heshima tunapohubiri habari njema. Tunatazamia kutendewa hivyo, kwa kuwa Kristo Yesu aliwaonya hivi mapema wanafunzi wake: “Ikiwa wamenitesa mimi, watawatesa ninyi pia.” (Yoh. 15:20) Lakini hatuwezi kupata matokeo mazuri kwa kuwatendea vibaya watu wanaosema mambo mabaya kutuhusu. Tunapaswa kuwatendea namna gani? Mtume Petro aliandika hivi: “Mtakaseni Kristo kuwa Bwana katika mioyo yenu, sikuzote mkiwa tayari kujitetea mbele ya kila mtu ambaye hutaka kutoka kwenu sababu ya tumaini lililo ndani yenu, lakini mkifanya hivyo kwa tabia-pole na heshima kubwa.” (1 Pet. 3:15) Tukionyesha adabu kwa kuongea kwa upole na heshima, tunaweza kubadili mtazamo wa wale ambao wanatutukana.—Tito 2:7, 8.

12 Je, tunaweza kujitayarisha kuwajibu wenye dhihaka kwa njia ambayo inakubaliwa na Mungu? Ndiyo. Paulo alipendekeza hivi: “Maneno yenu na yawe yenye neema sikuzote, yenye kukolezwa chumvi, ili mjue jinsi mnavyopaswa kumjibu kila mtu.” (Kol. 4:6) Ikiwa tutakuwa na mazoea ya kuwatendea kwa adabu washiriki wa familia yetu, wanafunzi wenzetu, wafanyakazi wenzetu, washiriki wenzetu kutanikoni, na majirani wetu, basi itakuwa rahisi zaidi kwetu kukabiliana kwa njia ya Kikristo na watu wanaotudhihaki na kututukana.—Soma Waroma 12:17-21.

13. Toa mfano unaoonyesha jinsi kutenda kwa adabu kunavyoweza kubadili mtazamo wa wapinzani.

13 Tukionyesha adabu tunapokabili hali ngumu tutapata matokeo mazuri. Kwa mfano, huko Japani, Shahidi mmoja alidhihakiwa na mwenye nyumba fulani na mgeni wake. Ndugu huyo aliondoka kwa heshima kwenye mlango wa mtu huyo. Alipokuwa akiendelea kuhubiri katika eneo hilo, alimwona yule mgeni akimtazama kwa mbali. Ndugu huyo alipomkaribia, mwanamume huyo alisema hivi: “Pole kwa yale yaliyotukia. Hata ingawa tulikudhihaki, niligundua kwamba uliendelea kutabasamu. Nifanye nini ili niwe kama wewe?” Kwa kuwa mwanamume huyo alikuwa amepoteza kazi na mama yake alikuwa amekufa karibuni, hakuwa na tumaini lolote la kupata furaha. Shahidi huyo alimweleza kuhusu mpango wa kujifunza Biblia, na mwanamume huyo akakubali. Muda si muda, alikuwa akijifunza mara mbili kwa juma.

Njia Bora ya Kusitawisha Mwenendo wa Adabu

14, 15. Watumishi wa Yehova katika nyakati za Biblia waliwazoeza jinsi gani watoto wao?

14 Wazazi waliomwogopa Mungu katika nyakati za Biblia walihakikisha kwamba watoto wao walijifunza mambo ya msingi kuhusu kuonyesha adabu nyumbani. Fikiria jinsi Abrahamu na mwana wake Isaka walivyozungumza kwa heshima kwenye andiko la Mwanzo 22:7. Pia, kisa cha Yosefu kinaonyesha kwamba alizoezwa vizuri na wazazi wake. Alipofungwa gerezani, aliwatendea kwa adabu hata wafungwa wenzake. (Mwa. 40:8, 14) Maneno aliyomwambia Farao yanaonyesha kwamba alikuwa amejifunza njia inayofaa ya kuzungumza na mtu mwenye cheo kikubwa.—Mwa. 41:16, 33, 34.

15 Zile Amri Kumi ambazo wana wa Israeli walipewa zilitia ndani amri hii: “Mheshimu baba yako na mama yako ili siku zako zipate kuwa ndefu juu ya nchi ambayo Yehova Mungu wako anakupa wewe.” (Kut. 20:12) Njia moja ambayo watoto wanaweza kuwaheshimu wazazi wao ni kujiendesha kwa adabu nyumbani. Binti ya Yeftha alionyesha kwamba alimheshimu sana baba yake kwa kutenda kupatana na nadhiri ya baba yake chini ya hali ngumu sana.—Amu. 11:35-40.

16-18. (a) Wazazi wanaweza kufanya nini ili kuwafundisha watoto wao kuwa na adabu? (b) Kuna faida gani za kuwafundisha watoto kuwa wenye adabu?

16 Kuwazoeza watoto wetu kujiendesha kwa adabu ni jambo la maana sana. Ili waishi vizuri na wengine wakiwa watu wazima, watoto wanahitaji kujifunza njia inayofaa ya kuwasalimu wageni, kujibu simu, na kula chakula pamoja na wengine. Wanapaswa kusaidiwa kuelewa kwa nini wanapaswa kushika mlango ili kuwaruhusu wengine wapite, kuwaonyesha fadhili waliozeeka na wagonjwa, na kuwasaidia watu wanaobeba mizigo mizito. Wanahitaji kuelewa faida ya kusema kwa unyoofu maneno kama vile “tafadhali,” “asante,” “unakaribishwa,” “ninaweza kukusaidia?,” na “pole.”

17 Kuwazoeza watoto kuonyesha adabu si jambo gumu. Njia bora ya kuwazoeza ni kuwawekea mfano mzuri. Kurt, mwenye umri wa miaka 25 anasema hivi kuhusu jinsi yeye na ndugu zake watatu walivyojifunza kuwa wenye adabu: “Tuliwatazama na kuwasikiliza Mama na Baba wakiongea pamoja kwa fadhili na kuwatendea watu wengine kwa subira na kuwajali. Kwenye Jumba la Ufalme, kwa kawaida Baba alinichukua kabla na baada ya mikutano alipoenda kuongea na ndugu na dada waliozeeka. Nilisikia jinsi alivyowasalimu na kuona jinsi alivyowaonyesha heshima.” Kurt anaendelea kusema: “Baada ya muda, niliiga mwenendo wake wa adabu. Hivyo, kuwatendea watu kwa heshima na adabu linakuwa jambo la kawaida. Jambo kuu si jinsi unavyopaswa kutenda, bali jinsi unavyotaka kutenda.”

18 Inaelekea matokeo yatakuwa nini ikiwa wazazi watawafundisha watoto wao kuwa na adabu? Watoto wataweza kupata marafiki na kuwa na amani pamoja na wengine. Watakuwa tayari kabisa kushirikiana na wasimamizi wao kazini na wafanyakazi wenzao. Zaidi ya hayo, watoto wenye adabu, wenye heshima, na wanyoofu watawaletea wazazi wao shangwe na uradhi.—Soma Methali 23:24, 25.

Kujiendesha kwa Adabu Kunafanya Tuwe Tofauti na Ulimwengu

19, 20. Kwa nini tunapaswa kuazimia kumwiga Mungu wetu mwenye heshima na Mwana wake?

19 Paulo aliandika hivi: “Iweni waigaji wa Mungu, kama watoto wapendwa.” (Efe. 5:1) Kumwiga Yehova Mungu na Mwana wake kunatia ndani kufuata kanuni za Biblia, kama zile ambazo zimezungumziwa katika habari hii. Tukifanya hivyo, tutaepuka unafiki wa kuonyesha adabu ili tupendwe tu na mtu fulani mwenye cheo au madaraka au ili tupate faida za kimwili.—Yuda 16.

20 Katika siku za mwisho za utawala wake mwovu, Shetani ameazimia kuondoa kabisa viwango vya mwenendo wenye heshima ambavyo Yehova ameweka. Lakini Ibilisi atashindwa kukomesha mwenendo wenye adabu wa Wakristo wa kweli. Kila mmoja wetu na aazimie kufuata mfano wa Mungu wetu mwenye heshima na wa Mwana wake. Tukifanya hivyo, sikuzote maneno na mwenendo wetu utakuwa tofauti na matendo ya wale wanaochagua kutenda kwa njia isiyo ya adabu. Tutaleta sifa kwa jina la Mungu wetu mwenye adabu, Yehova, na tutawavutia watu wanyoofu kwenye ibada yake ya kweli.

[Maelezo ya chini]

^ fu. 6 Katika tamaduni fulani, ni ukosefu wa adabu kumwita mtu mwenye umri mkubwa zaidi yako kwa jina lake la kwanza bila ruhusa yake. Ni vizuri kwa Wakristo kuheshimu desturi kama hizo.

Je, Unakumbuka?

• Tunajifunza nini kutokana na Yehova na Mwana wake kuhusu kuonyesha adabu?

• Kwa nini kuwasalimu watu kwa uchangamfu kunatuletea sifa tukiwa Wakristo?

• Kuwa wenye adabu kunatusaidia jinsi gani kupata matokeo mazuri katika huduma?

• Wazazi wanatimiza daraka gani katika kuwafundisha watoto kuwa wenye adabu?

[Maswali ya Funzo]

[Sanduku katika ukurasa wa 27]

 Anza kwa Tabasamu Changamfu

Watu wengi wanasita-sita kuanzisha mazungumzo na mtu ambaye hawamjui. Hata hivyo, kwa sababu Mashahidi wa Yehova wanampenda Mungu na majirani wao, wanajitahidi sana kujifunza jinsi ya kuzungumza na watu ili wawafundishe wengine kweli za Biblia. Ni nini kinachoweza kukusaidia ufanye maendeleo katika jambo hilo?

Kanuni ya maana sana inatajwa kwenye andiko la Wafilipi 2:4, ambalo linasema hivi: ‘Endeleeni kuangalia, si faida za kibinafsi za mambo yenu wenyewe tu, bali pia faida za kibinafsi za wengine.’ Fikiria maneno hayo kwa njia hii: Ikiwa hujawahi kukutana na mtu fulani, mtu huyo anakuona kuwa mgeni. Unaweza kufanya nini ili ajihisi kwamba amestarehe? Kutabasamu kwa uchangamfu na kumsalimu kwa njia ya kirafiki kunaweza kusaidia. Hata hivyo, kuna mambo mengine ya kufikiria.

Unapojaribu kuanzisha mazungumzo na mtu fulani, huenda umekatisha mawazo yake. Ukijaribu kumfanya azungumze kuhusu mambo unayofikiria bila kujali mawazo yake, huenda asifurahi. Kwa hiyo, ikiwa unaweza kutambua mambo ambayo huenda mtu huyo alikuwa akifikiria, kwa nini usiyatumie kuanzisha mazungumzo pamoja naye? Hivyo ndivyo Yesu alivyofanya alipokutana na mwanamke fulani kwenye kisima huko Samaria. (Yoh. 4:7-26) Mwanamke huyo alikuwa akifikiria kuhusu kuteka maji. Yesu alianzisha mazungumzo na mwanamke huyo kwa msingi huo, na punde si punde akayabadili kuwa mazungumzo machangamfu ya kiroho.

[Picha katika ukurasa wa 26]

Kuwa mwenye urafiki kunaweza kufungua njia ya kutoa ushahidi mzuri

[Picha katika ukurasa wa 28]

Sikuzote ni jambo linalofaa kuonyesha adabu